Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Kuvumilia Majaribu Huleta Baraka

Kuvumilia Majaribu Huleta Baraka

“WEWE ni baba mkatili sana,” akasema ofisa wa KGB kwa ukali. * “Umemwacha mke wako mjamzito na binti yako mdogo. Ni nani atawalisha na kuwatunza? Kana imani yako uende nyumbani!” Nikamjibu hivi: “Sijaiacha familia yangu. Ninyi ndio mlionikamata bila sababu!” Ofisa huyo akajibu hivi kwa dharau: “Ni bora ufanye uhalifu mwingine wowote kuliko kuwa Shahidi.”

Huo ulikuwa mwaka wa 1959 nilipokuwa katika gereza moja katika jiji la Irkutsk nchini Urusi. Acheni nisimulie kwa nini mimi na mke wangu, Maria, tulikuwa tayari “[kuteseka] kwa ajili ya uadilifu” na jinsi tulivyobarikiwa kwa kuendelea kuwa waaminifu.​—1 Pet. 3:13, 14.

Nilizaliwa nchini Ukrainia mwaka wa 1933 katika kijiji cha Zolotniki. Mwaka wa 1937 shangazi yangu na mume wake, ambao walikuwa Mashahidi wa Yehova, walitutembelea kutoka Ufaransa na kutuachia vitabu Government na Deliverance, vilivyochapishwa na shirika la Watch Tower Society. Baba aliposoma vitabu hivyo, alichochewa upya kumwamini Mungu. Kwa kusikitisha, mwaka wa 1939 akawa mgonjwa sana, lakini kabla ya kifo chake akamwambia mama hivi: “Hii ndiyo kweli. Wafundishe watoto kweli hiyo.”

SIBERIA​—ENEO JIPYA LA KUHUBIRI

Mnamo Aprili 1951, serikali ilianza kuwapeleka Mashahidi wote walioishi magharibi mwa Muungano wa Sovieti uhamishoni huko Siberia. Mimi, mama yangu, na mdogo wangu, Grigory, tulifukuzwa kutoka Ukrainia Magharibi. Baada ya kusafiri kwa kilomita 6,000 kwa garimoshi, tuliwasili jijini Tulun, Siberia. Majuma mawili baadaye, kaka yangu, Bogdan, aliwasili kwenye kambi moja jijini Angarsk, ambalo lilikuwa karibu na jiji la Tulun. Alikuwa amehukumiwa kifungo cha miaka 25 ya kazi ngumu.

Mimi, mama yangu, na Grigory tulihubiri katika vijiji vilivyokuwa karibu na jiji la Tulun, lakini tulilazimika kuwa wabunifu tulipokuwa tukihubiri. Kwa mfano, nyakati nyingine tungeuliza, “Umesikia mtu yeyote anayetaka kuuza ng’ombe?” Tulipopata mtu ambaye anataka kuuza ng’ombe, tungemtajia mtu huyo jinsi ng’ombe walivyoumbwa kwa njia ya ajabu. Muda si muda, tungeanza kuzungumza kuhusu Muumba. Katika kipindi hicho, gazeti moja liliandika kuhusu Mashahidi wanaouliza kuhusu ng’ombe lakini kihalisi wanatafuta kondoo! Na ni kweli tulipata watu walio mfano wa kondoo! Tulifurahia kujifunza Biblia na watu wanyenyekevu na wakarimu katika eneo hilo ambalo halikuwa limegawiwa kutaniko lolote. Kwa sasa, kuna kutaniko lenye wahubiri zaidi ya 100 jijini Tulun.

JINSI IMANI YA MARIA ILIVYOJARIBIWA

Mke wangu, Maria, alijifunza kweli akiwa nchini Ukrainia Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikiendelea. Alipokuwa na umri wa miaka 18, ofisa mmoja wa KGB alianza kumsumbua na kumshawishi afanye uasherati naye, lakini alikataa kwa uthabiti. Siku moja aliporudi nyumbani, alimkuta mwanamume huyo amelala kwenye kitanda chake. Maria alitoroka. Akiwa amekasirika, ofisa huyo alimtisha Maria kwa kumwambia kwamba atahakikisha kuwa atafungwa gerezani kwa sababu ya kuwa Shahidi, na kwa hakika, mwaka wa 1952, Maria alihukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani. Alihisi kama Yosefu aliyefungwa gerezani kwa sababu ya utimilifu wake. (Mwa. 39:​12, 20) Dereva aliyemsafirisha Maria kutoka mahakamani kwenda gerezani, alimwambia hivi: “Usiogope. Watu wengi huenda gerezani lakini wanapotoka bado wanaendelea kuheshimika.” Maneno hayo yalimwimarisha.

