Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Kile Unachoweka Naziri, Timiza’

‘Kile Unachoweka Naziri, Timiza’

‘Lazima umutimizie Yehova naziri zako.’—MATHAYO 5:33.

NYIMBO: 63, 59

1. (a) Yeftha na Hana walifanya mambo gani yenye kufanana? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.) (b) Tutajibia maulizo gani katika habari hii?

YEFTHA alikuwa kiongozi mwenye ujasiri na mupiganaji wa vita mwenye hakukuwa na woga. Hana alikuwa mwanamuke munyenyekevu mwenye alihangaikia bwana yake na nyumba yake. Wote wawili walikuwa wanamuabudu Yehova. Lakini walifanya pia jambo lingine lenye kufanana. Yeftha na Hana walifanya naziri kwa Yehova, na kila mumoja wao alitimiza naziri yake kwa uaminifu. Waliacha mufano muzuri kwa ajili ya wanaume na wanawake wenye wanaamua kufanya naziri kwa Yehova leo. Tuzungumuzie basi majibu ya maulizo haya tatu: Naziri ni nini? Sababu gani ni jambo nzito kufanya naziri kwa Mungu? Mufano wa Yeftha na Hana unaweza kutufundisha nini?

2, 3. (a) Naziri ni nini? (b) Maandiko yanasema nini juu ya kufanya naziri kwa Mungu?

2 Katika Biblia, naziri ni ahadi nzito yenye mutu anamutolea Mungu. Kwa mufano, mutu anaweza kumuahidi Yehova kama atafanya jambo fulani, atamutolea zawadi fulani, ataingia katika aina fulani ya utumishi, ao atajizuia kufanya mambo fulani. Mutu anafanya naziri kwa kujipendea, ni kusema, kwa kutumia uhuru wake wa kuchagua. Hakuna mutu mwenye anakazwa kufanya naziri. Lakini wakati mutu anaamua kufanya naziri, Yehova anaona naziri hiyo kuwa ahadi nzito yenye mutu anapaswa kuheshimia na kutimiza. Katika Biblia, naziri ni ya maana kama vile kiapo. Kiapo ni maneno yenye mutu anasema ili kuonyesha kuwa atafanya ao hatafanya jambo fulani. (Mwanzo 14:22, 23; Waebrania 6:16, 17) Biblia inasema nini juu ya uzito wa naziri zetu kwa Mungu?

3 Sheria ya Musa ilionyesha kama ikiwa mutu anafanya naziri kwa Yehova ‘hapaswe kulivunja neno lake. Anapaswa kufanya kulingana na yote ambayo yametoka kinywani mwake.’ (Hesabu 30:2) Sulemani alifikia kuandika hivi: ‘Wakati wowote unapoweka naziri kwa Mungu, usisite kuitimiza, kwa maana hapendezwe na wajinga. Kile unachoweka naziri, timiza.’ (Mhubiri 5:4) Yesu alifundisha kama kufanya naziri kwa Mungu ni jambo nzito. Alisema hivi: “Tena mulisikia kwamba watu wa kale waliambiwa, ‘Usiape bila kutimiza, bali lazima umutimizie Yehova naziri zako.’”—Mathayo 5:33.

4. (a) Sababu gani ni jambo nzito kufanya naziri kwa Mungu? (b) Tutajifunza nini juu ya Yeftha na Hana?

4 Ni wazi kwamba tunapaswa kuchukua kwa uzito kila ahadi yenye tunatoa kwa Yehova. Namna tunaona naziri zetu inaweza kuwa na matokeo ya muzuri ao ya mubaya juu ya urafiki wetu pamoja naye. Daudi alionyesha jambo hilo waziwazi wakati aliuliza hivi: ‘Ni nani anayeweza kuupanda mulima wa Yehova, na ni nani anayeweza kusimama katika mahali pake patakatifu?’ Kisha akajibia ulizo hilo kwa kusema kama Yehova atakubali mutu yeyote mwenye ‘hajaapa kwa udanganyifu.’ (Zaburi 24:3, 4) Yeftha na Hana walifanya naziri gani? Ilikuwa vyepesi kwa kila mumoja wao kutimiza naziri yake?

