Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utasuluhisha Kutoelewana na Kuendeleza Amani?

Je, Utasuluhisha Kutoelewana na Kuendeleza Amani?

YEHOVA MUNGU anawahimiza Wakristo wapende amani na wafanye amani iwe sifa muhimu maishani mwao. Tukiwa waabudu wa kweli tunafurahia amani kwa wingi tunapokuwa wenye kufanya amani. Hilo hufanya kutaniko la Kikristo liwavutie wengine ambao wanapenda amani.

Kwa mfano, mchawi fulani mashuhuri nchini Madagaska aliona jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyoishi kwa umoja. Alijiambia hivi, ‘Ikiwa ningechagua kujiunga na dini fulani, ningejiunga na Mashahidi wa Yehova.’ Baada ya muda, aliacha mazoea yake ya kuwasiliana na roho, akatumia miezi mingi kurekebisha ndoa yake ambayo haikuwa inapatana na Maandiko, na kuwa mwabudu wa Yehova, Mungu wa amani.

Kama mwanamume huyo, kila mwaka watu wengi hupata amani ambayo wamekuwa wakiitamani sana wanapojiunga na kutaniko la Kikristo. Lakini Biblia inaonyesha wazi kwamba “wivu mkali na ugomvi” kutanikoni unaweza kuharibu urafiki na kuleta matatizo. (Yak. 3:14-16) Pia, inafurahisha kwamba Biblia inatuandalia ushauri mzuri wa jinsi tunavyoweza kuepuka matatizo hayo na kuendeleza amani. Ili tuelewe jambo hilo, acheni tuchunguze visa fulani halisi.

MATATIZO NA SULUHISHO

“Sikuelewana na ndugu tuliyefanya kazi naye. Pindi fulani tulipokuwa tukigombana, watu wawili walikuja na kushuhudia tukio hilo.”—CHRIS.

“Dada mmoja niliyehubiri naye kwa ukawaida alisitisha ghafula mpango tuliokuwa nao wa kwenda kuhubiri. Kisha akaacha kuzungumza nami kabisa. Sikuelewa kwa nini alifanya hivyo.”—JANET.

“Nilikuwa nikizungumza kwa simu na watu wawili kwa wakati mmoja. Mmoja wao akatuaga, na nikafikiri amekata simu. Kisha nikasema maneno yasiyo ya fadhili kumhusu, lakini kumbe hakuwa amekata simu.”—MICHAEL.

“Katika kutaniko letu, mapainia wawili walianza kuwa na matatizo ya kutoelewana. Mmoja wao alikuwa akimzomea mwenzake. Watu walivunjwa moyo sana na ugomvi wao.”—GARY.

Unaweza kuhisi kwamba visa hivyo ni vidogo. Hata hivyo, kila kisa kingeweza kuumiza hisia na kudhoofisha hali ya kiroho ya wahusika kwa muda mrefu. Lakini utafurahi kujua kwamba ndugu na dada hao walifanya amani wakitumia mwongozo wa Biblia. Unafikiri walitumia miongozo gani ya Biblia ili wafanikiwe?

“Msigombane njiani.” (Mwa. 45:24) Yosefu aliwashauri hivyo ndugu zake waliokuwa wakirudi kwa baba yao. Maneno yake yalikuwa ya hekima kwelikweli! Mtu asipodhibiti hisia zake na kukasirika haraka, anaweza kuwakasirisha wengine. Chris aligundua kwamba udhaifu wake ulikuwa kiburi na kusita kukubali mwongozo. Kwa kuwa alitaka kubadilika, alimwomba msamaha ndugu aliyegombana naye, kisha akajitahidi kudhibiti hasira. Akitambua jitihada za Chris za kubadilika, mfanyakazi mwenzake alifanya mabadiliko pia. Sasa wanafurahia kumtumikia Yehova pamoja.

“Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.” (Met. 15:22) Janet alikata kauli kwamba alihitaji kufuata ushauri huo. Aliamua ‘kuzungumza’ na dada aliyekosana naye. Walipokuwa wakizungumza, Janet alimwomba kwa busara aeleze sababu iliyomfanya akasirike. Mwanzoni, ilikuwa vigumu kwao kujieleza, lakini hali ikawa nzuri walipoendelea kuzungumzia tatizo lao kwa utulivu. Dada huyo aligundua kwamba alielewa kimakosa jambo fulani ambalo hata halikumhusisha Janet. Aliomba msamaha, na sasa wanamtumikia Yehova tena kwa umoja.

“Ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako.” (Mt. 5:23, 24) Huenda ukakumbuka ushauri huo ambao Yesu alitoa kwenye Mahubiri ya Mlimani. Michael aliumia sana alipotambua jinsi alivyotenda bila fadhili na ufikirio. Aliazimia kujitahidi kufanya amani. Kwa unyenyekevu, alimwomba msamaha ana kwa ana ndugu aliyemkosea. Matokeo yalikuwa nini? Michael anasema, “Ndugu yangu alinisamehe kabisa.” Wakawa marafiki tena.

“Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.” (Kol. 3:12-14) Kuhusu kisa cha mapainia hao wa muda mrefu, mzee mmoja wa kutaniko mwenye fadhili aliwasaidia kutafakari maswali kama haya: ‘Je, sisi wawili tuna haki ya kuwahuzunisha wengine kwa sababu ya kutoelewana kwetu? Je, kweli tuna sababu nzuri ya kutovumiliana na kuendelea kumtumikia Yehova kwa amani?’ Walikubali shauri la mzee huyo na kulitumia. Sasa wao ni marafiki na wanaendelea kuhubiri habari njema.

Kabla ya kutumia maagizo ya Biblia yaliyotangulia kutajwa, tunaweza kuanza na andiko la Wakolosai 3:12-14 ikiwa mtu anatukosea. Watu wengi wameona kwamba wanaweza kusamehe na kusahau wanapoonyesha unyenyekevu. Ikiwa bado inakuwa vigumu kufanya hivyo, je, tunaweza kutumia kanuni iliyo katika Mathayo 18:15? Shauri la Yesu linahusu hatua ambazo tunapaswa kuchukua wakati mtu amemtendea mwingine dhambi nzito. Lakini huenda hiyo ndiyo kanuni unayohitaji kutumia. Mwendee ndugu au dada yako, na kwa fadhili na unyenyekevu, jaribu kuzungumzia tatizo hilo na kulisuluhisha.

Bila shaka, Biblia inaandaa mashauri mengine yanayofaa. Mashauri hayo yanatutia moyo tuonyeshe “matunda ya roho . . . upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Gal. 5:22, 23) Kama mafuta yanavyolainisha mashine, sifa hizo zinazotoka kwa Mungu zinafanya iwe rahisi kwetu kufanya amani.

NYUTU MBALIMBALI HUBORESHA KUTANIKO

Kila mmoja wetu ana kitu cha pekee, yaani, utu. Nyutu hutofautiana, lakini zinaweza kufanya tuwe na urafiki mzuri sana. Tofauti za nyutu pia zinaweza kusababisha kutoelewana. Mzee mmoja mwenye uzoefu anatoa mfano huu: “Inaweza kuwa vigumu kwa mtu mwenye haya kushirikiana na mtu mchangamfu na mwenye kuzungumza sana. Huenda tofauti hiyo ikaonekana kuwa ndogo; lakini inaweza kusababisha matatizo makubwa.” Hata hivyo, je, unahisi kwamba watu walio na nyutu tofauti kabisa lazima wakose kuelewana? Fikiria mitume hawa wawili. Petro alikuwa mtu wa namna gani? Unaweza kusema alikuwa mzungumzaji sana na mwenye kuongozwa na hisia. Namna gani Yohana? Tunaweza kusema alikuwa mtu mwenye upendo na aliyezungumza na kutenda kwa busara. Huenda kuna sababu za msingi za kuwaza hivyo. Inaonekana walikuwa na nyutu tofauti. Hata hivyo, walifurahia kufanya kazi pamoja. (Mdo. 8:14; Gal. 2:9) Vivyo hivyo leo, inawezekana kwa Wakristo walio na nyutu tofauti sana kufanya kazi pamoja.

Labda unaudhika na jinsi ndugu fulani katika kutaniko lenu anavyozungumza au kutenda. Lakini unatambua kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya mtu huyo na hivyo unapaswa kumpenda. (Yoh. 13:34, 35; Rom. 5:6-8) Kwa hiyo, badala ya kuvunja urafiki au kumwepuka, jiulize hivi: ‘Je, ndugu yangu anatenda jambo lolote lisilo la Kimaandiko? Je, anaponiudhi anafanya hivyo kwa nia mbaya? Au labda nyutu zetu ni tofauti tu?’ Pia, swali muhimu zaidi ni: ‘Ana sifa gani nzuri zinazoweza kuninufaisha?’

