Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kaza Moyo Wako juu ya Hazina za Kiroho

Kaza Moyo Wako juu ya Hazina za Kiroho

“Mahali ilipo hazina [utajiri] yenu, hapo pia mioyo yenu itakuwapo.” ​—LU. 12:34.

NYIMBO: 153, 104

1, 2. (a) Ni hazina gani tatu za kiroho zenye Yehova ametupatia? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

YEHOVA ndiye tajiri zaidi katika ulimwengu wote. (1 Nya. 29:11, 12) Kwa sababu yeye ni Baba mukarimu, anapatia utajiri wake wa kiroho wale wote wenye kuona kuwa utajiri huo ni wa maana sana. Tuko wenye shukrani sana kwa sababu Yehova ametupatia hazina za kiroho; hazina hizo zinatia ndani (1) Ufalme wa Mungu, (2) kazi yetu ya kuhubiri yenye kuokoa uzima, na (3) kweli za maana sana zenye kupatikana katika Neno lake! Lakini, ikiwa hatuko waangalifu tunaweza kuzarau hazina hizo, na tunaweza kufikia kuzitupa. Ili tuendelee kushikamana na utajiri huo, tunapaswa kuutumia muzuri na kuendelea kuupenda zaidi. Yesu alisema hivi: “Mahali ilipo hazina yenu, hapo pia mioyo yenu itakuwapo.”​—Lu. 12:34.

2 Tuzungumuzie basi namna tunaweza kuendelea kukomalisha upendo wetu na shukrani yetu juu ya Ufalme, kazi ya kuhubiri, na kweli. Wakati tutakuwa tunafanya hivyo, fikiria sana juu ya namna wewe mwenyewe unaweza kukomalisha upendo wako juu ya hazina hizo za kiroho.

UFALME WA MUNGU UKO KAMA LULU YA BEI SANA

3. Mufanya-biashara mwenye Yesu alizungumuzia katika mufano wake, alikuwa tayari kufanya nini ili apate lulu ya bei sana? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

3 Soma Mathayo 13:45, 46. Yesu alitoa mufano wa mufanya-biashara mwenye alikuwa anatafuta lulu (kitu chenye kuwa kama jiwe ndogo la bei sana). Kwa miaka mingi, mufanya-biashara huyo alikuwa ameuza na kuuzisha mamia ya lulu. Lakini, sasa alikuwa amepata lulu moja yenye kupendeza sana na moyo wake ulifurahi kisha tu kuiona. Lakini ili auze lulu hiyo, alipaswa kuuzisha vitu vingine vyote vyenye alikuwa navyo. Kwa kweli, aliona lulu hiyo kuwa ya maana sana.

4. Ikiwa tunapenda sana Ufalme wa Mungu kama vile mufanya-biashara alipenda lulu, tutafanya nini?

4 Mufano huo unatufundisha nini? Kweli ya Ufalme wa Mungu iko kama lulu ya bei sana. Ikiwa tunapenda Ufalme kama vile mufanya-biashara alipenda lulu hiyo, tutakuwa tayari kuacha kila kitu ili tukuwe na tubakie raia wa Ufalme huo. (Soma Marko 10:28-30.) Tuzungumuzie watu wawili wenye walifanya hiyo.

5. Namna gani Zakayo alionyesha kama anapenda kuwa raia wa Ufalme wa Mungu?

5 Zakayo alikuwa mukubwa wa watu wenye kulipisha kodi (taxe) na alikuwa amekuwa tajiri kwa sababu ya kunyanganya wengine feza. (Lu. 19:1-9) Lakini, wakati mwanaume huyo mutenda-zambi alisikia Yesu anahubiri juu ya Ufalme, alitambua kuwa mambo yenye alikuwa anasikia yalikuwa ya maana sana na akatenda bila kukawia. Alisema hivi: ‘Tazama! Nusu ya mali zangu, Bwana, mimi nitawapa masikini, na chochote nilichomunyanganya mutu yeyote kwa shitaka la uwongo nitarudisha mara ine.’ Kwa furaha, akaachana na utajiri wake wenye alipata kwa njia ya udanganyifu na tamaa yake ya kutafuta vitu vya kimwili.

