Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nina Tumaini kwa Mungu”

“Nina Tumaini kwa Mungu”

“Adamu wa mwisho akawa roho inayotoa uhai.”—1 KOR. 15:45.

NYIMBO: 151, 147

1-3. (a) Ni fundisho gani linalopaswa kuwa miongoni mwa mafundisho ya msingi ya imani yetu? (b) Kwa nini ufufuo ni jambo muhimu sana? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

UNGEJIBUJE ikiwa ungeulizwa, ‘Imani yako inategemea mafundisho gani ya msingi?’ Bila shaka ungekazia kwamba Yehova ndiye Muumba na Mpaji-Uhai. Huenda ukataja pia kwamba unamwamini Yesu Kristo, ambaye alitoa uhai wake kuwa fidia. Na huenda ukataja kwa furaha kwamba wakati ujao kutakuwa na paradiso duniani ambapo watu wa Mungu wataishi milele. Lakini, je, ungetaja fundisho la ufufuo kuwa miongoni mwa mafundisho unayothamini zaidi?

2 Tuna sababu nzuri za kuona fundisho la ufufuo kuwa miongoni mwa mafundisho yetu ya msingi hata ikiwa sisi binafsi tunatarajia kuokoka dhiki kuu na kuishi milele duniani. Mtume Paulo alionyesha kwa nini ufufuo ni fundisho muhimu sana la imani yetu aliposema hivi: “Ikiwa, kwa kweli, hakuna ufufuo wa wafu, basi Kristo hakufufuliwa.” Ikiwa Kristo hakufufuliwa, basi hangekuwa Mfalme wetu anayetawala, na fundisho letu kuhusu utawala wa Kristo halingekuwa na maana yoyote. (Soma 1 Wakorintho 15:12-19.) Hata hivyo, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa. Kwa sababu tunasadiki jambo hilo, tunatofautiana na Masadukayo ambao walipinga vikali fundisho la ufufuo. Hata tunapodhihakiwa, imani yetu katika ufufuo haiyumbishwi.—Marko 12:18; Mdo. 4:2, 3; 17:32; 23:6-8.

3 Paulo alipoandika kuhusu “fundisho la msingi juu ya Kristo,” alitaja pia kuhusu “fundisho juu ya . . . kufufuliwa kwa wafu.” (Ebr. 6:1, 2) Na Paulo alikazia kwamba aliamini ufufuo. (Mdo. 24:10, 15, 24, 25) Lakini ingawa fundisho la ufufuo ni miongoni mwa mafundisho ya msingi, yaani, mojawapo ya “mambo ya msingi ya maneno matakatifu ya Mungu,” hiyo haimaanishi kwamba ni fundisho la kijuujuu tu. (Ebr. 5:12) Kwa nini?

4. Ni maswali gani ambayo huenda yakazuka kuhusu ufufuo?

4 Watu wanapoanza kujifunza Biblia, wengi wao husoma kuhusu masimulizi ya watu waliofufuliwa zamani, kama vile Lazaro. Wao hujifunza kwamba Abrahamu, Ayubu, na Danieli walikuwa na uhakika kwamba wafu watafufuliwa wakati ujao. Hata hivyo, ungesema nini ikiwa ungeombwa utoe uthibitisho wa kwamba ahadi za ufufuo zinategemeka licha ya kuwa zilitolewa miaka mingi, au hata karne nyingi zilizopita? Na, je, kweli Biblia inaonyesha wakati ambapo ufufuo utatukia? Maswali hayo yanahusiana moja kwa moja na imani yetu, hivyo acheni tuone Maandiko yanasema nini.

