Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuvaa Utu Mpya na Kuudumisha

Jinsi ya Kuvaa Utu Mpya na Kuudumisha

“Mjivike utu mpya.”​—KOL. 3:​10.

NYIMBO: 126, 28

1, 2. (a) Tunajuaje kwamba tuna uwezo wa kuvaa utu mpya? (b) Ni sifa zipi za utu mpya zilizoandikwa katika Wakolosai 3:​10-14?

“UTU mpya.” Maneno haya hupatikana mara mbili katika Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. (Efe. 4:24; Kol. 3:10) Yanarejelea utu “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.” Tuna uwezo wa kuvaa utu mpya. Kwa nini? Kwa sababu Yehova aliwaumba wanadamu kwa mfano wake, hivyo, tuna uwezo wa kuonyesha sifa zake nzuri.​—Mwa. 1:26, 27; Efe. 5:1.

2 Ni kweli kwamba kwa sababu tumerithi kutokamilika kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, tunaathiriwa na tamaa mbaya. Huenda pia tumeathiriwa sana na mazingira yetu. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova na rehema zake, tunaweza kufaulu kuwa watu anaotaka tuwe. Ili kuimarisha tamaa yetu ya kufikia lengo hilo, tutachunguza sifa kadhaa za utu mpya ambazo mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika kuzihusu. (Soma Wakolosai 3:10-14.) Pia, tutachunguza jinsi tunavyoweza kuonyesha sifa hizo katika huduma yetu.

“NINYI NYOTE NI MTU MMOJA”

3. Taja sifa moja ya utu mpya.

3 Baada ya kutuhimiza tuvae utu mpya, Paulo anaeleza kwamba kutokuwa na ubaguzi ni sehemu muhimu ya utu huo. Anasema hivi: “Hakuna Mgiriki wala Myahudi, tohara wala kutotahiriwa, mgeni, Msikithe, mtumwa, mtu huru.” * Kwa nini hakupaswi kuwa na ubaguzi unaotegemea rangi, taifa, au hali ya kiuchumi ndani ya kutaniko? Kwa sababu wafuasi wa Kristo “ni mtu mmoja.”​—Kol. 3:11; Gal. 3:28.

4. (a) Watumishi wa Yehova wanapaswa kuwatendeaje wengine? (b) Ni hali gani inayoweza kuvuruga umoja wa Kikristo?

4 Wale waliovaa utu mpya huwatendea waabudu wenzao na watu wasiowafahamu kwa heshima, haidhuru hali yao ya kiuchumi au rangi yao. (Rom. 2:11) Kufanya hivyo kunaweza kuwa changamoto katika sehemu fulani za ulimwengu. Kwa mfano, nchini Afrika Kusini Mashahidi wengi bado wanaishi katika maeneo ambayo zamani yalitengewa watu wa jamii yao, iwe ni maeneo ya matajiri, ya watu weusi, au machotara. Kwa hiyo, ili kuwatia moyo akina ndugu ‘wapanuke,’ mnamo Oktoba 2013 Baraza Linaloongoza liliidhinisha mpango wa pekee wa kuwasaidia akina ndugu wafahamiane vizuri zaidi. (2 Kor. 6:13) Mpango huo ulihusisha nini?

5, 6. (a) Ni mipango gani ilifanywa ili kuimarisha umoja kati ya watu wa Mungu katika nchi fulani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kumekuwa na matokeo gani?

5 Mipango ilifanywa ili makutaniko mawili ya lugha au jamii tofauti yashirikiane baadhi ya miisho-juma. Ndugu na dada wa makutaniko yote mawili walihubiri pamoja, wakahudhuria mikutano pamoja, na kualikana kwenye nyumba zao. Makutaniko mengi yalishiriki katika mpango huo, na ofisi ya tawi ilipokea ripoti nyingi nzuri kuhusu mpango huo, hata kutoka kwa watu wasio Mashahidi. Kwa mfano, kiongozi mmoja wa kidini alichochewa kusema hivi: “Mimi si Shahidi, lakini nimetambua kwamba kazi yenu ya kuhubiri imepangwa vizuri sana na hamna ubaguzi.” Mpango huo ulikuwa na matokeo gani kwa Mashahidi wenyewe?

