Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Maono ya Zekaria Yanavyokuhusu

Jinsi Maono ya Zekaria Yanavyokuhusu

“Rudini kwangu, . . . nami nitarudi kwenu.”—ZEK. 1:3.

NYIMBO: 89, 86

1-3. (a) Watu wa Yehova walikuwa katika hali gani Zekaria alipoanza kutoa unabii? (b) Kwa nini Yehova aliwaomba watu wake ‘wamrudie’?

KITABU cha kukunjwa kinachoruka, mwanamke akiwa ndani ya chombo cha efa kilichofunikwa, na wanawake wawili wanaopaa katika upepo walio na mabawa kama ya korongo—mambo hayo yenye kustaajabisha yanapatikana katika kitabu cha Zekaria. (Zek. 5:1, 7-9) Kwa nini Yehova alimpa nabii wake maono hayo yenye kustaajabisha? Waisraeli walikuwa katika hali gani wakati huo? Maono hayo yaliyoandikwa na Zekaria yanatuhusuje leo?

2 Mwaka wa 537 K.W.K. ulikuwa mwaka wenye shangwe kwa watu wa Yehova waliojiweka wakfu. Baada ya kuwa utekwani kwa miaka 70, waliwekwa huru kutoka Babiloni. Wakiwa na bidii nyingi, walianza kazi ya kurudisha ibada ya kweli jijini Yerusalemu. Kufikia mwaka wa 536 K.W.K., msingi wa hekalu ulikuwa umewekwa. Wakati huo watu “[walipaaza] sauti kubwa, na sauti hiyo ikasikiwa hata mbali sana.” (Ezra 3:10-13) Hata hivyo, baada ya muda mfupi walikabili upinzani mkubwa walipokuwa wakijenga hekalu. Wakiwa wamevunjika moyo kwa sababu ya changamoto na matatizo mengi, watu hao waliacha kujenga hekalu hilo na kuanza kujenga nyumba zao wenyewe na kulima mashamba yao. Miaka 16 baadaye, ujenzi wa hekalu la Yehova bado ulikuwa umesimama. Watu wa Mungu walihitaji kukumbushwa kwamba wanapaswa kumrudia Yehova na kuacha kutanguliza mambo ya kibinafsi maishani. Yehova alitaka wamrudie na kuanza tena kumwabudu kwa ujasiri, na kwa moyo wao wote.

3 Mungu alimtuma nabii Zekaria mwaka wa 520 K.W.K. ili kuwasaidia watu wake wakumbuke sababu ya msingi iliyofanya wawekwe huru kutoka Babiloni. Vilevile jina la Zekaria linalomaanisha “Yehova Amekumbuka,” huenda liliwakumbusha ukweli muhimu. Bado Mungu alikuwa anawakumbuka watu wake, ingawa wao walikuwa wamesahau matendo ya Yehova ya wokovu. (Soma Zekaria 1:3, 4.) Kwa upendo aliwahakikishia kwamba angewasaidia kurudisha ibada safi, lakini pia kwa uthabiti aliwaonya kwamba hangevumilia ibada ya moyo nusu-nusu. Na tuone jinsi ambavyo Yehova alitumia maono ya sita na ya saba ya Zekaria kuwachochea watu wake kutenda, na pia mambo tunayojifunza kupitia maono hayo.

ADHABU YA MUNGU KWA WANAOIBA

4. Zekaria aliona nini katika maono yake ya sita, na kwa nini kitabu hicho cha kukunjwa kiliandikwa pande zote mbili? (Tazama picha ya 1 mwanzoni mwa makala hii.)

4 Sura ya 5 ya kitabu cha Zekaria inaanza kwa maono yenye kushangaza. (Soma Zekaria 5:1, 2.) Zekaria anaona kitabu cha kukunjwa kinachoruka angani chenye urefu wa karibu mita 9 na upana wa mita 4.5! Tayari kimekunjuliwa kwa ajili ya kusomwa. Kina ujumbe wa hukumu ulioandikwa pande zote mbili. (Zek 5:3) Kwa kawaida, vitabu vya kukunjwa viliandikwa upande mmoja tu, hivyo ni wazi kwamba kitabu hicho cha kukunjwa kilikuwa na ujumbe mzito na muhimu sana.

