Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Unanipenda Kuliko Hawa?”

“Unanipenda Kuliko Hawa?”

Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda kuliko hawa?YOHANA 21:15.

NYIMBO: 128, 45

1, 2. Kisha kupitisha usiku muzima katika kazi ya kuvua samaki, Petro alijifunza jambo gani?

WANAFUNZI saba wa Yesu wamepitisha usiku muzima katika kazi ya kuvua samaki katika Bahari ya Galilaya. Lakini hawapate hata samaki moja. Sasa ni asubuhi, na Yesu mwenye alifufuliwa anasimama pembeni ya bahari, na anawaangalia. Kisha anawaambia: “‘Mutupe wavu upande wa kuume wa mashua, nanyi mutapata.’ Basi wakautupa, lakini hawakuweza tena kuuvuta [kuukokota] ndani kwa sababu samaki walikuwa wengi sana.”—Yohana 21:1-6.

2 Yesu akapatia wanafunzi wake chakula cha asubuhi, ni kusema, mukate na samaki. Kisha akamugeukia Simoni Petro na kumuuliza hivi: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda kuliko hawa?” Yesu alijua kama Petro alikuwa anapenda kazi ya kuvua samaki. Inawezekana Yesu alikuwa anamuuliza Petro ikiwa anamupenda na kupenda mambo yenye alifundisha kuliko kazi ya kuvua samaki. Petro alimujibia Yesu hivi: “Bwana, unajua ninakupenda.” (Yohana 21:15) Kuanzia siku hiyo, Petro alionyesha kabisa kwamba alisema kweli. Alionyesha upendo wake kwa Kristo kwa kuendelea kuhubiri kwa bidii, na akakuwa mutu wa maana sana katika kutaniko la Kikristo.

3. Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu juu ya jambo gani?

3 Maneno yenye Yesu alimuambia Petro yanaweza kutufundisha nini? Tunapaswa kuwa waangalifu ili tusiruhusu upendo wetu kwa Kristo ukuwe zaifu. Yesu alijua kuwa maisha katika ulimwengu huu yangekuwa yenye kuchokesha akili na kwamba tungepatwa na mahangaiko na magumu mbalimbali. Katika mufano wake wa mupandaji wa mbegu, Yesu alisema kuwa watu fulani wangekubali “neno la Ufalme” na wangekuwa na bidii mwanzoni. Lakini kisha, “mahangaiko ya mufumo huu wa mambo nguvu za udanganyifu za utajiri” ‘zingelisonga neno,’ na watu hao wangepoteza bidii yao. (Mathayo 13:19-22; Marko 4:19) Ikiwa hatuko waangalifu, mahangaiko ya maisha ya kila siku yanaweza kutuzuia kuendelea kumutumikia Yehova. Kwa hiyo, Yesu alionya wanafunzi wake hivi: ‘Mujiangalie ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha.’—Luka 21:34.

4. Ni nini itatusaidia kujua ikiwa upendo wetu kwa Kristo ni wenye nguvu? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

4 Kama Petro, tunaweza kuonyesha kuwa tunamupenda Kristo kwa kutia kazi ya kuhubiri pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Namna gani tunaweza kuhakikisha kuwa tunaendelea kufanya hivyo? Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ni mambo gani yenye ninapenda sana katika maisha? Kazi ya Yehova ndiyo inaniletea furaha ao kazi zingine?’ Tuchunguze basi mambo tatu yenye yanaweza kuregeza upendo wetu kwa Kristo. Mambo hayo ni kazi ya kimwili, mambo ya kujifurahisha, na vitu vya kimwili.

ACHA KAZI YA KIMWILI PA NAFASI YAKE

5. Vichwa vya familia wako na daraka gani?

5 Petro hakukuwa anafanya kazi ya kuvua samaki ili kujifurahisha tu. Alikuwa anafanya kazi hiyo ili kutimiza mambo ya lazima ya watu wa familia yake. Leo pia, Yehova amepatia vichwa vya familia daraka la kutimizia watu wa familia zao mambo ya lazima. (1 Timotheo 5:8) Wanapaswa kutumika sana ili kutimiza daraka hilo. Hata hivyo, katika siku hizi za mwisho, kazi ya kimwili inaweza kuleta mahangaiko mengi sana.

