Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia “Wakaaji Wageni” ‘Wamtumikie Yehova kwa Kushangilia’

Kuwasaidia “Wakaaji Wageni” ‘Wamtumikie Yehova kwa Kushangilia’

“Yehova anawalinda wakaaji wageni.”—ZAB. 146:9.

NYIMBO: 84, 73

1, 2. (a) Baadhi ya ndugu na dada zetu wanakabili majaribu gani? (b) Ni maswali gani yanayozuka?

“VITA vya wenyewe kwa wenyewe vilipoanza nchini Burundi, familia yetu ilikuwa kusanyikoni,” anasema ndugu mmoja anayeitwa Lije. “Tuliona watu wakikimbia na kufyatua risasi. Wazazi wetu na sote watoto 11 tulikimbia ili kuokoa maisha yetu tukiwa tumebeba vitu vichache sana. Hatimaye, baadhi ya watu wa familia yetu walifika katika kambi ya wakimbizi nchini Malawi, mwendo wa kilomita zaidi ya 1,600. Sisi wengine tulitawanyika.”

2 Ulimwenguni pote, wakimbizi ambao wametoroka nyumbani kwao kwa sababu ya vita au mnyanyaso wamefikia zaidi ya 65,000,000, ambayo ndiyo idadi kubwa zaidi iliyowahi kurekodiwa. * Miongoni mwao ni maelfu ya Mashahidi wa Yehova. Wengi wao wamepoteza wapendwa wao na karibu mali zao zote. Baadhi yao wamekabili changamoto gani nyingine? Tunaweza kuwasaidiaje ndugu na dada hao “[wamtumikie] Yehova kwa kushangilia” licha ya majaribu wanayokabili? (Zab. 100:2) Na tunaweza kufaulu jinsi gani kuwahubiria habari njema wakimbizi ambao hawamjui Yehova?

MAISHA YA MKIMBIZI

3. Yesu na wengi wa wanafunzi wake walikuwa wakimbizi jinsi gani?

3 Baada ya malaika wa Yehova kumwonya Yosefu kwamba Mfalme Herode alitaka kumwua Yesu, Yesu mchanga na wazazi wake wakawa wakimbizi nchini Misri. Walibaki huko hadi Herode alipokufa. (Mt. 2:13, 14, 19-21) Miaka mingi baadaye, wanafunzi wa mapema wa Yesu “walitawanywa kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria” kwa sababu ya mnyanyaso. (Mdo. 8:1) Yesu alikuwa ametabiri kwamba wengi wa wafuasi wake wangefukuzwa kutoka makwao. Alisema hivi: “Wakati wanapowatesa ninyi katika jiji moja, kimbilieni jiji lingine.” (Mt. 10:23) Maisha ya mkimbizi si rahisi, haidhuru amekimbia kwa sababu gani.

4, 5. Wakimbizi hukabili hatari gani (a) wanapokuwa njiani wakikimbia? (b) wanapoishi kambini?

4 Wakimbizi wanaweza kukabili hatari wanapokimbia au wanapoishi katika kambi ya wakimbizi. Gad, ndugu mdogo wa Lije, anasema hivi: “Tulitembea kwa majuma mengi, tukipita miili ya watu wengi waliokufa. Nilikuwa na umri wa miaka 12. Miguu yangu ilikuwa imevimba sana hivi kwamba niliiambia familia yetu iniache. Kwa kuwa baba hangekubali kuniacha mikononi mwa wapiganaji waasi, alinibeba. Tulishughulikia mahangaiko yetu siku moja baada ya nyingine, tukisali kwa Yehova na kumtumaini, na nyakati nyingine tulikula tu maembe yaliyokua njiani.”—Flp. 4:12, 13.