UFUFUO ULIOTABIRIWA KARNE NYINGI MAPEMA

5. Ni jambo gani linalohusu ufufuo tutakalochunguza?

5 Huenda ikawa rahisi kwetu kuwazia mtu aliyekufa karibuni akifufuliwa. (Yoh. 11:11; Mdo. 20:9, 10) Lakini, vipi ukiahidiwa kwamba mtu huyo atafufuliwa miaka mingi ijayo, au hata karne nyingi baadaye? Je, unaweza kuamini jambo kama hilo ambalo litatimia baada ya muda mrefu, iwe inahusu mtu aliyekufa karibuni au aliyekufa muda mrefu uliopita? Ukweli ni kwamba kuna ufufuo fulani uliotabiriwa karne nyingi mapema ambao ulitimia, nawe unaamini kwamba ulitimia. Ni ufufuo gani huo? Nao unahusianaje na mambo unayoweza kutarajia kuhusiana na ufufuo wa wakati ujao?

6. Yesu alihusika jinsi gani katika utimizo wa Zaburi ya 118?

6 Kuhusu ufufuo huo uliotabiriwa miaka mingi mapema, chunguza Zaburi ya 118, ambayo watu fulani huhisi kwamba ilitungwa na Daudi. Zaburi hiyo inatia ndani ombi hili: “Ah, sasa, Yehova, uokoe, tafadhali! . . . Na abarikiwe Yeye anayekuja katika jina la Yehova.” Huenda unakumbuka kwamba watu walisema maneno hayo yanayomhusu Masihi wakati Yesu alipoingia Yerusalemu Nisani 9, akiwa amepanda mwana-punda, muda mfupi kabla ya kifo chake. (Zab. 118:25, 26; Mt. 21:7-9) Lakini Zaburi ya 118 inahusianaje na ufufuo ambao ungetukia miaka mingi baadaye? Ona jambo lingine lililotajwa katika zaburi hiyo ya kiunabii: “Jiwe ambalo wajenzi walilikataa limekuwa jiwe kuu la pembeni.”—Zab. 118:22.

‘Wajenzi walimkataa’ Masihi (Tazama fungu la 7)

7. Ni kwa kadiri gani Wayahudi walimkataa Yesu?

7 “Wajenzi,” yaani, viongozi wa Wayahudi, walimkataa Masihi. Kufanya hivyo kulihusisha mengi zaidi ya kukataa tu kumsikiliza au kumkubali kuwa Kristo. Wayahudi wengi walimkataa Yesu kufikia hatua ya kusisitiza kwamba auawe. (Luka 23:18-23) Naam, walihusika katika kifo cha Yesu.

Yesu alifufuliwa ili awe “jiwe kuu la pembeni” (Tazama fungu la 8 na 9)

8. Ni katika njia gani Yesu angeweza kuwa “jiwe kuu la pembeni”?

8 Kwa kuwa watu walimkataa Yesu na kumuua, angewezaje kuwa “jiwe kuu la pembeni”? Hilo lingewezekana tu ikiwa angefufuliwa na kuishi tena. Yesu alifafanua jambo hilo. Alisimulia mfano wa wakulima waliowatendea vibaya watu waliotumwa na mwenye shamba, kama ambavyo Waisraeli waliwatendea vibaya manabii ambao walitumwa na Mungu. Mwishowe katika mfano huo, Yesu alisema kwamba mwenye shamba alimtuma mwana wake mpendwa ambaye alikuwa pia mrithi wake. Je, walimkubali mwana huyo? La, hasha. Wakulima hao hata walimuua mwana huyo. Baada ya Yesu kusimulia mfano huo, alirejelea na kunukuu unabii wa Zaburi 118:22. (Luka 20:9-17) Mtume Petro alionyesha uhusiano huo tena alipozungumza na ‘watawala wa Wayahudi na wanaume wazee na waandishi katika Yerusalemu.’ Alizungumza kuhusu “Yesu Kristo Mnazareti, ambaye mlimtundika mtini lakini ambaye Mungu alimfufua kutoka kwa wafu.” Halafu Petro akasema hivi waziwazi: “Hilo ndilo ‘jiwe ambalo ninyi wajenzi mlilitendea kana kwamba si la maana ambalo limekuwa jiwe kuu la pembeni.’”—Mdo. 3:15; 4:5-11; 1 Pet. 2:5-7.