6. Sababu gani kazi ya kimwili inaweza kuleta mahangaiko ya akili?

6 Mara nyingi kuko watu wengi wenye kutafuta kazi, lakini ni hesabu kidogo ya watu ndiyo wanapata kazi. Ndio sababu watu wanapiganisha sana ili kupata kazi. Wengi wanaona kuwa wanapaswa kutumika kisha saa za kazi, lakini mara nyingi wanalipwa feza kidogo. Kuliko wakati mwengine wowote, kompanyi zinajikaza kutengeneza vitu vingi kwa kutumia hesabu kidogo ya wafanyakazi. Kwa hiyo, wafanyakazi wanaweza kuwa na mahangaiko ya akili, kuchoka, ao hata kugonjwa. Watu wengi wanaogopa kuwa watapoteza kazi yao ikiwa hawafanye kila jambo lenye mukubwa wao wa kazi anawaomba.

7, 8. (a) Tuko washikamanifu zaidi kwa nani? (b) Ndugu mumoja wa Thailandi alijifunza jambo gani juu ya kazi yake ya kimwili?

7 Sisi Wakristo, tuko washikamanifu zaidi kwa Yehova kuliko mutu mwengine yeyote, kutia ndani mukubwa wetu wa kazi. (Luka 10:27) Kazi yetu ya kimwili inatusaidia kutimiza mambo yetu ya lazima na kututegemeza katika kazi yetu ya kuhubiri. Lakini ikiwa hatuko waangalifu, kazi yetu inaweza kutuzuia kuendelea kumuabudu Yehova. Mufano wa ndugu mumoja wa Thailandi unaweza kutufundisha jambo fulani. Alisema hivi: “Kazi yangu ya kimwili ya kutengeneza ordinatere ilikuwa yenye kupendeza sana, lakini iliniomba kutumika saa nyingi. Kwa hiyo, iliniachia wakati kidogo sana wa kufanya mambo ya kiroho. Mwishowe nilitambua kwamba ili nitie faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza katika maisha, nilipaswa kufanya kazi ingine.” Ndugu huyo alifanya nini?

8 Alieleza hivi: “Kisha kufanya mipango kwa mwaka moja hivi, niliamua kuuzisha kreme ya baridi kwenye barabara. Mwanzoni nilikuwa na tatizo la kupata feza na nilivunjika moyo. Wakati nilikuwa ninakutana na wafanyakazi wenzangu wa zamani, walinichekelea na kuniuliza sababu gani niliona kuwa ni muzuri zaidi kuuzisha kreme kuliko kufanya kazi ya kutengeneza ordinatere mahali kwenye kuwa hewa ya muzuri. Nilisali kwa Yehova ili anisaidie kupambana na hali hiyo na kufikia muradi wangu wa kuwa na wakati mwingi wa kufanya mambo ya kiroho. Kisha muda mufupi, mambo yalianza kuwa muzuri. Nilijua muzuri zaidi kreme ya baridi yenye watu walipenda na nikakuwa na ufundi zaidi wa kuitengeneza. Kisha muda mufupi, nilikuwa ninauzisha kreme yangu yote kwa siku moja. Kwa kweli, nilipata feza nyingi kuliko wakati nilikuwa ninafanya kazi ya kutengeneza ordinatere. Nimekuwa na furaha sana kwa sababu sina tena mahangaiko ya akili yenye nilikuwa nayo wakati nilikuwa ninafanya kazi yangu ya zamani. Na jambo la maana zaidi, sasa ninajisikia kuwa karibu zaidi na Yehova.”—Soma Mathayo 5:3, 6.

