Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tusaidie “Wakaaji Wageni” ili ‘Wamutumikie Yehova kwa Furaha’

Tusaidie “Wakaaji Wageni” ili ‘Wamutumikie Yehova kwa Furaha’

“Yehova anawalinda wakaaji wageni.”—ZABURI 146:9.

NYIMBO: 84, 73

1, 2. (a) Ndugu na dada zetu fulani wanapata magumu gani? (b) Tunaweza kujiuliza maulizo gani?

NDUGU mumoja mwenye kuitwa Lije anasema hivi: “Wakati mauaji makubwa yalianza katika Burundi, mimi na watu wa familia yangu tulikuwa kwenye mukusanyiko. Tulikuwa tunaona namna watu walikuwa wanakimbia, na kupiga risasi. Wazazi wangu na sisi watoto 11 tulikimbia tu na vitu vidogo ili kuokoa uzima wetu. Mwishowe watu fulani wa familia yetu walifika katika kambi ya wakimbizi katika Malawi, walifanya safari ya kilometre 1600 ili kufika huko. Sisi wengine tulitawanyika.”

2 Katika dunia yote, kuko zaidi ya wakimbizi milioni 65 wenye wamelazimika kuacha makao yao kwa sababu ya vita ao mateso. Hiyo ndiyo hesabu kubwa zaidi ya wakimbizi yenye imekwisha kutolewa. * (Soma maelezo ya chini.) Maelfu kati ya wakimbizi hao ni Mashahidi wa Yehova. Wengi wamepoteza wapendwa wao na karibu vitu vyote vyenye walikuwa navyo. Ni magumu gani mengine yenye wamepata? Namna gani tunaweza kusaidia ndugu na dada zetu wamutumikie Yehova na kuendelea kuwa na furaha wakati wanapatwa na magumu kama hayo? (Zaburi 100:2) Na ni njia gani ya muzuri zaidi yenye tunaweza kutumia ili kuhubiria wakimbizi wenye hawajamujua Yehova?

MAISHA YA MUKIMBIZI

3. Namna gani Yesu na wengi kati ya wanafunzi wake walifikia kuwa wakimbizi?

3 Kisha malaika wa Yehova kuonya Yosefu kuwa Mufalme Herode alitaka kumuua Yesu, Yesu na wazazi wake walikimbilia Misri. Walibakia Misri mupaka wakati Herode alikufa. (Mathayo 2:13, 14, 19-21) Kisha kupita miaka mingi, wanafunzi wa Yesu “walitawanywa kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria” kwa sababu ya mateso. (Matendo 8:1) Yesu alijua kama wengi kati ya wanafunzi wake wangelazimika kuacha makao yao. Alisema hivi: ‘Wanapowatesa ninyi katika jiji moja, mukimbilie jiji lingine.’ (Mathayo 10:23) Hata ikuwe ni kwa sababu gani, kukimbia makao yetu haiko vyepesi hata kidogo.

4, 5. Wakimbizi wanapatwa na hatari gani wakati (a) wako wanakimbia makao yao? (b) wanaishi katika kambi?

4 Wakimbizi wengi wanapambana na hatari mbalimbali wakati wanakimbia makao yao ao wakati wanaishi katika kambi ya wakimbizi. Gad, mudogo wa Lije, anasema hivi: “Tulitembea kwa majuma mengi, na tulikuwa tunatambuka mamia ya watu wenye kufa. Nilikuwa na miaka 12. Miguu yangu ilivimba sana; kwa hiyo, niliambia watu wa familia yangu waniache. Baba yangu hakupenda kuniacha nafasi kwenye kulikuwa maaskari waasi, kwa hiyo alinibeba. Hatukuhangaikia mambo ya kesho, tulisali na kumutumainia Yehova, na wakati fulani tulikuwa tunakula tu hembe zenye zilikuwa zinakomaa pembeni ya barabara.”—Wafilipi 4:12, 13.

