Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Amani ya Mungu Ni Yenye Ubora Unaozidi Fikira Zote’

‘Amani ya Mungu Ni Yenye Ubora Unaozidi Fikira Zote’

“Amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu.”​—FLP. 4:7.

NYIMBO: 112, 58

1, 2. Ni mambo gani yaliyotukia jijini Filipi yaliyofanya Paulo na Sila wafungwe gerezani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

INAKARIBIA saa sita usiku. Wamishonari wawili, Paulo na Sila, wako gerezani jijini Filipi​—katika sehemu ya ndani zaidi ya gereza hilo. Miguu yao imefungwa kabisa ndani ya mikatale, wamepigwa, na migongo yao bado inauma. (Mdo. 16:23, 24) Mambo yalikuwa yamebadilika haraka! Bila taarifa, walikuwa wameburuzwa na umati wa watu hadi sokoni ili wasimame mbele ya waamuzi waliotafutwa haraka ili wasikilize kesi hiyo. Nguo zao zilikuwa zimeraruliwa, na walikuwa wamepigwa vibaya kwa mijeledi. (Mdo. 16:16-22) Huo ulikuwa ukosefu mkubwa sana wa haki! Paulo, ambaye alikuwa raia wa Roma, alistahili kushtakiwa kulingana na sheria. *

2 Paulo akiwa ameketi gizani, anatafakari mambo yaliyotukia mchana. Anawafikiria watu wa Filipi. Hata hawakuwa na sinagogi la Wayahudi katika jiji lao, tofauti na majiji mengine ambayo Paulo alikuwa ametembelea. Kwa kweli, waabudu Wayahudi walilazimika kukutanika nje ya malango ya jiji kando ya mto. (Mdo. 16:13, 14) Je, ni kwa sababu idadi ya wanaume Wayahudi jijini humo haikufika kumi, idadi inayohitajiwa ili waruhusiwe kuwa na sinagogi? Ni wazi kwamba watu wa jiji la Filipi wanajivunia kuwa raia wa Roma, hata ikiwa uraia wao ni wa kununua. (Mdo. 16:21) Je, hiyo inaweza kuwa ndiyo sababu inayofanya wasitarajie kwamba Wayahudi hao, Paulo na Sila, ni raia wa Roma? Hata iwe walifikiri nini, Wayahudi hao wamefungwa gerezani isivyo haki.

3. Kwa nini huenda Paulo hakuelewa sababu iliyofanya afungwe gerezani; hata hivyo, alikuwa na mtazamo gani?

3 Huenda Paulo anafikiria pia kuhusu mambo yaliyotukia miezi michache iliyopita. Alikuwa upande wa pili wa Bahari ya Aegea, katika Asia Ndogo. Akiwa huko, roho takatifu ilimkataza tena na tena kuhubiri katika maeneo fulani. Ni kana kwamba roho takatifu ilikuwa ikimchochea kwenda mahali pengine. (Mdo. 16:​6, 7) Wapi huko? Alipata jibu kupitia maono akiwa Troa. Paulo aliambiwa hivi: “Vuka uingie Makedonia.” Baada ya kupokea mwongozo huo ulio wazi wa mapenzi ya Yehova, mara moja Paulo akakubali mwaliko huo. (Soma Matendo 16:​8-​10.) Lakini ni nini kilichotokea baadaye? Muda mfupi baada ya kufika Makedonia, akafungwa gerezani! Kwa nini Yehova aliruhusu Paulo afungwe gerezani? Angebaki gerezani kwa muda gani? Hata ikiwa maswali hayo yalimhangaisha Paulo, hakuyaruhusu yadhoofishe imani na shangwe yake. Yeye na Sila wakaanza “[kusali] na kumsifu Mungu kwa wimbo.” (Mdo. 16:25) Amani ya Mungu ilituliza mioyo na akili zao.

4, 5. (a) Hali zetu zinaweza kufananaje na hali za Paulo? (b) Hali ya Paulo ilibadilikaje ghafla?

4 Kama Paulo, huenda nyakati fulani maishani mwako ulihisi kwamba umefuata mwongozo wa roho takatifu, lakini mambo hayakwenda kama ulivyotarajia. Ulikumbana moja kwa moja na hali ngumu, au ukajikuta katika hali mpya iliyokulazimu kufanya mabadiliko makubwa maishani. (Mhu. 9:​11) Unapotafakari, huenda bado ukajiuliza kwa nini Yehova aliruhusu mambo fulani yatukie. Ikiwa ndivyo, ni nini kinachoweza kukusaidia kuendelea kuvumilia huku ukimtegemea Yehova kabisa? Ili tupate jibu la swali hilo, acheni turudi kwenye simulizi la Paulo na Sila.