5 Wengi wa watu wa familia ya Lije waliishi kwa miaka mingi katika kambi za wakimbizi za Umoja wa Mataifa. Hata hivyo, bado hawakuwa salama. Lije, ambaye sasa ni mwangalizi wa mzunguko, anasema hivi: “Watu wengi hawakuwa na kazi. Walipiga porojo, walilewa, walicheza kamari, waliiba, na walikuwa na maadili mapotovu.” Ili kupinga uvutano huo mbaya, Mashahidi waliokuwa kambini walihitaji kushiriki kikamili katika utendaji wa kutaniko. (Ebr. 6: 11, 12; 10:24, 25) Ili kudumisha hali nzuri ya kiroho, walitumia wakati wao vizuri, wengi wao wakiwa mapainia. Walidumisha mtazamo mzuri kwa kukumbuka kwamba, kama Waisraeli ambao walivuka nyika, siku moja wangeondoka kambini.—2 Kor. 4:18.

KUWAONYESHA UPENDO WAKIMBIZI

6, 7. (a) “Kumpenda Mungu” kunawachocheaje Wakristo kuwasaidia ndugu walio na uhitaji? (b) Toa mfano.

6 “Kumpenda Mungu” hutuchochea tuonyeshane upendo, hasa tunapokabili hali ngumu. (Soma 1 Yohana 3:17, 18.) Wakristo wa Yudea katika karne ya kwanza walipokabili tishio la njaa, kutaniko lilipanga ili wapate msaada. (Mdo. 11:28, 29) Pia, mtume Paulo na Petro waliwahimiza Wakristo waonyeshane ukarimu. (Rom. 12:13; 1 Pet. 4:9) Ikiwa Wakristo wanapaswa kuwakaribisha ndugu wanaozuru, je, hawapaswi kufanya hivyo hata zaidi kwa waamini wenzao ambao maisha yao yamo hatarini au ambao wanateswa kwa sababu ya imani yao?—Soma Methali 3:27. *

7 Muda fulani uliopita, maelfu ya Mashahidi wa Yehova waliotia ndani wanaume, wanawake, na watoto walilazimika kukimbia kutoka mashariki mwa Ukrainia kwa sababu ya vita na mateso. Kwa kusikitisha, baadhi yao waliuawa. Lakini wengi walikaribishwa na ndugu zao wa kiroho walioishi sehemu tofauti-tofauti nchini Ukrainia, na wengine wengi walipewa makao na Mashahidi wenzao nchini Urusi. Katika nchi zote mbili, Mashahidi wanaendelea kudumisha msimamo wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa, kwa “[kutokuwa] sehemu ya ulimwengu,” na wanaendelea kwa bidii ‘kutangaza habari njema ya lile neno.’—Yoh. 15:19; Mdo. 8:4.

KUWASAIDIA WAKIMBIZI WAIMARISHE IMANI YAO

8, 9. (a) Wakimbizi wanaweza kukabili changamoto gani katika nchi ya kigeni? (b) Kwa nini tunahitaji kuwasaidia kwa subira?

8 Baadhi ya watu hukimbia makwao na kwenda sehemu nyingine katika nchi yao ilhali wengine wengi hujikuta katika mazingira mapya kabisa katika nchi nyingine. Huenda serikali zikawapa chakula, mavazi, au makao, lakini wanaweza kukosa vyakula walivyozoea. Wakimbizi wanaotoka kwenye nchi zenye joto wanaweza kukabili kwa mara ya kwanza hali ya hewa ya baridi na huenda wasijue wavae mavazi ya aina gani. Ikiwa wametoka katika eneo la vijijini, huenda wasifahamu jinsi ya kutumia vyombo vya kisasa vya nyumbani.

9 Baadhi ya serikali huwa na programu za kuwasaidia wakimbizi wazoee hali yao mpya. Hata hivyo, mara nyingi baada ya miezi kadhaa, wakimbizi hutarajiwa wajitegemeze. Badiliko hilo linaweza kuwalemea. Hebu wazia ukijitahidi kwa wakati uleule kujifunza lugha mpya, kujua sheria mpya, na mambo unayotarajiwa kufanya inapohusu kujiendesha, kufuata wakati, kulipa kodi, kulipia gharama mbalimbali, kwenda shule, na kumtia mtoto nidhamu! Je, unaweza kuwasaidia kwa subira na heshima ndugu na dada wanaokabili changamoto kama hizo?—Flp. 2:3, 4.

