Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi​—Wasaidieni Watoto Wenu Wawe ‘Wenye Hekima kwa Ajili ya Wokovu’

Wazazi​—Wasaidieni Watoto Wenu Wawe ‘Wenye Hekima kwa Ajili ya Wokovu’

“Tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.”​—2 TIM. 3:15.

NYIMBO: 141, 134

1, 2. Kwa nini huenda baadhi ya wazazi wakawa na wasiwasi watoto wao wanapotaka kujiweka wakfu na kubatizwa?

MAELFU ya wanafunzi wa Biblia hujiweka wakfu na kubatizwa. Wengi wao ni vijana ambao wamelelewa katika kweli na ambao wamechagua njia bora ya maisha. (Zab. 1:1-3) Ikiwa wewe ni mzazi Mkristo, bila shaka unatarajia kwa hamu siku ambayo mwana au binti yako atabatizwa.—Linganisha 3 Yohana 4.

2 Hata hivyo, huenda ukawa na wasiwasi. Labda umejionea baadhi ya vijana wakibatizwa lakini baadaye wanaanza kutilia shaka hekima ya kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Wengine wao hata wameacha njia ya ile kweli. Hivyo, huenda ukawa na wasiwasi kwamba mtoto wako ataanza kuishi maisha ya Kikristo lakini baadaye abadilike na kupoteza upendo aliokuwa nao mwanzoni kuelekea kweli. Anaweza kuwa kama watu fulani waliokuwa katika kutaniko la Efeso la karne ya kwanza ambao Yesu alisema hivi kuwahusu: “Umeacha upendo uliokuwa nao mwanzoni.” (Ufu. 2:4) Unaweza kufanya nini ili uepuke hali hiyo na kumsaidia mtoto wako ‘akue kufikia wokovu’? (1 Pet. 2:2) Ili tupate jibu la swali hilo, acheni tuchunguze mfano wa Timotheo.

“UMEYAJUA MAANDISHI MATAKATIFU”

3. (a) Timotheo alijifunzaje Ukristo, naye aliitikiaje mafundisho hayo? (b) Paulo alimhimiza Timotheo kuhusu mambo gani matatu yanayohusika katika kujifunza?

3 Huenda Timotheo alianza kufundishwa mafundisho ya Kikristo mwaka wa 47 W.K. mtume Paulo alipotembelea jiji la Listra kwa mara ya kwanza. Ingawa huenda wakati huo Timotheo alikuwa kijana, inaonekana kwamba alikuwa akifanya maendeleo ya kiroho. Kisha baada ya miaka miwili, akaanza kusafiri na Paulo. Miaka 16 hivi baadaye, Paulo alimwandikia hivi Timotheo: “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini, ukijua ni kutoka kwa watu gani ulijifunza hayo na kwamba tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu [Maandiko ya Kiebrania], ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (2 Tim. 3:14, 15) Ona kwamba Paulo anataja (1) kuyajua maandishi matakatifu, (2) kushawishiwa kuamini mambo uliyojifunza, na (3) kuwa na hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.

4. Ni vifaa gani ambavyo vimekusaidia kuwafundisha watoto wako wachanga? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 Ukiwa mzazi Mkristo, ungependa mtoto wako ayajue maandishi matakatifu, ambayo leo ni Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Ikitegemea uwezo wa watoto wako, hata watoto wachanga sana wanaweza kujifunza mambo ya msingi kuhusu watu na matukio yanayosimuliwa katika Biblia. Tengenezo la Yehova limeandaa vifaa mbalimbali ambavyo wazazi wanaweza kutumia ili kuwasaidia watoto wao. Ni vifaa gani vinavyopatikana katika lugha yako? Kumbuka, ujuzi wa Maandiko ndio msingi unaotusaidia kujenga uhusiano mzuri na Yehova.

“ULIYOSHAWISHIWA KUAMINI”

5. (a) Maneno “kushawishiwa kuamini” yanamaanisha nini? (b) Tunajuaje kwamba Timotheo alishawishiwa kuamini habari njema kumhusu Yesu?