9. Namna gani tunaweza kuendelea kuwa na mawazo yenye kusawazika juu ya kazi ya kimwili?

9 Yehova anafurahi wakati tunatumika sana. Kutumika sana kunaleta faida. (Methali 12:14) Lakini tunapaswa kuhakikisha kuwa hatuone kazi yetu ya kimwili kuwa ya maana zaidi kuliko utumishi wetu kwa Yehova. Wakati alizungumuzia mambo ya lazima ya kimwili, Yesu alisema hivi: ‘Basi, muendelee kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake, nanyi mutaongezewa hivi vitu vingine vyote.’ (Mathayo 6:33) Lakini namna gani tunaweza kujua ikiwa tuko na mawazo yenye kusawazika juu ya kazi ya kimwili? Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ninaona kazi yangu ya kimwili kuwa ya muzuri na yenye kuniletea furaha lakini ninaona utumishi wangu kwa Mungu kuwa jambo la kawaida tu na wenye kuchokesha?’ Kufikiria ulizo hili kunaweza kutusaidia kuona waziwazi ni mambo gani yenye tunapenda kabisa.

10. Yesu alifundisha jambo gani la maana?

10 Yesu alitufundisha jambo lenye tunapaswa kutia pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Wakati fulani, alitembelea dada wawili, ni kusema, Maria na Martha. Palepale, Martha alianza kumutayarishia chakula, lakini Maria alikaa pembeni ya Yesu na kusikiliza mafundisho yake. Martha alianza kunungunika kuwa Maria hakumusaidia. Yesu alimuambia Martha hivi: ‘Maria alichagua fungu njema, nalo halitaondolewa kwake.’ (Luka 10:38-42) Hapo, Yesu alifundisha jambo la maana. Ili tuepuke kukengeushwa na mahitaji yetu na kuonyesha kuwa tunamupenda Kristo, tunapaswa kuchagua ‘fungu njema.’ Hilo linamaanisha kwamba sikuzote urafiki wetu pamoja na Yehova unapaswa kuwa jambo la maana zaidi katika maisha yetu.

MAWAZO YETU JUU YA MAMBO YA KUJIFURAHISHA

11. Biblia inasema nini juu ya kupumuzika na kujifurahisha?

11 Tunafanya mambo mengi katika maisha; kwa hiyo, wakati fulani tuko na lazima ya kupumuzika na kujifurahisha. Biblia inasema hivi: ‘Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba akule, naam, akunywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.’ (Mhubiri 2:24) Yesu alijua kama lilikuwa jambo la lazima wanafunzi wake wapumuzike. Kwa mufano, kisha wanafunzi wake kutumika sana katika kazi ya kuhubiri, Yesu aliwaambia hivi: ‘Mukuje, ninyi wenyewe, faragani [nafasi ya siri] katika mahali pasipo na watu mupumuzike kidogo.’—Marko 6:31, 32.

12. Sababu gani tunapaswa kuwa waangalifu juu ya mambo ya kujifurahisha? Toa mufano.

12 Mambo ya kujifurahisha yanaweza kutusaidia tupumuzike na kujisikia muzuri. Lakini tunapaswa kuwa waangalifu ili kujifurahisha kusikuwe jambo la maana zaidi katika maisha yetu. Wakati wa mitume, watu wengi walikuwa na mawazo haya: ‘Tukule na tukunywe, kwa maana kesho tutakufa.’ (1 Wakorintho 15:32) Leo pia, watu wengi wako na mawazo kama hayo. Kwa mufano, kijana mumoja katika Ulaya ya Mangaribi alianza kuenda kwenye mikutano ya Kikristo. Kwa sababu alipenda sana mambo ya kujifurahisha, aliacha kujiunga pamoja na Mashahidi wa Yehova. Lakini, kisha alitambua kama alikuwa amepata matatizo mengi kwa sababu ya kupenda sana mambo ya kujifurahisha. Alianza kujifunza tena Biblia, na kisha wakati fulani, alianza kuhubiri habari njema. Kisha kubatizwa, alisema hivi: “Jambo moja tu lenye kunihuzunisha ni kwamba nilipoteza wakati mwingi mbele nielewe kama kumutumikia Yehova kunaleta furaha nyingi zaidi kuliko kufuatilia mambo ya kujifurahisha ya ulimwengu huu.”

