Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unalindwa na Magari ya Kukokotwa na Taji

Unalindwa na Magari ya Kukokotwa na Taji

“Nayo [itatukia]—bila shaka ikiwa mtaisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu.”—ZEK. 6:15.

NYIMBO: 61, 22

1, 2. Mwishoni mwa maono ya saba ya Zekaria, Wayahudi waliokuwa Yerusalemu walikuwa katika hali gani?

ZEKARIA ana mambo mengi ya kutafakari mwishoni mwa maono yake ya saba. Yehova alikuwa ameahidi kwamba angewaadhibu watu wasio wanyoofu kwa sababu ya matendo yao maovu. Bila shaka ahadi hiyo ilimwimarisha Zekaria. Hata hivyo, bado mambo hayakuwa yamebadilika. Udanganyifu na mambo mengine maovu bado yalikuwepo, na ujenzi wa hekalu la Yehova jijini Yerusalemu haukuwa umekamilika. Ilikuwaje Wayahudi wakaacha haraka hivyo kazi hiyo waliyopewa na Mungu? Je, walikuwa wamerudi katika nchi yao ili kuendeleza tu masilahi yao wenyewe?

2 Zekaria alijua kwamba Wayahudi waliorudi Yerusalemu walikuwa wanaume na wanawake wenye imani. Hao ndio watu ambao “Mungu wa kweli [alikuwa ameamsha] roho” yao ili waache nyumba na biashara zao huko Babiloni. (Ezra 1:2, 3, 5) Waliacha nchi waliyoijua na kuhamia nchi ambayo wengi wao hawakuijua. Ikiwa ujenzi wa hekalu la Yehova haungekuwa muhimu kwao, hawangefunga safari hiyo ngumu ya kilomita 1,600 hivi wakipita kwenye nchi yenye mabonde na milima.

3, 4. Wayahudi waliorudi Yerusalemu walipata vipingamizi gani?

3 Wazia jinsi safari hiyo ilivyokuwa. Bila shaka, Wayahudi hao walipokuwa wakisafiri walitumia saa nyingi wakifikiria kuhusu makao yao mapya. Walikuwa wamesikia kuhusu jinsi jiji la Yerusalemu lilivyokuwa maridadi hapo awali. Wazee waliokuwa miongoni mwao walikuwa wameona utukufu wa awali wa hekalu hilo. (Ezra 3:12) Ikiwa ungekuwa ukisafiri pamoja nao, ungehisije kuona kwa mara ya kwanza jiji la Yerusalemu, makao yako mapya? Je, ungehuzunika kuona majengo yaliyoharibika na kujaa magugu? Je, ungelilinganisha jiji la Babiloni lililozungukwa na kuta mbili kubwa na jiji la Yerusalemu lenye kuta zilizobomoka na sehemu zilizo wazi mahali ambako awali kulikuwa na malango na minara ya ulinzi? Licha ya hilo, watu hao hawakuvunjika moyo. Tayari walikuwa wamejionea mkono wa Yehova unaookoa wakati wote wa safari yao ndefu ya kurudi nyumbani. Jambo la kwanza walilofanya walipofika lilikuwa kujenga madhabahu mahali ambapo hekalu lilikuwa mwanzoni, nao wakaanza kumtolea Yehova dhabihu kila siku. (Ezra 3:1, 2) Walianza kazi kwa msisimko mkubwa, na ilionekana kwamba hakuna jambo lolote ambalo lingeweza kuwavunja moyo.

4 Mbali na kazi ya kujenga hekalu, Waisraeli walihitaji kujenga upya majiji yao. Walihitaji kujenga upya nyumba zao, kupanda mashamba, na kulisha familia zao. (Ezra 2:70) Kazi iliyokuwa ikiwasubiri ilionekana kuwa kubwa sana. Kisha upinzani mkali ukaja. Ingawa mwanzoni walikuwa thabiti, mwishowe walivunjwa moyo na upinzani huo uliochukua miaka 15. (Ezra 4:1-4) Walipatwa na pigo kubwa sana mwaka wa 522 K.W.K. mfalme wa Uajemi alipopiga marufuku ujenzi jijini Yerusalemu. Kulikuwa na shaka ikiwa jiji hilo lingejengwa tena.—Ezra 4:21-24.

5. Yehova alitendaje watu wake walipoacha ujenzi?

5 Yehova alijua kile ambacho watu wake walihitaji. Mungu alimpa Zekaria maono ya mwisho ili kuwahakikishia Wayahudi kwamba anawapenda na anathamini mambo yote waliyokuwa wametimiza kufikia wakati huo, na akawahakikishia kwamba angewalinda ikiwa wangerudi kufanya kazi aliyokuwa amewapa. Kuhusu kazi ya kujenga hekalu, Yehova alitoa ahadi hii: “Nayo [itatukia]—bila shaka ikiwa mtaisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu.”—Zek. 6:15.