6 Mwanzoni, Noma, dada anayezungumza Kixhosa aliogopa kuwaalika ndugu wazungu kutoka kutaniko la Kiingereza katika nyumba yake isiyo ya kifahari. Lakini baada ya kuhubiri na Mashahidi wazungu na kukaribishwa nyumbani kwao, alisema hivi kwa mshangao: “Kumbe hawa ni watu wa kawaida kama sisi!” Hivyo, ilipokuwa zamu ya kutaniko la Kixhosa kualika kutaniko la Kiingereza, alipika chakula na kukaribisha baadhi yao. Miongoni mwa wageni wake, kulikuwa na mzee wa kutaniko mzungu. Noma alisema, “Nilivutiwa sana kwamba alikuwa tayari kuketi kwenye kikasha kifupi cha plastiki.” Kwa sababu ya mpango huo unaoendelea, ndugu na dada wengi walipata marafiki wapya na wameazimia kuendelea kupanuka.

“UPENDO MWORORO WENYE HURUMA, FADHILI”

7. Kwa nini kuna uhitaji wa kuendelea kuonyesha fadhili?

7 Tutaendelea kukabili majaribu hadi ulimwengu wa Shetani utakapokwisha. Tunakabiliana na ukosefu wa kazi, matatizo makubwa ya afya, mnyanyaso, misiba ya asili, kupoteza mali kwa sababu ya uhalifu, au hali nyingine ngumu. Ili tutegemezane tunapoteseka au tunapopata matatizo, tunahitaji kusitawisha sifa halisi ya huruma. Kuwa na upendo mwororo kutatuchochea kuonyesha fadhili. (Efe. 4:32) Sifa hizo za utu mpya zitatusaidia kumwiga Mungu na kuwafariji wengine.​—2 Kor. 1:3, 4.

8. Kuwaonyesha watu wote kutanikoni sifa ya huruma na fadhili kunaweza kuwa na matokeo gani mazuri? Toa mfano.

8 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali sana wageni au watu wa hali ya chini katika kutaniko letu? Tunahitaji kuwa marafiki wa watu kama hao na kuwasaidia waone kwamba wao ni wenye thamani kutanikoni. (1 Kor. 12:22, 25) Fikiria kilichompata Dannykarl aliyehamia Japani kutoka Filipino. Akiwa kazini, hakutendewa vizuri kama wafanyakazi wenyeji. Kisha akahudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Dannykarl anasema hivi: “Karibu wote waliohudhuria walikuwa Wajapani, lakini walinikaribisha kwa uchangamfu sana kana kwamba nilikuwa rafiki yao tangu zamani.” Aliendelea kutendewa kwa fadhili, jambo ambalo lilimsaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Alibatizwa, na sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko. Wazee wenzake wanamwona Dannykarl na mkewe, Jennifer, kuwa baraka kutanikoni. Wazee wanasema hivi kuwahusu: “Wanaishi maisha rahisi wakiwa mapainia na wanaweka mfano mzuri wa kutanguliza Ufalme.”​—Luka 12:31.

9, 10. Toa mifano inayoonyesha thawabu za kuwa na sifa ya huruma katika huduma.

9 Tunapowahubiria wengine ujumbe wa Ufalme, tuna nafasi nzuri ya “[kuwatendea] wote mema.” (Gal. 6:​10) Wakichochewa na sifa ya huruma, Mashahidi wengi wanajitahidi kujifunza lugha za wahamiaji. (1 Kor. 9:23) Wamepata baraka nyingi kwa kufanya hivyo. Kwa mfano, Tiffany dada painia anayeishi nchini Australia alijifunza Kiswahili ili asaidie kutaniko la Kiswahili katika jiji la Brisbane. Ingawa ilikuwa vigumu kujifunza lugha hiyo, Tiffany amepata baraka nyingi. Anasema hivi: “Ikiwa ungependa kufanya huduma yako iwe yenye kusisimua, hamia kutaniko la lugha ya kigeni. Ni kama kwenda nchi nyingine bila kuhama nchi yako. Unafurahia undugu wetu wa ulimwenguni pote na kujionea umoja wenye kustaajabisha.”

