Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Watoto wa “Wakaaji Wageni”

Kuwasaidia Watoto wa “Wakaaji Wageni”

“Sina sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.”—3 YOH. 4.

NYIMBO: 88, 41

1, 2. (a) Watoto wengi wahamiaji hukabili tatizo lipi? (b) Makala hii itazungumzia maswali gani?

“TANGU utotoni, nilizungumza lugha ya wazazi wangu ambao ni wahamiaji nikiwa nyumbani na kutanikoni,” anasimulia Joshua. “Lakini nilipoanza shule, nilianza kupendelea lugha ya wenyeji. Baada ya miaka michache, nilibadilika kabisa. Sikuelewa mikutano, na niliacha utamaduni wa wazazi.” Kisa cha Joshua ni cha kawaida.

2 Leo, watu zaidi ya 240,000,000 huishi nje ya nchi walizozaliwa. Ikiwa wewe ni mzazi mhamiaji, unawezaje kuwapa watoto wako fursa nzuri zaidi ya kuwa watoto wa kiroho ambao “wanaendelea kutembea katika kweli”? (3 Yoh. 4) Na wengine wanaweza kusaidiaje?

WAZAZI, WEKENI MFANO MZURI

3, 4. (a) Wazazi wanaweza kuwawekeaje watoto wao mfano mzuri? (b) Wazazi hawapaswi kutarajia nini kutoka kwa watoto wao?

3 Wazazi, mfano wenu ni muhimu ili kuwasaidia watoto wenu watembee katika njia ya uzima wa milele. Watoto wenu wanapowaona ‘mkiutafuta kwanza ufalme,’ wanajifunza kumtegemea Yehova ili kupata mahitaji yao ya kila siku. (Mt. 6:33, 34) Kwa hiyo, muwe na maisha rahisi. Msidhabihu mambo ya kiroho ili kupata vitu vya kimwili, bali mdhabihu vitu vya kimwili ili kupata faida za kiroho. Jitahidini msiwe na madeni. Tafuteni “hazina [za] mbinguni,” yaani, kibali cha Yehova badala ya utajiri au “utukufu wa wanadamu.”—Soma Marko 10:21, 22; Yoh. 12:43.

4 Kamwe msiwe na shughuli nyingi hivi kwamba mkose muda wa kuwa pamoja na watoto wenu. Acheni waone kwamba mnawaonea fahari wanapoamua kumtanguliza Yehova, badala ya kujitafutia au kuwatafutia sifa au utajiri. Epukeni maoni yasiyo ya Kikristo kwamba watoto wanapaswa kuwaandalia wazazi wao maisha ya starehe. Kumbukeni, “watoto hawapaswi kuweka akiba kwa ajili ya wazazi wao, bali wazazi kwa ajili ya watoto wao.”—2 Kor. 12:14.

WAZAZI, JIFUNZENI LUGHA YA WENYEJI

5. Kwa nini wazazi wanapaswa kuzungumza na watoto wao kumhusu Yehova?

5 Kama ilivyotabiriwa, watu “kutoka katika lugha zote za mataifa” wanamiminika katika tengenezo la Yehova. (Zek. 8:23) Lakini kutojua lugha kunaweza kufanya iwe vigumu kwako kuwafundisha watoto wako kweli. Watoto wako ndio wanafunzi muhimu zaidi wa Biblia ambao utawahi kuwa nao, na “[wanapoendelea] kupata ujuzi” juu ya Yehova watapata uzima wa milele. (Yoh. 17:3) Ili watoto wako waelewe mafundisho ya Yehova, unapaswa “kuyasema” katika pindi zote zinazofaa.—Soma Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

6. Watoto wako wanaweza kunufaikaje kwa kujifunza lugha yako? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

6 Inaelekea watoto wako watajifunza lugha ya wenyeji wakiwa shuleni, au kwenye ujirani, lakini watajifunza lugha yako hasa kwa kuzungumza nawe mara nyingi. Zaidi ya kuwasaidia watoto wako wazungumze nawe kutoka moyoni, wanapojua lugha yako watapata faida nyingine. Kujua lugha mbili kutaboresha uwezo wao wa kufikiri na kutafanya iwe rahisi zaidi kwao kushirikiana na wengine. Pia, kunaweza kuwapa fursa za kupanua utumishi wao. Carolina, ambaye wazazi wake ni wahamiaji, anasema hivi: “Ninafurahia kuwa katika kutaniko la lugha ya kigeni. Na inapendeza kusaidia mahali palipo na uhitaji mkubwa wa wahubiri.”