5 Kuwa na ujuzi wa maandishi matakatifu ni muhimu. Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika katika kuwasaidia watoto wako wawe na elimu ya kiroho kuliko kuwafundisha tu kuhusu watu na matukio yanayosimuliwa katika Biblia. Timotheo pia ‘alishawishiwa kuamini.’ Katika lugha ya awali, maneno hayo yanamaanisha “kuhakikishiwa” au “kusadikishwa na kuwa na uhakika kuhusiana na ukweli wa jambo fulani.” Timotheo aliyajua Maandiko ya Kiebrania tangu alipokuwa mtoto mchanga. Lakini baadaye alisadikishwa kupitia uthibitisho ulio hakika kwamba Yesu alikuwa Masihi. Kwa maneno mengine, ujuzi aliokuwa nao ulitegemezwa na mambo hakika aliyosadiki. Kwa kweli, usadikisho ambao Timotheo alikuwa nao kuhusu habari njema ulikuwa wenye nguvu sana hivi kwamba akabatizwa na kujiunga na Paulo katika kazi ya umishonari.

6. Unaweza kuwasaidiaje watoto wako washawishiwe kuamini mambo wanayojifunza katika Neno la Mungu?

6 Unaweza kuwasaidiaje watoto wako wawe na usadikisho utakaowafanya washawishiwe kuamini, kama ilivyokuwa kwa Timotheo? Kwanza, uwe na subira. Usadikisho hauji kwa siku moja; wala mtoto hawezi kurithi usadikisho kutoka kwako eti kwa sababu wewe umeshawishiwa kuamini. Kila mtoto anahitaji kutumia ‘nguvu zake za kufikiri’ ili asitawishe usadikisho kuhusu kweli za Biblia. (Soma Waroma 12:1.) Ukiwa mzazi, una jukumu muhimu la kumsaidia mtoto wako asitawishe usadikisho, hasa anapouliza maswali. Fikiria mfano ufuatao.

7, 8. (a) Baba mmoja Mkristo anaonyeshaje subira anapomfundisha binti yake? (b) Ni nyakati zipi ulipohisi kwamba unahitaji kuwa mwenye subira unapomfundisha mtoto wako?

7 Thomas, baba mwenye binti aliye na umri wa miaka 11, anaeleza hivi: “Binti yangu anaweza kuniuliza hivi, ‛Je, inawezekana Yehova alitumia mageuzi kuanzisha uhai duniani?’ au, ‛Kwa nini hatujihusishi na mambo ya kijamii kama vile kupiga kura ili kuboresha mambo?’ Nyakati nyingine ninalazimika kujizuia ili nisimwambie tu mambo anayopaswa kuamini. Ukweli ni kwamba usadikisho hautokani na kujua tu habari nyingi kuhusu kweli. Unatokana na kujifunza mambo madogo-madogo yenye kusadikisha.”

8 Kama ambavyo Thomas amejifunza, kufundisha kunahitaji subira. Kwa kweli, sifa ya subira ni muhimu kwa Wakristo wote. (Kol. 3:12) Thomas anatambua kwamba huenda akahitaji kuendelea kuwa na mazungumzo ya mara kwa mara pamoja na binti yake kwa kipindi kirefu. Anahitaji kutoa sababu za Kimaandiko ili binti yake asitawishe usadikisho kuhusu mambo anayojifunza. Thomas anasema hivi: “Mimi na mke wangu hutaka kujua ikiwa kwa kweli binti yetu anaamini mambo anayojifunza na ikiwa anakubaliana na mambo hayo. Tunafurahi anapouliza maswali. Kwa kweli, ningekuwa na wasiwasi ikiwa angekubaliana tu na jambo fulani bila kuuliza maswali.”

9. Unaweza kufanya nini ili kukazia Neno la Mungu akilini na moyoni mwa watoto wako?

9 Wazazi wanapowafundisha watoto wao kwa subira, hatua kwa hatua watoto wao wataanza kuelewa “upana na urefu na kimo na kina” cha imani. (Efe. 3:18) Tunaweza kutafuta habari zinazowafaa kulingana na umri na uwezo wao. Kadiri wanavyosadiki mambo wanayojifunza, ndivyo watakavyokuwa tayari kutetea imani yao mbele ya wengine, kutia ndani wanafunzi wenzao. (1 Pet. 3:15) Kwa mfano, je, watoto wako wanaweza kutumia Biblia kueleza kinachotokea mtu anapokufa? Je, wanakubaliana na yale ambayo Biblia inasema? * Naam, kukazia Neno la Mungu akilini na moyoni mwa mtoto wako kunahitaji subira, hata hivyo, jitihada zako si za bure.—Kum. 6:6, 7.

