Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Je, Unanipenda Kuliko Hawa?”

“Je, Unanipenda Kuliko Hawa?”

“Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda kuliko hawa?” —YOH. 21:15.

NYIMBO: 128, 45

1, 2. Baada ya kukesha usiku kucha akivua, Petro alipatwa na tukio gani?

WANAFUNZI saba wa Yesu walikuwa wamekesha usiku kucha wakijaribu kuvua samaki katika Bahari ya Galilaya, lakini hawakupata chochote. Yesu aliyefufuliwa alikuwa akiwatazama kutoka ufuoni. Kisha akawaambia: “‘Utupeni wavu upande wa kuume wa mashua, nanyi mtapata.’ Basi wakautupa, lakini hawakuweza tena kuuvuta ndani kwa sababu samaki walikuwa wengi sana.”—Yoh. 21:1-6.

2 Baada ya kuwaandalia kiamsha-kinywa, Yesu alimgeukia Simoni Petro na kumwuliza: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda kuliko hawa?” Yesu alikuwa akirejelea nini? Petro alipenda sana uvuvi. Kwa hiyo, inaonekana Yesu alitaka kujua alipenda nini hasa. Je, alipenda samaki na biashara ya uvuvi kuliko Yesu na mafundisho yake? Petro alimjibu hivi: “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.” (Yoh. 21:15) Kwa kweli, Petro aliishi kulingana na maneno yake. Kuanzia wakati huo na kuendelea, alithibitisha kwamba alimpenda Kristo kwa kuwa na bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi, na hivyo kuwa nguzo katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza.

3. Wakristo wanapaswa kuwa macho kuhusu hatari zipi?

3 Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ambayo Yesu alimwambia Petro? Tunahitaji kuwa waangalifu tusiruhusu upendo wetu kwa Kristo udhoofike na kujiruhusu tukengeushwe kutoka masilahi ya Ufalme. Yesu alielewa vema mikazo inayotokana na mahangaiko ya mfumo huu wa mambo. Katika mfano wake wa mpandaji, Yesu alisema kwamba baadhi ya watu wangekubali “neno la ufalme” na kufanya maendeleo lakini “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri [zingelisonga] neno.” (Mt. 13:19-22; Marko 4:19) Kwa kweli, tusipokuwa waangalifu, mahangaiko ya kila siku ya maisha yanaweza kushawishi moyo wetu ufuatie vitu vya kimwili na kutufanya tupunguze bidii yetu katika mambo ya kiroho. Hivyo, Yesu aliwaonya hivi wanafunzi wake: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha.”—Luka 21:34.

4. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuchunguza kina cha upendo wetu kwa Kristo? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 Kama Petro alivyofanya baada ya kukutana na Yesu aliyefufuliwa, tunathibitisha kina cha upendo wetu kwa Kristo kwa kutanguliza kazi aliyotupatia tufanye. Tunaweza kuhakikishaje kwamba tutaendelea kufanya hivyo? Mara kwa mara, tunahitaji kujiuliza hivi: ‘Ninapenda nini hasa? Je, ninapata shangwe zaidi kwa kujihusisha na shughuli za kawaida za maisha au na mambo ya kiroho?’ Kuhusiana na hilo, acheni tuchunguze mambo matatu maishani ambayo yanaweza kupunguza upendo wetu kwa Kristo na kwa mambo ya kiroho ikiwa hatutakuwa na usawaziko kuyahusu. Mambo hayo ni kazi ya kimwili, burudani, na vitu vya kimwili.

UWE NA USAWAZIKO KUHUSU KAZI YA KIMWILI

5. Vichwa vya familia wana wajibu gani wa Kimaandiko?

5 Uvuvi haukuwa jambo ambalo Petro alifanya ili kujifurahisha tu, bali ilikuwa kazi iliyomtegemeza. Leo, vichwa vya familia wanatambua kwamba wana wajibu wa Kimaandiko wa kuandalia familia zao mahitaji ya kimwili. (1 Tim. 5:8) Lazima wafanye kazi kwa bidii ili watimize wajibu huo. Hata hivyo, katika siku hizi za mwisho, mara nyingi kazi ya kimwili huwa chanzo cha mahangaiko.

6. Wafanyakazi wanapata mikazo gani leo?

6 Kwa sababu ya uhaba wa kazi na idadi kubwa ya wanaotafuta kazi, wafanyakazi wengi hulazimika kufanya kazi kwa saa nyingi, na nyakati nyingine wakilipwa mshahara mdogo. Pia, mkazo wa kila siku wa kufikia malengo yanayozidi kuongezeka huwalemea watu sana kimwili, kiakili, na kihisia. Wafanyakazi ambao hawako tayari kujidhabihu kwa ajili ya kampuni zao wanahatarisha kazi zao.