Swali hilo la mwisho ni muhimu sana. Ikiwa mtu fulani huzungumza sana na wewe ni mkimya, fikiria jinsi ilivyo rahisi kwake kuanzisha mazungumzo anapohubiri. Unaweza kumwomba ahubiri pamoja nawe ili uone mambo unayoweza kujifunza kutoka kwake. Ikiwa yeye huonyesha wengine ukarimu kwa ukawaida, nawe si mkarimu sana, je, unaweza kutambua shangwe anayopata kwa kuwasaidia wenye umri mkubwa, wagonjwa, au wenye uhitaji? Jambo kuu ni hili, hata ikiwa wewe na ndugu yako mna nyutu tofauti, mnaweza kuwa marafiki kwa kuzingatia sifa nzuri mlizo nazo. Kufanya hivyo hakumaanishi kwamba mtakuwa marafiki wa karibu, lakini kunaweza kuwasaidia kushirikiana, na kutaongeza amani yako na ya kutaniko.

Huenda Euodia na Sintike walitofautiana katika njia zao za kufanya mambo au katika utu. Lakini mtume Paulo aliwatia moyo “wawe na akili moja katika Bwana.” (Flp. 4:2) Je, utajitahidi kufanya hivyo na pia kuwa mwenye kufanya amani?

USIRUHUSU KUTOELEWANA KUENDELEE

Kama magugu yanayomea kwa wingi katika bustani ya maua, hisia zisizofaa kuelekea wengine huenda zikaongezeka tusipojitahidi kuzing’oa. Chuki inapotawala moyo wa mtu, inaweza kuathiri roho ya kutaniko. Ikiwa tunampenda Yehova na ndugu zetu, tutajitahidi tuwezavyo kutoruhusu tofauti za kibinafsi zivuruge au kupunguza amani ya watu wa Mungu.

Ukiwa mnyenyekevu na ujitahidi kufanya amani, unaweza kupata matokeo mazuri sana

Tunaposhughulikia kutoelewana tukiwa na lengo la kufanya amani, tunaweza kushangazwa na matokeo mazuri tutakayopata. Fikiria kisa cha Shahidi mmoja: “Nilihisi kuwa dada fulani alinitendea kana kwamba mimi ni mtoto. Hilo lilinisumbua sana. Nilipozidi kuudhika, nilianza kuzungumza naye bila heshima. Niliwaza hivi, ‘Hanionyeshi heshima ninayostahili, kwa hiyo, hata mimi sitamwonyesha heshima.’”

Kisha, Shahidi huyo akaanza kufikiria matendo yake. “Nilianza kuona kasoro zangu, na nikahuzunishwa sana na matendo yangu. Nikatambua kwamba nilihitaji kubadili njia yangu ya kufikiri. Baada ya kusali kwa Yehova kuhusu jambo hilo, nilimnunulia dada huyo zawadi ndogo na kumwandikia kadi ya kuomba msamaha kwa kumtendea kwa njia isiyofaa. Tulikumbatiana na kusameheana. Tangu wakati huo, hatujakuwa na matatizo yoyote.”

Watu wanahitaji sana amani. Hata hivyo, wengi wanapohisi hawatambuliwi au mamlaka yao haitambuliwi, wao huanza kutenda kwa njia isiyo ya amani. Watu wengi wasiomwabudu Yehova hufanya hivyo, lakini miongoni mwa waabudu wa Yehova kunapaswa kuwa na amani na umoja kwa wingi. Yehova alimwongoza Paulo kuandika hivi: “Mimi . . . nawasihi ninyi mtembee kwa kuustahili mwito mlioitiwa, mkiwa na unyenyekevu kamili wa akili na upole, mkiwa na ustahimilivu, mkivumiliana katika upendo, mkijitahidi sana kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.” (Efe. 4:1-3) “Kifungo [hicho] chenye kuunganisha cha amani” ni chenye thamani sana. Acheni tuimarishe kifungo hicho na kuazimia kutatua kutoelewana kokote ambako kunaweza kutokea kati yetu.