7. Unaweza kufanya nini ikiwa kuna kizuizi cha lugha katika familia yako?

7 Hata hivyo, baadhi ya watoto wa wahamiaji wanapoanza kuzoea utamaduni na lugha ya wenyeji, wanaweza kupoteza tamaa na uwezo wa kuwasiliana na wazazi wao katika lugha ya mama. Wazazi, ikiwa watoto wenu wanakabili hali hiyo, je, mnaweza kujifunza kwa kiwango fulani lugha ya wenyeji? Itakuwa rahisi kwenu kuwalea watoto katika njia ya Kikristo ikiwa mtaelewa mazungumzo yao, burudani wanazopenda, kazi zao za shule, na ikiwa mtawasiliana moja kwa moja na walimu wao. Ni kweli kwamba kujifunza lugha mpya huhitaji muda, jitihada, na unyenyekevu. Lakini ikiwa mtoto wako angekuwa kiziwi, je, usingejaribu kujifunza lugha ya ishara ili kuzungumza naye? Je, hukubali kwamba mtoto anayeelewa vizuri zaidi lugha nyingine anahitaji pia kuhangaikiwa jinsi hiyo? *

8. Unaweza kuwasaidiaje watoto wako ikiwa unakabili kizuizi cha lugha?

8 Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kwa wazazi kuijua vizuri lugha ya wenyeji ambayo watoto wamejifunza. Kizuizi hicho cha lugha kinaweza kufanya iwe vigumu kwa wazazi kuwafundisha watoto wao ujuzi wa mambo mazito kupitia “maandishi matakatifu.” (2 Tim. 3:15) Ikiwa unakabili hali hiyo, bado unaweza kuwasaidia watoto wako kumjua na kumpenda Yehova. Mzee mmoja wa kutaniko anayeitwa Shan, anakumbuka hivi: “Mama yetu ambaye alitulea akiwa peke yake hakuelewa vizuri lugha tuliyoielewa, nami na dada zangu hatukuifahamu lugha yake vizuri. Lakini tulipomwona akijifunza, akisali, na kujitahidi awezavyo kuongoza ibada ya familia kila juma, tulielewa kwamba ni muhimu sana kumjua Yehova.”

9. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto ambao huenda wakahitaji kujifunza kwa kutumia lugha mbili?

9 Huenda wototo fulani wakahitaji kujifunza kumhusu Yehova katika lugha mbili, yaani, lugha wanayozungumza shuleni na ile wanayozungumza nyumbani. Ili kufanya hivyo, wazazi fulani hutumia machapisho, rekodi za kusikiliza, na video za lugha zote mbili. Ni wazi kwamba wazazi wahamiaji wanapaswa kutumia muda mwingi zaidi na kutia bidii ili kuwasaidia watoto wao wasitawishe uhusiano wa karibu na Yehova.

MTASHIRIKIANA NA KUTANIKO LA LUGHA GANI?

10. (a) Ni nani anayepaswa kuamua familia itashirikiana na kutaniko la lugha gani? (b) Anapaswa kufanya nini kabla ya kufanya uamuzi huo?

10 “Wakaaji wageni” wanapoishi mbali na Mashahidi wengine wanaozungumza lugha yao, wanahitaji kushirikiana na kutaniko la lugha ya wenyeji. (Zab. 146:9) Lakini ikiwa kuna kutaniko karibu ambalo linatumia lugha yako, swali hili linazuka: Ni kutaniko la lugha gani ambalo linafaa familia yako? Baada ya kufikiria kwa makini, kusali, na kushauriana na mwenzi na watoto wake, kichwa cha familia anapaswa kufanya uamuzi. (1 Kor. 11:3) Kichwa cha familia atazingatia mambo gani? Ni kanuni gani zinazohusika? Acheni tuchunguze baadhi ya kanuni hizo.

11, 12. (a) Lugha inaweza kuathirije kile ambacho mtoto anajifunza mikutanoni? (b) Kwa nini baadhi ya watoto hukataa kujifunza lugha ya wazazi wao?

11 Wazazi wanapaswa kuchanganua kwa usawaziko mahitaji ya watoto wao. Ni kweli kwamba ili mtoto achukue kweli kwa uzito, mambo mengi yanahusika zaidi tu ya kutumia saa chache kupata elimu ya kiroho akiwa mikutanoni, haidhuru lugha inayotumiwa. Lakini fikiria hili: Watoto wanapohudhuria mikutano ya lugha ambayo wanaelewa vizuri, wanaweza kuelewa mambo wanayojifunza kwa kuwapo tu mikutanoni, labda hata kuliko jinsi wazazi wanavyoweza kuwazia. Huenda isiwe hivyo ikiwa hawaelewi vizuri lugha inayotumiwa. (Soma 1 Wakorintho 14:9, 11.) Na huenda lugha ambayo mtoto alijifunza kwanza haitaendelea kuwa lugha inayomgusa moyoni au akilini. Kwa kweli, baadhi ya watoto wanaweza kujifunza kutoa maelezo, maonyesho, na hotuba wakitumia lugha ya wazazi wao lakini maneno hayo yasiwe yanatoka moyoni.