10. Tunaweza kuimarishaje imani ya wakimbizi wanaowasili katika nchi zetu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

10 Kwa kuongezea, nyakati nyingine wenye mamlaka wamefanya iwe vigumu kwa ndugu zetu wakimbizi kuwasiliana na kutaniko. Baadhi ya mashirika yametishia kuacha kuwasaidia au kuwanyima ndugu zetu mahali pa kuishi ikiwa wanakataa kukubali kazi ambayo itawafanya wakose mikutano. Kwa sababu ya woga na uhitaji walio nao, baadhi ya akina ndugu wamekubali kazi hizo. Hivyo, ni muhimu kukutana na ndugu zetu wakimbizi mara tu wanapowasili nchini mwetu. Wanahitaji kuona kwamba tunawajali. Tunaweza kuimarisha imani yao tunapowajali na kuwasaidia.—Met. 12:25; 17:17.

NJIA MBALIMBALI ZA KUWASAIDIA WAKIMBIZI

11. (a) Mwanzoni wakimbizi huhitaji nini? (b) Wakimbizi wanaweza kuonyeshaje uthamini?

11 Mwanzoni, huenda tukahitaji kuwapa ndugu zetu chakula, mavazi, au mahitaji mengine ya msingi. * Hata mambo madogo kama kumpa ndugu tai, yanaweza kumgusa moyo sana. Kwa upande mwingine, wakimbizi wanapoonyesha uthamini bila kudai chochote, wanawasaidia wenyeji wao kupata furaha inayotokana na kutoa. Ni kweli kwamba wakimbizi wanapoishi kwa kutegemea ukarimu wa wengine huenda wakakosa kujiheshimu na uhusiano wao pamoja na ndugu wengine ukaharibika. (2 The. 3:7-10) Lakini wanahitaji msaada.

Tunaweza kuwasaidiaje ndugu na dada zetu ambao ni wakimbizi? (Tazama fungu la 11-13)

12, 13. (a) Tunaweza kuwasaidia wakimbizi katika njia zipi? (b) Toa mfano.

12 Si lazima utumie pesa nyingi ili uwasaidie wakimbizi, kwa kuwa jambo lenye thamani hata zaidi ni kutumia muda wetu pamoja nao na kuwahangaikia. Huenda ukafanya mambo rahisi kama vile kuwaonyesha jinsi ya kutumia usafiri wa umma, kununua vyakula vya bei nafuu na vyenye lishe, au kupata vifaa kama vile cherehani au mashine ya kukata nyasi ili waweze kujitegemeza. Jambo muhimu hata zaidi, unaweza kuwasaidia washirikiane kikamili na kutaniko lao jipya. Ikiwezekana, unaweza kuwasafirisha kwenda mikutanoni. Pia, waonyeshe njia wanazoweza kutumia kuwafikia watu na ujumbe wa Ufalme katika eneo lenu. Ambatana na ndugu na dada hao katika huduma.

13 Wakimbizi wanne matineja walipowasili katika kutaniko fulani, baadhi ya wazee waliwafundisha kuendesha gari, kupiga chapa, kuandika wasifu wa kazi, na vilevile kuwa na ratiba nzuri ili wamtumikie Yehova kikamili. (Gal. 6:10) Muda si muda, wote wanne wakawa mapainia. Mwongozo huo, na vilevile jitihada zao binafsi za kufuatia miradi ya kiroho, ziliwasaidia kunawiri na kuepuka kumezwa na mfumo wa Shetani.

14. (a) Wakimbizi wanahitaji kupinga kishawishi gani? (b) Toa mfano.