7, 8. (a) Tunapaswa kuwa washikamanifu kwa nani kwanza? (b) Ndugu mmoja nchini Thailand alijifunza somo gani muhimu kuhusu kazi yake?

7 Tukiwa Wakristo, tunapaswa kuwa washikamanifu kwa Yehova Mungu kwanza, bali si kwa mwajiri wetu. (Luka 10:27) Kazi ya kimwili inapaswa kuwa njia ya kujiruzuku tu. Sisi hufanya kazi ili kupata mahitaji ya msingi ya kimwili na kutegemeza huduma yetu. Hata hivyo, tusipokuwa waangalifu, kazi ya kimwili inaweza kuingilia ibada yetu. Kwa mfano, ndugu mmoja nchini Thailand anasema hivi: “Nilipenda kazi yangu ya kurekebisha kompyuta, lakini ilihusisha kufanya kazi kwa saa nyingi. Kwa hiyo, nilikuwa na muda mfupi sana wa kufanya mambo ya kiroho. Mwishowe, nilitambua kwamba ili nitangulize masilahi ya Ufalme, nilihitaji kubadili kazi yangu.” Ndugu huyo alifanya nini?

8 Anaeleza hivi: “Baada ya kufikiria nitafanya kazi gani na kuweka akiba ya pesa kwa mwaka mmoja hivi, niliamua kuuza aiskrimu mtaani. Mwanzoni, biashara yangu haikuwa nzuri na nilivunjika moyo. Nilipokutana na watu niliofanya kazi nao, walinicheka na kuniuliza kwa nini nilifikiri kwamba kuuza aiskrimu ni bora kuliko kufanya kazi ya kompyuta katika vyumba vyenye viyoyozi. Nilisali kwa Yehova na kumwomba anisaidie kukabiliana na hali hiyo, na kufikia lengo la kuwa na muda zaidi wa kufanya mambo ya kiroho. Muda si muda, mambo yalianza kuwa mazuri. Nilielewa vizuri zaidi kile ambacho wateja wangu hupenda na nikaongeza ustadi wa kutengeneza aiskrimu. Punde si punde, nilikuwa nikiuza aiskrimu yote kila siku. Kwa kweli, nilipata pesa nyingi zaidi kuliko wakati nilipokuwa nikifanya kazi ya kompyuta. Mimi ni mwenye furaha zaidi kwa sababu sina mikazo na wasiwasi niliokuwa nao katika kazi niliyofanya mwanzoni. Na jambo muhimu hata zaidi, sasa ninahisi nikiwa karibu sana na Yehova.”—Soma Mathayo 5:3, 6.

9. Tunaweza kudumishaje maoni yenye usawaziko kuhusu kazi yetu ya kimwili?

9 Bidii ni sifa inayomfurahisha Mungu, na kufanya kazi kwa bidii huridhisha. (Met. 12:14) Hata hivyo, kama ndugu aliyetajwa awali alivyojionea, tunahitaji kuwa na usawaziko kuhusu kazi ya kimwili. Yesu alisema hivi: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote,” yaani, mahitaji ya msingi ya kimwili. (Mt. 6:33) Ili kujua ikiwa tuna maoni yenye usawaziko kuhusu mambo ya kimwili na majukumu ya kiroho, ni vizuri tujiulize hivi: ‘Je, ninaona kazi yangu ya kimwili kuwa nzuri na yenye kusisimua lakini mambo ya kiroho kuwa ya kawaida au ya kidesturi?’ Kufikiria na kutafakari hisia zetu kuhusu kazi ya kimwili na kuhusu mambo ya kiroho kunaweza kutusaidia kutambua tunapenda nini hasa.

10. Yesu alifundisha somo gani muhimu kuhusu mambo tunayopaswa kutanguliza?

10 Yesu aliweka mfano mzuri wa kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu mambo ya kimwili na mambo ya kiroho. Pindi moja, Yesu alimtembelea Maria na dada yake, Martha. Martha alipokuwa katika pilikapilika za kuandaa mlo, Maria alichagua kuketi miguuni pa Yesu na kumsikiliza. Martha alipolalamika kwamba Maria hamsaidii, Yesu alimwambia Martha hivi: “Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.” (Luka 10:38-42) Yesu alikuwa akimfundisha Martha somo muhimu. Ili tuepuke kukengeushwa na mambo ya kimwili na kuthibitisha kwamba tunampenda Kristo, tunapaswa kuendelea kuchagua “fungu jema,” yaani, kutanguliza mambo ya kiroho.

