Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna Tunavaa na Kulinda Utu Mupya

Namna Tunavaa na Kulinda Utu Mupya

‘Mujivike [muvae] utu mupya.’​—KOL. 3:10.

NYIMBO: 43, 106

1, 2. (a) Namna gani tunajua kuwa tuko na uwezo wa kuvaa utu mupya? (b) Ni sifa gani za utu mupya zenye kutajwa katika Wakolosai 3:10-14?

‘UTU mupya.’ Maneno hayo yanapatikana mara mbili katika Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. (Efe. 4:24; Kol. 3:10) Yanazungumuzia utu wenye “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.” Tuko na uwezo wa kuvaa utu huo mupya. Sababu gani? Kwa sababu Yehova aliumba wanadamu kwa mufano wake, kwa hiyo, alitupatia uwezo wa kuonyesha sifa zake za muzuri.​—Mwa. 1:26, 27; Efe. 5:1.

2 Ni kweli kwamba, kwa sababu ya hali ya kukosa kukamilika yenye tuliriti kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, tunakuwa na tamaa za mubaya. Pia pengine tumechochewa sana na watu wenye kutuzunguka. Lakini, kwa musaada wa Yehova wenye huruma, tunaweza kuwa watu wenye anapenda tukuwe. Ili kutia nguvu tamaa yetu ya kufikia muradi huo, tutazungumuzia sifa mbalimbali za utu mupya zenye mutume Paulo aliandika kupitia uongozi wa roho ya Mungu. (Soma Wakolosai 3:10-14.) Tutazungumuzia pia namna tunaweza kuonyesha sifa hizo katika kazi yetu ya kuhubiri.

‘NINYI NYOTE NI MUTU MUMOJA’

3. Ni sifa gani yenye kuwa sehemu ya utu mupya?

3 Kisha kututia moyo tuvae utu mupya, Paulo anaonyesha kuwa kuepuka kuwa na ubaguzi ni sehemu ya maana sana ya utu mupya. Alisema hivi: ‘Hakuna Mugiriki wala Muyahudi, tohara wala kutotahiriwa, mugeni, Musikithe, mutumwa, mutu huru.’ * Katika kutaniko, sababu gani tunapaswa kuepuka kubagua watu kwa sababu ya rangi yao ya ngozi, inchi yao, ao hali yao ya maisha? Kwa sababu wanafunzi wa kweli wa Kristo ‘wote ni mutu mumoja.’​—Kol. 3:11; Gal. 3:28.

4. (a) Watumishi wa Yehova wanapaswa kutendea wengine namna gani? (b) Ni hali gani inaweza kutokeza magumu juu ya umoja wa Wakristo?

4 Wale wenye kuvaa utu mupya wanatendea Wakristo wenzao na watu wengine kwa heshima, bila kuangalia hali yao ya maisha ao rangi yao ya ngozi. (Rom. 2:11) Inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo katika maeneo fulani ya dunia. Kwa mufano, katika Afrika ya Kusini, Mashahidi wengi wangali wanaishi katika maeneo yenye watu wa rangi fulani walipewa, iwe katika miji tajiri, miji ya watu weusi, ao maeneo kwenye watu wenye kutokana na muchanganyiko wa rangi ya ngozi wangepaswa kuishi. Kwa hiyo, ili kutia moyo ndugu zetu ‘wapanuke,’ katika Mwezi wa 10, 2013 Baraza Lenye Kuongoza lilikubali mupango wa pekee wa kusaidia ndugu wafikie kujuana zaidi. (2 Kor. 6:13) Mupango huo ulitia ndani nini?

5, 6. (a) Ili kutia nguvu umoja kati ya watu wa Mungu katika inchi fulani, ni mipango gani ilifanywa? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.) (b) Mupango huo umeleta matokeo gani?