WALITIMIZA NAZIRI ZAO KWA MUNGU

5. Yeftha alifanya naziri gani? Hilo lilikuwa na matokeo gani?

5 Yeftha alitoa ahadi kwa Yehova wakati alikuwa karibu kupigana vita na taifa la Waamoni. Watu wa taifa hilo walikuwa maadui wa watu wa Mungu. (Waamuzi 10:7-9) Yeftha alimuomba sana Yehova amupatie ushindi na alifanya naziri hii: ‘Hakika ukiwatia wana wa Amoni mukononi mwangu itatukia pia kwamba yule atakayetoka inje, atakayetoka inje ya milango ya nyumba yangu kuja kunipokea nitakaporudi kwa amani kutoka kwa wana wa Amoni, lazima atakuwa wa Yehova.’ Mungu alijibia sala ya Yeftha na akamusaidia kupata ushindi katika vita hiyo. Wakati Yeftha alirudia nyumbani, binti yake mupendwa alikuja kumupokea. Ni yeye ndiye ‘angekuwa wa Yehova.’ (Waamuzi 11:30-34) Hilo lingekuwa na maana gani kwake?

6. (a) Ilikuwa vyepesi kwa Yeftha pamoja na binti yake kutimiza naziri yake kwa Mungu? (b) Andiko la Kumbukumbu la Torati 23:21, 23 na Zaburi 15:4 yanatufundisha nini juu ya naziri?

6 Ili kutimiza naziri ya baba yake, binti ya Yeftha alipaswa kuenda kumutumikia Yehova wakati wote kwenye tabenakulo. Yeftha alifanya ahadi hiyo bila kuifikiria? Hapana. Kwa kweli, pengine Yeftha alijua kuwa binti yake ndiye angekuwa mutu wa kwanza kuja kumupokea. Lakini, iwe alijua ao hapana, kutimiza naziri yake kwa Yehova haikukuwa mwepesi kwa Yeftha ao binti yake. Wakati Yeftha alimuona, alisema kwamba moyo wake umevunjika. Binti yake alienda ‘kulilia ubikira wake.’ Sababu gani? Yeftha hakukuwa na mutoto mwanaume, na sasa binti yake mumoja tu hangeolewa hata siku moja na kuzaa watoto. Jina la familia ya Yeftha lingepotea. Lakini Yeftha na binti yake walitambua kuwa naziri hiyo ilikuwa jambo la maana zaidi kuliko namna walikuwa wanajisikia. Yeftha alisema hivi: ‘Nimemufungulia Yehova kinywa changu, nami siwezi kurudi nyuma.’ Binti yake alisema hivi: “Nitendee kulingana na neno lililotoka katika kinywa chako.” (Waamuzi 11:35-39) Yeftha na binti yake walikuwa watu washikamanifu wenye hawangefikiria hata kidogo kuvunja naziri hiyo kwa Mungu, hata kama ilikuwa vigumu sana kwao kutimiza naziri hiyo.​—Soma Kumbukumbu la Torati 23:21, 23; Zaburi 15:4.

7. (a) Hana alifanya naziri gani, na sababu gani? Hilo lilikuwa na matokeo gani? (b) Naziri ya Hana ilimaanisha nini kwa Samweli? (Ona maelezo ya chini.)

7 Hana pia alifanya naziri kwa Yehova wakati alikuwa na mahangaiko katika maisha yake. Alikuwa na huzuni kwa sababu hakukuwa na watoto, na alikuwa anateswa na kuzarauliwa kwa sababu ya jambo hilo. (1 Samweli 1:4-7, 10, 16) Aliambia Yehova namna alikuwa anajisikia, na akatoa ahadi hii: ‘Ee Yehova wa majeshi, ikiwa hakika utayaona mateso ya kijakazi wako, nawe kwa kweli unikumbuke, na ikiwa hautamusahau kijakazi wako na kwa kweli umupe kijakazi wako uzao wa kiume, mimi nitamutoa kwa Yehova siku zote za maisha yake, wala wembe hautapita juu ya kichwa chake.’ * (Soma maelezo ya chini.) (1 Samweli 1:11) Yehova alisikiliza sala ya Hana, na mwaka wenye ulifuata alizaa mutoto mwanaume, Samweli. Hana alifurahi sana! Lakini hakusahau naziri yenye alimutolea Mungu. Wakati mutoto wake mwanaume alizaliwa, alisema hivi: ‘Nimemuomba kutoka kwa Yehova.’—1 Samweli 1:20.

