Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Gayo Alivyowasaidia Ndugu Zake

Jinsi Gayo Alivyowasaidia Ndugu Zake

MWISHONI mwa karne ya kwanza, Gayo na Wakristo wengine walikabili changamoto mbalimbali. Watu waliokuwa wakieneza mafundisho ya uwongo walikuwa wakijaribu kudhoofisha na kugawanya makutaniko. (1 Yoh. 2:18, 19; 2 Yoh. 7) Mwanamume fulani aliyeitwa Diotrefe, alikuwa akipiga “porojo” kumhusu mtume Yohana na wengine, akikataa kuwaonyesha ukarimu waangalizi wanaosafiri, na akijaribu kuwashawishi wengine waige mfano wake. (3 Yoh. 9, 10) Hali ilikuwa hivyo Yohana alipomwandikia Gayo. Barua hiyo ya mtume Yohana iliyoandikwa 98 W.K. hivi, inajulikana katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuwa “Barua ya Tatu ya Yohana.”

Licha ya hali ngumu alizokabili, Gayo aliendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Alionyeshaje uaminifu? Kwa nini tungependa kuiga mfano wa Gayo? Barua ya Yohana inaweza kutusaidiaje kufanya hivyo?

BARUA KWA RAFIKI MPENDWA

Mwandikaji wa Yohana ya Tatu anajiita “mwanamume mzee.” Utangulizi huo ulimsaidia mwanaye mpendwa wa kiroho, Gayo, kutambua kwamba ni mtume Yohana. Kwa upendo, Yohana alimrejelea Gayo kuwa “mpendwa, ambaye mimi nampenda kweli.” Kisha Yohana akasema kwamba anatumaini Gayo ana afya nzuri ya kimwili kama alivyokuwa na hali nzuri kiroho. Ni wazi kwamba alimpenda na kumsifu!—3 Yoh. 1, 2, 4.

Inawezekana Gayo alikuwa mzee wa kutaniko, lakini barua hiyo haisemi hivyo kihususa. Yohana alimsifu Gayo kwa kuwakaribisha akina ndugu ingawa hakuwafahamu. Yohana aliona jambo hilo kuwa uthibitisho kwamba Gayo alikuwa mwaminifu, kwa kuwa sikuzote ukarimu huwatambulisha watumishi wa Mungu.—Mwa. 18:1-8; 1 Tim. 3:2; 3 Yoh. 5.

Yohana alithamini ukarimu ambao Gayo aliwaonyesha akina ndugu, na maneno yake yanathibitisha kwamba Wakristo walisafiri mara nyingi kutoka mahali ambapo Yohana aliishi kwenda kwenye makutaniko mbalimbali, na inaonekana wasafiri hao walimwambia Yohana kuhusu safari zao. Inaelekea Yohana alipata habari kuhusu makutaniko kwa njia hiyo.

Kwa kweli, waangalizi wanaosafiri walipenda kuishi na waamini wenzao. Nyumba za wageni zilikuwa na sifa mbaya sana, ziliwahudumia watu vibaya, na zilikuwa na upotovu mwingi wa maadili. Kwa hiyo, ilipowezekana, wasafiri wenye hekima waliishi na rafiki zao na waangalizi wanaosafiri waliishi na Wakristo wenzao.

“WALISAFIRI KWA AJILI YA JINA LAKE”

Yohana alimtia moyo Gayo aonyeshe tena ukarimu kwa kumwambia “[aishughulikie safari ya wasafiri hao] kwa namna inayomfaa Mungu.” Kufanya hivyo kulimaanisha angehitaji kuwaandalia mahitaji yao walipokuwa safarini hadi wafike eneo walilokuwa wakienda. Ilikuwa wazi kwamba Gayo alikuwa akiwafanyia hivyo wageni waliokuwa wakimtembelea, kwa kuwa walimweleza Yohana kwamba Gayo alikuwa mwenye upendo na imani.—3 Yoh. 3, 6.

Huenda wageni hao walikuwa wamishonari, wajumbe wa Yohana, au waangalizi wanaosafiri. Vyovyote vile, walisafiri ili waeneze habari njema. Yohana alisema hivi: “Walisafiri kwa ajili ya jina lake.” (3 Yoh. 7) Yohana alikuwa ametoka tu kumtaja Mungu (tazama mstari wa 6), kwa hiyo inaonekana maneno “kwa ajili ya jina lake” yanarejelea jina Yehova. Hivyo, ndugu hao walikuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo na walistahili kukaribishwa kwa uchangamfu. Ni kama Yohana alivyoandika: “Sisi tuna wajibu wa kuwakaribisha watu wa namna hiyo, ili tuwe wafanyakazi wenzi katika kweli.”—3 Yoh. 8.

MSAADA KUHUSU HALI FULANI NGUMU

Yohana hakumwandikia Gayo ili kumshukuru tu. Alitaka pia kumsaidia ashughulikie tatizo fulani zito. Kwa sababu fulani, mshiriki mmoja wa kutaniko la Kikristo aliyeitwa Diotrefe hakutaka kuwaonyesha ukarimu waangalizi wanaosafiri. Hata alijaribu kuwazuia wengine wasionyeshe ukarimu. —3 Yoh. 9, 10.