Kuanzia mwaka wa 1952 hadi 1956, Maria alifanya kazi katika kambi ya kazi ngumu iliyoko karibu na jiji la Gorkiy (sasa Nizhniy Novgorod) nchini Urusi. Aliamriwa ang’oe miti hata wakati wa majira ya baridi kali. Kwa sababu hiyo, alipata matatizo ya kiafya, lakini mwaka wa 1956 aliachiliwa huru na kuhamia jiji la Tulun.

NILITENGANISHWA NA MKE NA WATOTO WANGU

Ndugu mmoja jijini Tulun aliponiambia kwamba dada fulani anakuja, nilienda kumpokea na baiskeli yangu ili nimsaidie mzigo wake. Nilipomwona Maria, nilivutiwa naye mara moja. Haikuwa rahisi kumshawishi anipende, lakini mwishowe nilifaulu. Tulifunga ndoa mwaka wa 1957. Mwaka mmoja baadaye, binti yetu Irina akazaliwa, lakini shangwe ya kuwa pamoja naye ilikatizwa. Mwaka wa 1959, nilikamatwa kwa kuchapisha machapisho ya Biblia. Nilifungwa kifungo cha upweke kwa nusu mwaka. Ili kudumisha amani ya moyoni katika kipindi hicho, nilisali mara nyingi, nikaimba nyimbo za Ufalme, na nikawazia jinsi nitakavyohubiri nitakapoachiliwa huru.

Nikiwa kwenye kambi ya kazi ngumu, mwaka wa 1962

Pindi moja nikiwa gerezani nilipokuwa nikihojiwa, ofisa wa uchunguzi alipaaza sauti na kusema, “Hivi karibuni tutawakomesha kwa kuwakandamiza kama panya sakafuni!” Nikamjibu, “Yesu alisema kwamba habari njema za Ufalme ZITAHUBIRIWA katika mataifa yote na hakuna mtu anayeweza kuzuia.” Kisha, ofisi huyo akabadili mbinu na kujaribu kunishawishi nikane imani yangu, kama nilivyotaja kwenye utangulizi. Waliposhindwa kuvunja azimio langu, nilihukumiwa kifungo cha miaka saba kwenye kambi ya kazi ngumu iliyo karibu na jiji la Saransk. Nilipokuwa njiani kwenda kambini, nilipata habari kwamba binti yetu wa pili, Olga, amezaliwa. Ingawa mke na binti zangu walikuwa mbali, nilifarijika kujua kuwa mimi na Maria tulikuwa washikamanifu kwa Yehova.

Maria Sivulsky pamoja na binti zake, Olga na Irina, mwaka wa 1965

Mara moja kwa mwaka Maria alisafiri kuja Saransk kunitembelea, ingawa safari hiyo ilichukua siku 12 kwa garimoshi kwenda na kurudi. Kila mwaka angeniletea jozi mpya ya viatu, na kwenye visigino vya viatu hivyo angeficha nakala za karibuni za gazeti Mnara wa Mlinzi. Mwaka fulani ulikuwa wa pekee sana kwangu kwa kuwa Maria alinitembelea pamoja na binti zangu wawili. Wazia jinsi nilivyoguswa kuwaona na kuwa pamoja nao!

MAENEO MAPYA NA CHANGAMOTO MPYA

Mnamo 1966, niliachiliwa huru kutoka kambi ya kazi ngumu na sote wanne tulihamia jiji la Armavir, lililo karibu na Bahari Nyeusi. Tukiwa huko, wana wetu Yaroslav na Pavel wakazaliwa.