12 Isitoshe, moyo wa mtoto huchochewa na mengi zaidi ya lugha tu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Joshua, aliyetajwa mwanzoni. Kama dada yake, Esther, anavyosema, “watoto wachanga huathiriwa na lugha, utamaduni, na dini ya wazazi wao.” Ikiwa watoto hawafuati utamaduni wa wazazi, huenda wakakataa kujifunza lugha yao na hata imani yao. Wazazi wahamiaji wanaweza kufanya nini?

13, 14. (a) Kwa nini wazazi fulani wahamiaji walihamia kutaniko la lugha ya wenyeji pamoja na familia yao? (b) Wazazi walifanya nini ili wadumishe hali nzuri ya kiroho?

13 Wazazi Wakristo hutanguliza hali ya kiroho ya watoto wao kuliko mapendezi ya kibinafsi. (1 Kor. 10:24) Samuel, baba ya Joshua na Esther, anasema hivi: “Mimi na mke wangu tuliwachunguza watoto wetu ili tuone ni lugha gani inayowasaidia wafanye maendeleo ya kiroho na tukasali ili tupate hekima. Jibu la sala yetu halikutufaa sisi kibinafsi. Lakini tulipoona kwamba hawakunufaika sana na mikutano ya lugha yetu, tuliamua kuhamia kutaniko la lugha ya wenyeji. Tukiwa pamoja, tulihudhuria mikutano na kushiriki katika huduma kwa ukawaida. Pia, tuliwaalika marafiki wenyeji wajiunge nasi kwa ajili ya mlo na tafrija. Kufanya hivyo kuliwasaidia watoto wetu kuwafahamu akina ndugu na kumjua Yehova, si akiwa Mungu tu, bali pia Baba na Rafiki yao. Tuliona jambo hilo kuwa muhimu zaidi kwao kuliko kujifunza lugha yetu.”

14 Samuel anasema hivi pia: “Ili kudumisha hali nzuri ya kiroho, mimi na mke wangu pia tulihudhuria mikutano ya lugha yetu. Tulikuwa na shughuli nyingi, na tulichoka. Lakini tunamshukuru Yehova kwa kubariki jitihada zetu na jinsi tulivyojidhabihu. Watoto wetu wote watatu wanamtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote.”

VIJANA WANAWEZA KUFANYA NINI?

15. Kwa nini dada anayeitwa Kristina alihisi kwamba angefanya maendeleo ya kiroho ikiwa angekuwa katika kutaniko la lugha ya wenyeji?

15 Watoto ambao wana umri wa kutosha wa kujifanyia maamuzi huenda wakatambua kwamba wanaweza kumtumikia Yehova vizuri zaidi wakishirikiana na kutaniko la lugha wanayoielewa vizuri. Ikiwa ndivyo, wazazi hawapaswi kuhisi kwamba watoto wao wanawakana. Kristina anakumbuka hivi: “Nilielewa kwa kiasi fulani lugha ya wazazi wangu, lakini ilikuwa vigumu sana kuelewa mikutano. Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilihudhuria kusanyiko lililotumia lugha niliyozungumza shuleni. Kwa mara ya kwanza, nilielewa kwamba kile nilichokuwa nikisikia ni kweli! Maisha yangu yalibadilika pia nilipoanza kusali katika lugha niliyozungumza shuleni. Sasa ningeweza kuzungumza na Yehova kutoka moyoni!” (Mdo. 2:11, 41) Alipokuwa mtu mzima, Kristina alizungumzia jambo hilo na wazazi wake na akaamua kuhamia kutaniko la lugha ya wenyeji. Anakumbuka hivi: “Kujifunza kumhusu Yehova kwa kutumia lugha niliyozungumza shuleni kulinichochea kuchukua hatua.” Baada ya muda mfupi, Kristina akawa painia wa kawaida mwenye shangwe.

