Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uko Tayari Kungoja kwa Subira?

Je, Uko Tayari Kungoja kwa Subira?

“Ninyi pia onyesheni subira.”​—YAK. 5:8.

NYIMBO: 114, 79

1, 2. (a) Ni nini kinachoweza kufanya tuulize: “Ni mpaka wakati gani”? (b) Kwa nini mifano ya watumishi waaminifu wa nyakati za kale inaweza kututia moyo?

“NI MPAKA wakati gani?” Hilo ndilo swali ambalo manabii waaminifu Isaya na Habakuki waliuliza. (Isa. 6:11; Hab. 1:2) Mfalme Daudi pia aliuliza hivi mara nne alipoandika Zaburi ya 13: “Mpaka wakati gani?” (Zab. 13:​1, 2) Hata Bwana wetu Yesu Kristo aliuliza swali hilo alipoona mtazamo wa kukosa imani wa watu wa siku zake. (Mt. 17:17) Kwa hiyo, hatupaswi kushangaa tukijikuta tunauliza swali hilohilo pindi fulani.

2 Ni mambo gani yanayoweza kufanya tuulize, “Ni mpaka wakati gani”? Huenda tumekabiliana na namna fulani ya ukosefu wa haki. Au labda tunavumilia matatizo yanayosababishwa na uzee, ugonjwa, au mikazo ya kuishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu [sana] kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Au huenda tunachoshwa na mitazamo isiyofaa ya watu wengine. Vyovyote vile, tunatiwa moyo sana kujua kwamba watumishi waaminifu wa nyakati za kale wa Yehova, walihisi huru kuuliza swali hilo ambalo huenda likatuhangaisha, nao hawakushutumiwa kwa kufanya hivyo!

3. Ni nini kinachoweza kutusaidia tunapokabili hali ngumu?

3 Lakini ni nini kinachoweza kutusaidia tunapokumbana na hali ngumu kama hizo? Mwanafunzi Yakobo, aliyekuwa ndugu wa kambo wa Yesu, aliongozwa na roho kutuambia hivi: “Basi, onyesheni subira, akina ndugu, mpaka kuwapo kwa Bwana.” (Yak. 5:7) Naam, sote tunahitaji sifa ya subira. Lakini ni nini kinachohusika katika kuonyesha sifa hiyo ya Mungu?

SUBIRA NI NINI?

4, 5. (a) Ni nini kinachohusika katika kuonyesha subira? (b) Mwanafunzi Yakobo alitumia mfano gani kueleza sifa nyingine inayohusika katika kuonyesha subira? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 Biblia inaonyesha kwamba subira hutokana na roho takatifu; pasipo msaada wa Mungu, wanadamu wasio wakamilifu hawawezi kuwa na subira kwa kiwango kinachofaa. Subira ni zawadi kutoka kwa Mungu, na ni njia kuu ya kuonyesha kwamba tunampenda. Pia, kuwa wenye subira ni njia ya kuonyesha kwamba tunawapenda wengine. Kukosa subira tena na tena hudhoofisha kifungo cha upendo; kuwa na subira huimarisha kifungo hicho. (1 Kor. 13:4; Gal. 5:​22) Kuwa na subira huhusisha sifa nyingine muhimu za Kikristo. Kwa mfano, inahusiana kwa ukaribu na sifa ya uvumilivu, ambayo hutuwezesha kukabiliana na hali ngumu huku tukidumisha mtazamo mzuri. (Kol. 1:11; Yak. 1:3, 4) Kuwa na subira kunahusisha pia kuteseka bila kulipiza kisasi na kuendelea kuwa imara na thabiti licha ya hali zinazotupata. Vilevile, Biblia inatuhimiza tuwe tayari kukubali kwamba tunahitaji kuwa na subira. Wazo hilo linakaziwa katika andiko la Yakobo 5:7, 8. (Soma.)

5 Kwa nini tunapaswa kuwa tayari kumngojea Yehova achukue hatua? Yakobo analinganisha hali yetu na hali ya mkulima. Mkulima hufanya kazi kwa bidii ili kupanda mimea, lakini hawezi kudhibiti hali ya hewa au ukuzi wa mimea hiyo. Hawezi kuharakisha wakati. Anakubali kwamba anahitaji kuwa na subira ili angojee “matunda yenye thamani ya nchi.” Vivyo hivyo, kuna mambo mengi ambayo hatuwezi kudhibiti tunapongojea ahadi za Mungu zitimie. (Marko 13:32, 33; Mdo. 1:7) Kama mkulima huyo, tunahitaji kungoja kwa subira.