14 Kama Wakristo wengine wote, wakimbizi wanahitaji kupinga kishawishi na mkazo unaoweza kuharibu uhusiano wao na Yehova kwa kutafuta vitu vya kimwili. * Lije, aliyetajwa mwanzoni, pamoja na ndugu zake, wanakumbuka mambo ambayo baba yao aliwafundisha kuhusu imani hata walipokuwa njiani wakiwa wakimbizi. “Alitupa vitu ambavyo hatukuvihitaji, kimoja baada ya kingine. Mwishowe, aliinua mfuko mtupu na kusema hivi kwa tabasamu: ‘Mnaona? Huu tu ndio mnaohitaji!’”—Soma 1 Timotheo 6:8.

KUTIMIZA MAHITAJI MUHIMU ZAIDI YA WAKIMBIZI

15, 16. Tunaweza kuwategemezaje wakimbizi (a) kiroho? (b) kihisia?

15 Zaidi ya msaada wa kimwili, wakimbizi wanahitaji utegemezo wa kiroho na wa kihisia. (Mt. 4:4) Wazee wanaweza kuwasaidia kwa kuagiza machapisho katika lugha ya wakimbizi na kuwasaidia kuwasiliana na ndugu wanaozungumza lugha yao. Wakimbizi wengi wametenganishwa na familia, jamii, na makutaniko yao waliyokuwa na uhusiano wa karibu nayo. Wanahitaji kuhisi upendo wa Yehova na kuonyeshwa na Wakristo wenzao kwamba wanawajali. Tusipofanya hivyo, huenda wakavutwa na watu wa familia wasioamini au watu kutoka nchi zao ambao wanaweza kuelewa njia yao ya maisha na mambo waliyokabili. (1 Kor. 15:33) Tunapowafanya wajihisi kuwa sehemu ya kutaniko kikamili, tutakuwa na pendeleo la kushiriki pamoja na Yehova katika ‘kuwalinda wakaaji wageni.’—Zab. 146:9.

16 Kama ilivyokuwa kwa Yesu mchanga na familia yao, huenda wakimbizi wasiweze kurudi katika nchi zao ikiwa wanaowakandamiza wataendelea kutawala. Zaidi ya hilo, kama Lije anavyosema, “wazazi wengi ambao walishuhudia washiriki wa familia zao wakinajisiwa au kuuawa hawawezi kuwarudisha watoto wao katika sehemu ambazo mambo hayo yalitukia.” Ili kuwasaidia wale ambao wamekabili mambo hayo yenye kuhuzunisha, ndugu walio katika nchi ambazo wakimbizi wamekimbilia wanahitaji kuwa na ‘hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, huruma nyororo, na unyenyekevu.’ (1 Pet. 3:8) Baadhi ya wakimbizi wamejitenga na wengine kwa sababu ya mateso waliyopitia na huenda wakaona aibu kuzungumzia matatizo yao hasa wanapokuwa na watoto wao. Jiulize hivi: ‘Ikiwa ningekuwa katika hali yao, ningependa kutendewa jinsi gani?’—Mt. 7:12.

KUWAHUBIRIA WAKIMBIZI AMBAO SI MASHAHIDI

17. Ni kwa njia gani wakimbizi hupata kitulizo tunapowahubiria?

17 Leo, wakimbizi wengi hutoka katika nchi ambazo kazi yetu ya kuhubiri imezuiwa. Jambo la kupendeza ni kwamba kupitia Mashahidi wenye bidii katika nchi ambazo wakimbizi wamekimbilia, maelfu ya wakimbizi wanasikia “neno la Ufalme” kwa mara ya kwanza. (Mt. 13:19, 23) Wengi ambao ‘wamelemewa na mizigo’ wanapata burudisho la kiroho katika mikutano yetu na kutambua haraka kwamba ‘kwa kweli Mungu yupo katikati yetu.’— Mt. 11:28-30; 1 Kor. 14:25.

18, 19. Tunaweza kuonyeshaje hekima tunapowahubiria wakimbizi?