MAONI YETU KUHUSU TAFRIJA NA BURUDANI

11. Maandiko yanafundisha nini kuhusu kupumzika?

11 Tunahitaji muda wa burudani na kupumzika kutokana na kazi ngumu na ratiba yenye shughuli nyingi. Neno la Mungu linasema hivi: “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.” (Mhu. 2:24) Yesu alitambua uhitaji wa kupumzika nyakati fulani. Baada ya kampeni fulani kubwa ya kuhubiri, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Njooni, ninyi wenyewe, faraghani katika mahali pasipo na watu mpumzike kidogo.”—Marko 6:31, 32.

12. Tunapaswa kuchukua tahadhari gani kuhusu tafrija na burudani? Toa mfano.

12 Kwa kweli, kuwa na tafrija na burudani ni muhimu. Hata hivyo, hatari ni wakati mtu anatanguliza kujifurahisha maishani. Katika karne ya kwanza, wengi walikuwa na mtazamo huu: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Kor. 15:32) Roho hiyo imeenea sana ulimwenguni leo. Kwa mfano, miaka mingi iliyopita, mwanamume mmoja kijana huko Ulaya Magharibi alianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Lakini alipenda sana burudani hivi kwamba akaacha kushirikiana na watu wa Yehova. Hata hivyo, baada ya muda, alitambua kwamba kutanguliza burudani kulimletea matatizo na kumvunja moyo tu. Kwa hiyo, akaanza tena kujifunza Biblia na baadaye akastahili kuwa mhubiri wa habari njema. Baada ya kubatizwa, alisema hivi: “Ninajuta tu kwamba nilipoteza muda mwingi kabla ya kugundua kuwa kumtumikia Yehova huleta furaha nyingi zaidi kuliko kufuatia burudani za ulimwengu huu.”

13. (a) Toa mfano unaoonyesha hatari zinazohusiana na tafrija na burudani. (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu tafrija na burudani?

13 Kusudi la tafrija ni kutuburudisha na kutupatia nguvu. Tunapaswa kutumia muda gani ili tutimize kusudi hilo? Fikiria mfano huu: Wengi wetu hupenda kula kitinda mlo mara kwa mara, lakini tunatambua kwamba kula keki na peremende kwa muda mrefu kutadhuru afya yetu. Hivyo, sisi hula hasa chakula chenye lishe. Kwa njia hiyohiyo, kujihusisha sana katika tafrija na burudani kutadhoofisha hali yetu ya kiroho. Ili kuzuia hilo lisitupate, tunashiriki kwa ukawaida katika mambo ya Ufalme. Tunawezaje kujua ikiwa tuna maoni yenye usawaziko kuhusu burudani? Tunaweza kuchagua juma moja na kuandika saa tulizotumia kufanya mambo ya kiroho kama vile kuhudhuria mikutano, kushiriki katika huduma ya shambani, na kufanya funzo la Biblia la kibinafsi na la familia. Kisha tunaweza kulinganisha saa hizo na saa ambazo tulitumia juma hilohilo katika burudani kama vile michezo, kutazama televisheni, kucheza michezo ya video, au mambo tunayofanya ili kujifurahisha. Unatambua nini unapolinganisha mambo hayo? Je, unahitaji kupunguza “kitinda mlo”?—Soma Waefeso 5:15, 16.

14. Ni nini kinachopaswa kutuongoza tunapochagua tafrija na burudani?

14 Mtu mmoja-mmoja na vichwa vya familia wana uhuru wa kuchagua aina ya tafrija wanayopenda maadamu haihusishi mambo ambayo yanapingana na mwongozo wa Yehova ulio katika kanuni za Biblia. * Burudani inayofaa ni “zawadi ya Mungu.” (Mhu. 3:12, 13) Bila shaka, tunatambua kwamba maamuzi tunayofanya kuhusu burudani hutofautiana. (Gal. 6:4, 5) Hata iwe tunachagua burudani ya aina gani, tunapaswa kuwa wenye usawaziko. Yesu alisema: “Mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.” (Mt. 6:21) Kwa hiyo, upendo wetu wa kutoka moyoni kwa Yesu utachochea fikira, maneno, na matendo yetu yazingatie utendaji wa Ufalme kwanza badala ya shughuli za kila siku za maisha.—Flp. 1:9, 10.

