Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuvua Utu wa Zamani na Kutourudia Kamwe

Jinsi ya Kuvua Utu wa Zamani na Kutourudia Kamwe

“Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake.”​KOL. 3:9.

NYIMBO: 121, 142

1, 2. Watu wametambua nini kuhusu Mashahidi wa Yehova?

WATU wanaotutazama wamezungumzia sifa nzuri ambazo wameona miongoni mwa watu wa Yehova. Kwa mfano, mwandishi Anton Gill aliandika hivi kuhusu ndugu na dada walioishi Ujerumani wakati wa utawala wa Wanazi: “Mashahidi wa Yehova walichukiwa sana na Wanazi. . . . Kufikia mwaka wa 1939 kulikuwa na Mashahidi 6,000 kwenye [kambi za mateso].” Ingawa hivyo, licha ya mnyanyaso mkali waliovumilia, mwandishi huyo anaongeza kusema kwamba Mashahidi walikuwa wenye “kutegemeka na watulivu chini ya mkazo” na vilevile “walidumisha ushikamanifu na umoja.”

2 Katika siku za karibuni, watu nchini Afrika Kusini waliona sifa zenye kuvutia kama hizo miongoni mwa watu wa Mungu. Wakati uliopita, Mashahidi wa jamii tofauti-tofauti nchini humo hawangeweza kushirikiana kwa uhuru. Lakini Jumapili, Desemba 18, 2011, ilipendeza sana kuona ndugu zetu zaidi ya 78,000 wa jamii mbalimbali nchini Afrika Kusini na kutoka mataifa jirani wakiwa wamekusanyika katika uwanja mkubwa zaidi jijini Johannesburg ili kufurahia programu ya kiroho. Akizungumza kuhusu umati uliokusanyika, meneja mmoja wa uwanja huo alisema hivi: “Huu ndio umati wenye adabu zaidi ambao nimewahi kuona katika uwanja huu. Wote wamevalia vizuri. Nanyi mmesafisha uwanja vizuri sana. Lakini zaidi ya yote, kwa kweli ninyi hamna ubaguzi.”

3. Ni nini kinachofanya undugu wetu uwe wa pekee?

3 Maneno kama hayo kutoka kwa watu wasio Mashahidi yanaonyesha kwamba kwa kweli undugu wetu wa kimataifa ni wa pekee sana. (1 Pet. 5:​9) Hata hivyo, ni nini kinachofanya tuwe tofauti sana na matengenezo mengine? Kwa msaada wa Neno la Mungu na roho yake takatifu, tunajitahidi sana “[kuvua] utu wa zamani.” Badala yake, “[tunajivika] utu mpya.”​—Kol. 3:9, 10.

4. Tutachunguza nini katika makala hii, na kwa nini?

4 Kuvua utu wa zamani ni jambo moja, lakini kutourudia kamwe ni jambo tofauti kabisa. Katika makala hii tutachunguza jinsi ya kuvua utu wa zamani, kwa nini tunapaswa kufanya hivyo bila kukawia, na kwa nini inawezekana kubadilika hata iwe tumejihusisha kadiri gani katika mazoea mabaya. Pia, tutachunguza mambo ambayo wale ambao wamekuwa katika kweli kwa miaka mingi wanaweza kufanya ili wasirudie kamwe utu wa zamani. Kwa nini tunahitaji vikumbusho hivyo? Inasikitisha kwamba baadhi ya watu ambao walimtumikia Yehova wamelegeza msimamo wao na kurudia mazoea ya zamani. Kwa hiyo, sisi sote tunahitaji kutii onyo hili: “Yeye anayefikiri kuwa amesimama na ajihadhari kwamba asianguke.”​—1 Kor. 10:12.

‘UENI’ TAMAA YOYOTE MLIYO NAYO “KWA HABARI YA UASHERATI”

5. (a) Toa mfano unaoonyesha umuhimu wa kuvua utu wa zamani bila kukawia. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kulingana na Wakolosai 3:​5-9, ni mazoea gani yanayoonyesha kwamba tuna utu wa zamani?

5 Ungefanya nini ikiwa nguo zako zingepata uchafu au hata kunuka? Ungevua nguo hizo haraka iwezekanavyo. Vivyo hivyo, tunahitaji kutii bila kukawia amri ya kuvua mazoea yanayopingana na utu wa Mungu. Tungependa kutii mwongozo huu ulio wazi ambao Paulo aliwapa Wakristo wa siku zake: “Yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu.” Acheni tuchunguze mazoea mawili ya dhambi kati ya yale yaliyoorodheshwa na Paulo, yaani, uasherati na uchafu.​—Soma Wakolosai 3:5-9.