MAJESHI YA MALAIKA WANAOENDESHA MAGARI YA KUKOKOTWA

6. (a) Maono ya nane ya Zekaria yanaanzaje? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kwa nini farasi hao wana rangi tofauti-tofauti?

6 Kati ya maono nane ambayo Zekaria alipata huenda maono haya ya mwisho ndio yanayoimarisha imani zaidi. (Soma Zekaria 6:1-3.) Hebu wazia hali ilivyokuwa: Magari manne ya kukokotwa ambayo huenda yametayarishwa kwa ajili ya vita, yanasonga mbele kwa kasi “kutoka katikati ya milima miwili . . . ya shaba.” Farasi wanaokokota magari hayo wana rangi tofauti-tofauti. Hivyo inawezekana kuwatofautisha wanaoendesha magari hayo. Kisha Zekaria anauliza hivi: “Magari haya ni nini?” (Zek. 6:4) Sisi pia tungependa kujua kwa kuwa maono haya yanatuhusu moja kwa moja.

Yehova bado anawatumia malaika wake kuwalinda na kuwaimarisha watu wake

7, 8. (a) Ile milima miwili inafananisha nini? (b) Kwa nini milima hiyo imetengenezwa kwa shaba?

7 Katika Biblia, milima inaweza kufananisha falme, au serikali. Milima inayotajwa katika simulizi la Zekaria inafanana na milima miwili inayotajwa katika unabii wa Danieli. Mlima mmoja unafananisha utawala wa Yehova wa ulimwenguni pote unaodumu milele. Mlima ule mwingine unafananisha Ufalme wa Kimasihi ulio mikononi mwa Yesu. (Dan. 2:35, 45) Tangu Yesu alipowekwa kuwa mfalme mwaka wa 1914, milima yote miwili imekuwepo, nayo imetimiza jukumu muhimu katika kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu duniani.

8 Kwa nini milima hiyo imetengenezwa kwa shaba? Kama dhahabu ilivyo na thamani, shaba pia ni madini yenye thamani. Yehova aliagiza kwamba madini hayo yanayong’aa yatumiwe kutengeneza maskani na baadaye hekalu katika jiji la Yerusalemu. (Kut. 27:1-3; 1 Fal. 7:13-16) Basi kwa kufaa, shaba ya milima hiyo miwili ya mfano inatukumbusha ubora wa hali ya juu wa enzi kuu ya Yehova ya ulimwenguni pote na ubora wa Ufalme wa Kimasihi. Tawala hizo zitawaletea wanadamu wote usalama na baraka.

9. Ni nani wanaoendesha magari ya kukokotwa, nao wamepewa kazi gani?

9 Sasa tuzungumzie magari ya kukokotwa. Magari hayo na wale wanaoyaendesha wanafananisha nini? Waendeshaji wa magari hayo ni malaika, huenda ni vikundi au makundi ya malaika. (Soma Zekaria 6:5-8.) Wanaondoka mbele za “Bwana wa dunia yote” ili kwenda kutimiza kazi fulani ya pekee. Wanapewa kazi gani? Magari hayo ya kukokotwa na wale wanaoyaendesha wanatumwa kwenda maeneo fulani hususa. Jukumu lao ni kuwalinda watu wa Mungu, hasa dhidi ya “nchi ya kaskazini,” yaani Babiloni. Yehova atahakikisha kwamba Babiloni halitawafanya watu wa Mungu kuwa watumwa tena. Hapana shaka kwamba jambo hilo liliwafariji sana wajenzi wa hekalu katika siku za Zekaria! Hawakuhitaji kuwa na wasiwasi tena kwamba maadui wao wangewasumbua.

10. Unabii wa Zekaria kuhusu magari ya kukokotwa na wale wanaoyaendesha unawapa watu wa Mungu leo uhakikisho gani?

10 Kama ilivyokuwa katika siku za Zekaria, Yehova wa majeshi bado anatumia malaika wake kuwalinda na kuwaimarisha watu wake. (Mal. 3:6; Ebr. 1:7, 14) Tangu Israeli wa kiroho walipowekwa huru kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa mwaka wa 1919, ibada ya kweli imeendelea kupanuka licha ya upinzani mkali. (Ufu. 18:4) Kwa sababu malaika wanatulinda, hatupaswi kuogopa kwamba huenda tengenezo la Yehova likapitia kipindi kingine cha utekwa wa kiroho. (Zab. 34:7) Badala yake, tunaweza kuwa na uhakika kwamba watumishi wa Mungu ulimwenguni pote wataendelea kusitawi kiroho. Tunapotafakari maono ya Zekaria, hatuna shaka kwamba tuko salama kwenye kivuli cha ile milima miwili.