Wakristo wanapaswa kuepuka wizi wa aina yoyote (Tazama fungu la 5 hadi 7)

5, 6. Yehova ana maoni gani kuhusu wizi wa aina yoyote?

5 Soma Zekaria 5:3, 4Ingawa wanadamu wote watatoa hesabu mbele za Yehova, watu wanaoitwa kwa jina lake wana wajibu mkubwa zaidi. Wale wanaompenda Mungu wanatambua kwamba wizi wa aina yoyote ile ‘ungeshambulia au kuliaibisha jina la Mungu wao.’ (Met. 30:8, 9) Huenda watu fulani wakafikiri kwamba si vibaya kuiba ikiwa wana sababu nzuri ya kufanya hivyo. Lakini haidhuru mtu anayeiba ana nia gani au ametoa visingizio gani, mtu huyo anakuwa ametanguliza tamaa yake yenye pupa badala ya kumtanguliza Mungu, na anaona vitu vya kimwili kuwa vyenye thamani zaidi. Anapunguza uzito wa sheria ya Mungu, anampuuza Yehova na jina Lake, na anayaona mambo hayo kuwa hayana umuhimu wowote.

6 Je, uliona katika Zekaria 5:3, 4 kwamba “laana . . . [ingeingia] katika nyumba ya mwizi . . . nayo [ingekaa] katikati ya nyumba yake na kuiangamiza”? Hukumu kali ya Yehova haiwezi kuzuiwa na vyuma wala kufuli. Inapenya mahali popote palipojificha na kufunua makosa miongoni mwa watu wa Yehova. Hata ikiwa mtu anafanikiwa kuwaficha wenye mamlaka, mwajiri wake, wazee, au wazazi, hawezi kumficha Mungu anayetuhakikishia kwamba wizi wa aina yoyote utafunuliwa. (Ebr. 4:13) Inaburudisha sana kushirikiana na watu ambao sikuzote wanajitahidi kujiendesha kwa unyoofu “katika mambo yote”!—Ebr. 13:18.

7. Tunaweza kuepukaje laana ya kitabu cha kukunjwa kinachoruka?

7 Yehova anachukia aina zote za wizi. Tunaliona kuwa pendeleo kubwa kuishi kulingana na viwango vya juu vya maadili vya Yehova na kudumisha mwenendo ambao hauletei jina lake suto kwa njia yoyote. Tukifanya hivyo, huenda tukaepuka hukumu ya Yehova dhidi ya wale wanaovunja sheria yake kimakusudi.

ISHI KULINGANA NA AHADI YAKO “SIKU BAADA YA SIKU”

8-10. (a) Kiapo ni nini? (b) Mfalme Sedekia alishindwa kutimiza kiapo gani?

8 Ujumbe ulioandikwa katika kitabu cha kukunjwa kinachoruka unatoa onyo lingine kwa wale ‘wanaofanya kiapo rasmi katika jina la Mungu kwa uwongo.’ (Zek. 5:4) Kiapo ni taarifa inayotolewa kwa kuapa ili kuthibitisha kwamba jambo fulani ni la kweli au ni ahadi nzito ya kwamba mtu atafanya au hatafanya jambo fulani.

9 Kuapa katika jina la Yehova ni jambo zito sana. Na hivyo ndivyo alivyofanya Sedekia, mfalme wa mwisho kuketi katika kiti cha ufalme kilichokuwa Yerusalemu. Aliapa katika jina la Yehova kuwa angebaki mwaminifu akiwa mfalme kibaraka chini ya mfalme wa Babiloni. Hata hivyo, Sedekia hakutimiza kiapo chake. Kwa hiyo, Yehova akatoa hukumu hii juu yake: “Kama ninavyoishi, . . . mahali pa mfalme aliyemweka kuwa mfalme yule [Sedekia] aliyekidharau kiapo chake na ambaye alilivunja agano lake, atakufa pamoja naye katikati ya Babiloni.”—Eze. 17:16.

10 Mfalme Sedekia alikuwa na wajibu kwa Yehova wa kutimiza kiapo alichokuwa ameapa katika jina la Mungu. (2 Nya. 36:13) Badala ya kufanya hivyo, Sedekia aliomba msaada Misri akijaribu kujiweka huru kutokana na nira ya Wababiloni bila mafanikio.—Eze. 17:11-15, 17, 18.