6, 7. (a) Maneno ya Paulo yanaonyeshaje kwamba tunahitaji kuchukua hatua thabiti ili kuvua utu wa zamani? (b) Sakura aliishi maisha ya namna gani, na ni nini kilichompa nguvu za kuacha mazoea hayo?

6 Uasherati. Maana ya neno la awali la Biblia linalotafsiriwa “uasherati,” inatia ndani mahusiano ya kingono kati ya watu ambao hawajaoana kisheria na ngono kati ya watu wa jinsia moja. Paulo aliwaambia Wakristo wenzake “[waviue] viungo vya mwili” wao, yaani, waondoe tamaa zozote walizokuwa nazo “kwa habari ya uasherati.” Maneno mazito ambayo Paulo alitumia yanaonyesha wazi kwamba tunahitaji kuchukua hatua thabiti ili kuondoa tamaa hizo mbaya. Hata hivyo, tunaweza kushinda pambano dhidi ya tamaa zenye dhambi.

7 Mfikirie Sakura * anayeishi Japani. Alipokuwa akikua, alipambana na hisia za upweke na kwamba hafai. Tangu alipokuwa na umri wa miaka 15, alianza kuwa na mahusiano ya kingono na watu tofauti-tofauti ili kuondoa hisia za upweke. Alisema hivi kwa aibu: “Kwa sababu hiyo, nilitoa mimba mara tatu. Mwanzoni nilijihisi kuwa mwenye thamani nilipojihusisha katika mahusiano ya kingono, nikifikiri kwamba watu hao walinihitaji na kunipenda. Lakini kadiri nilivyoendelea kujihusisha katika mahusiano hayo, ndivyo nilivyozidi kukosa amani.” Sakura aliendelea kuishi maisha hayo hadi alipofika umri wa miaka 23. Kisha akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi. Sakura alifurahia mambo aliyojifunza na kwa msaada wa Yehova alifaulu kushinda hisia zake za hatia na aibu, na kuacha mwenendo mpotovu. Sasa Sakura anatumikia akiwa painia wa kawaida, naye si mpweke tena. Anasema, “Siku baada ya siku, ninafurahi sana kuona jinsi Yehova anavyonipenda.”

KUSHINDA MAZOEA MACHAFU

8. Taja baadhi ya mambo yanayoweza kutufanya tusiwe safi machoni pa Mungu.

8 Uchafu. Neno la awali la Biblia linalotafsiriwa “uchafu” lina maana pana inayotia ndani mambo mengi zaidi ya dhambi zinazohusisha ngono. Linaweza kurejelea mazoea yenye madhara kama vile kuvuta sigara au kusimulia mizaha michafu. (2 Kor. 7:1; Efe. 5:⁠3, 4) Pia, linatia ndani mazoea ambayo mtu anaweza kufanya akiwa faraghani, kama vile kusoma vitabu vinavyoamsha hamu ya ngono au kutazama ponografia, mambo ambayo yanaweza kumwongoza mtu kupiga punyeto.​—Kol. 3:5. *

9. Kukuza “hamu ya ngono” kunaweza kuwa na matokeo gani mabaya?

9 Watu walio na mazoea ya kutazama ponografia wanakuza “hamu ya ngono,” ambayo inaweza kuwafanya wawe waraibu wa ngono. Utafiti unaonyesha kwamba watu waliokiri kuwa na tamaa isiyoweza kudhibitiwa ya kutazama ponografia walikuwa na dalili zilezile za uraibu kama za waraibu wa kileo na wa dawa za kulevya. Haishangazi kwamba zoea la kutazama ponografia lina matokeo mabaya sana kama vile hisia nyingi za aibu, kutokuwa na bidii kazini, familia zisizo na furaha, talaka, na kujiua. Akisherehekea mwaka mmoja tangu aliposhinda uraibu wa ponografia, mwanamume mmoja aliandika hivi: “Sasa nimeanza kujiamini tena, jambo ambalo nilikuwa nimepoteza.”