5 Watu wengi wa familia ya Lije walifanya miaka mingi katika kambi za wakimbizi za Umoja wa Mataifa. Lakini, kulikuwa pia hatari katika kambi hizo. Lije, ambaye sasa ni mwangalizi wa muzunguko, anafasiria hivi: “Watu wengi hawakukuwa na kazi. Walikuwa wanasema-sema wengine mubaya, wanalewa, wanacheza michezo ya feza, na walikuwa na mwenendo muchafu.” Ili kuepuka kuchochewa na mwenendo mubaya wa wengine, Mashahidi walipaswa kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kutaniko. (Waebrania 6:11, 12; 10:24, 25) Walitumia wakati wao kwa hekima ili waendelee kuwa wenye nguvu kiroho, na wengi walianza kufanya kazi ya upainia. Waliendelea kukumbuka kuwa mwishowe wao pia wangetoka katika kambi ya wakimbizi kama vile Waisraeli walifikia kutoka katika jangwa. Hilo liliwasaidia waendelee kuwa na mawazo ya muzuri.​—2 Wakorintho 4:18.

ONYESHA WAKIMBIZI UPENDO

6, 7. (a) Kumupenda Yehova kunatuchochea kutendea ndugu na dada zetu namna gani? (b) Toa mufano.

6 ‘Kumupenda Mungu’ kunatuchochea kuonyesha ndugu na dada zetu upendo, zaidi sana wakati wako katika magumu. (Soma 1 Yohana 3:17, 18.) Kwa mufano, wakati Wakristo wa kwanza-kwanza katika Yudea walikuwa na lazima ya chakula kwa sababu ya njaa, kutaniko lilifanya mipango ili kuwasaidia. (Matendo 11:28, 29) Mutume Paulo na Petro walitia pia moyo Wakristo waonyeshane ukaribishaji-wageni. (Waroma 12:13; 1 Petro 4:9) Kwa sababu Wakristo wanatiwa moyo kuonyesha wema ndugu na dada zao wenye kutoka mahali pengine, tunapaswa kabisa kuonyesha wema ndugu na dada zetu wenye kuwa katika hatari ao wenye wameteswa kwa sababu ya imani yao!—Soma Methali 3:27. *—Soma maelezo ya chini.

7 Hivi karibuni, maelfu ya Mashahidi wa Yehova walilazimika kuacha makao yao kwa sababu ya vita na mateso katika mashariki mwa Ukrania. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wamoja kati yao waliuawa. Lakini, ndugu na dada wengi wenye walikimbia makao yao, walikaribishwa katika nyumba za ndugu na dada wenye kuwa katika sehemu zingine za Ukrania na katika Urusi. Katika inchi hizo mbili, ndugu na dada hawakujiingiza katika mambo ya vita, hawakukuwa “sehemu ya ulimwengu,” na waliendelea kuhubiri kwa bidii “habari njema ya lile neno.”—Yohana 15:19; Matendo 8:4.

UWASAIDIE WAKIMBIZI KUTIA NGUVU IMANI YAO

8, 9. (a) Wakimbizi wanaweza kupambana na magumu gani katika inchi ingine? (b) Sababu gani wako na lazima tuwasaidie kwa uvumilivu?

8 Wakimbizi fulani wanalazimika kuishi katika sehemu ingine ya inchi yao. Lakini, wengine wengi wanapaswa kukimbilia katika inchi ingine yenye hawazoee. Ni kweli kwamba serikali zinaweza kutolea wakimbizi chakula, manguo na mahali pa kuishi, lakini kungali magumu. Kwa mufano, chakula kinaweza kuwa tofauti sana na chakula chenye walizoea. Wakimbizi fulani wenye kutoka katika inchi zenye joto, pengine hawajue namna ya kuvaa wakati wa baridi. Wengine wanaweza kuwa na lazima ya kujifunza namna ya kutumikisha vyombo vya sasa vya nyumbani vyenye kutumia umeme.

9 Serikali fulani zinafanya mipango ili kusaidia wakimbizi wazoee maisha katika inchi ingine. Lakini mara nyingi, kisha miezi fulani, wakimbizi wanaombwa kujihangaikia wao wenyewe. Inaweza kuwa vigumu sana kufanya hivyo. Fikiria mambo yenye wanaombwa kujifunza mara moja: luga mupya, desturi za mupya, na sheria za mupya zenye kuhusu mambo kama vile kulipia vitu fulani vyenye wametumia, kwa mufano maji na moto, kulipa kodi (taxe), kuenda kwenye masomo, na hata namna ya kupatia watoto nizamu! Unaweza kusaidia kwa uvumilivu na heshima ndugu na dada zetu wenye kuwa wakimbizi na wenye kupambana na magumu kama hayo?—Wafilipi 2:3, 4.