6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa nabii Mika?

6 Hali tunazokabili leo zinafanana na za nabii Mika. Aliishi wakati wa utawala wa Mfalme mwovu Ahazi, kipindi ambacho ufisadi wa kila namna ulikuwa mwingi sana. Kwa kweli, mikono ya watu ilikuwa “juu ya lililo baya, ili kulifanya vema.” (Soma Mika 7:1-3.) Mika alitambua kwamba yeye mwenyewe hangeweza kubadili hali hizo. Hivyo, angefanya nini? Anatuambia hivi: “Mimi, nitaendelea kumtazamia Yehova. Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wangu. Mungu wangu atanisikia.” (Mika 7:7) Kama Mika, sisi pia tunahitaji kuwa na ‘mtazamo wa kungojea.’

7. Kwa nini tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kumngojea Yehova atimize ahadi zake?

7 Ikiwa tuna imani kama ya Mika, tutakuwa tayari kumngojea Yehova. Hali yetu si kama ya mfungwa aliye gerezani akingoja kuuawa. Analazimika kungoja, lakini hatazamii kwa hamu jambo litakalompata. Hali yetu ni tofauti sana na hiyo! Tuko tayari kumngojea Yehova kwa sababu tunajua kuwa atatimiza ahadi yake ya kutupatia uzima wa milele kwa wakati unaofaa, wakati barabara kabisa! Kwa hiyo, “[tunavumilia] kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.” (Kol. 1:11, 12) Kutenda kinyume cha hilo, yaani, kusubiri huku tukilalamika na kunung’unika kwamba Yehova hachukui hatua haraka, kungemkasirisha Mungu wetu.​—Kol. 3:12.

MIFANO YA WATU WAAMINIFU WALIOKUWA NA SUBIRA

8. Tunahitaji kukumbuka nini tunapotafakari mifano ya wanaume na wanawake waaminifu wa kale?

8 Tutakuwa tayari zaidi kungoja ikiwa tutakumbuka mifano ya wanaume na wanawake waaminifu wa kale ambao walingoja kwa subira Yehova atimize ahadi zake. (Rom. 15:4) Tunapotafakari mifano yao, itafaa tukumbuke muda waliohitaji kungoja, sababu zilizowafanya wawe tayari kungoja, na baraka walizopata kwa sababu ya kuwa na subira.

Abrahamu alihitaji kungoja kwa miaka mingi kabla ya wajukuu wake, Esau na Yakobo, kuzaliwa (Tazama fungu la 9 na 10)

9, 10. Abrahamu na Sara walihitaji kumngojea Yehova kwa muda gani?

9 Fikiria mfano wa Abrahamu na Sara. Wao ni kati ya “wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” Maandiko yanatuambia kuwa “baada ya Abrahamu kuonyesha subira,” Yehova alimwahidi kwamba angembariki na kuuzidisha uzao wake. (Ebr. 6:12, 15) Kwa nini Abrahamu alihitaji kuwa na subira? Kwa maneno machache, ahadi hiyo ingechukua muda kutimia. Agano ambalo Yehova alifanya na Abrahamu lilianza kufanya kazi Nisani 14, 1943 K.W.K. Huo ndio mwaka ambao Abrahamu, Sara, pamoja na watu wa nyumba yao walivuka Mto Efrati na kuingia katika Nchi ya Ahadi. Kisha, Abrahamu alihitaji kusubiri kwa miaka 25 kabla ya mwanawe Isaka kuzaliwa mwaka wa 1918 K.W.K., na alihitaji kusubiri kwa miaka mingine 60 kabla ya wajukuu wake Esau na Yakobo kuzaliwa mwaka wa 1858 K.W.K.​—Ebr. 11:9.

10 Abrahamu alirithi eneo kubwa kadiri gani katika Nchi ya Ahadi? Tunaambiwa hivi: “Bado [Yehova] hakumpa [Abrahamu] urithi wowote ndani yake, hapana, hata upana wa wayo mmoja wa mguu; bali aliahidi kumpa hiyo kuwa miliki, na uzao wake baada yake, alipokuwa bado hana mtoto.” (Mdo. 7:5) Kwa kweli, miaka 430 ilipita baada ya Abrahamu kuvuka Mto Efrati, ndipo wazao wake wakapangwa kuwa taifa ambalo lingerithi nchi ya Ahadi.​—Kut. 12:​40-42; Gal. 3:​17.

