Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kweli Huleta, “Si Amani, Bali Upanga”

Kweli Huleta, “Si Amani, Bali Upanga”

“Msifikiri nilikuja kuleta amani duniani; nilikuja kuleta, si amani, bali upanga.”—MT. 10:34.

NYIMBO: 123, 128

1, 2. (a) Tunafurahia amani gani sasa? (b) Kwa nini hatuwezi kuwa na amani kamili wakati huu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

SISI sote tunapenda kuishi kwa amani, bila mahangaiko. Tunashukuru sana kwamba Yehova anatupatia “amani ya Mungu”—utulivu wa moyoni unaoweza kutulinda dhidi ya fikira na hisia zinazotuhangaisha! (Flp. 4:6, 7) Pia, kwa kuwa tumejiweka wakfu kwa Yehova, tunafurahia “amani pamoja na Mungu,” yaani, uhusiano mzuri pamoja naye.—Rom. 5:1.

2 Hata hivyo, wakati wa Mungu wa kuleta amani kamili bado haujafika. Siku hizi za mwisho zilizo hatari zimejaa migogoro, na watu wengi ni wagomvi. (2 Tim. 3:1-4) Tukiwa Wakristo, ni lazima tupigane vita vya kiroho dhidi ya Shetani na mafundisho ya uwongo anayoendeleza. (2 Kor. 10:4, 5) Hata hivyo, huenda watu wa ukoo ambao si waamini wakahatarisha hata zaidi amani yetu. Baadhi yao huenda wakadhihaki mambo tunayoamini, wakadai kwamba tunaleta migawanyiko katika familia, au wakatishia kututenga na familia ikiwa hatutaacha imani yetu. Tunapaswa kuonaje upinzani kutoka kwa watu wa familia? Tunaweza kukabilianaje kwa mafanikio na changamoto zinazotokana na upinzani huo?

TUNAPASWA KUONAJE UPINZANI KUTOKA KWA WATU WA FAMILIA?

3, 4. (a) Mafundisho ya Yesu yana matokeo gani? (b) Ni wakati gani hasa inapokuwa vigumu kuwa mfuasi wa Yesu?

3 Yesu alijua kwamba mafundisho yake yangeleta mgawanyiko na kwamba wafuasi wake wangehitaji kuwa na ujasiri wanapokabili upinzani. Upinzani huo ungeweza kuathiri uhusiano wenye amani kati ya watu wa familia. Yesu alisema hivi: “Msifikiri nilikuja kuleta amani duniani; nilikuja kuleta, si amani, bali upanga. Kwa maana nilikuja kuleta mgawanyiko, mtu kumpinga baba yake, binti kumpinga mama yake, mke aliye mchanga kumpinga mama-mkwe wake. Kwa kweli, adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.”—Mt. 10:34-36.

4 Yesu aliposema “Msifikiri nilikuja kuleta amani,” alimaanisha kwamba baadhi ya wasikilizaji wake walihitaji kufikiria kuhusu matokeo ya kuwa wafuasi wake. Mafundisho yake yangeweza kuleta mgawanyiko. Bila shaka, nia ya Yesu ilikuwa ni kutangaza ujumbe wa kweli wa Mungu, na si kuharibu uhusiano kati ya watu wa familia. (Yoh 18:37) Hata hivyo, kushika kwa uaminifu mafundisho ya Kristo kungetokeza changamoto ikiwa marafiki wa karibu au watu wa familia wangeikataa kweli.

5. Wafuasi wa Yesu wamekabili mambo gani?

5 Yesu alionyesha kuwa maumivu yanayotokana na kupingwa na watu wa familia ni sehemu ya mateso ambayo wafuasi wake walipaswa kuwa tayari kuvumilia. (Mt. 10:38) Ili kumpendeza Kristo, wanafunzi wake wamelazimika kuvumilia dhihaka na hata wengine wametengwa na familia zao. Hata hivyo, wamepata mengi zaidi kuliko waliyopoteza.—Soma Marko 10:29, 30.

6. Tunapaswa kukumbuka nini watu wetu wa ukoo wanapopinga jitihada zetu za kumwabudu Yehova?

6 Hata ikiwa watu wa ukoo wanapinga jitihada zetu za kumwabudu Yehova, bado tunaendelea kuwapenda. Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba upendo wetu kwa Mungu na Kristo ndio unaochukua nafasi ya kwanza. (Mt. 10:37) Pia, tunapaswa kutambua kwamba Shetani atajaribu kutumia upendo wetu kwa watu wa familia ili kuvunja utimilifu wetu. Hebu tuchunguze baadhi ya hali zinazosababisha upinzani katika familia na tuone jinsi tunavyoweza kukabiliana kwa mafanikio na changamoto zinazotokezwa na hali hizo.