5 Mipango ilifanywa ili makutaniko mbili ya luga tofauti ao ya watu wenye kuwa na rangi tofauti ya ngozi wakutane pamoja katika siku fulani za mwisho wa juma. Ndugu na dada wa makutaniko hayo walihubiri pamoja, walikusanyika pamoja, na kukaribishana kwa furaha katika nyumba zao. Mamia ya makutaniko yalifanya hivyo, na biro ya tawi ilipata ripoti nyingi za muzuri juu ya mupango huo, hata kutoka kwa watu wa inje. Kwa mufano, kiongozi mumoja wa dini alichochewa kusema hivi: “Siko Shahidi, lakini ninaweza kusema kuwa kazi yenu ya kuhubiri inapangwa muzuri sana, na muko na umoja kati ya watu wa rangi tofauti ya ngozi.” Mupango huo ulikuwa na matokeo gani juu ya Mashahidi wa Yehova?

6 Mwanzoni, dada Noma mwenye kuzungumuza luga ya Xhosa alikuwa anasita kualika katika nyumba yake ya hali ya chini ndugu wazungu wa kutaniko la Kiingereza. Lakini kisha kuhubiri pamoja na Mashahidi wazungu na kukaribishwa muzuri katika nyumba zao, alisema hivi: “Ni watu wa kawaida kama sisi!” Kwa hiyo, wakati kutaniko la luga ya Xhosa lilipaswa kukaribisha ndugu wa kutaniko la luga ya Kiingereza, alitayarisha chakula na kualika wageni fulani. Kati ya wageni hao kulikuwa muzungu mumoja mwenye kuwa muzee wa kutaniko. Noma alisema hivi: “Nilishangaa kuona kuwa alikuwa tayari kukaa kwenye kiti cha hali ya chini.” Kwa sababu ya mupango huo wenye kuendelea, ndugu na dada wengi walipata marafiki wapya na wameazimia kuendelea kupanuka ili kujua ndugu na dada wengine.

MUVAE HURUMA NA FAZILI

7. Sababu gani tunapaswa kuendelea kuonyesha sifa ya huruma?

7 Tutaendelea kupatwa na magumu mupaka mwisho wa ulimwengu wa Shetani ufike. Tunapambana na hali ya kukosa kazi, magonjwa hatari, mateso, misiba ya asili, kupoteza vitu vya kimwili kwa sababu ya jeuri, ao magumu mengine. Ili tutegemezane katika magumu ao mateso yetu, tunapaswa kuwa na huruma yenye kutoka moyoni. Kuwa na huruma kutatuchochea kutendea wengine kwa fazili ao wema. (Efe. 4:32) Sifa hizo za utu mupya zitatusaidia kumuiga Mungu na kufariji wengine.​—2 Kor. 1:3, 4.

8. Ikiwa tunaonyesha wengine huruma na wema katika kutaniko, hilo linaweza kuwa na matokeo gani ya muzuri? Toa mufano.

8 Namna gani tunaweza kuonyesha kuwa tunahangaikia hata zaidi watu wenye kutoka katika inchi zingine ao wale wenye kuwa na maisha ya hali ya chini katika kutaniko letu? Tunapaswa kuwategemeza na kuwasaidia waone kuwa ni wa maana katika kutaniko. (1 Kor. 12:22, 25) Fikiria mambo yenye yalimufikia Dannykarl mwenye alitoka katika Ufilipino na kuhamia katika Japani. Kwenye alikuwa anatumika, hakutendewa sawasawa na wafanyakazi wengine wa inchi hiyo. Kisha akahuzuria mukutano wa Mashahidi wa Yehova. Dannykarl anasema hivi: “Karibu watu wote walikuwa Wajapani, lakini walinikaribisha kwa furaha, ilikuwa kama vile nilikuwa ninawajua zamani.” Waliendelea kumutendea kwa wema, na hilo lilimusaidia afanye maendeleo ya kiroho. Alibatizwa na leo iko muzee wa kutaniko. Wazee wengine wanamuona Dannykarl na Jennifer bibi yake, kuwa baraka katika kutaniko. Wazee wanasema hivi juu yao: “Wanaishi maisha mepesi sana na wanafanya kazi ya upainia na wanaweka mufano muzuri wa kutafuta Ufalme kwanza.”​—Lu. 12:31.