11, 12. (a) Ni nadhiri gani iliyo muhimu zaidi maishani tunayoweza kuweka? (b) Nadhiri yetu ya wakfu inapaswa kuongoza maisha yetu ya kila siku jinsi gani?

11 Yehova anasikiliza tunapotoa ahadi zetu pia. Anachukua kwa uzito nadhiri tulizoweka. Kwa hiyo, ni lazima tutimize nadhiri hizo ili tupate kibali chake. (Zab. 76:11) Kati ya ahadi zote tulizotoa, ya muhimu zaidi ni ile tuliyotoa tulipojiweka wakfu kwa Yehova. Kujiweka wakfu ni kuweka nadhiri nzito kwa Yehova kwamba tutamtumikia chini ya hali zozote zile.

12 Tunaweza kutimizaje nadhiri tuliyotoa tulipojiweka wakfu kwa Yehova? Tunapokabili majaribu makubwa au madogo, msimamo wetu unapaswa kuonyesha kwamba tunachukua kwa uzito ahadi yetu ya kumsifu Yehova “siku baada ya siku.” (Zab. 61:8) Kwa mfano, ikiwa mtu fulani kazini au shuleni anatuchezea kimapenzi, je, tunaonyesha kwamba ‘tunapendezwa na njia za Yehova’ kwa kupinga kishawishi hicho? (Met. 23:26) Ikiwa tunaishi katika nyumba iliyogawanyika kidini, je, sisi humwomba Yehova atusaidie kudumisha utu wa Kikristo hata ikiwa waliotuzunguka hawafanyi hivyo? Je, sisi humshukuru Baba yetu wa mbinguni kila siku katika sala kwa kutuleta chini ya utawala wake na kwa upendo wake? Je, tunatenga wakati wa kusoma Biblia kila siku? Kimsingi tulipojiweka wakfu tuliahidi kufanya mambo hayo. Kutimiza wakfu wetu kunahusisha utii. Tunaposhiriki kikamili katika ibada tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na kwamba tumejiweka wakfu kwake kikamili. Ibada yetu ni njia yetu ya maisha na si jambo tunalofanya kidesturi tu. Tunafaidika tunapotimiza ahadi yetu; tukiwa waaminifu tutafurahia wakati ujao ulio salama.—Kum. 10:12, 13.

13. Tunajifunza nini kutokana na maono ya sita ya Zekaria?

13 Maono ya sita ya Zekaria yametusaidia kuona kwamba wale wanaompenda Yehova hawapaswi kujihusisha na wizi wa aina yoyote au kuapa kwa uwongo. Pia, tumeona kwamba licha ya udhaifu wa Waisraeli, Yehova hakukata tamaa. Alielewa mikazo waliyokabili walipokuwa wamezungukwa na maadui. Yehova anatuwekea kielelezo kwa kutimiza ahadi zake, naye atatusaidia kutimiza ahadi zetu pia. Njia moja anayotumia kutusaidia ni kwa kutupa tumaini kwamba karibuni ataondoa uovu wote duniani. Maono ya saba ya Zekaria yanatupa uhakika wa tumaini hilo jangavu.

UOVU ‘ANAWEKWA MAHALI ANAPOPASWA KUWA’

14, 15. (a) Zekaria anaona nini katika maono yake ya saba? (Tazama picha ya 2 mwanzoni mwa makala hii.) (b) Mwanamke aliye ndani ya chombo cha efa anafananisha nini, na kwa nini amedhibitiwa na kufungiwa ndani ya chombo hicho?

14 Baada ya kuona kitabu cha kukunjwa kinachoruka, malaika anamwambia Zekaria hivi: “Inua macho yako.” Maono yake ya saba yatafunua nini? Sasa anaona chombo cha kupimia kinachoitwa “efa” kikitoka. (Soma Zekaria 5:5-8.) Chombo hicho chenye ukubwa wa wastani, kina “kifuniko cha mviringo cha madini ya risasi.” Kifuniko hicho kinapoinuliwa, Zekaria anamwona “mwanamke fulani amekaa ndani.” Kisha malaika anamweleza kwamba mwanamke huyo aliye ndani ya chombo cha efa ni “Uovu.” Wazia jinsi Zekaria alivyoshtuka kumwona mwanamke huyo akijaribu kutoka katika chombo hicho! Mara moja yule malaika akamtupa mwanamke huyo tena ndani ya chombo hicho na kukifunga kabisa kwa kifuniko chake kizito. Hilo linamaanisha nini?

