Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Weka Moyo Wako Juu ya Hazina za Kiroho

Weka Moyo Wako Juu ya Hazina za Kiroho

“Mahali ilipo hazina yenu, hapo pia mioyo yenu itakuwapo.” —LUKA 12:34.

NYIMBO: 76, 59

1, 2. (a) Yehova ametupatia hazina zipi tatu za kiroho? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

YEHOVA ndiye tajiri zaidi ulimwenguni. (1 Nya. 29:11, 12) Kwa kuwa yeye ni Baba mkarimu, anawaandalia kwa wingi utajiri wa kiroho wale wote wanaotambua thamani kubwa ya utajiri huo. Tunathamini sana kwamba Yehova ametupatia hazina za kiroho zinazotia ndani (1) Ufalme wa Mungu, (2) huduma yetu inayookoa uhai, na (3) kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno lake! Lakini tusipokuwa waangalifu, tunaweza kuacha kuthamini hazina hizo, na kwa njia hiyo tukazitupa. Ili tusizipoteze, tunapaswa kuzitumia vizuri na kuendelea kusitawisha upendo wetu kuzielekea. Yesu alisema hivi: “Mahali ilipo hazina yenu, hapo pia mioyo yenu itakuwapo.”—Luka 12:34.

2 Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kusitawisha na kudumisha upendo kuelekea Ufalme, huduma, na kweli na kuonyesha kuwa tunazithamini. Tunapochunguza mambo hayo, tafakari jinsi wewe binafsi unavyoweza kuongeza kina cha upendo wako kwa hazina hizo za kiroho.

UFALME WA MUNGU NI KAMA LULU YENYE THAMANI KUBWA

3. Mwanabiashara katika mfano wa Yesu alikuwa tayari kufanya nini ili apate lulu yenye thamani kubwa? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Soma Mathayo 13:45, 46. Yesu alitoa mfano wa mwanabiashara aliyekuwa akitafuta lulu. Hapana shaka kwamba kwa miaka mingi, mwanabiashara huyo alikuwa amenunua na kuuza lulu nyingi. Lakini sasa alikuwa amepata lulu moja iliyokuwa ya pekee sana hivi kwamba alishangilia moyoni alipoiona. Hata hivyo, ili ainunue angehitaji kuuza vitu vyote alivyokuwa navyo. Je, unaweza kuwazia jinsi lulu hiyo ilivyokuwa yenye thamani kwake?

4. Ikiwa tunapenda Ufalme wa Mungu kama mwanabiashara alivyoipenda lulu, tutafanya nini?

4 Tunajifunza nini? Kweli ya Ufalme wa Mungu ni kama lulu hiyo yenye thamani kubwa. Ikiwa tutapenda kweli ya Ufalme wa Mungu kama mwanabiashara alivyopenda lulu, tutakuwa tayari kuacha kitu chochote ili tuwe raia wa Ufalme na kuendelea kudumisha uraia huo. (Soma Marko 10:28-30.) Fikiria watu wawili waliofanya hivyo.

5. Zakayo alikuwa tayari kufanya nini kwa ajili ya Ufalme wa Mungu?

5 Zakayo alikuwa mkuu wa wakusanya-kodi ambaye alijikusanyia utajiri kwa kuwapunja watu. (Luka 19:1-9) Lakini mtu huyo ambaye hakuwa mwadilifu alipomsikia Yesu akihubiri kuhusu Ufalme, alitambua thamani kubwa ya kile alichokuwa akisikia na akachukua hatua mara moja. Alisema hivi: “Tazama! Nusu ya mali zangu, Bwana, mimi nitawapa maskini, na chochote nilichomnyang’anya mtu yeyote kwa shtaka la uwongo nitarudisha mara nne.” Alirudisha kwa hiari utajiri aliokuwa amepata kwa njia isiyo halali na akaacha kuwa na pupa ya vitu vya kimwili.

6. Rose alifanya mabadiliko gani ili awe raia wa Ufalme wa Mungu, na kwa nini?

6 Miaka kadhaa iliyopita, mwanamke fulani tutakayemwita Rose alikuwa katika uhusiano wa kimapenzi na mwanamke mwenzake aliposikia ujumbe wa Ufalme. Alikuwa rais wa shirika linalopigania haki za mashoga. Hata hivyo, kadiri Rose alivyojifunza Biblia, ndivyo alivyotambua thamani kubwa ya kweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Lakini alitambua kwamba angehitaji kufanya mabadiliko makubwa. (1 Kor. 6:9, 10) Moyo wake ulimchochea kujiuzulu kama rais na kusitisha uhusiano na huyo mwanamke. Rose alibatizwa mwaka 2009, na mwaka uliofuata, akaanza kutumikia akiwa painia wa kawaida. Upendo wake kwa Yehova na kwa Ufalme wake ulikuwa wenye nguvu kuliko tamaa yoyote ya kimwili.—Marko 12:29, 30.

7. Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuupenda Ufalme wa Mungu kwa moyo wetu wote?

7 Ni kweli kwamba wengi wetu tumefanya mabadiliko makubwa maishani ili tuwe raia wa Ufalme wa Mungu. (Rom. 12:2) Hata hivyo, tunahitaji kuendelea kufanya mabadiliko zaidi. Ni lazima tuwe macho kuhusiana na vitu ambavyo vinaweza kuteka hisia zetu, kutia ndani tamaa ya vitu vya kimwili na tamaa yoyote ya maadili mapotovu kingono. (Met. 4:23; Mt. 5:27-29) Ili tuendelee kuupenda Ufalme wa Mungu kwa moyo wetu wote, Yehova ametupatia hazina nyingine yenye thamani kubwa.

HUDUMA YETU INAYOOKOA UHAI

8. (a) Kwa nini mtume Paulo alifafanua huduma yetu kuwa “hazina . . . katika vyombo vya udongo”? (b) Paulo alionyeshaje kwamba aliiona huduma yake kuwa yenye thamani?

8 Kumbuka kwamba Yesu ametupatia mgawo wa kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 28:19, 20) Mtume Paulo alitambua jinsi huduma ilivyo na thamani kubwa. Alifafanua huduma ya agano jipya kuwa “hazina . . . katika vyombo vya udongo.” (2 Kor. 4:7; 1 Tim. 1:12) Ijapokuwa sisi ni vyombo vya udongo visivyo vikamilifu, ujumbe tunaohubiri unaweza kutusaidia sisi na wale wanaotusikiliza kupata uzima wa milele. Akijua hilo, Paulo alisema hivi: “Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.” (1 Kor. 9:23) Naam, kupenda huduma kulimchochea Paulo kuwa na bidii ya kufanya wanafunzi. (Soma Waroma 1:14, 15; 2 Timotheo 4:2.) Hilo lilimsaidia avumilie upinzani mkali. (1 The. 2:2) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaipenda huduma kama Paulo?

9. Taja baadhi ya njia ambazo tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini huduma.

9 Njia moja ambayo Paulo alionyesha kwamba alithamini huduma ni kwa kuwa macho kutambua fursa za kuzungumza na wengine. Kama mitume na Wakristo wa mapema, tunahubiri isivyo rasmi, hadharani, na nyumba kwa nyumba. (Mdo. 5:42; 20:20) Kadiri hali zetu zinavyoruhusu, tunatafuta fursa za kupanua huduma yetu labda kwa kutumikia tukiwa mapainia wasaidizi au wa kawaida. Pia, tunaweza kujifunza lugha nyingine, kuhamia eneo lingine katika nchi yetu, au kuhamia nchi nyingine.—Mdo. 16:9, 10.

10. Irene alipata baraka gani kwa kuazimia kueneza habari njema?

10 Fikiria mfano wa Irene, dada mseja nchini Marekani. Alitamani sana kuwahubiria wahamiaji waliozungumza Kirusi. Alipoanza kuwahubiria mwaka 1993, kulikuwa na wahubiri 20 tu waliokuwa katika kikundi cha Kirusi jijini New York City. Irene amehubiri kwa bidii katika lugha hiyo kwa miaka 20 hivi. Anakiri hivi: “Bado sizungumzi Kirusi vizuri.” Hata hivyo, Yehova amebariki bidii yake na ya wengine walio kama yeye. Leo, kuna makutaniko sita ya Kirusi jijini New York City. Watu 15 kati ya wale ambao Irene alijifunza nao Biblia wamebatizwa. Baadhi yao ni Wanabetheli, mapainia, na wazee. Irene anasema hivi: “Ninapofikiria malengo ambayo ningefuatia, siwezi kuwazia lengo lingine ambalo lingeniletea shangwe zaidi.” Naam, anaiona huduma yake kuwa yenye thamani!

