Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ninajua Atafufuka”

“Ninajua Atafufuka”

“Rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda huko ili kumwamsha kutoka usingizini.”—YOH. 11:11.

NYIMBO: 142, 129

1. Martha alikuwa na uhakika gani kuhusu ndugu yake? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

MARTHA, rafiki wa karibu wa Yesu na pia mwanafunzi wake, alikuwa akiomboleza. Lazaro ndugu yake alikuwa amekufa. Je, kuna jambo lolote ambalo lingeweza kumfariji? Ndiyo. Yesu alimhakikishia hivi: “Ndugu yako atafufuka.” Huenda maneno hayo hayakuondoa kabisa huzuni yake, hata hivyo Martha alikubaliana nayo. Alisema hivi: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yoh. 11:20-24) Alikuwa na uhakika kwamba kungekuwa na ufufuo wakati ujao. Kisha Yesu akafanya muujiza. Akamfufua Lazaro siku hiyohiyo.

2. Kwa nini ungependa kuwa na uhakika kama wa Martha kwamba kutakuwa na ufufuo?

2 Hatutarajii kwamba Yesu au Baba yake watatufanyia muujiza kama huo leo. Hata hivyo, je, wewe una uhakika kama wa Martha kwamba mpendwa wako atafufuliwa wakati ujao. Labda umefiwa na mwenzi wako, mama yako, baba yako, babu, au nyanya (bibi) yako mpendwa. Au huenda unaomboleza kifo cha mtoto wako. Unatamani sana kumkumbatia, kuzungumza, na kucheka na mpendwa wako. Kama Martha, jambo linalofurahisha ni kwamba una sababu nzuri za kusema, ‘Ninajua mpendwa wangu atafufuka katika ufufuo.’ Ingawa hivyo, inafaa kwa kila Mkristo kutafakari kwa nini ufufuo ni jambo hakika.

3, 4. Uhakika ambao Martha alikuwa nao uliimarishwaje na miujiza ambayo Yesu alikuwa amefanya?

3 Kwa kuwa Martha aliishi Yerusalemu, huenda hakushuhudia Yesu akimfufua mwana wa mjane karibu na jiji la Naini huko Galilaya. Hata hivyo, huenda alisikia kuhusu ufufuo huo. Huenda pia alisikia kuhusu kufufuliwa kwa binti ya Yairo. Watu waliokuwa katika nyumba ya Yairo “walijua [binti yake] alikuwa amekufa.” Lakini Yesu aliushika mkono wa binti huyo na kusema hivi: “Msichana, inuka!” Na mara moja, akainuka. (Luka 7:11-17; 8:41, 42, 49-55) Martha na Maria walijua kwamba Yesu anaweza kuwaponya wagonjwa. Hivyo walihisi kwamba ikiwa Yesu angekuwa pamoja nao, Lazaro hangekufa. Lakini kwa kuwa sasa rafiki mpendwa wa Yesu alikuwa amekufa, walikuwa na matarajio gani? Ona kwamba Martha alisema Lazaro angefufuliwa wakati ujao, katika “siku ya mwisho.” Kwa nini alikuwa na uhakika huo? Na kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba kutakuwa na ufufuo wakati ujao ambapo huenda wapendwa wako watafufuliwa?

4 Una sababu nzuri za kuamini jambo hilo. Unapochunguza baadhi ya sababu hizo, huenda ukaona mambo fulani katika Neno la Mungu ambayo kwa kawaida hungeyahusianisha na tumaini lako hakika la kuwaona tena wapendwa wako.

MATUKIO YANAYOTUPATIA TUMAINI!

5. Ni nini kilichomfanya Martha awe na uhakika kwamba Lazaro angefufuliwa?

5 Ona kwamba Martha hakusema: ‘Ninatumaini kuwa ndugu yangu atafufuka.’ Bali alisema: “Ninajua atafufuka.” Martha alisadiki jambo hilo kwa sababu huenda alisikia kuhusu miujiza ambayo ilikuwa imetukia hata kabla ya Yesu kuanza huduma yake. Akiwa kijana, Martha alijifunza kuhusu miujiza hiyo nyumbani kwao na kwenye sinagogi. Huenda unakumbuka masimulizi matatu yanayopatikana katika Biblia.