9. Zaburi 118:22 ilitabiri kuhusu tukio gani la pekee?

9 Naam, miaka mingi mapema, unabii unaopatikana katika Zaburi 118:22 ulionyesha kwamba kungekuwa na ufufuo. Masihi angekataliwa na kuuawa, lakini angefufuliwa na kuishi tena ili awe jiwe kuu la pembeni. Hivyo, Mwana huyo aliyefufuliwa akawa ndiye pekee ambaye jina lake ‘wanadamu walipewa, ambalo kupitia hilo lazima sisi tupate kuokolewa.’—Mdo. 4:12; Efe. 1:20.

10. (a) Zaburi 16:10 ilitabiri nini? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Zaburi 16:10 haikumhusu Daudi?

10 Fikiria mstari mwingine uliotabiri kuhusu ufufuo. Uliandikwa zaidi ya miaka elfu moja kabla ya ufufuo wenyewe kutukia, jambo ambalo linapaswa kuimarisha uhakika wako kwamba ufufuo unaweza kutukia miaka mingi baada ya kutabiriwa au kuahidiwa. Kwenye Zaburi ya 16, ambayo huenda iliandikwa na Daudi, tunasoma hivi: “Hutaiacha nafsi yangu katika Kaburi. Hutamruhusu mshikamanifu wako aone shimo.” (Zab. 16:10) Daudi hakumaanisha kwamba hangekufa kamwe au kuingia kaburini. Neno la Mungu linaonyesha wazi kwamba Daudi alizeeka. Baada ya Daudi kufa “[alilala] pamoja na mababu zake, akazikwa katika Jiji la Daudi.” (1 Fal. 2:1, 10) Hivyo basi, Zaburi 16:10 inamaanisha nini?

11. Petro alizungumzia Zaburi 16:10 wakati gani?

11 Hatujaachwa gizani. Zaidi ya miaka elfu moja baada ya zaburi hiyo kuandikwa na majuma machache baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, Petro alizungumza na maelfu ya Wayahudi na wageuzwa-imani kuhusu Zaburi 16:10. (Soma Matendo 2:29-32.) Alitaja kwamba kwa kweli Daudi alikufa na kuzikwa. Watu waliokuwa wakimsikiliza Petro walijua jambo hilo. Na Maandiko hayasemi kwamba yeyote kati yao alipinga maneno ya Petro kwamba Daudi “aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo” wa Masihi aliyeahidiwa.

12. Zaburi 16:10 ilitimizwaje, na hilo linatoa uhakika gani kuhusu ahadi ya ufufuo?

12 Petro alikazia hoja yake kwa kunukuu maneno ya Daudi yanayopatikana kwenye Zaburi 110:1. (Soma Matendo 2:33-36.) Hoja za Kimaandiko ambazo Petro alitoa zilisadikisha umati huo wa watu kwamba Yesu alikuwa “Bwana na pia Kristo.” Kwa kuongezea, watu walitambua kwamba Zaburi 16:10 ilitimizwa Yesu alipofufuliwa kutoka kwa wafu. Baadaye, mtume Paulo alitumia hoja hizohizo zenye kusadikisha alipozungumza na Wayahudi katika jiji la Antiokia huko Pisidia. Walivutiwa sana na hoja alizotumia, nao walitaka kuendelea kumsikiliza. (Soma Matendo 13:32-37, 42.) Je, hatuvutiwi kwamba unabii mbalimbali wa Biblia uliotabiri kuhusu ufufuo huo ulithibitika kuwa wenye kutegemeka, ingawa karne nyingi zilipita tangu muujiza huo ulipotabiriwa?

UFUFUO UTATUKIA LINI?