Ni nini huwachochea wahudumu Wakristo wawahubirie wahamiaji? (Tazama fungu la 10)

10 Fikiria pia kisa cha familia fulani nchini Japani. Binti yao Sakiko, anaeleza hivi: “Katika miaka ya 1990, tulikutana mara nyingi na wahamiaji kutoka Brazili tulipokuwa tukihubiri. Tulipowaonyesha maandiko kama vile Ufunuo 21:3, 4 au Zaburi 37:​10, 11, 29 katika Biblia yao ya Kireno, walisikiliza kwa makini na hata nyakati fulani walitokwa na machozi.” Lakini familia hiyo iliendelea kuonyesha huruma katika njia nyingine. Sakiko anasema hivi: “Tulipoona jinsi walivyokuwa na njaa ya kiroho, tulianza kujifunza Kireno tukiwa familia.” Baadaye, familia hiyo ilisaidia kuanzisha kutaniko la Kireno. Kwa miaka mingi, familia hiyo imewasaidia wahamiaji wengi kuwa watumishi wa Yehova. Sakiko anaongeza hivi: “Tulihitaji kujitahidi sana ili kujifunza Kireno, lakini baraka tulizopata ni nyingi kuliko jitihada tulizofanya. Tunamshukuru sana Yehova.”​—Soma Matendo 10:34, 35.

‘JIVIKENI UNYENYEKEVU WA AKILI’

11, 12. (a) Kwa nini ni muhimu sana kuwa na nia inayofaa ya kuvaa utu mpya? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kuwa wanyenyekevu?

11 Nia yetu ya kujivika utu mpya inapaswa kuwa kumheshimu Yehova, si kupata sifa kutoka kwa watu. Kumbuka kwamba hata kiumbe mmoja wa roho ambaye mwanzoni alikuwa mkamilifu alitenda dhambi kwa sababu alijiruhusu kuwa na kiburi. (Linganisha Ezekieli 28:17.) Hilo linaonyesha kwamba ni vigumu hata zaidi kwa wanadamu wenye dhambi kuepuka kiburi na majivuno! Hata hivyo, inawezekana kujivika unyenyekevu. Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo?

12 Ili tuendelee kuwa wanyenyekevu, tunahitaji kutenga wakati wa kutafakari mambo tunayosoma katika Neno la Mungu kila siku. (Kum. 17:18-20) Tunapaswa kutafakari hasa mafundisho ya Yesu na mfano wake bora wa kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu. (Mt. 20:28) Yesu hata aliosha miguu ya mitume wake. (Yoh. 13:12-17) Pia, tunahitaji kumwomba Yehova mara nyingi atupe roho yake ili itusaidie kupambana na mwelekeo wowote wa kujiona kuwa bora kuliko wengine.​—Gal. 6:3, 4; Flp. 2:3.

13. Tutapata thawabu gani kwa kuwa wanyenyekevu?

13 Soma Methali 22:4. Unyenyekevu ni takwa kwa waabudu wote wa kweli, na kusitawisha sifa hiyo huleta thawabu nyingi. Kuwa wanyenyekevu kutatusaidia kuchangia amani na umoja kutanikoni. Pia, kusitawisha na kuimarisha sifa ya unyenyekevu kutatuwezesha kupokea fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Mtume Petro alisema hivi: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu wa akili kuelekeana ninyi wenyewe, kwa sababu Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”​—1 Pet. 5:5.

“JIVIKENI . . . UPOLE . . . NA USTAHIMILIVU”

14. Ni nani aliye kielelezo bora cha kuonyesha upole na subira?

14 Ulimwenguni leo, watu wapole na wenye ustahimilivu au subira huonwa kuwa dhaifu. Maoni hayo si ya kweli hata kidogo! Sifa hizo nzuri zinatokana na Mungu Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. Yehova Mungu ndiye kielelezo bora cha kuonyesha upole na subira. (2 Pet. 3:9) Fikiria jinsi Yehova, kupitia malaika wake, alivyojibu maswali ya Abrahamu na Loti. (Mwa. 18:22-33; 19:18-21) Pia, kwa zaidi ya miaka 1,500, Yehova alilivumilia taifa lililoasi la Israeli.​—Eze. 33:11.