9, 10. Kuonyesha huruma katika kazi ya kuhubiri kunaleta baraka gani? Toa mufano.

9 Wakati tunatangazia wengine ujumbe wa Ufalme, tunakuwa na nafasi ya muzuri ya kuwatendea “wote mema.” (Gal. 6:10) Kwa sababu ya kuonea huruma watu wenye kuhamia katika inchi yao, Mashahidi wengi wanajikaza kujifunza luga mupya. (1 Kor. 9:23) Hilo limeleta baraka kubwa. Kwa mufano, dada mumoja painia wa Australia mwenye kuitwa Tiffany alijifunza Kiswahili ili aweze kusaidia katika kutaniko la luga ya Kiswahili katika muji wa Brisbane. Hata kama ilikuwa vigumu kwa Tiffany kujifunza luga hiyo, amepata baraka katika maisha yake. Anasema hivi: “Ikiwa unapenda utumishi wenye kufurahisha, utumikie katika kutaniko la luga ya kigeni. Ni kama vile unafanya safari bila kutoka katika muji wako. Unajionea kama tuko familia ya ndugu na dada ya ulimwenguni pote na unajionea umoja wao wa ajabu.”

Ni nini inachochea Wakristo wasaidie watu wenye kuhamia katika inchi yao? (Picha hii inapatana na fungu la 10)

10 Fikiria pia mufano wa familia moja katika Japani. Sakiko, mutoto mwanamuke katika familia hiyo, anasema hivi: “Katika miaka ya 1990, katika mahubiri tulizoea kukutana na watu wenye kutoka Brazili. Wakati tulikuwa tunawaonyesha maandiko katika Biblia yao ya luga ya Kireno (Portugais), kama vile Ufunuo 21:3, 4 ao Zaburi 37:10, 11, 29, walisikiliza kwa uangalifu na wakati fulani walitoa hata machozi.” Lakini huruma ya familia hiyo haikuishia hapo. Sakiko anasema hivi: “Wakati tuliona njaa yao ya kiroho, sisi wote katika familia tulianza kujifunza luga ya Kireno.” Kisha, familia hiyo ilisaidia kuanzisha kutaniko la luga ya Kireno. Kwa miaka mingi, familia hiyo ilisaidia watu wengi wenye kuhamia katika inchi yao wakuwe watumishi wa Yehova. Sakiko anaongezea hivi: “Iliomba bidii nyingi ili kujifunza Kireno, lakini baraka zenye tumepata ni nyingi zaidi kuliko bidii yenye tulifanya. Tuko wenye shukrani sana kwa Yehova.”​—Soma Matendo 10:34, 35.

MUVAE ‘UNYENYEKEVU’

11, 12. (a) Sababu gani tunapaswa kuwa na kusudi lenye kufaa la kuvaa utu mupya? (b) Ni nini itatusaidia tuendelee kuwa wanyenyekevu?

11 Kusudi letu la kuvaa utu mupya linapaswa kuwa kumutukuza Yehova, hatufanye hivyo ili wanadamu watusifu. Kumbuka kuwa hata kiumbe wa roho mwenye alikuwa mukamilifu alifanya zambi kwa sababu aliruhusu majivuno yakomae ndani ya moyo wake. (Linganisha Ezekieli 28:17.) Kwa hiyo, ni vigumu zaidi kwa wanadamu wenye hawakamilike kuepuka majivuno na kiburi! Lakini, inawezekana tuvae unyenyekevu. Ni nini itatusaidia kufanya hivyo?