8. (a) Ilikuwa mwepesi Hana atimize naziri yake? (b) Zaburi ya 61 inakukumbusha nini juu ya mufano muzuri wa Hana?

8 Wakati Samweli alikuwa na miaka tatu hivi, Hana alifanya kama vile tu alikuwa ameahidi Yehova. Alimupeleka Samweli kwa Kuhani Mukubwa Eli kwenye tabenakulo katika Shilo, na akasema hivi: ‘Ilikuwa kuhusu muvulana [mutoto mwanaume] huyu kwamba nilisali ili Yehova anipe ombi langu nililomuomba. Na mimi nimemuazima Yehova muvulana huyu.’ (1 Samweli 1:24-28) Kuanzia wakati huo, Samweli aliishi kwenye tabenakulo. Biblia inasema kama ‘yule muvulana Samweli akaendelea kukua [kukomaa] akiwa na Yehova.’ (1 Samweli 2:21) Haingekuwa mwepesi kwa Hana kutimiza naziri yake. Hilo lilimaanisha kuwa hangepitisha wakati kila siku pamoja na mutoto wake mwanaume mwenye alipenda sana. Hangeona namna alikuwa anakomaa. Lakini Hana alichukua kwa uzito naziri yenye alifanya kwa Yehova. Alikuwa tayari kujinyima mambo yenye yalikuwa ya maana kwake ili kutimiza ahadi yake kwa Mungu.​—1 Samweli 2:1, 2; soma Zaburi 61:1, 5, 8.

Unatimiza naziri zako kwa Yehova?

9. Tutazungumuzia sasa nini?

9 Kwa sababu tunaelewa kama kufanya naziri kwa Yehova ni jambo nzito sana, tuzungumuzie sasa maulizo haya: Ni naziri gani mbalimbali zenye tunaweza kufanya leo? Sababu gani tunapaswa kuazimia kutimiza naziri hizo?

NAZIRI YAKO YA KUJITOA KWA YEHOVA

Naziri ya kujitoa kwa Mungu (Picha hii inapatana na fungu la 10)

10. Ni naziri gani ya maana zaidi yenye Mukristo anaweza kufanya? Naziri hiyo inamaanisha nini?

10 Naziri ya maana zaidi yenye Mukristo anaweza kufanya ni ile ya kutoa maisha yake kwa Yehova. Katika sala ya pekee, mutu anaahidi kutumia maisha yake ili kumutumikia Mungu milele, hata kutokee nini. Yesu alisema kama ‘tunajikana’ wenyewe, ni kusema, tunaahidi kutia Yehova pa nafasi ya kwanza, hapana sisi wenyewe. (Mathayo 16:24) Kuanzia wakati huo, “sisi ni wa Yehova.” (Waroma 14:8) Tunachukua kwa uzito naziri yetu ya kujitoa kwa Yehova. Tunajisikia kama vile muandikaji mumoja wa zaburi mwenye aliandika hivi: ‘Nitamulipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu? Naziri zangu nitamutimizia Yehova, naam, mbele ya watu wake wote.’—Zaburi 116:12, 14.

11. Mambo yalikuwa namna gani siku yenye ulibatizwa?

11 Umetoa maisha yako kwa Yehova na kuonyesha jambo hilo kwa kubatizwa katika maji? Ikiwa umefanya hivyo, ni muzuri sana! Unakumbuka wakati ndugu mwenye alikuwa anatoa hotuba ya ubatizo aliuliza ikiwa umetoa maisha yako kwa Yehova na kuelewa kama “kujitoa kwako na ubatizo wako vinakutambulisha kuwa Shahidi wa Yehova”? Wakati ulijibu ndiyo, watu wote wenye kuwa hapo walijua kama ulikuwa umetoa maisha yako kwa Yehova na kama ulistahili kubatizwa na kuwa mutumishi wa Yehova mwenye kukubaliwa. Kwa kweli, ulimufurahisha sana Yehova!