6. Rose alifanya mabadiliko gani ili akuwe raia wa Ufalme wa Mungu, na sababu gani alifanya hivyo?

6 Miaka fulani yenye imepita, mwanamuke mumoja mwenye tunaweza kuita Rose alisikia ujumbe wa Ufalme; wakati huo alikuwa mwanamuke mwenye kulala na mwanamuke mwenzake. Alikuwa musimamizi wa shirika fulani lenye kupigania haki za wanaume wenye kulala na wanaume na wanawake wenye kulala na wanawake. Lakini, wakati Rose aliendelea kujifunza Biblia alielewa kuwa kweli juu ya Ufalme wa Mungu ilikuwa ya maana sana. Hata hivyo, alitambua kwamba alipaswa kufanya mabadiliko makubwa. (1 Kor. 6:9, 10) Moyo wake ulimuchochea aache cheo chake na aache kulala na wanawake wenzake. Rose alibatizwa katika mwaka wa 2009, na mwaka wenye ulifuata alianza kufanya kazi ya upainia. Upendo wake kwa Yehova na Ufalme ulikuwa wenye nguvu zaidi kuliko tamaa yoyote ya kimwili.​—Mk. 12:29, 30.

7. Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kupenda Ufalme wa Mungu kwa moyo wetu wote?

7 Kwa kweli, wengi kati yetu wamefanya mabadiliko makubwa ili wakuwe raia wa Ufalme wa Mungu. (Rom. 12:2) Hata hivyo, haitoshe tu kufanya hivyo. Tunapaswa kuendelea kuwa waangalifu juu ya mambo yenye yanaweza kuregeza upendo wetu juu ya Ufalme, kama vile tamaa ya kupata vitu vingi vya kimwili na tamaa yoyote ya mambo ya uasherati. (Met. 4:23; Mt. 5:27-29) Ili kutusaidia tuendelee kupenda Ufalme wa Mungu kwa moyo wetu wote, Yehova ametupatia hazina ingine ya maana sana.

KAZI YETU YA KUHUBIRI YENYE KUOKOA UZIMA

8. (a) Sababu gani mutume Paulo aliita kazi yetu ya kuhubiri kuwa “hazina katika vyombo vya udongo”? (b) Namna gani Paulo alionyesha kuwa alipenda sana kazi yake ya kuhubiri?

8 Kumbuka kwamba Yesu ametupatia daraka la kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 28:19, 20) Mutume Paulo aliona kuwa kazi ya kuhubiri ilikuwa ya maana sana. Aliita huduma ya agano jipya kuwa “hazina katika vyombo vya udongo.” (2 Kor. 4:7; 1 Tim. 1:12) Hata kama tuko tu vyombo vya udongo vyenye havikamilike, ujumbe wenye tunahubiri unaweza kutuletea uzima wa milele na pia wale wenye kutusikiliza. Kwa sababu Paulo alijua jambo hilo alisema hivi: “Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.” (1 Kor. 9:23) Kwa kweli, upendo wa Paulo juu ya kazi ya kuhubiri ulimuchochea atumike kwa bidii ili kufanya wanafunzi. (Soma Waroma 1:14, 15; 2 Timotheo 4:2.) Hilo lilimusaidia avumilie upinzani mukali. (1 Tes. 2:2) Namna gani tunaweza kuonyesha upendo kama huo juu ya kazi ya kuhubiri?

9. Ni katika njia gani fulani tunaweza kuonyesha kuwa tunapenda kazi ya kuhubiri?

9 Njia moja yenye Paulo alitumia ili kuonyesha kuwa alipenda kazi ya kuhubiri ni kwa kutumia kila nafasi yenye ilijitokeza ili kuzungumuza na wengine. Kama mitume na Wakristo wa kwanza-kwanza, tunahubiri wakati nafasi inajitokeza, mahali pa watu wengi, na nyumba kwa nyumba. (Mdo. 5:42; 20:20) Kulingana na hali yetu, tunajikaza sana ili kupanua utumishi wetu, pengine kwa kufanya kazi ya upainia musaidizi ao wa kawaida. Tunaweza pia kujifunza luga ingine, kuhamia katika eneo lingine katika inchi yetu, ao hata kuhamia katika inchi ingine.​—Mdo. 16:9, 10.