Haikuchukua muda mrefu kabla ya maofisa wa KGB kuanza kuvamia nyumba yetu, wakitafuta machapisho ya Biblia. Waliyatafuta kila mahali, hata kwenye hori la ng’ombe. Katika moja ya pindi hizo, maofisa hao walitokwa na jasho, na suti zao zilipata vumbi jingi. Maria aliwahurumia, kwa kuwa walikuwa wakifanya yale tu waliyokuwa wameagizwa. Hivyo, akawapa maji ya matunda, na kuwaletea brashi, maji ndani ya beseni, na taulo ili wapanguse vumbi. Baadaye, ofisa mkuu wa KGB alipofika, maofisa walimweleza jinsi walivyotendewa kwa fadhili. Walipoondoka, ofisa huyo alitabasamu na kutupungia mkono. Tulifurahi kuona kwamba tunaweza kupata matokeo mazuri kwa “[kuendelea] kuushinda uovu kwa wema.”​—Rom. 12:21.

Licha ya kuvamiwa mara nyingi, tuliendelea kuhubiri jijini Armavir. Tulisaidia pia kutegemeza kikundi kidogo cha wahubiri katika mji jirani wa Kurganinsk. Ninapata shangwe nyingi sana kujua kwamba sasa kuna makutaniko sita jijini Armavir na manne mjini Kurganinsk.

Hata hivyo, kuna pindi fulani maishani mwetu ambapo hali yetu ya kiroho ilidhoofika. Lakini tunamshukuru Yehova kwamba aliwatumia ndugu waaminifu kuturekebisha na kutuimarisha kiroho. (Zab. 130:3) Pia, lilikuwa jaribu kali kutumikia pamoja na wapelelezi wa KGB ambao waliingia kutanikoni bila sisi kujua. Walionekana kuwa wenye bidii katika huduma. Baadhi yao hata walipata mapendeleo ndani ya tengenezo. Hata hivyo, baada ya muda, tuliwagundua.

Katika mwaka wa 1978, Maria alipata ujauzito alipokuwa na umri wa miaka 45. Kwa kuwa alikuwa na tatizo kubwa la moyo, madaktari waliogopa kwamba angekufa, hivyo wakajaribu kumsadikisha atoe mimba hiyo. Maria akakataa. Kwa sababu hiyo, madaktari fulani walianza kumfuata kotekote hospitalini wakiwa na sindano yenye dawa ambayo ingemfanya apate uchungu wa kuzaa mapema. Ili kumlinda mtoto huyo, ilimbidi Maria atoroke.

Askari wa KGB walituamuru tuhame jiji hilo. Tulihamia kijiji kilichokuwa karibu na jiji la Tallinn nchini Estonia, ambayo wakati huo ilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti. Tukiwa huko, Maria alijifungua mwana mwenye afya nzuri kinyume cha maoni ya madaktari, nasi tukamwita Vitaly.

Baadaye, tulihama Estonia na kwenda kwenye kijiji cha Nezlobnaya kilicho kusini mwa Urusi. Kwa tahadhari tulihubiri kwenye miji ya watalii iliyokuwa karibu, ambayo ilitembelewa na watu kutoka sehemu zote za nchi ya Urusi. Walikuja kwa sababu za kiafya, lakini baadhi yao waliondoka wakiwa na tumaini la uzima wa milele!

KUWALEA WATOTO WETU WAMPENDE YEHOVA

Tulijitahidi sana kuwafundisha wana na binti zetu kumpenda Yehova na kuwachochea wamtumikie. Mara nyingi tuliwakaribisha nyumbani kwetu ndugu waliowawekea watoto wetu mfano mzuri. Mmoja wa wageni hao aliyetutembelea kwa ukawaida alikuwa mdogo wangu Grigory, ambaye alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko kuanzia mwaka wa 1970 hadi 1995. Familia nzima ilifurahi alipotutembelea, kwa kuwa alikuwa mwenye shangwe na mcheshi. Mara kwa mara, wageni walipotutembelea, tulicheza michezo ya Biblia, na watoto wetu wakaanza kupenda masimulizi ya Biblia.

Wanangu na wake zao.