13. Ni maswali gani kuhusu ufufuo ambayo huenda yakazuka?

13 Tunatiwa moyo kujua kwamba ufufuo unaweza kutukia karne nyingi baada ya kuahidiwa. Ingawa hivyo, huenda mtu akajiuliza hivi: ‘Je, hilo linamaanisha kwamba nitasubiri kwa muda mrefu sana ili kumwona mpendwa wangu? Ufufuo ninaotazamia utatukia lini?’ Yesu aliwaambia mitume wake kwamba kuna mambo ambayo hawakujua na hawangeweza kuyajua. Kuna habari kuhusu “nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.” (Mdo. 1:6, 7; Yoh. 16:12) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba hatuna habari zozote kuhusu wakati ambapo ufufuo utatukia.

14. Ufufuo wa Yesu ulitofautianaje na ufufuo mbalimbali uliotukia awali?

14 Ili kuelewa jambo hilo, kumbuka ufufuo mbalimbali ambao ulitabiriwa katika Biblia. Bila shaka, ufufuo muhimu zaidi ni ule wa Yesu. Ikiwa Yesu hangefufuliwa, hatungekuwa na tumaini lolote la kuwaona tena wapendwa wetu waliokufa. Watu waliofufuliwa kabla ya Yesu, kama vile watu waliofufuliwa na Eliya na Elisha, hawakuendelea kuishi siku zote. Walikufa tena na miili yao ikaoza. Tofauti nao, Yesu “amekwisha kufufuliwa kutoka kwa wafu; kifo si bwana juu yake tena.” Akiwa mbinguni, anaishi “milele na milele,” hatakufa kamwe.—Rom. 6:9; Ufu. 1:5, 18; Kol. 1:18; 1 Pet. 3:18.

15. Kwa nini Yesu anaitwa “matunda ya kwanza”?

15 Yesu ndiye wa kwanza kufufuliwa akiwa kiumbe wa roho, na bila shaka ufufuo wake ndio muhimu zaidi. (Mdo. 26:23) Lakini si yeye tu aliyeahidiwa kufufuliwa na kwenda mbinguni akiwa kiumbe wa roho. Yesu aliwahakikishia mitume wake waaminifu kwamba wangetawala pamoja naye mbinguni. (Luka 22:28-30) Ili wapokee thawabu hiyo, ni lazima wangekufa kwanza. Baadaye, kama Kristo, wangefufuliwa wakiwa na miili ya roho. Paulo aliandika kwamba “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” Paulo alionyesha kwamba wengine pia wangefufuliwa na kwenda kuishi mbinguni aliposema hivi: “Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.”1 Kor. 15:20, 23.

16. Ni nini kinachoweza kutusaidia kujua wakati ambapo ufufuo wa mbinguni ungetukia?

16 Kwa ujumla, maneno hayo ya Paulo yanatusaidia kujua wakati ambapo ufufuo wa mbinguni ungetukia. Ungetukia “wakati wa kuwapo kwake.” Kwa muda mrefu, Mashahidi wa Yehova wamethibitisha kupitia Maandiko kwamba tangu mwaka wa 1914 tumekuwa tukiishi wakati wa “kuwapo” kwa Yesu kulikoahidiwa. Tungali tunaishi katika kipindi hicho, na sasa mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo umekaribia sana.

17, 18. Ni nini kitakachowapata baadhi ya watiwa mafuta wakati wa kuwapo kwa Kristo?

17 Biblia inatupatia habari zaidi kuhusu ufufuo wa mbinguni: “Hatutaki mkose kujua kuhusu wale walalao usingizi katika kifo . . . Kwa maana ikiwa imani yetu ni kwamba Yesu alikufa na kufufuliwa tena, vivyo hivyo pia, wale ambao wamelala usingizi katika kifo kupitia Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye . . . Sisi tulio hai ambao tutabaki mpaka kuwapo kwa Bwana hatutawatangulia kwa vyovyote wale ambao wamelala usingizi katika kifo; kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wenye amri, . . . na wale walio wafu katika muungano na Kristo watafufuliwa kwanza. Baadaye sisi tulio hai tuliobaki tutanyakuliwa, pamoja nao, katika mawingu ili kukutana na Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana sikuzote.”—1 The. 4:13-17.