Je, unaiona huduma yako kuwa hazina na kuonyesha hivyo katika ratiba yako ya kila juma? (Tazama fungu la 11 na 12)

11. Kunaweza kuwa na matokeo gani mazuri tunapoendelea kuhubiri licha ya mnyanyaso?

11 Ikiwa tunaiona huduma yetu kuwa yenye thamani, tutamwiga mtume Paulo kwa kuendelea kuhubiri licha ya mnyanyaso. (Mdo. 14:19-22) Katika miaka ya 1930 na mapema 1940, ndugu zetu nchini Marekani walikabili upinzani mkali sana. Lakini kama Paulo, walibaki imara na kuendelea kuhubiri. Ili kulinda haki yetu ya kuhubiri, ndugu hao walichukua hatua za kisheria mara nyingi. Katika 1943, Ndugu Nathan H. Knorr, alisema hivi alipokuwa akizungumzia ushindi wa kesi fulani katika Mahakama Kuu ya Marekani: “Tumeshinda kwa sababu mliendelea kupambana. Ikiwa mhubiri hangeendelea kuhubiri, hakungekuwa na kesi yoyote katika Mahakama Kuu; lakini mnyanyaso haufanikiwi kwa sababu wewe mhubiri, na ndugu ulimwenguni pote, mnaendelea kuhubiri bila kuacha. Ushindi huo umetolewa kwa sababu watu wa Bwana wameendelea kusimama imara.” Msimamo huo imara wa ndugu zetu katika nchi mbalimbali umetokeza ushindi kama huo. Naam, tunaweza kushinda mnyanyaso kwa kupenda huduma.

12. Umeazimia kufanya nini kuhusiana na huduma yako?

12 Tunapoiona huduma kuwa hazina yenye thamani kubwa kutoka kwa Yehova, hatutaridhika tu na “kuhesabu saa.” Badala yake, tutafanya yote tuwezayo “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.” (Mdo. 20:24; 2 Tim. 4:5) Lakini tutawafundisha watu wengine nini? Fikiria hazina hii nyingine kutoka kwa Mungu.

HAZINA YETU YA KWELI ZILIZOFUNULIWA

13, 14. “Hazina” ambayo Yesu alitaja katika Mathayo 13:52 ni nini, na tunaweza kuijaza jinsi gani?

13 Hazina ya tatu ya kiroho ni hifadhi yetu ya kweli zilizofunuliwa. Yehova ni Mungu wa kweli. (2 Sam. 7:28; Zab. 31:5) Kwa kuwa yeye ni Baba mkarimu, anawafunulia kweli wale wanaomwogopa. Tangu tuliposikia kweli kwa mara ya kwanza, tumekuwa na fursa za kukusanya kweli kutoka Neno lake, Biblia, machapisho ya Kikristo, makusanyiko, na mikutano yetu ya kila juma. Baada ya muda, tunakuwa na kile ambacho Yesu anafafanua kuwa “hazina” ya kweli mpya na za zamani. (Soma Mathayo 13:52.) Yehova atatusaidia kukusanya kweli mpya zenye thamani katika “hazina” yetu ikiwa tutazitafuta kama hazina zilizofichika. (Soma Methali 2:4-7.) Tunafanyaje hivyo?

14 Tunapaswa kusitawisha mazoea mazuri ya kujifunza kibinafsi na kufanya utafiti kwa makini katika Neno la Mungu na machapisho yetu. Kufanya hivyo kutatusaidia kugundua kweli “mpya” katika maana ya kwamba hatukuzijua mwanzoni. (Yos. 1:8, 9; Zab. 1:2, 3) Toleo la kwanza kabisa la gazeti hili lililochapishwa Julai 1879, lilisema hivi: “Kama ua dogo katika jangwa la maisha, kweli imezungukwa na hata kukaribia kusongwa na magugu mengi ya makosa. Ili uipate ni lazima uwe macho wakati wote. . . . Ili uipate ni lazima uiname kuichukua. Usiridhike na ua moja la kweli. . . . Endelea kukusanya, tafuta mengine zaidi.” Naam, tunapaswa kuwa na hamu ya kujaza hazina yetu kweli zinazotoka kwa Mungu.

15. Kwa nini tunaweza kurejelea kweli fulani kuwa za “zamani,” na wewe binafsi unathamini kweli zipi hasa?

15 Tuligundua baadhi ya kweli zenye thamani tulipoanza kushirikiana na watu wa Mungu. Tunaweza kusema kweli hizo ni za “zamani” kwa kuwa tumezijua na kuzithamini tangu mwanzo wa mwendo wetu wa Kikristo. Kweli hizo zenye thamani zinatia ndani nini? Tulijifunza kuwa Yehova ndiye Muumba wetu na Mpaji-Uhai na kwamba ana kusudi kwa wanadamu. Pia, tulijifunza kuwa Mungu alichochewa na upendo kumtoa Mwana wake kuwa fidia ili tuwekwe huru kutokana na dhambi na kifo. Vilevile, tulijifunza kuwa Ufalme wake utakomesha kila namna ya kuteseka na kwamba tuna tumaini la kuishi milele kwa amani na furaha chini ya utawala wa Ufalme.—Yoh. 3:16; Ufu. 4:11; 21:3, 4.