10. Namna gani Irene alibarikiwa kwa sababu ya bidii yake ya kuhubiri habari njema?

10 Fikiria mufano wa Irene, dada wa Amerika mwenye hajaolewa. Alipenda sana kuhubiria watu wenye wamehamia katika inchi ya Amerika wenye kuzungumuza luga ya Kirusi. Wakati alianza kufanya hivyo katika mwaka wa 1993, kulikuwa tu wahubiri 20 hivi katika kikundi cha luga ya Kirusi katika muji wa New York. Kwa miaka 20 hivi, Irene amehubiria kwa bidii watu wenye kuzungumuza luga hiyo. Irene anasema hivi: “Mupaka sasa sijue kuzungumuza muzuri luga ya Kirusi.” Lakini, Yehova amebariki bidii yake na wengine wenye kuwa na bidii kama yeye. Leo, kuko makutaniko sita za luga ya Kirusi katika muji wa New York. Watu kumi na tano kati ya watu wenye Irene alijifunza nao Biblia, wamebatizwa. Wamoja kati yao ni Wanabeteli, mapainia na wazee. Irene anasema hivi: “Wakati ninafikiria miradi mingine yenye ningefuatilia, ninaona kwamba hakuna muradi wenye ungeniletea furaha zaidi.” Kwa kweli, anapenda sana kazi yake ya kuhubiri!

Unaona kazi yako ya kuhubiri kuwa hazina na unaonyesha hivyo kwa kupanga kuhubiri kila juma? (Picha hii inapatana na fungu la 11, 12)

11. Tunapata matokeo gani ya muzuri kwa sababu tunaendelea kuhubiri hata wakati wa mateso?

11 Ikiwa tunapenda sana kazi yetu ya kuhubiri, tutakuwa kama mutume Paulo kwa kuendelea kuhubiri hata wakati wa mateso. (Mdo. 14:19-22) Katika miaka ya 1930 na mwanzo-mwanzo wa miaka ya 1940, ndugu zetu katika inchi ya Amerika walipambana na upinzani mukali sana. Lakini, kama Paulo, walibaki imara na waliendelea kuhubiri. Ili kulinda haki yetu ya kuhubiri, ndugu walijitetea sana kwenye tribinali mbalimbali. Katika mwaka wa 1943, wakati Ndugu Nathan Knorr alikuwa anazungumuzia ushindi mumoja wenye tulipata kwenye Tribinali Kubwa Zaidi ya Amerika, alisema hivi: “Tumepata ushindi huo kwa sababu ya bidii yenu. Ikiwa wahubiri hawangeendelea kuhubiri, hatungejitetea kwenye Tribinali Kubwa Zaidi; lakini ni kwa sababu nyinyi wahubiri, ndugu na dada katika dunia yote munaendelea na hamutaacha kuhubiri, ndiyo sababu tunakaribia kupata ushindi juu ya mateso. Mwishowe tumepata ushindi huo kwa sababu watu wa Bwana walibakia imara.” Katika inchi zingine pia tumepata ushindi kama huo kwa sababu ndugu na dada wamebakia imara. Kwa kweli, upendo wetu juu ya kazi ya kuhubiri unaweza kupata ushindi juu ya mateso.

12. Juu ya kazi ya kuhubiri, umeazimia kufanya nini?

12 Wakati tunaona kazi ya kuhubiri kuwa hazina ya bei sana kutoka kwa Yehova, hatutatosheka tu na saa zenye tunaandika kwenye ripoti. Lakini tutafanya yetu yote ili “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.” (Mdo. 20:24; 2 Tim. 4:5) Lakini tutafundisha wengine mambo gani? Fikiria hazina ingine yenye Mungu ametupatia.