10. Namna gani tunaweza kutia nguvu imani ya wakimbizi wakati wanafika? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

10 Wakati fulani wakubwa wanafanya ikuwe vigumu kwa ndugu na dada zetu wakimbizi kukutana na ndugu na dada wa kutaniko la eneo kwenye wanaishi. Mashirika fulani ya serikali yanaogopesha ndugu na dada zetu kuwa yataacha kuwasaidia. Watu wa mashirika hayo wanaweza kuwaambia kama watawafukuza katika inchi hiyo ikiwa hawakubali kazi yenye inawazuia kuenda kwenye mikutano. Kwa sababu ya kuogopa na kuona kuwa hakuna mutu wa kuwasaidia, wamoja wamekubali kazi hizo. Kwa hiyo, inaomba kutenda haraka ili kukutana na ndugu na dada zetu wenye kuwa wakimbizi kisha tu wao kufika. Wanapaswa kuona kuwa tunawahangaikia. Ikiwa tunawahangaikia hivyo na kuwatolea musaada wenye kufaa, hilo linaweza kutia nguvu imani yao.​—Methali 12:25; 17:17.

TOLEA WAKIMBIZI MUSAADA WENYE KUFAA

11. (a) Wakimbizi wako na lazima ya nini kwanza? (b) Namna gani wakimbizi wanaweza kuonyesha shukrani?

11 Mwanzoni, inaweza kuwa lazima kupatia ndugu na dada zetu chakula, manguo, ao mambo mengine ya lazima. * (Soma maelezo ya chini.) Hata kupatia ndugu fulani zawadi ndogo kama vile kravate, inaweza kumufurahisha sana. Kwa kweli, wakimbizi hawataomba wafanyiwe mambo mengi, lakini wataonyesha kuwa ni wenye shukrani kwa ajili ya mambo yenye wengine wanawafanyia. Hilo litaletea furaha ndugu na dada wenye kuwatolea musaada. Lakini, ni jambo la maana kwa wakimbizi wafikie kujikaza kujitimizia wao wenyewe mambo ya lazima. Kufanya hivyo, kutawasaidia waendelee kuheshimiwa na kuwa na urafiki wa muzuri pamoja na ndugu na dada zao. (2 Wathesalonike 3:7-10) Hata hivyo, wakimbizi wangali na lazima ya musaada wetu.

Namna gani tunaweza kusaidia ndugu na dada zetu wenye kuwa wakimbizi? (Picha hii inapatana na fungu la 11-13)

12, 13. (a) Namna gani tunaweza kutolea wakimbizi musaada wenye kufaa? (b) Toa mufano.

12 Ili kusaidia wakimbizi, hatuna lazima ya kuwa na feza nyingi. Jambo lenye wako nalo lazima sana ni upendo wetu na wakati wetu. Kwa mufano, unaweza kuwaonyesha namna ya kutumia vyombo vya kusafirisha watu wengi kama vile motokari, ao namna ya kuuza chakula chenye kujenga mwili lakini cha bei chini. Unaweza pia kuwaonyesha namna ya kupata vyombo kama vile mashini ya kushona ao vyombo vingine vya kazi ili wavitumie juu ya kupata feza za kuwasaidia kujitimizia mambo yao ya lazima. Na zaidi sana, unaweza kuwasaidia wazoee kutaniko lao mupya. Ikiwa inawezekana, uwasaidie wapate namna ya kufika kwenye mikutano. Unaweza pia kuwaelezea njia ya muzuri zaidi ya kuhubiria watu katika eneo lenu, na unaweza kutumika nao katika kazi ya kuhubiri.

13 Wakati vijana ine wanaume wakimbizi walifika katika kutaniko moja, wazee mbalimbali waliwatolea musaada wenye kufaa. Waliwafundisha namna ya kutembeza motokari, namna ya kuandika barua kwa kutumia mashini, na namna ya kuandika barua ya kuomba kazi. Waliwaonyesha pia namna ya kupanga wakati wao ili watie kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza. (Wagalatia 6:10) Kisha muda mufupi, vijana hao ine wakakuwa mapainia. Kwa sababu ya musaada wa wazee na bidii yao wenyewe ya kujiwekea miradi katika kazi ya Yehova, walifanya maendeleo ya kiroho na waliepuka kujiingiza katika mambo ya ulimwengu wa Shetani.

14. (a) Sababu gani wakimbizi wanapaswa kuendelea kutia urafiki wao pamoja na Yehova pa nafasi ya kwanza? (b) Toa mufano.