16. Tunahitaji kufanya nini tunapopata uelewaji mpya wa kweli?

16 Mara kwa mara, huenda uelewaji wetu wa unabii wa Biblia au Maandiko fulani ukarekebishwa. Tunapopata uelewaji mpya, tunapaswa kutumia wakati kujifunza habari hiyo kwa makini na kuitafakari. (Mdo. 17:11; 1 Tim. 4:15) Tunajitahidi kuelewa vizuri si tu mabadiliko makubwa kati ya uelewaji wetu wa zamani na uelewaji wetu mpya, bali pia mabadiliko madogo-madogo. Tukifanya hivyo, tutafanikiwa kuiweka kweli mpya mahali salama ndani ya hazina yetu. Kwa nini jitihada hizo ni muhimu?

17, 18. Roho takatifu inaweza kutusaidiaje?

17 Yesu alifundisha kwamba roho ya Mungu inaweza kutukumbusha yale tuliyojifunza. (Yoh. 14:25, 26) Roho hiyo inaweza kutusaidiaje tukiwa wafundishaji wa watu wote wa habari njema? Fikiria mfano wa ndugu anayeitwa Peter. Katika 1970 akiwa na umri wa miaka 19, alikuwa Mwanabetheli mpya katika Betheli ya Uingereza. Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, alikutana na mwanamume wa umri wa makamo mwenye ndevu nyingi. Peter alimwuliza mwanamume huyo ikiwa angependa kuelewa Biblia. Akiwa ameshtuka kidogo, mwanamume huyo alimjibu kwamba nyumba hiyo ilikuwa ya marabi Wayahudi. Ili kumjaribu Peter, rabi huyo alimwuliza, “Hivyo mwanangu, kitabu cha Danieli kiliandikwa katika lugha gani?” Peter akajibu, “Sehemu fulani iliandikwa katika Kiaramu.” Peter anakumbuka hivi: “Rabi huyo alishangaa kwamba nilijua jibu, lakini mimi nilishangaa hata zaidi! Nilijuaje jibu? Niliporudi nyumbani, nilichunguza magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ya miezi iliyotangulia, na nikapata makala iliyoeleza kwamba kitabu cha Danieli kiliandikwa katika Kiaramu.” (Dan. 2:4) Naam, roho takatifu inaweza kutukumbusha mambo tuliyosoma na kuyaweka mahali salama katika hazina yetu.—Luka 12:11, 12; 21:13-15.

18 Ikiwa tunaona hekima inayotoka kwa Yehova kuwa yenye thamani, moyo wetu utatuchochea kujaza hazina yetu kweli mpya na za zamani. Kadiri tunavyozidi kupenda na kuthamini hekima kutoka kwa Yehova, ndivyo tutakavyoboresha uwezo wetu wa kuwa wafundishaji wa watu wote.

LINDA HAZINA ZAKO

19. Kwa nini tunapaswa kulinda hazina zetu za kiroho?

19 Shetani na ulimwengu wake unajitahidi kufanya tudhoofishe au tuache kuthamini hazina za kiroho ambazo tumechunguza katika makala hii. Tunaweza kuathiriwa na mbinu zake. Tunaweza kuvutiwa kwa urahisi na ahadi za kazi zenye mshahara mnono, kutamani maisha yenye kustarehesha, au tamaa ya kujionyesha mali zetu. Mtume Yohana anatukumbusha kuwa ulimwengu huu unapitilia mbali na pia tamaa yake. (1 Yoh. 2:15-17) Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi kulinda hisia na upendo wetu na kuonyesha kwamba tunathamini utajiri wa kiroho.

20. Umeazimia kufanya nini ili ulinde utajiri wako wa kiroho?

20 Uwe tayari kuacha kitu chochote kinachoweza kuchukua mahali pa upendo wako wa moyo wote kwa Ufalme wa Mungu. Endelea kuhubiri kwa bidii, na kamwe usiache kuthamini huduma yetu inayookoa uhai. Endelea kutafuta kwa bidii kweli zinazotoka kwa Mungu. Unapoendelea kufanya hivyo, utajenga “hazina isiyopungua kamwe katika mbingu, ambapo mwizi hakaribii wala nondo hali. Kwa maana mahali ilipo hazina [yako, hapo pia moyo wako utakuwapo].”—Luka 12:33, 34.