12. (a) Tunapaswa kujiuliza maulizo gani? (b) Petro alitutia moyo tukomalishe sifa gani?

12 Wakati ulibatizwa, ulimuahidi Yehova kama utatumia maisha yako ili kumutumikia na kufanya yako yote ili kufuata kanuni zake. Lakini ubatizo ni mwanzo tu. Kadiri wakati unapita, sisi wote tunapaswa kuendelea kujichunguza. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Urafiki wangu pamoja na Yehova umekomaa kwa kiasi gani tangu nibatizwe? Ninaendelea kumutumikia kwa moyo wangu wote? (Wakolosai 3:23) Ninasali kwa ukawaida? Ninasoma Biblia kila siku? Ninakusanyika kwa ukawaida? Ninafanya yangu yote ili kufanya kazi ya kuhubiri kwa ukawaida? Ao nimepunguza bidii yangu kwa ajili ya mambo hayo?’ Mutume Petro alituonya kama kuko hatari ya kufikia kuwa watu wasiotenda katika utumishi wetu kwa Yehova. Tunaweza kuepuka jambo hilo ikiwa tunajikaza sana kukomalisha imani, ujuzi, uvumilivu, na ushikamanifu wetu kwa Mungu.​—Soma 2 Petro 1:5-8.

13. Mukristo mwenye kujitoa kwa Yehova na kubatizwa, anapaswa kujua nini?

13 Kisha kufanya naziri ya kumutumikia Yehova, hatuwezi tena kuibadilisha. Mutu mwenye anachoka kumutumikia Yehova ao kuishi maisha ya Mukristo hawezi kufikia kusema kama hakujitoa kabisa kwa Yehova ao ubatizo wake haukustahili. * (Soma maelezo ya chini.) Ikiwa mutu mwenye kujitoa kwa Yehova anafanya zambi nzito, atatoa hesabu kwa Yehova na kwa kutaniko. (Waroma 14:12) Hatupendi hata kidogo kuwa kama wale wenye Yesu aliambia maneno haya: ‘Mumeacha upendo muliokuwa nao mwanzoni.’ Lakini, tunapenda aseme maneno haya juu yetu: ‘Mimi ninajua matendo yako, na upendo wako na imani na huduma na uvumilivu wako, na kwamba matendo yako ya hivi karibuni yanazidi [yanapita] yale ya zamani.’ (Ufunuo 2:4, 19) Tunapenda kufurahisha Yehova kwa kufanya yetu yote ili kuishi kulingana na naziri yetu ya kumutumikia.

NAZIRI YAKO YA NDOA

Naziri ya ndoa (Picha hii inapatana na fungu la 14)

14. Ni naziri gani ya pili ya maana sana yenye mutu anaweza kufanya? Sababu gani?

14 Naziri ya pili ya maana sana yenye mutu anaweza kufanya ni naziri ya ndoa. Ndoa ni takatifu. Yehova anaona naziri ya ndoa kuwa jambo nzito sana. Wakati mwanaume na mwanamuke wanafanya naziri zao, wanatoa ahadi mbele ya Yehova na mbele ya watu wote wenye kuwasikiliza. Kwa ukawaida wanaahidi kupendana, kutunzana, na kuheshimiana kwa muda wote ambao wote wawili wataishi pamoja duniani kulingana na mupango wa ndoa wa Mungu. Pengine wengine hawatumie maneno hayohayo, lakini wao pia wanafanya naziri kwa Mungu. Wakati wanafanya naziri hizo wanakuwa bibi na bwana. Kulingana na kusudi la Mungu, ndoa ni kifungo cha maisha yote. (Mwanzo 2:24; 1 Wakorintho 7:39) Yesu alisema hivi: ‘Kile ambacho Mungu ameunganisha mutu yeyote asikitenganishe.’ Bibi na bwana wenye wanapenda kuoana hawapaswe kufikiri kuwa ikiwa mambo hayaendeke muzuri katika ndoa yao, wanaweza tu kuvunja ndoa.—Marko 10:9.