11. Kwa nini Abrahamu alikuwa tayari kumngojea Yehova, naye atapata baraka gani kwa sababu alionyesha subira?

11 Abrahamu alikuwa tayari kungoja kwa sababu subira yake ilitegemea imani yake kwa Yehova. (Soma Waebrania 11:8-12.) Abrahamu alikuwa tayari kungoja, hata ingawa hakuona ahadi hiyo ikitimizwa kikamili katika siku zake. Lakini wazia shangwe ambayo Abrahamu atakuwa nayo atakapofufuliwa katika dunia paradiso. Atashangaa kuona kwamba historia yake na ya wazao wake iliandikwa katika sehemu kubwa ya Biblia. * Hebu wazia jinsi atakavyofurahi kuelewa kwa mara ya kwanza fungu lake muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova kuhusiana na uzao ulioahidiwa! Bila shaka, atahisi kwamba ingawa alingoja kwa muda mrefu, kulikuwa na sababu nzuri za kufanya hivyo.

12, 13. Kwa nini Yosefu alihitaji kuwa na subira, naye alikuwa na mtazamo gani mzuri?

12 Vilevile Yosefu, kitukuu wa Abrahamu, alikuwa tayari kuonyesha subira. Alivumilia ukosefu mkubwa sana wa haki. Kwanza, kaka zake walimwuza akiwa mtumwa alipokuwa na umri wa miaka 17 hivi. Kisha akashtakiwa kwa uwongo kwamba amejaribu kumlala kinguvu mke wa bwana wake, na akafungwa gerezani. (Mwa. 39:11-20; Zab. 105:17, 18) Ilionekana kana kwamba anaadhibiwa kwa matendo yake ya uadilifu, badala ya kubarikiwa. Lakini baada ya miaka 13, kila kitu kilibadilika haraka sana. Aliachiliwa kutoka gerezani na kupewa cheo cha pili nchini Misri.​—Mwa. 41:​14, 37-​43; Mdo. 7:9, 10.

13 Je, ukosefu huo wa haki ulimfanya Yosefu awe na uchungu moyoni? Je, aliacha kumtegemea Mungu wake, Yehova? Hapana. Ni nini kilichomsaidia Yosefu kungoja kwa subira? Ni imani yake katika Yehova. Aliona kuwa Yehova alikuwa akielekeza mambo. Ona jinsi hilo linavyoonyeshwa katika maneno haya aliyowaambia kaka zake: “Msiogope, kwa maana je, mimi niko mahali pa Mungu? Kwa upande wenu, ninyi mlikuwa na uovu akilini mwenu kunielekea mimi. Mungu alikuwa na wema akilini kwa kusudi la kutenda kama ilivyo leo hii ili kuhifadhi hai watu wengi.” (Mwa. 50:​19, 20) Mwishowe, Yosefu alitambua kwamba kulikuwa na sababu nzuri za kungoja.

14, 15. (a) Ni nini kilichokuwa cha pekee kuhusu subira ya Daudi? (b) Ni nini kilichomsaidia Daudi kungoja kwa subira?

14 Mfalme Daudi pia alitendewa isivyo haki mara nyingi. Ingawa Yehova alimtia mafuta kuwa mfalme wa Israeli akiwa na umri mdogo, Daudi alilazimika kungoja miaka 15 hivi kabla ya kuwa mfalme juu ya kabila lake. (2 Sam. 2:​3, 4) Katika kipindi fulani cha miaka hiyo, Mfalme Sauli asiye mwaminifu alimwinda Daudi akitaka kumwua. * Kwa sababu hiyo, Daudi alilazimika kuishi akiwa mkimbizi, pindi fulani akikimbilia nchi ya kigeni na nyakati nyingine akiishi kwenye mapango nyikani. Hata Sauli alipouawa vitani, bado Daudi alihitaji kungoja kwa miaka saba zaidi kabla ya kupewa ufalme juu ya taifa lote la Israeli.​—2 Sam. 5:4, 5.