5 Paulo na Sila wanapoendelea kuimba nyimbo za sifa, kunakuwa na mfuatano wa matukio yasiyotarajiwa kabisa. Ghafla, tetemeko kubwa la nchi linatokea. Milango ya gereza inafunguka. Vifungo vya wafungwa wote vinafunguka. Paulo anamzuia mlinzi wa jela asijiue. Mlinzi huyo na watu wote wa familia yake wanabatizwa. Mapema siku inayofuata, mahakimu wa raia wanawatuma maofisa wa polisi wawaachilie huru Paulo na Sila. Maofisa hao wanawaomba waondoke jijini kwa amani. Kisha, mahakimu wa raia wanapogundua kwamba Paulo na Sila ni raia wa Roma, wanatambua kuwa wamefanya kosa kubwa, nao wenyewe wanakuja kuwasindikiza. Lakini Paulo na Sila wanasisitiza kwamba lazima wamuage Lidia, dada yao aliyebatizwa karibuni. Isitoshe, wanatumia fursa hiyo kuwaimarisha akina ndugu katika jiji hilo. (Mdo. 16:​26-​40) Mambo yalikuwa yamebadilika haraka!

NI “YENYE UBORA UNAOZIDI FIKIRA ZOTE”

6. Tutachunguza mambo gani sasa?

6 Tunajifunza nini kutokana na matukio hayo? Yehova anaweza kufanya mambo yanayopita matarajio yetu, kwa hiyo hatuhitaji kuhangaika tunapokabili majaribu. Ni wazi kwamba Paulo hangesahau mambo aliyojifunza, kama ilivyoonyeshwa na yale aliyowaandikia ndugu zake jijini Filipi kuhusu mahangaiko na amani ya Mungu. Acheni kwanza tuzungumzie maneno ya Paulo yaliyo katika Wafilipi 4:6, 7.(Soma.) Halafu, baadaye tutazungumzia mifano mingine ya Kimaandiko ya jinsi Yehova alivyofanya mambo yanayopita matarajio ya kibinadamu. Mwishowe, tutachunguza jinsi “amani ya Mungu” inavyoweza kutusaidia kuvumilia huku tukimtegemea Yehova kabisa.

7. Paulo alikazia nini alipowaandikia akina ndugu jijini Filipi, na tunaweza kujifunza somo gani kutokana na maneno yake?

7 Hapana shaka kwamba akina ndugu jijini Filipi waliposoma barua ya Paulo walikumbuka mambo yaliyompata na jinsi ambavyo hakuna yeyote aliyetazamia Yehova achukue hatua aliyochukua. Paulo alikuwa akiwafundisha nini? Kwa ufupi: Wasiwe na wasiwasi. Wasali, kisha watapokea amani ya Mungu. Lakini ona kwamba “amani ya Mungu [ni] yenye ubora unaozidi fikira zote.” Hilo linamaanisha nini? Watafsiri fulani wanatafsiri maneno hayo kuwa “ni bora kuliko tunavyoweza kuwazia” au “inapita uwezo wote wa mwanadamu wa kupangia mambo.” Kihalisi, Paulo alikuwa akisema kwamba “amani ya Mungu” ni bora kuliko tunavyoweza kufikiri. Kwa hiyo, ingawa kulingana na maoni ya kibinadamu huenda tusione suluhisho la matatizo yetu, Yehova anaweza kuona suluhisho, na anaweza kufanya jambo linalopita matarajio yetu.​—Soma 2 Petro 2:9.

8, 9. (a) Ingawa Paulo alitendewa isivyo haki jijini Filipi, kulikuwa na matokeo gani mazuri? (b) Kwa nini akina ndugu jijini Filipi wangechukua kwa uzito maneno ya Paulo?

8 Akina ndugu jijini Filipi walipofikiria mambo yaliyotukia miaka kumi iliyopita, bila shaka waliimarishwa. Mambo ambayo Paulo aliandika yalikuwa ya kweli. Ingawa Yehova aliruhusu ukosefu huo wa haki, matokeo yalikuwa ni “kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema.” (Flp. 1:7) Hivyo, wakati ujao mahakimu wa raia wangetafakari kabla ya kuchukua hatua yoyote dhidi ya kutaniko jipya la Kikristo katika jiji lao. Baada ya Paulo na Sila kuondoka, inaelekea Luka, daktari na mwandamani wa Paulo, angeweza kubaki Filipi kwa sababu ya mambo ambayo Paulo alifanya. Kwa hiyo, Luka angeweza kuwasaidia sana Wakristo wapya katika jiji hilo.