HAZINA YETU YA KWELI ZENYE KUFUNULIWA

13, 14. “Hazina” yenye Yesu alizungumuzia katika Mathayo 13:52 ni nini? Namna gani tunajaza hazina yetu?

13 Hazina ya tatu ya kiroho ni kweli zenye kufunuliwa. Yehova ni Mungu wa ukweli. (2 Sam. 7:28; Zab. 31:5) Kwa sababu yeye ni Baba mwenye kuwa mukarimu, anafundisha wale wenye kumuogopa. Kuanzia wakati tulisikia kwa mara ya kwanza kweli, tumepata nafasi ya kukusanya kweli mbalimbali kutoka katika Neno lake Biblia, vichapo vyetu, na kwenye mikusanyiko, na mikutano yetu ya kila juma. Kadiri wakati unapita, tunakuwa na jambo lenye Yesu aliita “hazina” ya kweli za zamani na za mupya. (Soma Mathayo 13:52.) Yehova atatusaidia kukusanya kweli mupya za maana katika “hazina” yetu ikiwa tunatafuta kweli hizo kama hazina zenye kufichwa. (Soma Methali 2:4-7.) Tunafanya hivyo namna gani?

14 Tunapaswa kuendelea kufanya funzo la pekee na kutafuta habari kwa uangalifu katika Neno la Mungu na katika vichapo vyetu. Hilo litatusaidia kuvumbua kweli ‘mupya’, ni kusema, kweli zenye hatukujua zamani. (Yos. 1:8, 9; Zab. 1:2, 3) Gazeti la kwanza la Munara wa Mulinzi lenye lilichapishwa katika Mwezi wa 7, 1879, lilisema hivi: “Kweli iko kama ua ndogo lenye kuwa katikati ya mimea mingi sana, imezungukwa na hata karibu kusongwa na magugu mengi sana ya makosa. Ili uipate unapaswa kuwa macho wakati wote. . . . Ili uipate unapaswa kuinama na kuichukua. Usitosheke na ua moja tu la kweli. . . . Endelea kukusanya, tafuta mengine zaidi.” Kwa hiyo, tunapaswa kuwa na hamu ya kujaza hazina yetu kweli zenye kutoka kwa Mungu.

15. Sababu gani tunaweza kuita kweli fulani kuwa za “zamani,” na ni kweli gani fulani zenye wewe unapenda sana?

15 Tulivumbua kweli fulani za maana sana wakati tulianza kujifunza Biblia pamoja na watu wa Mungu. Kweli hizo zinaweza kuitwa kuwa za “zamani” kwa sababu tumezijua na kuzipenda tangu wakati tulianza kuishi maisha ya Mukristo. Ni kweli gani hizo? Kwa mufano, tulijifunza kuwa Yehova ni Muumbaji wetu, na yeye ndiye alitupatia uzima na kwamba iko na kusudi fulani kwa ajili ya wanadamu. Tulijifunza pia kuwa upendo ulimuchochea Yehova atoe Mwana wake kuwa zabihu ya ukombozi ili tuokolewe kutoka katika zambi na kifo. Tena, tulijifunza kuwa Ufalme wa Mungu utamaliza mateso yote na kwamba tuko na tumaini la kuishi milele katika amani na furaha wakati Ufalme wa Mungu utatawala dunia.​—Yoh. 3:16; Ufu. 4:11; 21:3, 4.

16. Tunapaswa kufanya nini wakati tunapata mafasirio mapya juu ya kweli fulani?

16 Wakati fulani, tunapata mafasirio mapya juu ya unabii fulani ao andiko fulani la Biblia. Wakati tunapewa mafasirio hayo mapya, tunapaswa kuchukua wakati wa kujifunza habari hiyo kwa uangalifu na kufikiri sana juu ya habari hiyo. (Mdo. 17:11; 1 Tim. 4:15) Zaidi ya kutafuta kuelewa mambo makubwa yenye yamebadilishwa, tunatafuta pia kuelewa muzuri mambo madogo-madogo yenye kutofautisha mafasirio ya zamani na mafasirio mapya. Ikiwa tunafanya hivyo, tutakuwa hakika kuwa tumeweka muzuri kweli hizo mupya katika hazina yetu ya kiroho. Sababu gani kufanya hivyo kunaleta faida?