15. Sababu gani Wakristo hawapaswe kuwa na mawazo kama ya watu wa ulimwengu juu ya ndoa?

15 Kwa kweli, kwa sababu hakuna mwanadamu mukamilifu, hakuna ndoa yenye kukamilika. Ndiyo sababu Biblia inatuambia kama kila mutu mwenye kufunga ndoa ‘atakuwa na ziki [taabu]’ wakati fulani. (1 Wakorintho 7:28) Katika ulimwengu leo, watu wengi hawachukue ndoa kwa uzito. Wanafikiri kama ikiwa mambo hayaendeke muzuri wanaweza tu kuvunja ndoa yao. Lakini wanaume na wanawake Wakristo hawana mawazo hayo juu ya ndoa. Wanaelewa kwamba walifanya naziri yao ya ndoa mbele ya Mungu. Ikiwa wanavunja naziri hiyo, itakuwa kama vile wanamudanganya, na Mungu anachukia wasema uongo. (Mambo ya Walawi 19:12; Methali 6:16-19) Wakristo wenye kufunga ndoa wanapaswa kukumbuka maneno haya ya mutume Paulo: ‘Umefungwa kwa muke? Uache kutafuta kufunguliwa.’ (1 Wakorintho 7:27) Mutume Paulo alisema hivyo kwa sababu alijua kwamba Yehova anachukia pia watu wenye kutumia udanganyifu ili kuvunja ndoa yao.​—Malaki 2:13-16.

16. Biblia inasema nini juu ya kuvunja ndoa na kutengana?

16 Yesu alifundisha kuwa sababu moja yenye kuwa katika Maandiko ya kuvunja ndoa ni ikiwa bibi ao bwana anafanya uzinzi, na mwenzake mwenye hana kosa anaamua kuwa hatamusamehe. (Mathayo 19:9; Waebrania 13:4) Tuseme nini juu ya mutu kutengana na bibi ao bwana yake? Mawazo ya Biblia yako pia wazi juu ya jambo hilo. (Soma 1 Wakorintho 7:10, 11.) Hakuna sababu yenye kuwa katika Maandiko yenye kuruhusu bibi na bwana watengane. Lakini, wakati fulani kunaweza kuwa hali yenye inafanya Mukristo aone kama ni jambo la lazima kabisa atengane na bibi ao bwana yake. Kwa mufano, bibi ao bwana fulani anaweza kuona kama maisha ao urafiki wake pamoja na Yehova utakuwa katika hatari kabisa ikiwa anaendelea kuishi pamoja na bibi ao bwana mwenye kumutendea mubaya kimwili ao mwenye kuwa muasi-imani. * (Soma maelezo ya chini.)

17. Bibi na bwana Wakristo wanaweza kufanya nini ili ndoa yao iendelee?

17 Ikiwa bibi na bwana wanaomba wazee wa kutaniko mashauri juu ya namna ya kufanya ndoa yao ikuwe ya muzuri zaidi, wazee wanaweza kuwauliza ikiwa wameangalia video Upendo wa Kweli Ni Nini? na kujifunza broshua Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha. Video na broshua hiyo vinakazia kanuni za Biblia zenye zinaweza kusaidia ndoa ikuwe yenye nguvu zaidi. Bibi na bwana fulani walisema hivi: “Tangu wakati tulianza kujifunza broshua hiyo, ndoa yetu imekuwa yenye furaha zaidi kuliko wakati mwengine wowote.” Dada mwenye amekuwa katika ndoa kwa miaka 22 aliwaza kama ndoa yao ilikuwa karibu kuvunjika. Kisha, akaangalia video hiyo. Alisema hivi: “Sisi wawili tumebatizwa, lakini tulikuwa na mawazo yenye kutofautiana juu ya maisha. Video hiyo ilitolewa kwa wakati wenye kufaa kabisa! Sasa ndoa yetu ni yenye furaha zaidi.” Kwa kweli, ikiwa bibi na bwana wanatumikisha kanuni za Yehova katika ndoa yao, uhusiano wao utakuwa wenye furaha zaidi na wenye nguvu zaidi.