9 Kwa hakika, akina ndugu jijini Filipi waliposoma barua ya Paulo, walijua wazi kwamba maneno hayo hayakuwa ya msomi aliyekuwa akiandika akiwa mahali fulani ofisini. Paulo alikuwa amekabili hali ngumu sana, lakini bado alionyesha kwamba alikuwa na “amani ya Mungu.” Kwa kweli, Paulo alipowaandikia ndugu hao, alikuwa katika kifungo cha nyumbani huko Roma. Lakini bado alionyesha kwamba alikuwa na “amani ya Mungu.”​—Flp. 1:12-14; 4:7, 11, 22.

“MSIHANGAIKE JUU YA KITU CHOCHOTE”

10, 11. Tunahitaji kufanya nini tunapohangaishwa sana na tatizo fulani, na tunaweza kutarajia nini?

10 Ni nini kinachoweza kutusaidia tusihangaike juu ya kitu chochote na tupate “amani ya Mungu”? Maneno ya Paulo kwa Wafilipi yanaonyesha kwamba dawa ya wasiwasi ni sala. Kwa hiyo, tunapohangaika, tunapaswa kumimina mahangaiko yetu katika sala. (Soma 1 Petro 5:​6, 7.) Sali kwa Yehova ukiamini kabisa kwamba anakujali. Sali kwake na “kutoa shukrani,” ukikumbuka baraka ulizopokea. Uhakika wetu kwake utaimarishwa tunapokumbuka kwamba anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.”​—Efe. 3:​20.

11 Kama katika kisa cha Paulo na Sila walipokuwa Filipi, huenda tukashangazwa na mambo ambayo Yehova anatufanyia sisi binafsi. Labda si jambo la ajabu, lakini sikuzote ni kile tunachohitaji hasa. (1 Kor. 10:13) Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba tukae kitako tu bila kufanya lolote, tukisubiri Yehova arekebishe hali au kutatua tatizo. Tunahitaji kutenda kupatana na sala zetu. (Rom. 12:11) Hivyo, matendo yetu yanathibitisha kwamba sisi ni wanyoofu na tunajitahidi kupata baraka za Yehova. Lakini wakati huohuo, tunahitaji kutambua kwamba Yehova haongozwi na mambo tunayoomba, mipango, au matarajio yetu. Nyakati nyingine anatushangaza kwa kufanya jambo linalopita matarajio yetu. Acheni tuchunguze masimulizi fulani ya Biblia yanayoimarisha uhakika wetu katika uwezo wa Yehova wa kutufanyia mambo yanayopita matarajio yetu.

YEHOVA ALIFANYA MAMBO YANAYOPITA MATARAJIO YA KIBINADAMU

12. (a) Mfalme Hezekia alifanya nini Mfalme Senakeribu wa Ashuru alipotishia kumvamia? (b) Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulikia tatizo hilo?

12 Tunapochunguza Maandiko, tunapata tena na tena mifano ya mambo yanayopita matarajio ya kibinadamu ambayo Yehova alifanya. Mfalme Hezekia aliishi kipindi ambacho Mfalme Senakeribu wa Ashuru alivamia Yuda na kuteka majiji yote yenye ngome, isipokuwa Yerusalemu. (2 Fal. 18:1-3, 13) Baadaye, Senakeribu akageukia jiji hilo. Mfalme Hezekia alifanya nini ilipokuwa wazi kwamba angeshambuliwa? Alisali kwa Yehova na kumwomba ushauri Isaya, nabii wa Yehova. (2 Fal. 19:5, 15-20) Pia, Hezekia alijaribu kuonyesha usawaziko kwa kulipa faini ambayo Senakeribu alimtoza. (2 Fal. 18:14, 15) Wakati huohuo, Hezekia alifanya mipango ili kujitayarisha iwapo wangezingirwa kwa muda mrefu. (2 Nya. 32:2-4) Lakini hali hiyo ilishughulikiwaje? Yehova alimtuma malaika kuwaangamiza wanajeshi 185,000 wa Senakeribu katika usiku mmoja. Kwa kweli, hata Hezekia hakutarajia hilo litokee!​—2 Fal. 19:35.

Tunajifunza nini kutokana na mambo yaliyompata Yosefu?​—Mwa. 41:42 (Tazama fungu la 13)

13. (a) Tunajifunza nini kutokana na mambo yaliyompata Yosefu? (b) Ni jambo gani lililopita matarajio ya kibinadamu ambalo lilimpata Sara, mke wa Abrahamu?