15 Kwa nini Daudi alikuwa tayari kungoja kwa subira? Anatupatia jibu katika zaburi ileile ambayo aliuliza hivi mara nne: “Ni mpaka wakati gani?” Anasema hivi: “Nami nimezitegemea fadhili zako zenye upendo; moyo wangu na ushangilie katika wokovu wako. Nitamwimbia Yehova, kwa maana amenitendea kwa njia ya kunipa thawabu.” (Zab. 13:​5, 6) Daudi alitegemea upendo mshikamanifu wa Yehova. Akiwa mwenye shangwe alitazamia kwa hamu kukombolewa, na alitafakari jinsi Yehova alivyomthawabisha. Naam, Daudi alihisi kwamba kulikuwa na sababu nzuri za kungoja.

Yehova hatarajii tufanye jambo ambalo yeye mwenyewe hayuko tayari kufanya. Sikuzote, yeye pia amekuwa tayari kuonyesha subira

16, 17. Yehova Mungu na Yesu Kristo wametuwekea mfano gani bora wa kuwa tayari kungoja?

16 Yehova hatarajii tufanye jambo ambalo yeye mwenyewe hayuko tayari kufanya. Sikuzote, yeye pia amekuwa tayari kuonyesha subira. Ameweka mfano bora wa kuwa tayari kungoja. (Soma 2 Petro 3:9.) Kwa miaka mingi, Yehova amekuwa akingoja kwa subira ili mwishowe masuala yaliyozushwa katika bustani ya Edeni yatatuliwe kabisa. ‘Anaendelea kutarajia’ wakati ambapo jina lake litatakaswa kikamili. Hilo litawaletea baraka nyingi sana wale “wanaoendelea kumtarajia.”​—Isa. 30:18.

17 Yesu vilevile amekuwa tayari kungoja. Ingawa alishinda jaribu la utimilifu alipokuwa duniani na kutoa thamani ya dhabihu ya fidia mwaka wa 33 W.K., alihitaji kungoja mpaka mwaka wa 1914 kabla ya kuanza kutawala. (Mdo. 2:33-35; Ebr. 10:12, 13) Na hadi mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu ndipo maadui wote wa Yesu watakapoharibiwa kabisa. (1 Kor. 15:25) Atakuwa amengoja kwa muda mrefu, lakini tunaweza kuwa na uhakika kwamba kulikuwa na sababu nzuri za kungoja.

NI NINI KITAKACHOTUSAIDIA?

18, 19. Ni nini kitakachotusaidia kuwa tayari kungoja kwa subira?

18 Kwa hiyo, hapana shaka kwamba kila mmoja wetu anahitaji kuwa tayari kungoja na kuwa na subira. Lakini ni nini kitakachotusaidia? Sali upate roho ya Mungu. Kumbuka, subira ni sifa ya tunda la roho. (Efe. 3:16; 6:18; 1 The. 5:17-19) Msihi Yehova akusaidie uvumilie kwa subira.

19 Je, unakumbuka pia kilichomsaidia Abrahamu, Yosefu, na Daudi kungoja kwa subira ili ahadi za Yehova zitimizwe? Ni imani yao katika Yehova na kumtegemea alipokuwa akishughulika nao. Hawakujifikiria sana au kukazia fikira mapendezi yao wenyewe. Tunapotafakari jinsi walivyobarikiwa, sisi pia tutatiwa moyo kuwa na mtazamo wa kungoja.

20. Kila mmoja wetu anapaswa kuazimia nini?

20 Kwa hiyo, hata ingawa tunakabili majaribu, tumeazimia kuwa na “mtazamo wa kumngojea.” Ni kweli kwamba huenda nyakati nyingine tukauliza hivi: “Mpaka wakati gani, Ee Yehova?” (Isa. 6:​11) Lakini kwa nguvu za roho takatifu ya Mungu, kila mmoja wetu atasema maneno haya yaliyosemwa na Yeremia: “Yehova ni fungu langu . . . Ndiyo sababu nitaonyesha mtazamo wa kumngojea.”​—Omb. 3:​21, 24.

^ fu. 11 Sura 15 hivi za kitabu cha Mwanzo zinasimulia kumhusu Abrahamu. Kwa kuongezea, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo wanamtaja Abrahamu zaidi ya mara 70.

^ fu. 14 Ingawa Yehova alimkataa Sauli baada ya kutawala kwa miaka miwili hivi, alimruhusu aendelee kutawala kwa miaka mingine 38 mpaka alipokufa.​—1 Sam. 13:1; Mdo. 13:21.