18 Wale wanaowahubiria wakimbizi wanahitaji kuwa wenye “kujihadhari” na hata kuwa ‘werevu.’ (Mt. 10:16; Met. 22:3) Sikiliza kwa subira mahangaiko yao, lakini usizungumzie siasa. Fuata miongozo kutoka ofisi ya tawi na kutoka kwa wenye mamlaka. Kamwe usihatarishe maisha yako wala ya watu wengine. Jifunze na uheshimu dini na utamaduni wao. Kwa mfano, watu kutoka nchi fulani huwa na hisia kali kuhusu nguo zinazowafaa wanawake. Hivyo, unapowahubiria wakimbizi valia katika njia ambayo haitawakwaza wengine.

19 Kama Msamaria mwema katika mfano wa Yesu, tunataka kuwasaidia watu wanaoteseka kutia ndani wale ambao si Mashahidi. (Luka 10:33-37) Njia bora zaidi ya kufanya hivyo ni kwa kuwahubiria habari njema. Mzee fulani ambaye amewasaidia wakimbizi wengi anasema hivi: “Ni muhimu kueleza wazi papo hapo kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova na kwamba lengo letu kuu ni kuwasaidia kiroho wala si kimwili. Tusipofanya hivyo, huenda baadhi yao wakashirikiana nasi kwa sababu tu ya faida za kibinafsi.”

MATOKEO YANAYOLETA SHANGWE

20, 21. (a) Tunapata matokeo gani mazuri tunapowaonyesha wakimbizi upendo wa Kikristo? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Kuwaonyesha upendo wa Kikristo “wakaaji wageni” huleta matokeo mazuri. Dada mmoja Mkristo anaeleza kwamba yeye na familia yake walitoroka mateso nchini Eritrea. Baada ya safari yenye kuchosha ya siku nane wakipita jangwani, watoto wake wanne walifika nchini Sudan. Anasema hivi: “Ndugu waliwatendea kama watu wa karibu wa familia wakiwapatia chakula, mavazi, makao, na usafiri. Ni nani wengine wangeweza kuwakaribisha watu wasiowajua katika nyumba zao kwa sababu tu wanaabudu Mungu yuleyule? Ni Mashahidi wa Yehova pekee!”—Soma Yohana 13:35.

21 Namna gani kuhusu watoto wengi wanaowasili pamoja na wazazi wao iwe ni wakimbizi au wahamiaji wengine? Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi sisi sote tunavyoweza kuwasaidia wamtumikie Yehova kwa shangwe.

^ fu. 2 Katika makala hii, tutatumia neno “wakimbizi” kurejelea wale ambao wamekimbia kutoka sehemu moja katika nchi yao kwenda nyingine au kwenda nchi nyingine, iwe ni kwa sababu ya vita, mnyanyaso, au majanga. Kulingana na Tume ya Umoja wa Mataifa Inayoshughulikia Wakimbizi (UNHCR), leo “mtu 1 kati ya watu 113” ulimwenguni pote “amelazimishwa kukimbia kutoka mahali anapoishi.”

^ fu. 6 Tazama makala “Msisahau Ukaribishaji-Wageni” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 2016, uku. 8-12.

^ fu. 11 Baada tu ya mkimbizi kufika eneo la kigeni, wazee wanapaswa kufuata mwongozo unaopatikana katika kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, sura ya 8, fungu la 30. Wazee wanaweza kuwasiliana na makutaniko katika nchi nyingine kwa kutuma barua kwenye ofisi yao ya tawi kupitia jw.org. Wakati huohuo, wanaweza kumwuliza mkimbizi huyo maswali kwa busara kuhusu huduma na kutaniko ambalo ametoka ili kujua hali yake ya kiroho.

^ fu. 14 Tazama makala “Hakuna Anayeweza Kuwatumikia Mabwana Wawili” na “Uwe Hodari Yehova Ni Msaidizi Wako!” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 2014, uku. 17-26.