16. Kwa nini dada anayeitwa Nadia anashukuru kwamba alibaki katika kutaniko la lugha yake?

16 Enyi vijana, je, mnahisi kwamba mngependelea kuwa katika kutaniko la lugha ya wenyeji? Ikiwa ndivyo, jiulize ni kwa nini. Je, kuhamia kutaniko lingine kutakusaidia kumkaribia Yehova zaidi? (Yak. 4:8) Au huenda unataka kuhama ili wazazi wako wasikufuatilie au tu kwa sababu hutaki kujitahidi katika mambo ya kiroho? Nadia, ambaye sasa anatumikia Betheli, anasema hivi: “Mimi na ndugu zangu tulipokuwa matineja, tulitaka kuhamia kutaniko la lugha ya wenyeji.” Lakini wazazi wao walijua kwamba kufanya hivyo hakungewanufaisha kiroho. “Sasa tunashukuru kwamba wazazi wetu walijitahidi kutufundisha lugha yao na kuamua tubaki katika kutaniko la lugha yetu. Kufanya hivyo kumeboresha maisha yetu na kumeongeza fursa zetu za kuwasaidia wengine kumjua Yehova.”

WENGINE WANAWEZA KUSAIDIAJE?

17. (a) Yehova amewapa nani jukumu la kuwalea watoto? (b) Wazazi wanawezaje kupata msaada wanapowafundisha watoto wao kweli?

17 Yehova amewapa wazazi jukumu la kuwalea watoto wao katika kweli, bali si nyanya (bibi), babu, au mtu mwingine yeyote. (Soma Methali 1:8; 31:10, 27, 28.) Hata hivyo, wazazi ambao hawajui lugha ya wenyeji huenda wakahitaji msaada ili kufikia mioyo ya watoto wao. Kufanya mpango ili wapokee msaada huo hakumaanishi wapuuze jukumu lao la kiroho, badala yake inaweza kuwa sehemu ya kuwalea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Kwa mfano, wazazi wanaweza kuwaomba wazee wa kutaniko madokezo ya jinsi ya kuongoza ibada ya familia na kuwasaidia kupata marafiki wanaowafaa watoto wao.

Watoto na wazazi hunufaika kwa kushirikiana na kutaniko (Tazama fungu la 18 na 19)

18, 19. (a) Ndugu na dada waliokomaa kiroho wanaweza kuwanufaishaje vijana? (b) Wazazi wanapaswa kuendelea kufanya nini?

18 Mara kwa mara, wazazi wanaweza kualika familia nyingine wajiunge nao katika ibada ya familia. Zaidi ya hilo, vijana wengi hufanya maendeleo wanaposhirikiana na watu waliokomaa kiroho. Kwa mfano, wanaweza kuandamana nao katika huduma au kwenye tafrija zenye kujenga. (Met. 27:17) Shan aliyenukuliwa awali anakumbuka hivi: “Ninawakumbuka vizuri ndugu walionizoeza. Nilijifunza mambo mengi waliponisaidia kutayarisha migawo ya hotuba ya wanafunzi kwa ajili ya mikutano. Na nilifurahia tafrija tulizofanya tukiwa kikundi.”

19 Sikuzote, ndugu wanaochaguliwa na wazazi kuwasaidia watoto wao wanapaswa kuwachochea watoto wawaheshimu wazazi wao, kuzungumza mambo yanayofaa kuwahusu, bali si kuchukua jukumu la wazazi. Isitoshe, wale wanaowasaidia watoto wanapaswa kuepuka kujiendesha kwa njia inayoweza kutiliwa shaka na wale walio ndani au nje ya kutaniko. (1 Pet. 2:12) Wazazi hawapaswi kupuuza wajibu wao wanapowaruhusu watu wengine wawazoeze watoto wao kiroho. Lazima wachunguze mara kwa mara na kujua msaada unaotolewa na wakati huohuo waendelee kuwafundisha watoto wao.

20. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao wawe watumishi waaminifu wa Yehova?

20 Wazazi, mwombeni Yehova msaada na mfanye yote mwezayo. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 15:7.) Tangulizeni uhusiano wa mtoto wenu pamoja na Yehova kuliko mapendezi yenu binafsi. Fanyeni yote mwezayo kuhakikisha kwamba Neno la Mungu linafikia moyo wa mtoto wenu. Msiache kamwe kuamini kwamba mtoto wenu anaweza kuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova. Watoto wenu wanapofuata Neno la Mungu na mfano wenu mzuri, mtahisi kama mtume Yohana alivyohisi kuhusu watoto wake wa kiroho: “Sina sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.”—3 Yoh. 4.

^ fu. 7 Tazama makala “Unaweza Kujifunza Lugha Nyingine!” katika gazeti Amkeni! la Machi 2007, uku. 10-12.