15. Yesu aliweka mfano gani katika kuonyesha upole na subira?

15 Yesu alikuwa mwenye “tabia-pole.” (Mt. 11:29) Alionyesha subira ya hali ya juu aliposhughulika na udhaifu wa wafuasi wake. Katika huduma yake yote duniani, Yesu alivumilia alipochambuliwa isivyo haki na viongozi wa kidini. Ingawa hivyo, bado alikuwa mwenye tabia pole na subira hata alipouawa bila hatia. Akiwa na maumivu makali sana juu ya mti wa mateso, Yesu alimwomba Baba yake awasamehe waliomwua kwa sababu, kama alivyosema, “hawajui wanalofanya.” (Luka 23:34) Huo ni mfano mzuri sana wa upole na subira hata alipokuwa na mkazo na maumivu makali!​—Soma 1 Petro 2:21-23.

16. Tunaweza kuonyeshaje upole na subira?

16 Tunaweza kuonyeshaje upole na subira? Paulo alitaja njia moja alipowaandikia waamini wenzake hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.” (Kol. 3:​13) Kwa hakika, tunahitaji kuwa na sifa ya upole na subira ili kutii amri hiyo. Lakini tunaposamehe, tunachangia na kudumisha umoja kutanikoni.

17. Kwa nini sifa ya upole na subira ni muhimu?

17 Kujivika sifa ya upole na subira ni takwa kwa kila Mkristo. Ni lazima tusitawishe sifa hizo ili tupate wokovu. (Mt. 5:5; Yak. 1:21) Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba tunapoonyesha sifa hizo, tunamheshimu Yehova na kuwasaidia wengine watii shauri la Biblia.​—Gal. 6:1; 2 Tim. 2:24, 25.

“JIVIKENI UPENDO”

18. Kuna uhusiano gani kati ya upendo na kutokuwa na ubaguzi?

18 Sifa zote ambazo tumechunguza kufikia sasa zinahusiana sana na sifa ya upendo. Kwa mfano, mwanafunzi Yakobo alihitaji kuwashauri ndugu zake waliowapendelea matajiri na kuwapuuza maskini. Alionyesha kwamba kufanya hivyo kulipingana na sheria hii ya kifalme: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” Halafu akaongeza hivi: “Mkiendelea kuonyesha upendeleo, mnafanya dhambi.” (Yak. 2:8, 9) Kinyume cha hilo, upendo utatuchochea kuepuka ubaguzi wowote unaoweza kutokana na tofauti za kielimu, za rangi, au za kiuchumi. Kwa hakika, kutokuwa na ubaguzi kunamaanisha mengi zaidi ya mambo yanayoonekana kwa nje. Ni lazima kuwe sehemu ya utu wetu.

19. Kwa nini ni muhimu tujivike upendo?

19 Pia, upendo ni wenye “ustahimilivu na wenye fadhili” na “haujivuni.” (1 Kor. 13:4) Kwa kweli, tunahitaji subira, fadhili, na unyenyekevu ili tuendelee kushiriki na jirani zetu ujumbe wa Ufalme. (Mt. 28:19) Sifa hizohizo zinafanya iwe rahisi zaidi kwetu kuishi kwa amani na ndugu na dada wote kutanikoni. Tunapata thawabu gani kwa kuonyesha upendo huo? Unatokeza makutaniko yenye umoja yanayomletea Yehova sifa na kuwavutia watu wanaopendezwa. Inafaa kwamba Biblia inamalizia ufafanuzi wa utu mpya kwa maneno haya mazito: “Zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”​—Kol. 3:14.

“MNAPASWA KUFANYWA UPYA”

20. (a) Tunapaswa kujiuliza maswali gani, na kwa nini? (b) Tunatazamia nini wakati ujao?

20 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi, ‘Ni mambo gani mengine ninayoweza kufanya ili kuvua utu wa zamani na kutourudia kamwe?’ Tunahitaji kusali kwa bidii ili tupate msaada wa Mungu na kujitahidi sana kushinda mwelekeo au zoea lolote linaloweza kutuzuia kurithi Ufalme wa Mungu. (Gal. 5:19-21) Pia, tunahitaji kujiuliza hivi, ‘Je, ninahitaji kuendelea kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yangu?’ (Efe. 4:23, 24) Kuvaa na kudumisha utu mpya ni jambo ambalo Wakristo wote wanapaswa kuendelea kufanya mpaka tutakapofaulu kuuvaa utu huo kikamili. Wazia jinsi maisha yatakavyokuwa mazuri wakati watu wote watakapokuwa wamevaa utu mpya kikamilifu!

^ fu. 3 Katika nyakati za Biblia, Wasikithe walionwa kuwa watu wasio wastaarabu.