18 Ufufuo wa kwanza ungetukia wakati fulani baada ya kuanza kwa “kuwapo” kwa Kristo. Watiwa mafuta watakaokuwa hai wakati wa dhiki kuu ‘watanyakuliwa katika mawingu.’ (Mt. 24:31) Wale ‘watakaonyakuliwa hawatalala usingizi katika kifo,’ katika maana ya kwamba hawatalala katika usingizi wa kifo kwa muda mrefu. ‘Wote watabadilishwa, kwa muda mfupi, kufumba na kufumbua jicho, wakati wa tarumbeta ya mwisho.’—1 Kor. 15:51, 52.

19. Tunatarajia ‘ufufuo gani ulio bora’?

19 Leo, Wakristo wengi waaminifu si watiwa mafuta na hawajapokea mwito wa kwenda kutawala pamoja na Kristo mbinguni. Badala yake, wanangojea mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo utakaoharibiwa katika “siku ya Yehova.” Hakuna yeyote anayeweza kujua ni lini hasa mwisho huo utafika, lakini uthibitisho unaonyesha kwamba umekaribia sana. (1 The. 5:1-3) Baada ya mwisho huo, ufufuo wa aina nyingine utatukia ambapo watu watafufuliwa ili waishi katika dunia itakayokuwa paradiso. Wale watakaofufuliwa watakuwa na tumaini la kuwa wanadamu wakamilifu na hawatalazimika kufa tena. Kwa hakika, huo utakuwa “ufufuo ulio bora” kuliko ufufuo uliotukia zamani ambapo “wanawake waliwapokea wafu wao kwa ufufuo” lakini watu hao walikufa tena.—Ebr. 11:35.

20. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba ufufuo utatukia kwa mpangilio?

20 Biblia inaposema kuhusu wale watakaofufuliwa ili wakaishi mbinguni, inasema kwamba watafufuliwa “kila mmoja katika daraja lake mwenyewe.” (1 Kor. 15:23) Vivyo hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba wale watakaofufuliwa ili waishi duniani watafufuliwa kwa mpangilio unaofaa. Hilo ni tumaini linalosisimua sana. Je, wale waliokufa karibuni watafufuliwa mwanzoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo na kukaribishwa na wapendwa wao wanaowafahamu? Je, wanaume waaminifu wa zamani na wenye uwezo wa kuongoza mambo watafufuliwa mapema ili wasaidie kusimamia watu wa Mungu katika ulimwengu mpya? Vipi kuhusu watu ambao hawakumtumikia Yehova? Watafufuliwa lini, na wapi? Tunaweza kujiuliza maswali mengi. Lakini je, kweli mambo hayo yanapaswa kutuhangaisha kwa sasa? Je, haingefaa kusubiri na kuona mambo yatakavyokuwa? Tuna uhakika kwamba tutafurahi kushuhudia jinsi Yehova atakavyoshughulikia mambo hayo.

21. Una tumaini gani kuhusu ufufuo?

21 Kwa sasa, tunapaswa kuimarisha imani yetu katika Yehova, ambaye kupitia Yesu alituhakikishia kwamba wafu walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa. (Yoh. 5:28, 29; 11:23) Akithibitisha kwamba Yehova ana uwezo wa kuwafufua wafu, Yesu alisema kwamba Abrahamu, Isaka, na Yakobo “kwake, hao wote wako hai.” (Luka 20:37, 38) Hivyo, tuna sababu za kutosha kusema kama alivyosema mtume Paulo: “Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo.”—Mdo. 24:15.