6. Eliya alifanya muujiza gani wa pekee, na hilo linahusianaje na Martha?

6 Ufufuo wa kwanza ulitukia katika kipindi ambacho Mungu alikuwa akimwezesha nabii Eliya kufanya miujiza. Katika mji wa Sarefathi ulioko pwani ya Foinike, mjane fulani maskini alimwonyesha ukarimu nabii Eliya. Kisha kwa njia ya kimuujiza, Mungu alihakikisha kwamba unga na mafuta ya mjane huyo hayakwisha, na hivyo yeye na mwanaye wakaendelea kuishi. (1 Fal. 17:8-16) Baadaye, mwanaye akawa mgonjwa na kufa. Lakini Eliya akamsaidia. Eliya alisali hivi huku mwili wake ukiwa umegusa mwili wa mvulana huyo: “Mungu . . . , tafadhali, irudishe nafsi ya mtoto huyu ndani yake.” Na ikawa hivyo! Mungu alimsikia Eliya, na mtoto huyo akawa hai tena. Huo ndio ufufuo wa kwanza ulioandikwa katika Biblia. (Soma 1 Wafalme 17:17-24.) Bila shaka, Martha alikuwa amesikia kuhusu tukio hilo la pekee.

7, 8. (a) Simulia jambo ambalo Elisha alifanya ili kuondoa huzuni ya mwanamke fulani. (b) Muujiza wa Elisha unathibitisha nini kumhusu Yehova?

7 Ufufuo wa pili unaosimuliwa katika Maandiko ulifanywa na nabii Elisha, aliyechukua mahali pa Eliya. Mwanamke fulani Mwisraeli ambaye alikuwa mashuhuri na aliyeishi katika jiji la Shunemu, alimwonyesha Elisha ukarimu wa pekee. Mwanamke huyo hakuwa na mtoto. Kupitia nabii Elisha, Mungu alimthawabisha kwa kumpa mtoto, ingawa mume wake alikuwa amezeeka. Miaka kadhaa baadaye, mvulana huyo akafa. Wazia huzuni kubwa ambayo mwanamke huyo alikuwa nayo. Baada ya kupewa ruhusa na mume wake, mwanamke huyo alisafiri kilomita 30 hivi hadi kwenye Mlima Karmeli ambako alikutana na Elisha. Nabii huyo alimtuma Gehazi mtumishi wake awatangulie kwenda Shunemu. Lakini Gehazi alishindwa kumfufua mvulana huyo. Kisha mama ya mvulana huyo pamoja na Elisha wakawasili.—2 Fal. 4:8-31.

8 Elisha akaingia ndani ya nyumba ambako mvulana huyo alikuwa amelazwa, kisha akaanza kusali. Mvulana huyo aliyekuwa amekufa akafufuka kimuujiza na kuungana tena na mama yake ambaye sasa alikuwa amefurahi sana! (Soma 2 Wafalme 4:32-37.) Inawezekana mwanamke huyo alikumbuka mambo ambayo Hana, ambaye mwanzoni alikuwa tasa, alisali alipomleta Samweli katika maskani ili atumikie huko: “Yehova . . . ni Mwenye Kushusha mpaka katika Kaburi, na Yeye huinua.” (1 Sam. 2:6) Ni wazi kwamba Mungu alimfanya mvulana huyo wa Shunemu kuwa hai tena, na kuthibitisha kwamba ana uwezo wa kufufua.

9. Eleza jinsi Elisha alivyohusika katika ufufuo wa tatu unaotajwa katika Biblia.

9 Lakini hilo halikuwa tukio la mwisho lenye kustaajabisha lililomhusisha Elisha. Alikuwa ametumikia kwa zaidi ya miaka 50 akiwa nabii, kisha ‘akashikwa na ugonjwa ambao hatimaye ulimuua.’ Baadaye, mwili wa Elisha ulipokuwa umeoza na kubaki mifupa mitupu, maadui waliingia nchini. Waisraeli fulani walikuwa wakienda kumzika mtu mmoja. Hata hivyo, ili kuwakimbia maadui, Waisraeli hao walimtupa mtu huyo ndani ya kaburi lililokuwa na mifupa ya Elisha. Tunasoma hivi: “Mtu yule alipoigusa mifupa ya Elisha, akawa hai mara moja na kusimama kwa miguu yake.” (2 Fal. 13:14, 20, 21) Fikiria jinsi masimulizi hayo yalivyomwimarisha Martha! Hapana shaka yoyote kwamba Mungu ana nguvu za kushinda kifo. Tafakari pia jinsi masimulizi hayo yanavyoweza kukuimarisha. Yanapaswa kukusadikisha kwamba nguvu za Mungu ni nyingi sana, hazina mipaka.