17, 18. Namna gani roho takatifu inaweza kutusaidia?

17 Yesu alifundisha kama roho ya Mungu inaweza kutusaidia kukumbuka mambo yenye tumekwisha kujifunza. (Yoh. 14:25, 26) Namna gani hilo linaweza kutusaidia sisi wahubiri wa habari njema? Fikiria mufano wa ndugu mwenye kuitwa Peter. Katika mwaka wa 1970, alikuwa na miaka 19 na alikuwa ameanza kutumikia kwenye Beteli ya Uingereza. Wakati alikuwa anahubiri nyumba kwa nyumba, alikutana na mwanaume mumoja wa miaka 50 hivi, mwenye alikuwa na ndevu nyingi. Peter aliuliza mwanaume huyo ikiwa anapenda kuelewa Biblia. Mwanaume huyo alishangaa na kusema kama hiyo ilikuwa nyumba ya marabi Wayahudi. Ili kumujaribu Peter, rabi huyo alimuuliza hivi: “Sasa, mutoto wangu, kitabu cha Danieli kiliandikwa katika luga gani?” Peter alijibia hivi: “Sehemu fulani iliandikwa katika Kiaramu.” Peter anakumbuka hivi: “Rabi huyo alishangaa sana kuona kuwa nilikuwa ninajua jibu, lakini mimi nilishangaa hata zaidi!” Nilijua jibu namna gani? Wakati nilirudia nyumbani na kuchunguza magazeti Munara wa Mulinzi na Amuka! ya miezi yenye ilikuwa imepita, nilipata habari fulani yenye ilikuwa inafasiria kama sehemu fulani ya kitabu cha Danieli iliandikwa katika Kiaramu.” (Dan. 2:4) Kwa kweli, roho takatifu inaweza kutukumbusha mambo yenye tumekwisha kusoma na kuweka muzuri katika hazina yetu.​—Lu. 12:11, 12; 21:13-15.

18 Ikiwa tunapenda sana hekima ya Yehova, moyo wetu utatuchochea kujaza hazina yetu kweli za mupya na za zamani. Kadiri upendo na shukrani yetu juu ya hekima ya Yehova vinaendelea kukomaa, tutakuwa wahubiri wenye ufundi zaidi.

LINDA HAZINA ZAKO ZA KIROHO

19. Sababu gani tunapaswa kulinda hazina zetu za kiroho?

19 Shetani na ulimwengu wake wanatafuta kila mara kuregeza ao kuharibu upendo wetu juu ya hazina zetu za kiroho zenye tumezungumuzia katika habari hii. Jambo hilo linaweza kutufikia. Tunaweza kukengeushwa na ahadi ya kupata kazi ya muzuri sana, kuwa na maisha ya raha, ao tamaa ya mutu kuonyesha mali yake ya kimwili katika maisha. Mutume Yohana anatukumbusha kwamba ulimwengu huu unapitilia mbali na tamaa zake. (1 Yoh. 2:15-17) Kwa hiyo, tunapaswa kujikaza sana ili kulinda upendo na shukrani yetu juu ya utajiri wa kiroho.

20. Umeazimia kufanya nini ili kulinda utajiri wako wa kiroho?

20 Ukuwe tayari kuacha kitu chochote chenye kinaweza kukuzuia kupenda Ufalme wa Mungu kwa moyo wako wote. Endelea kuhubiri kwa bidii, usipoteze hata kidogo upendo wako juu ya kazi hiyo yenye kuokoa uzima. Endelea kutafuta kwa bidii kweli zenye kutoka kwa Mungu. Kwa kufanya hivyo, utajiwekea ‘hazina isiyopungua kamwe katika mbingu, ambapo mwizi hakaribie wala nondo hakule. Kwa maana mahali ilipo hazina yako, hapo pia moyo wako utakuwapo.’​—Lu. 12:33, 34.