10. Ni jambo gani linalopaswa kuwa sehemu muhimu ya ufundishaji wako?

10 Bila shaka, mfano unaowawekea watoto wako ni muhimu sana ili kuwasaidia wawe na usadikisho. Stephanie, mama mwenye mabinti watatu, anasema hivi: “Tangu watoto wangu walipokuwa wachanga, nimejiuliza, ‘Je, mimi huwaeleza watoto wangu kwa nini mimi ninasadiki kwamba Yehova yupo, ananipenda, na kwamba njia zake ni za uadilifu? Je, watoto wangu wanaona waziwazi kwamba mimi ninampenda Yehova kutoka moyoni?’ Siwezi kutarajia watoto wangu washawishiwe kuamini ilhali mimi sijashawishiwa kuamini.”

“MWENYE HEKIMA KWA AJILI YA WOKOVU”

11, 12. Hekima ni nini, na kwa nini tunaweza kusema kwamba haitegemei tu umri wa mtu?

11 Kama tulivyoona, Timotheo alikuwa na (1) ujuzi wa Maandiko na (2) alisadiki mambo aliyoamini. Lakini Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba maandishi matakatifu yangemfanya Timotheo awe “mwenye hekima kwa ajili ya wokovu”?

12 Kitabu Insight on the Scriptures, Buku la 2, kinasema kwamba katika Biblia, hekima inatia ndani “uwezo wa kutumia ujuzi na ufahamu kwa mafanikio ili kutatua matatizo, kuepuka au kujilinda dhidi ya hatari, kufikia malengo fulani, au kuwasaidia wengine kufanya hivyo. Hekima ni kinyume cha upumbavu.” Biblia inasema kwamba “ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” (Met. 22:15) Hivyo basi, sifa ya hekima, ambayo ni kinyume cha upumbavu, ni mojawapo ya sifa zinazothibitisha kwamba mtu amekomaa. Ukomavu wa kiroho hautegemei tu umri, bali mtu huonyesha kwamba yeye ni mkomavu kiroho kwa kuonyesha woga unaofaa kumwelekea Yehova na kwa utayari wake wa kutii amri zake.—Soma Zaburi 111:10.

13. Kijana anaweza kuonyeshaje kwamba ana hekima kwa ajili ya wokovu?

13 Vijana ambao kwa kadiri fulani ni wakomavu kiroho ‘hawarushwi huku na huku kama kwa mawimbi’ kwa tamaa zao au kushinikizwa na marafiki wao. (Efe. 4:14) Badala yake, wanafanya maendeleo kwa kuzoeza “nguvu zao za ufahamu . . . kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Ebr. 5:14) Wanaonyesha kwamba wanajitahidi kufikia ukomavu kwa kufanya maamuzi kwa hekima hata wakati ambapo wazazi au watu wengine wazima hawapo. (Flp. 2:12) Hekima ya aina hiyo ni ya lazima ili kupata wokovu. (Soma Methali 24:14.) Unaweza kuwasaidiaje watoto wako waipate? Kwanza kabisa, hakikisha kwamba unawaeleza waziwazi watoto wako viwango vyako vinavyotegemea Biblia. Acha watoto wako watambue kupitia maneno na mfano wako kwamba viwango vya Biblia ndivyo viwango vyako pia.—Rom. 2:21-23.

Kwa nini ni muhimu mzazi aendelee kujitahidi bila kuchoka? (Tazama fungu la 14 hadi 18)

14, 15. (a) Kijana anayetaka kubatizwa anapaswa kufikiria mambo gani muhimu? (b) Unaweza kuwasaidiaje watoto wako watafakari baraka zinazotokana na kutii sheria za Mungu?