15 Sehemu hii ya maono ya Zekaria inakazia kwamba Yehova hatavumilia uovu wa aina yoyote miongoni mwa watu wake. Atahakikisha uovu unadhibitiwa na kuondolewa mara moja. (1 Kor. 5:13) Yule malaika anatuhakikishia jambo hilo kwa kukirudisha kwa nguvu kile kifuniko cha risasi juu ya kile chombo cha efa.

Yehova alifanya kila jitihada kudumisha ibada yake ikiwa safi (Tazama fungu la 16 hadi 18)

16. (a) Zekaria anaona jambo gani lingine? (Tazama picha ya 3 mwanzoni mwa makala hii.) (b) Wale wanawake wenye mabawa wanapeleka wapi kile chombo cha efa?

16 Kisha Zekaria anawaona wanawake wawili wenye mabawa yenye nguvu kama ya korongo. (Soma Zekaria 5:9-11.) Wanawake hao wanatofautiana kabisa na yule mwanamke aliye ndani ya chombo cha efa! Wao wanatumia mabawa yao yenye nguvu kushuka haraka na kukiinua kile chombo cha efa chenye yule mwanamke anayefananisha “Uovu.” Wanampeleka wapi? “Uovu” anapelekwa katika “nchi ya Shinari,” au Babiloni. Lakini kwa nini wanawake hao wanapeleka chombo hicho Babiloni?

17, 18. (a) Kwa nini Shinari ndipo ‘mahali anapopaswa’ kupelekwa yule mwanamke “Uovu”? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini kuhusu uovu?

17 Kwa Waisraeli wa siku za Zekaria, eneo la Shinari lilikuwa mahali panapofaa kumpeleka Uovu. Katika siku hizo, Zekaria na Wayahudi wenzake walijua kwamba jiji la Babiloni lilikuwa mahali penye uovu. Wakiwa wamelelewa katika mazingira ya jiji hilo lenye mambo machafu na ibada ya sanamu, walihitaji kupambana kila siku ili kupinga roho ya ulimwengu huo wa kipagani. Ni wazi kwamba maono hayo yaliwaletea kitulizo kikubwa sana, yaani, uhakika wa kwamba Yehova angedumisha ibada yake ikiwa safi!

18 Hata hivyo, maono hayo pia yaliwakumbusha Wayahudi jukumu lao la kudumisha ibada yao ikiwa safi. Uovu hauwezi na hautaruhusiwa kupenya na kukaa miongoni mwa watu wa Yehova. Baada ya Yehova kutuleta ndani ya tengenezo lake lililo safi, linalotupa ulinzi na kututunza kwa upendo, tuna wajibu wa kusaidia kudumisha usafi huo. Je, tunachochewa kudumisha usafi wa tengenezo letu? Uovu wa aina yoyote haustahili kuwepo katika paradiso yetu ya kiroho.

WATU SAFI HUMHESHIMU YEHOVA

19. Maono yenye kustaajabisha ambayo Zekaria aliona yanatuhusuje leo?

19 Maono ya sita na ya saba ya Zekaria ni onyo zito kwa wale wanaodumu katika njia za udanganyifu na yanatukumbusha kwamba Yehova hatavumilia uovu. Wale wanaomwabudu Yehova kutoka moyoni, wanapaswa kuchukia uovu kikweli. Pia, maono hayo ni uhakikisho wenye kufariji kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Ikiwa tutajitahidi kwa bidii kupata kibali na ulinzi wa Mungu, hatutapatwa na laana inayoleta kifo. Badala yake, Yehova atatubariki sana. Jitihada zetu zote za kubaki tukiwa safi katika ulimwengu uliojaa uovu hazitakuwa za bure. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutafanikiwa kwa msaada wa Yehova! Lakini kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba ibada ya kweli itashinda katika ulimwengu huu uliojaa watu wasiomwogopa Mungu? Kadiri ile dhiki kuu inavyokaribia, tuna uhakika gani kwamba Yehova atalilinda tengenezo lake? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.