13. (a) Sababu gani haiko muzuri kupitisha saa nyingi katika mambo ya kujifurahisha? Toa mufano. (b) Ni nini inaweza kutusaidia tukuwe na mawazo yenye kusawazika juu ya mambo ya kujifurahisha?

13 Mambo ya kujifurahisha yanapaswa kutusaidia tujisikie muzuri na kupata tena nguvu. Kwa hiyo, tunapaswa kutumia muda gani katika mambo ya kujifurahisha? Ili kujibia ulizo hilo, tufikirie mufano huu. Watu wengi wanapenda kula keki ao bonbon. Lakini tunajua kuwa ikiwa tunakula vyakula hivyo wakati wote, vinaweza kuharibu afya yetu. Ikiwa tunapenda kuwa na afya ya muzuri, tunapaswa kula chakula chenye kujenga mwili wetu. Vilevile, ikiwa tunatumia wakati mwingi ili kujifurahisha, hilo linaweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. Ni nini inaweza kutusaidia kujua ikiwa tuko na mawazo yenye kusawazika juu ya mambo ya kujifurahisha ao hapana? Jambo moja lenye tunaweza kufanya ni kuchagua juma moja na kuandika saa zenye tulipitisha katika mambo yenye kuhusu utumishi wetu kwa Yehova kama vile, mikutano ya Kikristo, kazi ya kuhubiri, na kujifunza Biblia. Kisha tunaweza kuandika saa zenye tulipitisha katika mambo ya kujifurahisha katika juma hilo, kama vile michezo, kuangalia televizyo, ao kucheza michezo ya video. Wakati tunalinganisha saa hizo, tunajifunza nini? Tuko na lazima ya kufanya mabadiliko?—Soma Waefeso 5:15, 16.

14. Ni nini inaweza kutusaidia kuchagua muzuri mambo ya kujifurahisha?

14 Yehova anaturuhusu tuchague sisi wenyewe mambo ya kujifurahisha, na vichwa vya familia wanaweza kuchagulia watu wa familia zao. Katika Biblia, Yehova ametupatia kanuni zenye kutuonyesha mawazo yake. Kanuni hizo zinatusaidia kukamata maamuzi ya muzuri. * (Soma maelezo ya chini.) Mambo ya muzuri ya kujifurahisha ni “zawadi ya Mungu.” (Mhubiri 3:12, 13) Ni kweli kwamba watu mbalimbali wanapenda aina mbalimbali ya mambo ya kujifurahisha. (Wagalatia 6:4, 5) Lakini, tunapaswa kuwa waangalifu wakati tunachagua aina yoyote ya mambo ya kujifurahisha. Yesu alisema hivi: “Mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.” (Mathayo 6:21) Upendo wetu kwa Mufalme wetu Yesu, unatuchochea tuwaze, tuseme, na kutenda katika njia yenye kuonyesha kuwa Ufalme ndio wa maana zaidi kwetu kuliko kitu kingine chochote.​—Wafilipi 1:9, 10.

KUPIGANISHA TAMAA YA KUPENDA VITU VYA KIMWILI

15, 16. (a) Namna gani kupenda vitu vya kimwili kunaweza kuwa mutego kwetu? (b) Yesu alitoa shauri gani la hekima juu ya vitu vya kimwili?

15 Watu wengi wanafikiri kama wanapaswa kuwa na vitu kama vile nguo, telefone, na ordinatere za sasa. Wanapenda sana vitu vya kimwili na hilo linafanya waone kuwa vitu na feza ndiyo mambo ya maana sana kuliko mambo mengine yote katika maisha. Wewe Mukristo, ni mambo gani yenye kuwa ya maana zaidi kwako? Ujiulize hivi: ‘Ninatumia wakati mwingi zaidi ili kufikiria motokari ao aina fulani ya manguo ya sasa kuliko wakati wenye ninatumia ili kutayarisha mikutano ya kutaniko? Ninatumia wakati mwingi katika kazi za kila siku mupaka ninabakia na wakati kidogo wa kusali na kusoma Biblia?’ Ikiwa hatuko waangalifu, kupenda vitu vya kimwili kunaweza kuwa jambo la maana zaidi kuliko upendo wetu kwa Kristo. Tunapaswa kufikiria maneno haya ya Yesu: ‘Mujilinde na kila namna ya tamaa.’ (Luka 12:15) Sababu gani alisema hivyo?

