Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Busara Yako na Ibarikiwe!”

“Busara Yako na Ibarikiwe!”

MANENO hayo yalisemwa na Daudi wa Israeli la kale akimsifu mwanamke fulani aliyekutana naye. Mwanamke huyo aliitwa Abigaili. Ni nini kilichomchochea Daudi amsifu, na tunaweza kunufaikaje kutokana na mfano wake?

Daudi alipokuwa akimtoroka Mfalme Sauli, alikutana na mwanamke huyo aliyekuwa ameolewa. Abigaili alikuwa ameolewa na Nabali, mwanamume tajiri aliyelisha kundi lake kubwa la mifugo katika eneo la milimani lililo kusini mwa Yuda. Daudi na wanaume wake “walikuwa ukuta” kuzunguka wachungaji na mifugo ya Nabali. Baadaye, Daudi alituma wajumbe kwa Nabali akiomba “chochote ambacho mkono [wake] unaweza kupata,” akimaanisha chakula. (1 Sam. 25:8, 15, 16) Ombi hilo lilipatana na akili kwa kuwa Daudi na wanaume wake walikuwa wamelinda mali ya Nabali.

Lakini Nabali alitenda kama jina lake linalomaanisha “Asiye na Akili” au “Mjinga.” Aliwajibu kwa ukali, akawatukana, na kumnyima Daudi ombi lake. Kwa hiyo, Daudi alijitayarisha kumwadhibu Nabali kwa sababu ya jibu lake lililomkasirisha na la kipumbavu. Nabali na nyumba yake wangeadhibiwa kwa sababu ya ujinga wake.—1 Sam. 25:2-13, 21, 22.

Kwa kuwa alitambua matokeo mabaya ya hatua ambayo ingechukuliwa bila kufikiri, kwa ujasiri Abigaili aliingilia kati. Kwa heshima, alimsihi Daudi asifanye hivyo ili asiharibu uhusiano wake na Yehova. Na akampa Daudi, ambaye angekuwa mfalme, chakula cha kumtosha yeye na wanaume wake. Naye Daudi alisema kwamba Yehova alimtumia Abigaili ili amzuie kufanya jambo ambalo lingemfanya awe na hatia mbele za Mungu. Daudi alimwambia hivi Abigaili: “Busara yako na ibarikiwe, nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu.”—1 Sam. 25:18, 19, 23-35.

Ni wazi kwamba hatungependa kamwe kuwa kama Nabali kwa kutothamini mambo mazuri ambayo wengine wanatutendea. Kwa kuongezea, tunapoona hali mbaya ikijitokeza, inafaa tufanye yote tuwezayo kuzuia hali hiyo. Naam, tunaweza kuwa na maoni kama ya mtunga zaburi aliyemwambia Mungu hivi: “Unifundishe wema, kuwa na akili na ujuzi.”—Zab. 119:66.

Wengine wanaweza kutambua tunapotenda kwa hekima na busara. Iwe watasema au la, huenda wakahisi kama Daudi aliyesema hivi: “Busara yako na ibarikiwe!”