MWENZI WA NDOA AMBAYE SI MWAMINI

7. Wale walio na mwenzi ambaye si mwamini wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu hali yao?

7 Biblia inaonya kwamba wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Kor. 7:28) Ikiwa una mwenzi ambaye si mwamini, huenda ukawa na mikazo na mahangaiko yanayozidi yale ya kawaida katika ndoa. Hata hivyo, ni muhimu uwe na maoni kama ya Yehova kuhusu hali yako. Ingawa mwenzi wako hayuko tayari kumfuata Kristo kwa sasa, hiyo si sababu halali ya kutengana au kutalikiana. (1 Kor. 7:12-16) Ijapokuwa mume ambaye si mwamini haongozi familia yake katika mambo ya kiroho, anapaswa kuheshimiwa kwa sababu ya daraka lake akiwa kichwa cha familia. Vivyo hivyo, mume Mkristo anapaswa kumwonyesha mke wake ambaye si mwamini upendo wa kujidhabihu na wororo.—Efe. 5:22, 23, 28, 29.

8. Unaweza kujiuliza maswali gani ikiwa mwenzi wako anaiwekea ibada yako vizuizi fulani?

8 Vipi ikiwa mwenzi wako anaiwekea ibada yako vizuizi fulani? Kwa mfano, dada mmoja aliambiwa na mume wake kwamba anaweza kushiriki huduma ya shambani katika siku fulani tu za juma. Ikiwa unakabili hali kama hiyo, jiulize hivi: ‘Je, mwenzi wangu anataka niache kabisa kumwabudu Mungu wangu? Ikiwa sivyo, je, ninaweza kukubali ombi hilo?’ Kuwa na usawaziko kutakusaidia kuepuka ugomvi usio wa lazima katika ndoa.—Flp. 4:5.

9. Mkristo anaweza kuwafundishaje watoto wake kumheshimu mzazi ambaye si mwamini?

9 Inaweza kuwa vigumu zaidi kuwazoeza watoto wako ikiwa mwenzi wako si mwamini. Kwa mfano, unahitaji kuwafundisha watoto wako kutii amri hii ya Biblia: “Mheshimu baba yako na mama yako.” (Efe. 6:1-3) Lakini vipi ikiwa mwenzi wako hafuati viwango vya juu vya maadili vya Biblia? Weka mfano mzuri kwa kumheshimu mwenzi wako. Kazia sifa zake nzuri, na umweleze kwamba unamthamini. Epuka kuzungumzia udhaifu wa mwenzi wako unapokuwa na watoto wako. Badala yake, waeleze kwamba kila mtu anapaswa kujiamulia ikiwa atamtumikia Yehova. Huenda mwenendo mzuri wa watoto wako ukamvuta mzazi ambaye si mwamini kwenye ibada ya kweli.

Wafundishe watoto wako kweli ya Biblia kila unapopata fursa (Tazama fungu la 10)

10. Wazazi Wakristo walio katika familia zilizogawanyika kidini wanaweza kuwafundishaje watoto wao kweli za Biblia?

10 Nyakati nyingine, wenzi ambao si waamini wanaweza kusisitiza kwamba watoto wao washiriki katika sherehe za kipagani au wafundishwe mafundisho ya dini za uwongo. Huenda baadhi ya waume wakawakataza wake Wakristo kuwafundisha watoto wao Biblia. Hata hivyo, mke Mkristo atafanya yote awezayo ili kuwafundisha watoto wake kweli za Biblia. (Mdo. 16:1; 2 Tim. 3:14, 15) Kwa mfano, huenda mume ambaye mke wake ni Shahidi asimruhusu mke wake kuongoza funzo rasmi la Biblia pamoja na watoto wake wadogo au kwenda nao kwenye mikutano ya Kikristo. Mke ataheshimu uamuzi wa mume wake, lakini bado atatumia fursa zinazojitokeza akiwa na watoto wake kuzungumzia imani yake. Kwa njia hiyo atawazoeza kuwa na maadili mazuri na kuwafundisha kumhusu Yehova. (Mdo. 4:19, 20) Bila shaka, mwishowe watoto wake watahitaji kufanya uamuzi wao wenyewe kuhusu ibada.—Kum. 30:19, 20. *

WATU WA UKOO WANAOPINGA IBADA YA KWELI

11. Ni nini kinachoweza kusababisha matatizo kati yako na watu wa ukoo ambao si Mashahidi?

11 Mwanzoni, huenda hatukuwaambia watu wetu wa familia kwamba tunashirikiana na Mashahidi wa Yehova. Lakini kadiri imani yetu ilivyoendelea kukua, tuliona umuhimu wa kuwaeleza kuhusu imani yetu. (Marko 8:38) Ikiwa msimamo wako thabiti umesababisha matatizo kati yako na watu wa ukoo ambao si Mashahidi, hatua zifuatazo zinaweza kukusaidia kupunguza hali za kutoelewana huku ukidumisha utimilifu wako.