10. Ni nini kilichomsaidia Ribeiro kushinda uraibu wa ponografia?

10 Kwa watu wengi, kuepuka kutazama ponografia ni pambano la kila siku. Lakini kama kisa cha Ribeiro kutoka Brazili kinavyoonyesha, tunaweza kushinda pambano hilo. Ribeiro alihama nyumbani kwao alipokuwa tineja na baada ya muda akaajiriwa katika kiwanda cha kutengeneza karatasi upya ili zitumiwe tena. Akiwa huko alianza kutazama ponografia. Anasimulia hivi: “Hatua kwa hatua nikawa mraibu. Hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba nisingeweza kusubiri mwanamke niliyeishi naye atoke nyumbani ili nitazame video za ponografia.” Kisha siku moja akiwa kazini, Ribeiro akaona kitabu chenye kichwa Siri ya Kupata Furaha ya Familia katika rundo la vitabu vilivyohitaji kutengenezwa upya. Alikichukua na kukisoma. Mambo aliyojifunza yalimchochea kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, lakini alichukua muda mrefu kuacha mazoea yake. Mwishowe ni nini kilichomsaidia? Anaeleza hivi: “Kupitia sala, kujifunza Biblia, na kutafakari mambo niliyojifunza, nilianza kuthamini hata zaidi sifa za Mungu na upendo wangu kwake ukaongezeka na kunisaidia kushinda tamaa yangu ya kutazama ponografia.” Ribeiro alisaidiwa na nguvu za Neno la Mungu na roho takatifu kuvua utu wa zamani, akabatizwa, na sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko.

11. Ni nini kinachohitajiwa ili mtu ashinde zoea la kutazama ponografia?

11 Ona kwamba Ribeiro alihitaji kufanya mengi zaidi ya kujifunza tu Biblia ili afaulu kushinda pambano lake. Muda ulihitajiwa ili aruhusu ujumbe wa Biblia uguse moyo wake. Kupitia sala na kutafakari, upendo wake kwa Mungu ulizidi tamaa yake ya ponografia. Kusitawisha upendo wenye nguvu kwa Yehova na kuchukia mambo mabaya ndiyo njia bora ya kuepuka ponografia.​—Soma Zaburi 97:10.

ONDOLEENI MBALI HASIRA, MATUKANO, NA KUSEMA UWONGO

12. Ni nini kilichomsaidia Stephen aache kuwa mwenye hasira na matukano?

12 Watu ambao hukasirika upesi mara nyingi hutumia matusi wanapojieleza. Ni wazi kwamba tabia hiyo haiwezi kuchangia furaha katika familia. Stephen, baba anayeishi Australia, anasema hivi: “Nilikuwa na zoea la kutumia lugha chafu na hata mambo madogo yalinikasirisha. Mimi na mke wangu tulitengana mara tatu na hivyo tukaanza kufanya mipango ya kutafuta talaka.” Kisha, Mashahidi wakaanza kujifunza Biblia na wenzi hao. Kulikuwa na matokeo gani Stephen alipoanza kufuata ushauri wa Biblia? Anasema hivi: “Maisha yetu ya familia yalibadilika sana. Kwa msaada wa Yehova, sasa nina amani na utulivu mwingi, ilhali wakati uliopita ningelipuka kwa hasira wakati wowote hata ikiwa ni jambo dogo tu lililoniudhi.” Sasa, Stephen anatumikia akiwa mtumishi wa huduma na mke wake ametumikia akiwa painia wa kawaida kwa miaka kadhaa. Wazee wa kutaniko la Stephen wanasema hivi: “Stephen ni ndugu mkimya, mwenye bidii, na mnyenyekevu.” Hawakumbuki pindi yoyote walipomwona akiwa mwenye hasira. Je, Stephen anahisi kwamba amefanya maendeleo hayo kwa jitihada zake mwenyewe? Anasema hivi: “Nisingekuwa na baraka hizo ikiwa nisingekubali Yehova anisaidie kubadili utu wangu kabisa.”

13. Kwa nini kuwa wenye hasira ni hatari sana, na Biblia inatoa onyo gani?

13 Biblia ina sababu nzuri za kutuonya dhidi ya hasira, matukano, na kupiga kelele kwa ghadhabu. (Efe. 4:​31) Inasikitisha kwamba mara nyingi tabia hizo husababisha jeuri. Ingawa ulimwengu unaona hasira kuwa jambo la kawaida, ni jambo linalomvunjia heshima Muumba. Watu wengi walilazimika kuvua tabia hizo mbaya kabla ya kuvaa utu mpya.​—Soma Zaburi 37:8-11.