11. Kwa nini hatupaswi kuogopa shambulizi linalokuja dhidi ya watu wa Mungu?

11 Hivi karibuni serikali za ulimwengu wa Shetani zitaungana pamoja zikiwa na nia ya kuwaangamiza watu wa Mungu. (Eze. 38:2, 10-12; Dan. 11:40, 44, 45; Ufu. 19:19) Unabii wa Ezekieli unafafanua serikali hizo kuwa jeshi la wapanda-farasi linaloifunika nchi kama mawingu na likija kutushambulia kwa hasira kali. (Eze. 38:15, 16) * Je, tunapaswa kuogopa chochote? La hasha! Tuna jeshi la wapanda-farasi lililo upande wetu. Wakati wa shambulizi hilo kwenye dhiki kuu, kikosi hicho cha malaika wa Yehova wa majeshi kitawalinda watu wa Mungu na kuwaangamiza wale wanaopinga enzi yake kuu. (2 The. 1:7, 8) Itakuwa siku ya pekee sana! Lakini ni nani anayeliongoza jeshi hilo la kimbingu la Yehova?

YEHOVA AMVIKA TAJI MFALME NA KUHANI WAKE

12, 13. (a) Zekaria anaagizwa afanye nini sasa? (b) Eleza ni katika njia gani jina la kiunabii la mwanamume anayeitwa Chipukizi linamrejelea Yesu Kristo.

12 Zekaria amejionea maono nane akiwa peke yake. Sasa anashiriki kuigiza jambo fulani la kiunabii ili kuwatia moyo wale wanaojenga upya hekalu la Mungu. (Soma Zekaria 6:9-12.) Zekaria anaagizwa akusanye fedha na dhahabu kutoka kwa Heldai, Tobaya, na Yedaya—wanaume watatu waliorudi hivi karibuni kutoka Babiloni—na kutengeneza “taji la fahari” kwa kutumia vitu hivyo. (Zek. 6:11) Je, Zekaria anaagizwa amvike taji Gavana Zerubabeli wa kabila la Yuda aliye mzao wa Daudi? Hapana. Bila shaka, watazamaji walishangaa kumwona akimvika taji hilo Kuhani Mkuu Yoshua.

13 Kuhani Mkuu Yoshua alipovikwa taji, je, hilo lilimaanisha kwamba aliwekwa kuwa mfalme? Hapana, Yoshua hakutoka katika uzao wa kifalme wa Daudi na kwa hiyo hakustahili kuwa mfalme. Tendo hilo la kumvika taji lilionyesha kwa njia ya kiunabii kwamba wakati ujao kungekuwa na mfalme na kuhani ambaye angedumu milele. Kuhani huyo mkuu anayewekwa kuwa mfalme anaitwa Chipukizi. Maandiko yanaonyesha wazi kwamba Chipukizi ni Yesu Kristo.—Isa. 11:1; Mt. 2:23. *

14. Akiwa Mfalme na Kuhani Mkuu Yesu ana kazi gani?

14 Akiwa Mfalme na Kuhani Mkuu, Yesu ndiye kiongozi wa jeshi la kimbingu la Yehova. Kwa sababu hiyo anafanya kazi kwa bidii ili watu wa Mungu wakae kwa usalama licha ya kwamba wanaishi katika ulimwengu wenye ukatili. (Yer. 23:5, 6) Hivi karibuni, Kristo ataongoza majeshi ya kimbingu kuyashinda mataifa ili kuunga mkono enzi kuu ya Mungu na pia kuwalinda watu wa Yehova. (Ufu. 17:12-14; 19:11, 14, 15) Hata hivyo, kabla ya kutekeleza hukumu hiyo, Chipukizi ana kazi kubwa ya kutimiza.

ATALIJENGA HEKALU

15, 16. (a) Ni kazi gani ya kurudisha na kusafisha watu wa Mungu ambayo inafanywa katika nyakati zetu, nayo inafanywa na nani? (b) Ni nini kitakachotokea mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo?

15 Mbali na kukabidhiwa kazi ya kuwa Mfalme na Kuhani Mkuu, Yesu alipewa kazi ya ‘kulijenga hekalu la Yehova.’ (Soma Zekaria 6:13.) Katika nyakati zetu, kazi ya ujenzi ambayo Yesu anafanya imehusisha kuwaweka huru waabudu wa kweli kutoka katika Babiloni Mkubwa na kulipanga upya kutaniko la Kikristo katika mwaka wa 1919. Pia alimweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili asimamie kazi katika nyua za kidunia za hekalu kubwa la kiroho. (Mt. 24:45) Yesu pia amekuwa akiwasafisha watu wa Mungu na kuwasaidia wamtolee Mungu ibada iliyo safi.—Mal. 3:1-3.