12 Ili tuendelee kuwa wanyenyekevu, tunapaswa kupanga wakati wa kutafakari kila siku juu ya mambo yenye tunasoma katika Neno la Mungu. (Kum. 17:18-20) Zaidi sana, ni muzuri tufikirie mafundisho ya Yesu na mufano wake muzuri sana wa kutenda kwa unyenyekevu. (Mt. 20:28) Na hata Yesu alinawisha mitume wake miguu. (Yoh. 13:12-17) Pia, tunapaswa kuendelea kumuomba Mungu roho yake takatifu ili itusaidie kupiganisha mawazo yoyote ya kujiona kuwa wa maana kuliko wengine.​—Gal. 6:3, 4; Flp. 2:3.

13. Kuwa wanyenyekevu kunaleta baraka gani?

13 Soma Methali 22:4. Wakristo wote wanapaswa kuwa na sifa ya unyenyekevu, na sifa hiyo inaleta baraka kubwa. Kuwa wanyenyekevu kutatusaidia kuendeleza amani na umoja katika kutaniko. Pia Mungu atatuonyesha fazili zake zisizostahiliwa ikiwa tunakuwa na sifa ya unyenyekevu na kuikomalisha. Mutume Petro alisema hivi: ‘Ninyi nyote mujifunge unyenyekevu wa akili kuelekeana ninyi wenyewe, kwa sababu Mungu anawapinga wenye majivuno, lakini anawapa wanyenyekevu fazili zisizostahiliwa.’​—1 Pet. 5:5.

MUVAE ‘UPOLE NA USTAHIMILIVU’

14. Ni nani mwenye kuwa mufano muzuri zaidi wa kuonyesha upole na ustahimilivu?

14 Katika ulimwengu wa leo watu wenye kuonyesha sifa ya upole na ustahimilivu ao subira wanaonwa kuwa wazaifu. Mawazo hayo hayako ya kweli hata kidogo! Sifa hizo za muzuri zinatoka kwa Mutu mwenye nguvu zaidi katika ulimwengu. Yehova ni mufano muzuri zaidi wa kuonyesha upole na ustahimilivu. (2 Pet. 3:9) Fikiria namna alijibia kupitia malaika zake wakati Abrahamu na Loti walimuuliza maulizo. (Mwa. 18:22-33; 19:18-21) Pia, kwa miaka zaidi ya 1 500 Yehova alivumilia taifa la Israeli lenye kuasi.​—Eze. 33:11.

15. Yesu aliweka mufano gani juu ya kuonyesha upole na ustahimilivu?

15 Yesu alikuwa mwenye “tabia-pole.” (Mt. 11:29) Alionyesha subira kubwa kwa kuvumilia makosa ya wanafunzi wake. Wakati wa utumishi wake hapa duniani, Yesu alivumilia maneno yenye kuchambua ya viongozi wa dini wenye walimupinga. Na aliendelea kuonyesha sifa ya upole na uvumilivu mupaka wakati aliuawa bila sababu. Wakati Yesu alikuwa katika maumivu makali sana kwenye muti wa mateso, alisali kwa Baba yake na kumuomba asamehe wale wenye walimuhukumu kifo. Alisema hivi: ‘Kwa maana hawajue wanalofanya.’ (Lu. 23:34) Huo ni mufano muzuri sana wa kuonyesha upole na ustahimilivu wakati wa hali zenye maumivu na mahangaiko!​—Soma 1 Petro 2:21-23.

16. Namna gani tunaweza kuonyesha sifa ya upole na ustahimilivu?

16 Namna gani tunaweza kuonyesha sifa ya upole na ustahimilivu? Paulo alitaja njia moja ya kufanya hivyo wakati aliandikia hivi Wakristo wenzake: ‘Muendelee kuvumiliana na kusameheana kwa hiari [kwa kupenda] ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi mufanye vivyo hivyo pia.’ (Kol. 3:13) Kwa kweli, inaomba tukuwe na sifa ya upole na ustahimilivu ili tutii amri hiyo. Lakini wakati tunasamehe wengine, tunaendeleza na kulinda umoja katika kutaniko.