Kuanzia kushoto kwenda kulia, mstari wa nyuma: Yaroslav, Pavel, Jr., Vitaly

Mstari wa mbele: Alyona, Raya, Svetlana

Mnamo 1987, mwana wetu Yaroslav alihamia jiji la Riga nchini Latvia, ambako aliweza kuhubiri bila vizuizi. Lakini alipokataa utumishi wa kijeshi, alihukumiwa kifungo cha mwaka mmoja na nusu na kufungwa katika magereza tisa tofauti-tofauti. Mambo niliyokuwa nimemsimulia kuhusu maisha yangu nikiwa gerezani, yalimsaidia kuvumilia. Baadaye, alianza kutumikia akiwa painia. Mwaka wa 1990, mwana wetu Pavel, aliyekuwa na umri wa miaka 19, alitaka kuwa painia kwenye kisiwa cha Sakhalin, kilicho kaskazini mwa Japani. Mwanzoni hatukutaka aende. Kisiwa hicho kilikuwa na wahubiri 20 tu na kilikuwa umbali wa kilomita 9,000 kutoka nyumbani. Lakini mwishowe tulikubali na huo ulikuwa uamuzi mzuri. Watu kisiwani humo walikubali ujumbe wa Ufalme. Baada ya miaka michache, makutaniko manane yakaanzishwa. Pavel alitumikia huko Sakhalin hadi mwaka wa 1995. Kufikia wakati huo, Vitaly, mwana wetu wa mwisho, ndiye tu aliyekuwa nyumbani. Tangu alipokuwa mtoto, alipenda kusoma Biblia. Alipofika umri wa miaka 14, alianza upainia, na tulipainia pamoja kwa miaka miwili. Tulifurahia sana. Alipofika umri wa miaka 19, Vitaly alipata mgawo wa upainia wa pekee.

Miaka mingi iliyopita katika mwaka wa 1952, ofisa mmoja wa KGB alikuwa amemwambia Maria hivi: “Kana imani yako au ufungwe gerezani kwa miaka kumi. Utakapoachiliwa, utakuwa mpweke na mzee.” Lakini mambo hayakuwa hivyo hata kidogo. Tulihisi kwamba tunapendwa na Mungu wetu mshikamanifu Yehova, watoto wetu, na wengi ambao tulipata pendeleo la kuwasaidia kupata kweli. Mimi na Maria tumepata shangwe ya kutembelea maeneo ambayo watoto wetu walitumikia. Tulijionea jinsi wale waliosaidiwa na watoto wetu walivyothamini kumjua Yehova.

KUTHAMINI WEMA WA YEHOVA

Katika mwaka wa 1991, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria katika eneo letu. Uamuzi huo ulituchochea upya kuhubiri. Kutaniko letu hata lilinunua basi la kutusafirisha kwenda kwenye miji na vijiji vya karibu katika miisho-juma.

Nikiwa na mke wangu mwaka wa 2011

Ninafurahi kwamba Yaroslav na mke wake, Alyona, na Pavel na mke wake, Raya, wanatumikia Betheli, ilhali Vitaly ni mwangalizi wa mzunguko akiungwa mkono na mke wake, Svetlana. Binti yetu mkubwa, Irina, anaishi Ujerumani pamoja na familia yake. Mume wake, Vladimir, na wana wao watatu ni wazee wa kutaniko. Binti yetu Olga anayeishi Estonia hunipigia simu kwa ukawaida. Kwa kusikitisha mke wangu mpendwa, Maria, alikufa mwaka wa 2014. Ninatazamia kwa hamu kumwona tena katika ufufuo! Sasa ninaishi katika jiji la Belgorod, na ndugu kutanikoni wananitegemeza sana.

Kwa miaka ambayo nimemtumikia Yehova, nimejifunza kwamba tunagharimika tunapodumisha utimilifu lakini amani ya akili ambayo Yehova hutupatia ni yenye thamani isiyoelezeka. Baraka ambazo mimi na Maria tumepata kwa kubaki imara zimekuwa nyingi kuliko nilivyowazia. Kabla ya kuanguka kwa Muungano wa Sovieti mwaka wa 1991, kulikuwa na wahubiri 40,000 hivi. Leo, kuna wahubiri zaidi ya 400,000 katika nchi ambazo mwanzoni zilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti! Nina umri wa miaka 83 sasa na ninaendelea kutumikia nikiwa mzee wa kutaniko. Sikuzote, msaada wa Yehova umenipa nguvu za kuendelea kuvumilia. Naam, Yehova amenithawabisha sana.​—Zab. 13:5, 6.

^ fu. 4 KGB ni ufupisho wa Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti katika Kirusi.