12. Kwa nini huenda watu wetu wa ukoo wakatupinga, lakini tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaelewa hisia zao?

12 Elewa hisia za watu wako wa ukoo ambao si waamini. Ingawa huenda tuna shangwe kubwa kuhusu kweli za Biblia tulizojifunza, watu wetu wa ukoo wanaweza kuamini kimakosa kwamba tumedanganywa au tumejiunga na dhehebu fulani la ajabu. Wanaweza kufikiri kwamba hatuwapendi kwa sababu hatushirikiani nao kwenye pindi za sherehe. Huenda hata wakahofia kwamba Mungu atatuadhibu tutakapokufa. Tunapaswa kuelewa hisia zao kwa kujitahidi kuona mambo kama wanavyoyaona na kuwasikiliza kwa makini ili kuelewa kile kinachowahangaisha. (Met. 20:5) Mtume Paulo alijitahidi kuwaelewa “watu wa namna zote” ili ashiriki habari njema nao, na kufanya hivyo kunaweza kutusaidia pia.—1 Kor. 9:19-23.

13. Tunapaswa kuzungumza kwa njia gani na watu wetu wa ukoo ambao si waamini?

13 Zungumza kwa upole. Biblia inasema hivi: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote.” (Kol. 4:6) Tunaweza kumwomba Yehova atupatie roho yake takatifu ili tuonyeshe sifa za tunda la roho tunapozungumza na watu wetu wa ukoo. Hatupaswi kubishana nao kuhusu mafundisho yote ya kidini ambayo ni ya uwongo. Ikiwa watatuumiza kwa maneno au matendo yao, tunaweza kuiga kielelezo cha mitume. Paulo aliandika hivi: “Tunapotukanwa, tunabariki; tunapoteswa, tunavumilia; tunapoharibiwa sifa, tunasihi,” au kujibu kwa upole.—1 Kor. 4:12, 13.

14. Tunaweza kupata faida gani kwa kudumisha mwenendo mzuri?

14 Dumisha mwenendo mzuri. Ingawa kuzungumza kwa upole tunaposhughulika na watu wetu wa ukoo wanaotupinga kunasaidia, mwenendo wetu mzuri una nguvu hata zaidi. (Soma 1 Petro 3:1, 2, 16.) Kupitia mfano wako mzuri, acha watu wako wa ukoo waone kwamba Mashahidi wa Yehova huwa na ndoa zenye furaha, huwatunza watoto wao, na huishi maisha safi kiadili na yanayoridhisha. Hata ikiwa watu wetu wa ukoo hawataikubali kweli, tunaweza kupata shangwe inayotokana na kumfurahisha Yehova kwa kuendelea kuwa waaminifu.

15. Tunaweza kujitayarishaje mapema kukabiliana na hali zinazoweza kutokeza kutoelewana?

15 Jitayarishe mapema. Fikiria hali zinazoweza kusababisha kutoelewana na upange jinsi utakavyokabiliana nazo. (Met. 12:16, 23) Dada mmoja kutoka Australia anaeleza hivi: “Baba-mkwe aliipinga kweli vikali. Sikuzote kabla ya kumpigia simu ili kumjulia hali, mimi na mume wangu tulisali kwa Yehova ili atusaidie kumjibu kwa upole ikiwa angezungumza kwa hasira. Tulitayarisha habari ambazo zingefanya mazungumzo yawe ya kirafiki. Ili kuepuka mazungumzo marefu ambayo mara nyingi yangeongoza kwenye mabishano makali kuhusu dini, tuliamua mapema muda hususa tutakaotumia kuzungumza naye.”