MATUKIO YALIYOTUKIA KATIKA KARNE YA KWANZA

10. Petro alimsaidiaje dada Mkristo ambaye alikuwa amekufa?

10 Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tunasoma pia kuhusu watu ambao walifufuliwa na wawakilishi wa Mungu. Tunaweza kuona hilo kupitia ufufuo ambao Yesu alifanya alipokuwa nje ya jiji la Naini na alipokuwa nyumbani kwa Yairo. Mtume Petro pia alimfufua mwanamke Mkristo aliyeitwa Dorkasi (Tabitha). Petro alienda mahali ambapo mwili wake ulikuwa umelazwa ukisubiri kuzikwa. Akiwa karibu na mwili huo, Petro alisali. Kisha akasema hivi: “Tabitha, inuka!” Papo hapo akawa hai, na Petro “akamweka mbele [ya Wakristo wenzake] akiwa hai.” Tukio hilo lilikuwa lenye kusadikisha sana hivi kwamba “wengi wakamwamini Bwana.” Wote wangeweza kutoa ushahidi kumhusu Bwana na hasa kuhusu uwezo wa Yehova wa kuwafufua wafu.—Mdo. 9:36-42.

11. Tabibu Luka anasema ni jambo gani lililompata kijana fulani, na hilo liliwafanya wengine wahisije?

11 Wengine pia walishuhudia ufufuo mwingine. Pindi moja, mtume Paulo alikuwa kwenye mkutano katika chumba cha juu katika jiji la Troa, ambalo kwa sasa ni kaskazini-magharibi mwa Uturuki. Paulo alizungumza hadi saa sita usiku. Kijana aliyeitwa Eutiko alikuwa ameketi dirishani akisikiliza. Lakini akasinzia na kuanguka chini kutoka ghorofa ya tatu. Huenda tabibu Luka ndiye aliyekuwa wa kwanza kufika chini na kumfanyia uchunguzi: Eutiko hakuwa amejeruhiwa tu au kupoteza fahamu—alikuwa amekufa! Paulo alipofika chini aliukumbatia mwili wa kijana huyo, kisha akatangaza hivi kwa furaha: ‘Yuko hai.’ Bila shaka tukio hilo liliwaimarisha sana wale waliolishuhudia! Walijua kabisa kwamba kijana huyo alikuwa amekufa na kwamba sasa alikuwa amefufuliwa, hivyo ‘walifarijiwa kupita kiasi.’—Mdo. 20:7-12.

TUMAINI HAKIKA

12, 13. Kwa msingi wa masimulizi ya ufufuo ambayo tumezungumzia, ni maswali gani ambayo tunapaswa kufikiria?

12 Masimulizi yaliyotajwa hapo juu yanapaswa kukusaidia uwe na uhakika kama ule ambao Martha alikuwa nao kwamba Mungu wetu na Mpaji-Uhai ana uwezo wa kuwafufua wafu. Hata hivyo, ona kwamba wakati Yehova alipokuwa akifanya miujiza hiyo, angalau kulikuwa na mtumishi mmoja mwaminifu wa Mungu kama vile Eliya, Yesu, au Petro. Lakini tunaweza kusema nini kuhusu watu waliokufa katika pindi nyingine tofauti? Ikiwa katika kipindi fulani cha wakati Mungu hakuwa akiwafufua wafu, je, wanaume na wanawake waaminifu wangeweza kutarajia kwamba Mungu atawafufua wafu wakati ujao? Je, wangekuwa na uhakika kama wa Martha, ambaye alisema: “Ninajua [ndugu yangu] atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho”? Martha aliamini kwamba kungekuwa na ufufuo wakati ujao. Kwa nini wewe pia unaweza kuamini jambo hilo?

13 Kwa kweli, kuna masimulizi kadhaa katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho yanayoonyesha kwamba watumishi washikamanifu wa Yehova walijua kwamba kutakuwa na ufufuo wakati ujao. Acheni tuchunguze baadhi ya masimulizi hayo.

14. Simulizi la Abrahamu linatufunza nini kuhusu ufufuo?

14 Fikiria kile ambacho Mungu alimwambia Abrahamu amfanyie Isaka, mrithi wake aliyesubiriwa kwa muda mrefu. Yehova alisema: “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana, Isaka, . . . umtoe kama toleo la kuteketezwa.” (Mwa. 22:2) Unafikiri Abrahamu alihisije alipoambiwa afanye hivyo? Yehova alikuwa ameahidi kwamba kupitia uzao wa Abrahamu mataifa yote yangebarikiwa. (Mwa. 13:14-16; 18:18; Rom. 4:17, 18) Pia, Yehova alikuwa amesema kwamba baraka hizo zingekuja “kupitia Isaka.” (Mwa. 21:12) Lakini hilo lingetimiaje ikiwa Abrahamu angemtoa Isaka kuwa dhabihu? Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kueleza kwamba Abrahamu aliamini kwamba Mungu angeweza kumfufua Isaka. (Soma Waebrania 11:17-19.) Biblia haisemi Abrahamu alihisi kwamba ikiwa angetii, Isaka angefufuliwa baada ya saa chache, siku moja, au juma moja. Abrahamu hangeweza kujua mwanaye angefufuliwa lini. Lakini aliamini kwamba Yehova angemfufua Isaka.