14 Kama vile Wakristo wengine wote, wakimbizi wanapaswa kupinga majaribu na mikazo ya kutia vitu vya kimwili pa nafasi ya kwanza kuliko urafiki wao pamoja na Yehova. * (Soma maelezo ya chini.) Lije, mwenye tumekwisha kuzungumuzia, na ndugu na dada zake wanakumbuka namna baba yao alikuwa anawafundisha mambo ya maana juu ya imani wakati walikuwa wanakimbia. Wanasema hivi: “Hatua kwa hatua alitupa vitu vyenye havikukuwa vya lazima vyenye tulikuwa tunabeba. Mwishowe, aliinua sakoshi yenye haikukuwa na kitu na alisema hivi kwa furaha: ‘Munaona? Hatuna lazima ya vitu hivyo vyote!’”—Soma 1 Timotheo 6:8.

KUTIMIZIA WAKIMBIZI MAMBO YA LAZIMA ZAIDI

15, 16. (a) Namna gani tunaweza kutia nguvu imani ya ndugu na dada zetu? (b) Namna gani tunaweza kuwasaidia wajisikie muzuri?

15 Zaidi ya manguo na chakula, wakimbizi wako na lazima ya mambo mengine. Wako na lazima ya musaada ili kupiganisha mahangaiko ya moyoni na kutiwa moyo kupitia Biblia. (Mathayo 4:4) Wazee wanaweza kusaidia wakimbizi wapate vichapo katika luga yao na kuwasaidia kukutana na ndugu na dada wenye kuzungumuza luga yao. Jambo hilo ni la lazima sana kwa sababu wakimbizi wengi wamelazimika kuacha mambo yote yenye walikuwa wanazoea. Wanakumbuka watu wa familia yao, watu wa eneo lao, na kutaniko lao. Wako na lazima ya kujionea upendo wa Yehova na huruma yake kati ya Wakristo wenzao. Ikiwa hawajionee mambo hayo, wakimbizi wanaweza kutafuta musaada kwa watu wengine wenye walitoka katika inchi yao lakini wenye hawamutumikie Yehova. (1 Wakorintho 15:33) Wakati tunawafanya wajisikie kuwa wamekaribishwa muzuri katika kutaniko, tunatumika pamoja na Yehova ili kulinda “wakaaji wageni.”—Zaburi 146:9.

16 Yesu na watu wa familia yake hawangerudia kwao wakati wale wenye walikuwa wanawatesa walikuwa wangali wanatawala. Kwa sababu kama hizo, leo wakimbizi wanaweza kushindwa kurudia kwao. Hata hivyo, wengine wanaweza kukataa kurudia kwao. Lije anasema kama wazazi wengi wenye waliona namna watu wa familia zao wanalalwa kinguvu na kuuawa katika inchi yao, hawapendi kurudia huko pamoja na watoto wao. Ili kusaidia ndugu na dada zetu, tunapaswa kuonyesha ‘hisia-mwenzi [ao, sifa ya kujitia pa nafasi ya wengine], tukikuwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili.’ (1 Petro 3:8) Mateso yamefanya wakimbizi fulani waepuke kujiunga na watu wengine, na wanaweza kusikia haya ya kuzungumuza na wengine juu ya mateso yao, zaidi sana ikiwa watoto wao wako karibu nao. Ujiulize hivi: ‘Ikiwa ninapata mateso kama hayo, ningependa wengine wanitendee namna gani?’—Mathayo 7:12.

WAKATI TUNAHUBIRIA WAKIMBIZI WENYE HAWAKO MASHAHIDI

17. Namna gani kazi yetu ya kuhubiri inaletea wakimbizi kitulizo?

17 Leo wakimbizi wengi wanatoka katika inchi ambamo kazi yetu ya kuhubiri inakatazwa. Kwa musaada wa Mashahidi wenye bidii, maelfu ya wakimbizi wanasikia “neno la Ufalme” kwa mara ya kwanza. (Mathayo 13:19, 23) Wengi wenye “kulemewa na mizigo” wanaendelea kupata faraja na kitulizo kwenye mikutano yetu na wanasema hivi bila kukawia: “Kwa kweli Mungu yupo katikati yenu.”—Mathayo 11:28-30; 1 Wakorintho 14:25.

18, 19. Namna gani tunaweza kuwa wenye hekima wakati tunahubiria wakimbizi?