KUPAMBANA NA TAMAA YA KUPENDA VITU VYA KIMWILI

15, 16. (a) Ni kwa njia gani kupenda vitu vya kimwili kunaweza kuwa mtego kwa Mkristo? (b) Yesu alitoa ushauri gani wa hekima kuhusu vitu vya kimwili?

15 Leo, watu wengi wanatamani sana mavazi ya kisasa, vifaa vya kielektroni, na kadhalika. Kwa hiyo, kila Mkristo anahitaji kuchunguza kwa ukawaida vitu anavyotamani kwa kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, ninaona vitu vya kimwili kuwa vya muhimu sana kwangu hivi kwamba ninatumia muda mwingi zaidi kutafiti na kufikiria kuhusu magari au mitindo ya kisasa kuliko muda ninaotumia kutayarisha mikutano ya kutaniko? Je, nimeanza kujishughulisha sana na shughuli za kila siku za maisha hivi kwamba ninatumia muda mchache zaidi kusali au kusoma Biblia?’ Ikiwa tunatambua kwamba upendo wetu kuelekea vitu vya kimwili unazidi upendo wetu kwa Kristo, tunapaswa kutafakari maneno haya ya Yesu: “Mjilinde na kila namna ya tamaa.” (Luka 12:15) Kwa nini Yesu alitoa onyo hilo zito?

16 Yesu alisema kwamba “hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.” Aliongeza hivi: “Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” Hiyo ni kwa sababu “mabwana” wote wawili wanataka tujitoe kikamili. Yesu alisema ama “[tutamchukia] mmoja na kumpenda yule mwingine” ama “[tutashikamana] na mmoja na kumdharau yule mwingine.” (Mt. 6:24) Kwa kuwa sisi ni wanadamu wasio wakamilifu, sote tunahitaji kujitahidi kupambana na “tamaa za mwili wetu,” kutia ndani kupenda vitu vya kimwili.—Efe. 2:3.

17. (a) Kwa nini ni vigumu kwa watu wa kimwili kusitawisha maoni yenye usawaziko kuhusu vitu vya kimwili? (b) Ni nini kinachotusaidia kupambana na tamaa ya kupenda vitu vya kimwili?

17 Ni vigumu kwa watu wa kimwili kusitawisha maoni yenye usawaziko kuhusu vitu vya kimwili. Kwa nini? Kwa sababu hisi zao za kiroho zimedhoofika. (Soma 1 Wakorintho 2:14.) Nguvu zao za utambuzi zinapopungua, inakuwa vigumu sana kwao kutofautisha lililo sawa na lililo kosa. (Ebr. 5:11-14) Matokeo ni kuwa baadhi yao huongozwa na tamaa ya vitu vya kimwili; tamaa ambayo haiwezi kamwe kutoshelezwa kikamili. (Mhu. 5:10) Jambo linalopendeza ni kwamba tunaweza kushinda mwelekeo wa kupenda vitu vya kimwili. Tunaweza kufanya hivyo kwa kusoma kwa ukawaida Neno la Mungu, Biblia. (1 Pet. 2:2) Kama ambavyo kutafakari kweli zinazotoka kwa Mungu kulimwimarisha Yesu kupinga kishawishi, ndivyo kutumia kanuni za Biblia kunavyotusaidia kupambana na tamaa ya kupenda vitu vya kimwili. (Mt. 4:8-10) Tunapofanya hivyo, tunamwonyesha Yesu kwamba tunampenda kuliko vitu vyovyote vya kimwili.

Unatanguliza nini maishani? (Tazama fungu la 18)

18. Umeazimia kufanya nini?

18 Yesu alipomwuliza Petro: “Je, unanipenda kuliko hawa?” alikuwa akimkumbusha uhitaji wa kutanguliza mambo ya kiroho maishani. Kwa hakika, Petro, ambaye jina lake linamaanisha “Kipande cha Mwamba,” aliishi kulingana na jina lake, kwa kuwa alikuwa imara na mwenye kutegemeka kama mwamba. (Mdo. 4:5-20) Sisi pia tumeazimia kuendelea kuwa imara katika upendo wetu kwa Kristo huku tukiwa na usawaziko kuelekea kazi ya kimwili, burudani, na vitu vya kimwili. Maamuzi yetu maishani na yaonyeshe kwamba tuna maoni kama ya Petro aliyemwambia hivi Yesu: “Bwana, unajua ninakupenda.”

^ fu. 14 Tazama makala “Je, Tafrija Unayochagua Inakujenga?” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2011, uku. 9-12, fu. 6-15.