13 Mfikirie kijana Yosefu, mwana wa Yakobo. Alipokuwa gerezani nchini Misri, je, Yosefu alitarajia kwamba angechaguliwa kuwa wa pili katika mamlaka nchini humo, au kwamba Yehova angemtumia kuokoa familia yake isife njaa? (Mwa. 40:15; 41:39-43; 50:20) Bila shaka mambo ambayo Yehova alifanya yalipita kabisa matarajio ya Yosefu. Mfikirie pia Sara, bibi (nyanya) wa ukoo wa Yosefu. Je, Sara, aliyekuwa amezeeka, alitarajia kwamba Yehova angemwezesha kuzaa mtoto, na si kupata mtoto kupitia kijakazi wake? Hapana shaka kwamba kuzaliwa kwa Isaka kulipita kabisa mambo yote ambayo Sara angeweza kutarajia.​—Mwa. 21:1-3, 6, 7.

14. Tunaweza kuwa na uhakika gani katika Yehova?

14 Ni kweli kwamba hatutarajii Yehova aondoe matatizo yetu yote kimuujiza kabla ya ulimwengu mpya ulioahidiwa; wala hatudai tufanyiwe mambo yanayopita matarajio yetu. Lakini tunajua kuwa Mungu aliyewasaidia watumishi wake kwa njia za ajabu, ndiye Mungu wetu, Yehova. (Soma Isaya 43:10-13.) Uhakika huo unatusaidia kuwa na imani katika yeye. Tunajua kwamba anaweza kufanya lolote linalohitajiwa ili kututia nguvu tutimize mapenzi yake kikamili. (2 Kor. 4:​7-9) Tunajifunza nini kutokana na masimulizi hayo ya Biblia? Kama mfano wa Hezekia, Yosefu, na Sara unavyoonyesha, ikiwa tutabaki waaminifu kwa Yehova, anaweza kutusaidia kushinda hali zinazoonekana kana kwamba hatuwezi kuzishinda.

Ikiwa tutabaki waaminifu kwa Yehova, anaweza kutusaidia kushinda hali zinazoonekana kana kwamba hatuwezi kuzishinda

15. Ni nini kitakachotusaidia kudumisha “amani ya Mungu,” na hilo linawezekanaje?

15 Tunaweza kukabilianaje na hali ngumu na wakati uleule tudumishe “amani ya Mungu”? Ni kwa kudumisha uhusiano mzuri na Mungu wetu, Yehova. Uhusiano huo unawezekana tu “kwa njia ya Kristo Yesu,” aliyetoa uhai wake kuwa dhabihu ya fidia. Uandalizi huo wa fidia ni mojawapo ya mambo mazuri ajabu ambayo Baba yetu amefanya. Yehova anatumia fidia kufunika dhambi zetu, na hilo linatuwezesha kuwa na dhamiri safi na kumkaribia.​—Yoh. 14:6; Yak. 4:8; 1 Pet. 3:21.

ITAILINDA MIOYO YETU NA NGUVU ZETU ZA AKILI

16. Tutapata matokeo gani tunapokuwa na “amani ya Mungu”? Toa mfano.

16 Tutapata matokeo gani tunapokuwa na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote”? Maandiko yanatuambia kwamba ‘itailinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ (Flp. 4:7) Neno la awali lililotafsiriwa ‘linda’ lilitumiwa jeshini. Lilirejelea kikosi cha wanajeshi kilichopewa kazi ya kulinda jiji lenye ngome katika nyakati za kale. Filipi lilikuwa moja ya majiji hayo. Wakaaji wa Filipi walilala bila wasiwasi, wakijua kwamba wanajeshi walikuwa wakilinda malango ya jiji lao. Katika maana hiyohiyo, tunapokuwa na “amani ya Mungu,” akili na mioyo yetu haiingiwi na wasiwasi. Tunajua kwamba Yehova anatujali na anataka tufanikiwe. (1 Pet. 5:10) Kujua hilo kunatulinda tusilemewe na mahangaiko au kuvunjika moyo.

17. Ni nini kitakachotusaidia kukabili wakati ujao tukiwa na uhakika?

17 Hivi karibuni wanadamu watakabili dhiki kubwa zaidi ambayo haijawahi kamwe kutokea hapa duniani. (Mt. 24:21, 22) Hatujui mambo yote yatakayotupata sisi mmoja-mmoja. Hata hivyo, hakuna haja ya kulemewa na mahangaiko. Hata ingawa hatujui kila kitu ambacho Yehova atafanya, tunamjua Mungu wetu. Kutokana na mambo aliyofanya wakati uliopita, tumeona kwamba hata nini kitokee, sikuzote Yehova atatimiza kusudi lake, na nyakati nyingine yeye hufanya hivyo kwa njia inayopita matarajio yetu. Kila mara Yehova anapotufanyia hivyo, tunaweza kujionea “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote” katika njia mpya kabisa.

^ fu. 1 Inaelekea Sila pia alikuwa raia wa Roma.​—Mdo. 16:37.