15. Mzee wa ukoo Ayubu alikuwa na tumaini gani?

15 Vivyo hivyo, mzee wa ukoo Ayubu alitazamia kwamba kungekuwa na ufufuo wakati ujao. Alijua kwamba mti unapokatwa unaweza kuchipuka tena. Lakini sivyo ilivyo kwa mwanadamu. (Ayu. 14:7-12; 19:25-27) Mwanadamu akifa, hawezi kujifufua kutoka kaburini na kuishi tena. (2 Sam. 12:23; Zab. 89:48) Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba Mungu hawezi kumfufua mwanadamu. Ukweli ni kwamba Ayubu aliamini kwamba Yehova angeweka wakati hususa wa kumkumbuka. (Soma Ayubu 14:13-15.) Ayubu hangeweza kujua wakati huo ungefika lini. Lakini bado aliamini kwamba Yule aliyemuumba mwanadamu anaweza kumkumbuka na kumfufua, na aliamini kwamba atafanya hivyo.

16. Malaika alimpa nabii Danieli kitia-moyo gani?

16 Mwanamume mwingine mwaminifu tunayesoma kumhusu katika Maandiko ya Kiebrania ni Danieli. Alimtumikia Mungu kwa ushikamanifu kwa miaka mingi, na Yehova alimtegemeza. Wakati fulani, malaika mmoja aliyetumwa na Mungu alimtia moyo Danieli, “mtu mwenye kutamanika sana,” awe “na amani” na awe “na nguvu.”—Dan. 9:22, 23; 10:11, 18, 19.

17, 18. Ni jambo gani ambalo Danieli aliahidiwa kuhusu wakati ujao?

17 Danieli alikuwa na umri wa miaka 100 hivi na alikuwa akikaribia mwisho wa maisha yake. Huenda aliwaza kuhusu wakati wake ujao. Je, Danieli angeishi tena? Bila shaka! Mwishoni mwa kitabu cha Danieli, Mungu alimhakikishia hivi: “Wewe nawe, nenda zako kuelekea ule mwisho; nawe utapumzika.” (Dan. 12:13) Mzee Danieli alijua kwamba wafu wamepumzika, na kwamba hakuna “utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi.” Na baada ya muda mfupi Danieli angekufa na kwenda kaburini. (Mhu. 9:10) Lakini huo haungekuwa mwisho wake. Aliahidiwa jambo zuri sana wakati ujao.

18 Malaika aliendelea kumwambia hivi Danieli: “Utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.” Hakujulishwa tarehe wala kipindi cha wakati ambacho kingepita. Danieli angekufa na kupumzika. Hata hivyo, malaika alipomwambia kwamba ‘angesimama kwa ajili ya fungu lake’ wakati ujao, kihalisi alikuwa akimwahidi kwamba kungekuwa na ufufuo wakati ujao—muda mrefu baada ya yeye kufa. Hilo lingetendeka “mwishoni mwa zile siku.” Tafsiri ya Jerusalem Bible inasema hivi kuhusu ahadi hiyo ambayo Danieli alipewa: “Utainuka kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa nyakati.”

Kama Martha, wewe pia unaweza kuwa na uhakika kwamba kutakuwa na ufufuo (Tazama fungu la 19 na 20)

19, 20. (a) Mambo tuliyochunguza kufikia sasa yanahusianaje na maneno ambayo Martha alimwambia Yesu? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

19 Ni wazi kwamba Martha alikuwa na sababu za kutosha za kuwa na uhakika kwamba Lazaro, ndugu yake mwaminifu, ‘angefufuka katika ufufuo siku ya mwisho.’ Ahadi ambayo Danieli alipewa, na pia uhakika ambao Martha alikuwa nao alipomjibu Yesu, unapaswa kuwahakikishia Wakristo leo kwamba kutakuwa na ufufuo.

20 Tumeona kwamba masimulizi halisi ya ufufuo ya wakati uliopita yanathibitisha kwamba ufufuo ni jambo linalowezekana, yaani, wafu wanaweza kuwa hai tena. Na wanaume na wanawake waliomtumikia Mungu walitazamia kwamba kungekuwa na ufufuo wakati fulani ujao. Hata hivyo, je, kuna jambo lolote linaloonyesha kwamba ahadi ya ufufuo inaweza kutimia hata baada ya muda mrefu kupita? Ikiwa ndivyo, hilo linatupatia sababu nyingine ya kutazamia kwa hamu kipindi hicho cha ufufuo, kama Martha alivyotazamia. Hata hivyo, ufufuo utatukia lini? Tutazungumzia mambo hayo katika makala inayofuata.