14. Je, inawezekana kwa mtu mwenye jeuri kuwa mpole?

14 Fikiria mfano wa Hans, ambaye anatumikia akiwa mzee wa kutaniko nchini Austria. Mratibu wa baraza la wazee la kutaniko la Hans anasema hivi kumhusu: “Hans ni mmoja wa ndugu wapole zaidi unayeweza kukutana naye.” Lakini Hans hakuwa mpole sikuzote. Alipokuwa tineja alianza kunywa pombe kupita kiasi, na kwa sababu hiyo akawa mjeuri. Pindi fulani alipokuwa amelewa, alikasirika sana na kumwua mpenzi wake, jambo lililofanya ahukumiwe kifungo cha miaka 20. Mwanzoni, maisha ya gerezani hayakubadili utu wake wenye jeuri. Baada ya muda, mama yake alimwomba mzee wa kutaniko awasiliane na mwanawe huko gerezani, na Hans akaanza kujifunza Biblia. Anaeleza hivi: “Nilihitaji kupambana sana ili kuvua utu wangu wa zamani. Baadhi ya Maandiko yaliyonitia moyo ni Isaya 55:7, linalosema: ‘Mtu mwovu aiache njia yake,’ na 1 Wakorintho 6:11, linalosema hivi kuhusu wale walioacha mwenendo wenye dhambi: ‘Na bado wengine wenu mlikuwa hivyo.’ Kwa miaka mingi, Yehova amenisaidia kwa subira kupitia roho yake takatifu kuvaa utu mpya.” Baada ya kutumikia miaka 17 na nusu ya kifungo chake, Hans aliachiliwa kutoka gerezani akiwa Mkristo aliyebatizwa. Anaeleza hivi: “Ninamshukuru Yehova kwa sababu ya huruma zake nyingi na msamaha.”

15. Ni zoea gani ambalo ni la kawaida sana, lakini Biblia inasema nini kulihusu?

15 Mbali na matukano, zoea la kusema uwongo ni sehemu ya utu wa zamani. Kwa mfano, ni jambo la kawaida kwa watu kudanganya ili waepuke malipo ya kodi au waepuke kuwajibika kwa sababu ya dhambi zao. Tofauti na hilo, Yehova ni “Mungu wa ukweli.” (Zab. 31:⁠5) Kwa hiyo, anataka “kila mmoja” wa waabudu wake “[aseme] kweli . . . na jirani yake” na ‘aondolee mbali uwongo.’ (Efe. 4:25; Kol. 3:9) Kwa hiyo, ni lazima tuseme kweli hata ikiwa tutaaibika au mambo hayatatuendea vizuri.​—Met. 6:16-19.

JINSI WALIVYOSHINDA

16. Ni mambo gani yanayoweza kumsaidia mtu kuvua utu wa zamani?

16 Hatuwezi kuvua utu wa zamani kwa nguvu zetu wenyewe. Watu wanaotajwa katika makala hii, yaani, Sakura, Ribeiro, Stephen, na Hans walihitaji kupambana vikali ili kuacha mazoea mabaya waliyokuwa nayo. Walishinda kwa kuruhusu nguvu za Neno la Mungu na roho yake takatifu iongoze akili na mioyo yao. (Luka 11:13; Ebr. 4:12) Ili tunufaike na nguvu za Neno la Mungu na roho yake takatifu, tunapaswa kusoma Biblia kila siku, kutafakari tunayosoma, na kusali daima tupate hekima na nguvu za kutumia shauri la Biblia. (Yos. 1:8; Zab. 119:97; 1 The. 5:17) Tunanufaika pia na Neno la Mungu na roho yake takatifu tunapotayarisha na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. (Ebr. 10:24, 25) Isitoshe, tungependa kutumia vizuri chakula cha kiroho kinachoandaliwa leo kwa ajili ya watu wa Mungu ulimwenguni pote kupitia njia mbalimbali.​—Luka 12:42.

Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuvua utu wa zamani? (Tazama fungu la 16)

17. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

17 Tumechunguza baadhi ya mazoea mabaya ambayo Wakristo wanapaswa kuyavua na kutoyarudia kamwe. Lakini je, hayo tu ndiyo matakwa ya kupata kibali cha Mungu? Hapana. Tunapaswa pia kujivika utu mpya. Katika makala inayofuata, tutachunguza sifa kadhaa za utu mpya tunazohitaji kusitawisha ili ziwe sehemu ya kudumu ya mavazi yetu ya mfano.