18 Tunapaswa kuwa wenye hekima na wenye ‘kujihazari [wangaalifu]’ wakati tunahubiria wakimbizi. (Mathayo 10:16; Methali 22:3) Wakati wakimbizi wanazungumuza, uwasikilize kwa uvumilivu, lakini usizungumuzie mambo ya politike. Tunapaswa kufuata maagizo yenye tunapata kutoka kwenye biro ya tawi na kwa wakubwa wa eneo ili tusijitie sisi wenyewe katika hatari na wengine pia. Kwa sababu wakimbizi wanatoka katika dini na desturi mbalimbali, tunapaswa kujifunza kuheshimia mawazo yao. Kwa mufano, watu wenye kutoka katika inchi fulani wanashikilia sana mawazo fulani juu ya namna wanawake wanapaswa kuvaa. Kwa hiyo, wakati tunawahubiria, ni muzuri tuvae muzuri ili tusiwakwaze.

19 Tunapenda kusaidia watu wenye kuteseka, hata wale wenye hawamutumikie Yehova. Wakati tunafanya hivyo, tunaiga mufano muzuri wa Musamaria mwenye Yesu alizungumuzia katika mufano wake. (Luka 10:33-37) Njia ya muzuri zaidi ya kusaidia watu ni kuwafundisha habari njema. Muzee mumoja mwenye amesaidia wakimbizi wengi alisema kama ni jambo la maana kuwaambia bila kukawia kama sisi ni Mashahidi wa Yehova. Tunapaswa kuwajulisha kama tunapenda kwanza kuwasaidia waelewe tumaini la muzuri sana lenye Biblia inatoa kuliko kuwatolea musaada wa kimwili.

MATOKEO YENYE KULETA FURAHA

20, 21. (a) Tunapata matokeo gani ya muzuri wakati tunaonyesha wakimbizi upendo wa kweli? (b) Tutajifunza nini katika habari yenye kufuata?

20 Wakati tunaonyesha “wakaaji wageni” upendo wa kweli, hilo linaleta matokeo ya muzuri. Wakati bwana yake alikufa, dada mumoja mwenye kuitwa Alganesh alikimbia mateso katika Eritrea pamoja na watoto wake wadogo sita. Walipaswa kufanya safari ya siku munane katika jangwa. Mwishowe, kisha safari yenye kuchokesha sana, walifika Sudani. Anasema hivi: “Ndugu na dada wa huko walitutendea kama vile watu wa jamaa zao, walitupatia chakula, manguo, nafasi ya kuishi, na feza za kulipa wakati tunaenda mahali fulani. Ni watu gani wengine wangeweza kukaribisha katika nyumba zao watu wenye hawajue kwa sababu tu wote wanaabudu Mungu uleule? Ni Mashahidi wa Yehova tu!”—Soma Yohana 13:35.

21 Tuseme nini juu ya watoto wengi wenye wanahama pamoja na wazazi wao? Katika habari yenye kufuata, tutajifunza namna gani sisi wote tunaweza kusaidia familia hizo zimutumikie Yehova kwa furaha.

^ fu. 2 Katika habari hii, neno “wakimbizi” linazungumuzia watu wenye wamelazimika kuacha makao yao kwa sababu ya vita, mateso, ao misiba ya asili. Wanaweza kulazimika kuishi katika inchi ingine ao katika sehemu ingine ya inchi yao. Tume ya Umoja wa Mataifa Inayoshughulikia Wakimbizi (UNHCR) inasema kama katika dunia yote, mutu 1 kati ya watu 113 analazimika kuacha makao yake.

^ fu. 6 Soma habari yenye kichwa “Musisahau Ukaribishaji-Wageni,” katika gazeti Munara wa Mulinzi la Mwezi wa 10, 2016, ukurasa wa 8-12.

^ fu. 11 Wakati tu wakimbizi wanafika katika eneo, wazee wanapaswa kufuata muongozo wenye kupatikana katika kitabu Tengenezo Lenye Kufanya Mapenzi ya Yehova, sura ya 8, fungu la 30. Ili kuzungumuza na kutaniko la wakimbizi wenye kutoka katika inchi fulani, wazee wanaweza kuandikia biro yao ya tawi kwa kutumia adresi yetu ya Internete jw.org. Na wakati huohuo, wanaweza kuuliza mukimbizi kwa hekima habari juu ya kutaniko lake na utumishi wake ili kujua muzuri hali yake ya kiroho.

^ fu. 14 Soma habari “Hauwezi Kuwatumikia Mabwana Wawili” na habari “Usiogope—Yehova Atakusaidia!” katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 4, 2014, ukurasa wa 17-26.