NAZIRI YA WATUMISHI WA PEKEE WA WAKATI WOTE

18, 19. (a) Wazazi wengi Wakristo wamefanya nini? (b) Wale wenye kuwa katika utumishi wa pekee wa wakati wote wanafanya naziri gani?

18 Mwanzoni tulizungumuzia naziri zenye Yeftha na Hana walifanya. Kwa sababu ya naziri hizo, binti ya Yeftha na mutoto mwanaume wa Hana walitumia maisha yao ili kumutumikia Yehova katika njia za pekee. Wazazi wengi Wakristo wametia moyo watoto wao waanze utumishi wa wakati wote na wakaze akili yao juu ya utumishi wao kwa Mungu katika maisha yao. Na sisi wote tunaweza kufanya jambo fulani ili kutia moyo vijana hao waendelee katika utumishi wao.​—Waamuzi 11:40; Zaburi 110:3.

Naziri ya utumishi wa pekee wa wakati wote (Picha hii inapatana na fungu la 19)

19 Leo, kuko karibu ndugu na dada 67000 wenye kuwa katika Kikundi cha Ulimwenguni Pote cha Watumishi wa Pekee wa Wakati Wote cha Mashahidi wa Yehova. Wamoja wanatumika kwenye Beteli ao katika kazi ya ujenzi ao katika kazi ya muzunguko. Wengine wanatumika katika kazi ya kufundisha kwenye masomo mbalimbali ya kiteokrasi yenye kufanywa inje ya Beteli, wengine ni mapainia wa pekee, wamisionere, wengine wanatunza Majumba ya Mikusanyiko ao majengo ya masomo ya Biblia. Kila mumoja wao amefanya naziri ya “Utii na Umasikini.” Katika naziri hiyo, wanaahidi kutumika kwa bidii katika kila mugawo wenye wanapewa katika utumishi wa Yehova, kuishi maisha mepesi, na kuwa hawatafanya kazi ya kimwili bila ruhusa. Ndugu na dada hao hawako wa pekee lakini migawo yao ndiyo inaonwa kuwa ya pekee. Ni wanyenyekevu na wanaazimia kutimiza naziri yao kwa muda wote wenye wanaendelea kuwa katika utumishi wa pekee wa wakati wote.

20. Namna gani tunapaswa kuona naziri zenye tumefanya kwa Mungu? Sababu gani?

20 Katika habari hii, tumezungumuzia naziri tatu zenye tunaweza kufanya kwa Mungu. Pengine umefanya naziri fulani kati ya naziri hizo. Tunajua kwamba tunapaswa kuchukua naziri zetu kwa uzito na kwamba tunapaswa kufanya yetu yote ili kutimiza naziri zetu. (Methali 20:25) Ikiwa hatutimize naziri zetu kwa Yehova, tunaweza kupatwa na matokeo ya mubaya sana. (Mhubiri 5:6) Kwa hiyo tukuwe kama muandikaji mumoja wa zaburi mwenye aliambia Yehova hivi: ‘Jina lako nitalipigia muziki milele, ili nipate kutimiza naziri zangu siku baada ya siku.’— Zaburi 61:8.

^ fu. 7 Hana alimuahidi Yehova kama ikiwa angezaa mutoto mwanaume, mutoto huyo angekuwa Munaziri maisha yake yote. Hilo lilimaanisha kama mutoto wake mwanaume angetolewa kwa Mungu na kutiwa pembeni kwa ajili ya kazi ya Yehova.—Hesabu 6:2, 5, 8.

^ fu. 13 Kwa sababu kuko mambo mengi yenye wazee wanapaswa kuchunguza pamoja na mutu mbele ya kukubali ikiwa anastahili kubatizwa, kusema kama ubatizo wa mutu fulani haukustahili kunapaswa kutokea mara chache sana.

^ fu. 16 Soma kitabu Mubaki Katika “Upendo wa Mungu,” ukurasa wa219-221.