16. Unaweza kufanya nini ili ushinde hisia za hatia zinazosababishwa na kutoelewana na watu wa ukoo?

16 Bila shaka, huwezi kutarajia kwamba utaepuka kabisa hali zote zinazosababisha kutoelewana kati yako na watu wako wa ukoo ambao si waamini. Unaweza kuhisi hatia unapokosa kuelewana nao, kwa sababu unawapenda sana na sikuzote umekuwa ukijaribu kuwafurahisha. Ikiwa unahisi hivyo, jitahidi kutanguliza ushikamanifu wako kwa Yehova badala ya upendo wako kwa watu wa ukoo. Kwa kweli, msimamo huo unaweza kuwasaidia watu wako wa ukoo watambue kwamba kuishi kulingana na kweli ya Biblia ni jambo linalohusisha uhai au kifo. Kwa vyovyote vile, kumbuka kwamba huwezi kuwalazimisha wengine kukubali kweli. Badala yake, acha waone manufaa ya kufuata njia za Yehova kupitia kielelezo chako. Mungu wetu mwenye upendo amewapa fursa ya kuchagua maisha wanayotaka kuishi, kama tu alivyotupatia sisi fursa hiyo.—Isa. 48:17, 18.

MTU WA FAMILIA ANAPOMWACHA YEHOVA

17, 18. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuvumilia mtu wa familia anapomwacha Yehova?

17 Mtu wa familia anapotengwa au kujitenga na kutaniko, tunaweza kuhisi maumivu makali. Unaweza kufanya nini ili kukabiliana na maumivu hayo?

18 Dumisha ratiba yako ya mambo ya kiroho. Jiimarishe kwa kusoma Biblia kwa ukawaida, kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kuhubiri, na kusali ili upate nguvu za kuvumilia. (Yuda 20, 21) Vipi ikiwa unahisi kwamba unafanya mambo hayo kidesturi tu na si kutoka moyoni? Usikate tamaa! Ratiba nzuri ya kiroho inaweza kukusaidia kudhibiti mawazo na hisia zako. Fikiria kilichompata mwandikaji wa Zaburi ya 73. Alikuwa ameanza kusitawisha mtazamo usiofaa na hilo lilimhangaisha sana, lakini alifaulu kurekebisha maoni yake alipoingia katika mahali pa ibada pa Mungu. (Zab. 73:16, 17) Ukiendelea kumwabudu Yehova kwa uaminifu utafanikiwa kufanya hivyo pia.

19. Unaweza kuonyeshaje kwamba unaheshimu mpango wa Yehova wa kuwatia nidhamu wakosaji?

19 Heshimu nidhamu ya Yehova. Mpango wa Yehova wa kutia nidhamu unaweza kuleta manufaa ya kudumu kwa wote, kutia ndani mkosaji, hata ikiwa mwanzoni nidhamu hiyo inasababisha maumivu. (Soma Waebrania 12:11.) Kwa mfano, Yehova anatuagiza “[tuache] kuchangamana katika ushirika” pamoja na watenda dhambi wasiotubu. (1 Kor. 5:11-13) Licha ya kuumia sana moyoni, ni lazima tuepuke mawasiliano ya kawaida na watu wa familia waliotengwa, iwe ni kupitia simu, ujumbe mfupi, barua, barua-pepe, au kupitia mitandao ya kijamii.

20. Tunaweza kuwa na tumaini gani?

20 Endelea kuwa na tumaini. Upendo “hutumaini mambo yote,” kutia ndani tumaini la kwamba wale ambao wamemwacha Yehova watamrudia. (1 Kor. 13:7) Ukiona ishara ya kwamba mtu wa karibu wa familia ameanza kubadili mtazamo wake, unaweza kusali aimarishwe na Maandiko na akubali mwaliko huu wa Yehova: “Rudi kwangu.”—Isa. 44:22.

21. Unapaswa kufanya nini ikiwa kuna mgawanyiko katika familia yako kwa sababu unamfuata Yesu?

21 Yesu alisema kwamba ikiwa tunamtanguliza mwanadamu yeyote badala ya kumtanguliza yeye, hatumstahili. Hata hivyo, alikuwa na uhakika kwamba wanafunzi wake wangekuwa na ujasiri wa kudumisha ushikamanifu wao kwake licha ya kupingwa na familia zao. Ikiwa kumfuata Yesu kumeleta “upanga” katika familia yako, mtegemee Yehova akusaidie kukabiliana na changamoto hizo kwa mafanikio. (Isa. 41:10, 13) Pata shangwe kwa kujua kwamba Yehova na Yesu wanafurahishwa nawe, na kwamba watakuthawabisha ukiendelea kuwa mwaminifu.

^ fu. 10 Kwa habari zaidi kuhusu kuwazoeza watoto katika familia zilizogawanyika kidini, tazama makala yenye kichwa, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 2002.