16 Wakati wa ule Utawala wa Miaka Elfu Moja, Yesu pamoja na wale 144,000 watakaotumikia pamoja naye wakiwa wafalme na makuhani watawasaidia wanadamu waaminifu wafikie ukamilifu. Jambo hilo litakapotimia, ni waabudu wa kweli wa Mungu tu ndio watakaobaki katika dunia iliyosafishwa. Hatimaye, ibada ya kweli itakuwa imerudishwa kikamili!

SHIRIKI KATIKA KAZI YA UJENZI

17. Ni uhakikisho gani mwingine ambao Yehova anawapa Wayahudi, na ujumbe huo unawachocheaje?

17 Ujumbe wa Zekaria uliwachocheaje Wayahudi walioishi wakati huo? Yehova alikuwa amewahakikishia kwamba angewasaidia na kuwalinda ili wakamilishe ujenzi wa hekalu. Hapana shaka kwamba uhakikisho aliowapa kwamba hekalu lingejengwa upya uliwapa tumaini watu hao waliokuwa wamevunjika moyo. Lakini kazi hiyo ingetimizwaje na watu wachache tu? Maneno yanayofuata ya Zekaria yangewaondolea hofu au shaka lolote ambalo bado walikuwa nalo. Mbali na utegemezo ambao watu waaminifu kama vile Heldai, Tobaya, na Yedaya walitoa, Mungu alisema pia kwamba wengine wengi ‘wangekuja na kujenga hekalu la Yehova.’ (Soma Zekaria 6:15.) Wakiwa na uhakika kwamba Mungu angewategemeza, Wayahudi hao walianza kuchapa kazi bila kukawia licha ya marufuku iliyokuwepo. Punde si punde Yehova akaondoa kipingamizi hicho cha marufuku kilichokuwa kama mlima mkubwa, na hekalu likakamilishwa katika mwaka wa 515 K.W.K. (Ezra 6:22; Zek. 4:6, 7) Hata hivyo, maneno hayo ya Yehova yanarejelea mambo makubwa zaidi yanayotendeka katika siku zetu.

Yehova hatasahau kamwe upendo tunaomwonyesha! (Tazama fungu la 18 na 19)

18. Andiko la Zekaria 6:15 linatimizwaje leo?

18 Leo, mamilioni ya watu wamejiunga na ibada ya kweli, nao wamechochewa kutoka moyoni kutoa “vitu [vyao] vyenye thamani,” vinavyotia ndani wakati wao, nguvu zao, na mali zao ili kutegemeza hekalu kubwa la kiroho la Yehova. (Met. 3:9) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anathamini tunapolitegemeza kwa ushikamanifu hekalu hilo? Kumbuka kwamba Heldai, Tobaya, na Yedaya walitoa vitu ambavyo Zekaria alitumia kutengeneza taji. Kisha taji hilo lilitumiwa kama “ukumbusho” wa mchango waliotoa ili kutegemeza ibada ya kweli. (Zek. 6:14) Vivyo hivyo, Yehova hatasahau kamwe kazi yetu na upendo tunaomwonyesha. (Ebr. 6:10) Mambo hayo yatadumu milele katika kumbukumbu ya Yehova.

19. Maono ya Zekaria yanapaswa kutuchocheaje leo?

19 Mambo yote ambayo yametimizwa kuhusiana na ibada ya kweli katika siku hizi za mwisho ni uthibitisho ulio wazi kwamba Yehova anatubariki na kwamba Kristo ndiye anayetuongoza. Sisi ni sehemu ya tengenezo lililo salama, thabiti, na linalodumu milele. Kusudi la Yehova kuelekea ibada safi ‘litatukia.’ Thamini sehemu yako miongoni mwa watu wa Yehova, nawe usikose ‘kusikiliza sauti ya Yehova Mungu wako.’ Ukifanya hivyo, utabaki katika ulinzi wa Mfalme na Kuhani wetu Mkuu na ulinzi wa waendeshaji wa magari ya kimbingu. Jitahidi kadiri uwezavyo kutegemeza kikamili ibada ya kweli. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova wa majeshi atakuhifadhi ukiwa salama na kukulinda katika siku zilizobaki za mfumo huu wa mambo—na kwa umilele wote!

^ fu. 11 Kwa habari zaidi, tazama makala yenye kichwa “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2015, ukurasa wa 29-30.

^ fu. 13 Neno “Mnazareti” linatokana na neno la Kiebrania “chipukizi.”