17. Sababu gani sifa ya upole na ustahimilivu ni za maana?

17 Kila Mukristo anapaswa kuonyesha sifa ya upole na ustahimilivu. Ni sifa za maana zenye tunapaswa kuwa nazo ili tuokolewe. (Mt. 5:5; Yak. 1:21) Na jambo la maana zaidi ni kwamba wakati tunaonyesha sifa hizo tunamutukuza Yehova na tunasaidia wengine wafuate mashauri ya Biblia.​—Gal. 6:1; 2 Tim. 2:24, 25.

MUVAE ‘UPENDO’

18. Sifa ya upendo inapatana namna gani na sifa na kuepuka kuwa na ubaguzi?

18 Sifa zote zenye tumezungumuzia zinapatana sana na upendo. Kwa mufano, mwanafunzi Yakobo alishauria ndugu zake kwa sababu walikuwa wanaonyesha matajiri upendeleo na kuzarau watu masikini. Alionyesha kuwa tabia hiyo ilivunja sheria ya kifalme yenye kusema hivi: ‘Mupende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Kisha, aliongezea hivi: ‘Mukiendelea kuonyesha upendeleo, munafanya zambi.’ (Yak. 2:8, 9) Lakini, upendo utatuchochea tuepuke kubagua wengine kwa sababu ya masomo yao, rangi yao ya ngozi, ao hali yao ya maisha. Kwa kweli, sifa ya kuepuka kuwa na ubaguzi haipaswe kuwa ya inje tu. Inapaswa kutoka kabisa katika moyo wetu.

19. Sababu gani ni jambo la maana tuvae upendo?

19 Pia, upendo ‘ni wenye ustahimilivu na wenye fazili’ na ‘haujivune.’ (1 Kor. 13:4) Inaomba kabisa kuwa na ustahimilivu, fazili, na unyenyekevu ili kuendelea kutangazia majirani wetu ujumbe wa Ufalme. (Mt. 28:19) Sifa hizo zinafanya pia ikuwe vyepesi kusikilizana na ndugu na dada wote katika kutaniko. Kuonyesha upendo kama huo kunaleta baraka gani? Kunasaidia makutaniko yakuwe na umoja wenye kumuletea Yehova utukufu na kunafanya wapya wapendezwe na kweli. Ndiyo sababu Biblia inamalizia mafasirio ya utu mupya kwa kusema kweli hii yenye nguvu: ‘Zaidi ya mambo haya yote, mujivike upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.’​—Kol. 3:14.

MUENDELEE “KUFANYWA UPYA”

20. (a) Tunapaswa kujiuliza maulizo gani, na sababu gani? (b) Tunangojea kwa hamu wakati gani?

20 Kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninapaswa kufanya mambo gani mengine ili kuvua na kuepuka utu wa zamani?’ Tunapaswa kusali sana kwa Mungu atusaidie na kujikaza sana ili kuachana na mawazo ao matendo yoyote yenye yanaweza kutuzuia kuriti Ufalme wa Mungu. (Gal. 5:19-21) Tunapaswa pia kujiuliza hivi: ‘Ninaendelea kubadilisha namna yangu ya kufikiri ili nimupendeze Yehova?’ (Efe. 4:23, 24) Wakristo wote wanapaswa kuendelea kuvaa na kulinda utu mupya mupaka wakati wataweza kufanya hivyo kwa ukamili. Wazia namna maisha yatakuwa muzuri sana wakati watu wote wenye tunajua watakuwa wamevaa utu mupya kwa ukamilifu!

^ fu. 3 Wakati wa zamani, Wasikithe walizarauliwa na kuonwa kuwa watu washenzi.