16 Yesu alisema kuwa “hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.” Aliongezea hivi: ‘Hamuwezi kutumikia Mungu na Utajiri.’ Haiwezekane tumutumikie Yehova kwa uwezo wetu wote na wakati huohuo tukaze akili yetu juu ya vitu vya kimwili. Yesu alieleza kama ‘ama tutamuchukia mumoja na kumupenda yule mwingine’ ao ‘tutashikamana na mumoja na kumuzarau yule mwingine.’ (Mathayo 6:24) Kwa sababu hatukamilike, tunapaswa kuendelea kupiganisha “tamaa za mwili,” kutia ndani tamaa ya kupenda vitu vya kimwili.​—Waefeso 2:3.

17. (a) Sababu gani watu wanaona kuwa ni vigumu kuwa na mawazo yenye kusawazika juu ya vitu vya kimwili? (b) Ni nini inatusaidia kupiganisha tamaa ya kupenda vitu vya kimwili?

17 Watu wengi wanakaza sana akili zao juu ya tamaa zao wenyewe na mambo ya kujifurahisha mupaka wanaona kuwa ni vigumu kuwa na mawazo yenye kusawazika juu ya vitu vya kimwili. (Soma 1 Wakorintho 2:14.) Kwa sababu hawafikiri muzuri kabisa, inaweza kuwa vigumu kwao kutofautisha mambo ya muzuri na ya mubaya. (Waebrania 5:11-14) Tamaa yao ya kupenda vitu vya kimwili inaweza kuendelea kuongezeka zaidi. Na hawatosheke, wanapenda kupata vitu vingi zaidi na zaidi. (Mhubiri 5:10) Lakini kuko jambo fulani lenye tunaweza kufanya ili kupiganisha mawazo hayo. Kusoma kwa ukawaida Neno la Mungu kutatutia nguvu ili tuweze kupiganisha tamaa ya kupenda vitu vya kimwili. (1 Petro 2:2) Yesu alifikiri sana juu ya hekima ya Yehova, na hilo lilimusaidia kupinga majaribu ya Shetani. (Mathayo 4:8-10) Leo pia, ikiwa tunapenda kupinga tamaa ya kupenda vitu vya kimwili, tunapaswa kutumikisha hekima ya Yehova katika maisha yetu. Ikiwa tunafanya hivyo, Yesu ataona kuwa tunamupenda zaidi kuliko vitu vya kimwili.

Ni mambo gani yenye kuwa ya maana zaidi katika maisha yako? (Picha hii inapatana na fungu la 18)

18. Umeazimia kufanya nini?

18 Wakati Yesu alimuuliza Petro hivi: “Je, unanipenda kuliko hawa?” alikuwa anafundisha Petro kama anapaswa kutia utumishi wake kwa Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yake. Inafurahisha kujua kama jina la Petro linamaanisha “Kipande cha Jiwe.” Sifa za muzuri za Petro zinaweza kulinganishwa na jiwe. (Matendo 4:5-20) Leo, sisi pia tunataka upendo wetu kwa Kristo ukuwe wenye nguvu. Kwa hiyo, tunapenda kuhakikisha kuwa kazi ya kimwili, mambo ya kujifurahisha, na vitu vya kimwili havichukue nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Kisha, kama Petro itakuwa kama vile tunasema hivi: “Bwana, unajua ninakupenda.”

^ fu. 14 Soma habari “Je, Tafrija Unayochagua Inakujenga?” katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 10, 2011, ukurasa wa 9-12, fungu la 6-15.