Hapana shaka kwamba Wakristo waaminifu hawangependa kuishi na Diotrefe hata ikiwa wangeweza kufanya hivyo. Alipenda kuwa na mahali pa kwanza kutanikoni, hakupokea kwa heshima jambo lolote kutoka kwa Yohana, na alipiga porojo kuhusu mtume huyo na wengine. Ingawa Yohana hakuwahi kumwita mwalimu wa uwongo, Diotrefe alipinga mamlaka yake. Tamaa ya Diotrefe ya kujitafutia makuu na mtazamo wake usio wa Kikristo ulifanya ushikamanifu wake utiliwe shaka. Kisa cha Diotrefe kinaonyesha roho ya mgawanyiko ambayo watu wenye kujitafutia makuu na wenye majivuno wanaweza kuleta kutanikoni. Kwa hiyo, Yohana alimwambia Gayo maneno haya ambayo pia yanahusu kila mmoja wetu: “Uwe mwigaji, si wa yaliyo mabaya.”—3 Yoh. 11.

SABABU NZURI SANA YA KUFANYA MEMA

Tofauti na Diotrefe, Mkristo anayeitwa Demetrio anatajwa na Yohana kuwa mfano mzuri. Yohana aliandika hivi: “Kila mtu anamsifu Demetrio . . . Nasi pia tunatoa ushahidi wetu juu yake, nawe wajua kwamba tunachosema ni kweli.” (3 Yoh. 12, Biblia Habari Njema.) Inawezekana kwamba Demetrio alihitaji msaada wa Gayo, na inaelekea Barua ya Tatu ya Yohana ilitumiwa kumtambulisha na kumpendekeza. Huenda Demetrio mwenyewe ndiye aliyempa Gayo barua hiyo. Kwa kuwa alikuwa mjumbe wa Yohana, au mwangalizi anayesafiri, inaelekea Demetrio alithibitisha kile ambacho Yohana aliandika.

Kwa nini Yohana alimhimiza Gayo aendelee kuonyesha ukarimu ijapokuwa tayari alikuwa akifanya hivyo? Je, Yohana aliona uhitaji wa kumwimarisha Gayo ili aendelee kuwa jasiri? Je, mtume huyo aliogopa kwamba huenda Gayo angesita kuonyesha ukarimu kwa sababu Diotrefe alikuwa akijaribu kuwaondoa Wakristo wakarimu nje ya kutaniko? Vyovyote vile, Yohana alimhakikishia hivi Gayo: “Yeye ambaye hutenda mema anatokana na Mungu.” (3 Yoh. 11) Hiyo ni sababu nzuri sana ya kuendelea kutenda mema.

Je, barua ya Yohana ilimchochea Gayo kuendelea kuwa mkarimu? Inaonekana ilifanya hivyo kwa kuwa Barua ya Tatu ya Yohana ilihifadhiwa katika rekodi za Biblia na ilitumiwa kuwatia moyo wengine ‘wawe waigaji wa yaliyo mema.’

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KATIKA BARUA YA TATU YA YOHANA

Hatuna habari zaidi kumhusu Gayo, ndugu yetu mpendwa wa nyakati za kale. Lakini tunajifunza mambo kadhaa kwa kuchunguza habari hizo chache kuhusu maisha yake.

Tunaweza kufuataje “mwendo wa ukaribishaji-wageni”?

Kwanza, huenda wengi wetu tumepata ujuzi wa kweli kupitia waaminifu ambao walikuwa tayari kusafiri ili kutufundisha Biblia. Ni kweli kwamba si washiriki wote wa kutaniko la Kikristo leo wanaosafiri mbali ili kueneza habari njema. Hata hivyo, kama Gayo, kwa njia moja ama nyingine tunaweza kuwategemeza na kuwatia moyo wale wanaosafiri, kama vile mwangalizi wa mzunguko na mke wake. Au tunaweza kuwategemeza ndugu na dada wanaohamia maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme katika nchi yao, au hata nje ya nchi. Kwa hiyo, acheni “[tufuate] mwendo wa ukaribishaji-wageni.”—Rom. 12:13; 1 Tim. 5:9, 10.

Pili, hatupaswi kushangaa ikiwa kwa nadra watu fulani wanapinga mamlaka kutanikoni leo. Mamlaka ya Yohana ilipingwa na vilevile mamlaka ya mtume Paulo. (2 Kor. 10:7-12; 12:11-13) Hivyo basi, tunapaswa kutendaje tunapokabili hali kama hiyo kutoka kwa baadhi ya watu kutanikoni? Paulo alimshauri hivi Timotheo: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, mwenye sifa za kustahili kufundisha, akiendelea kujizuia chini ya uovu, akiwafundisha kwa upole wale wasio na mwelekeo unaofaa.” Tunapodumisha upole hata tunapochokozwa, huenda watu fulani wanaochambua mamlaka wakabadili mtazamo wao. Na huenda Yehova “akawapa toba inayoongoza kwenye ujuzi sahihi juu ya kweli.”—2 Tim. 2:24, 25.

Tatu, Wakristo wenzetu wanaomtumikia Yehova kwa ushikamanifu licha ya upinzani wanahitaji kuthaminiwa na kupongezwa kwa uchangamfu kwa sababu ya uaminifu wao. Ni wazi kuwa mtume Yohana alimtia moyo Gayo na kumhakikishia kwamba alikuwa akifanya yaliyo sawa. Vivyo hivyo leo, wazee wa kutaniko wanapaswa kufuata mfano wa Yohana kwa kuwatia moyo ndugu na dada zao ili ‘wasizimie.’—Isa. 40:31; 1 The. 5:11.

Barua ya Yohana kwa Gayo ndiyo kitabu kifupi zaidi katika Biblia, chenye maneno 219 tu katika Kigiriki. Hata hivyo, ni chenye thamani kubwa kwelikweli kwa Wakristo leo.