14 Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika kuliko kuwaambia tu watoto wako mambo yanayofaa na yasiyofaa. Itafaa pia kuwasaidia wafikirie kuhusu maswali kama vile: ‘Kwa nini Biblia inakataza mambo fulani yanayoonekana kuwa yenye kuvutia? Ni nini kinachonisadikisha kwamba nitanufaika sikuzote ninapofuata viwango vya Biblia?’—Isa. 48:17, 18.

15 Mtoto anayetaka kubatizwa anapaswa kusaidiwa afikirie jambo lingine pia—anahisije kuhusu wajibu atakaohitaji kutimiza akiwa Mkristo? Kuna manufaa gani ya kuwa Mkristo? Atakabili changamoto zipi? Ni kwa njia gani manufaa atakayopata yatazidi changamoto atakazokabili? (Marko 10:29, 30) Hayo ni baadhi ya mambo ambayo mtu anaweza kukabili baada ya kubatizwa. Kwa hiyo, inafaa afikirie kwa uzito mambo hayo kabla ya kuchukua hatua hiyo muhimu. Watoto wanaposaidiwa kufikiria kwa uzito baraka za kutii na matokeo mabaya ya kutotii, kuna uwezekano mkubwa kwamba watasitawisha usadikisho wao wenyewe. Usadikisho kuhusu nini? Kwamba sikuzote viwango vya Biblia ni vyenye manufaa wanapovifuata.—Kum. 30:19, 20.

KIJANA ALIYEBATIZWA ANAPOANZA KUWA NA MASHAKA

16. Wazazi wanapaswa kuzingatia nini ikiwa imani ya mtoto wao ambaye amebatizwa inaanza kuyumbayumba?

16 Vipi ikiwa mwana au binti yako anaanza kutilia shaka imani yake baada ya kubatizwa? Kwa mfano, kijana ambaye amebatizwa anaweza kuanza kuvutiwa na mambo ya ulimwengu au anaweza kuanza kutilia shaka hekima ya kuishi kulingana na kanuni za Biblia. (Zab. 73:1-3, 12, 13) Ukiwa mzazi, tambua kwamba jinsi unavyoshughulikia mashaka ambayo mwana au binti yako anayo, kunaweza kumfanya ama achague kushikamana na imani yako ama ajiondoe kutoka katika imani hiyo. Azimia kutozozana na mtoto wako kuhusu jambo hilo, iwe mtoto wako ana umri mdogo au ni kijana anayebalehe. Unapaswa kuwa na lengo la kumsaidia kwa upendo ili asitawishe tena usadikisho.

17, 18. Ikiwa kijana ana mashaka fulani, wazazi wanaweza kumsaidiaje?

17 Bila shaka, kijana aliyebatizwa amejiweka wakfu kwa Yehova. Kujiweka wakfu ni kutoa ahadi kwa Mungu kwamba utampenda na kutanguliza mapenzi yake maishani. (Soma Marko 12:30.) Yehova hachukulii kivivihivi ahadi hiyo, na haipaswi kuchukuliwa kivivihivi na yeyote ambaye ameitoa. (Mhu. 5:4, 5) Tafuta wakati unaofaa kumkumbusha mtoto wako kuhusu jambo hilo, na ufanye hivyo kwa fadhili. Lakini kabla ya kufanya hivyo fanya utafiti katika vifaa ambavyo tengenezo la Yehova limeandaa kwa ajili ya wazazi. Hilo litakusaidia kuweka msingi utakaokuwezesha kukazia akilini mwa mtoto wako uzito na baraka za kujiweka wakfu kwa Yehova na kuwa Mkristo aliyebatizwa.

18 Kwa mfano, unaweza kupata ushauri mzuri katika nyongeza yenye kichwa “Maswali Ambayo Wazazi Huuliza,” iliyo kwenye kurasa za nyuma za kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1. Nyongeza hiyo inasema hivi: “Usikate kauli kwamba kijana wako ameikataa imani yako. Mara nyingi, huenda kukawa na sababu nyingine.” Huenda anashinikizwa na marafiki wake. Inawezekana pia ni mpweke au anahisi kwamba vijana wengine Wakristo wanafanya maendeleo ya kiroho kuliko yeye. Nyongeza hiyo inaendelea kusema hivi: “Kumbuka kwamba, mambo kama haya hayahusiani na mafundisho ya imani yako. Kwa sasa, yanahusiana sana na hali zinazofanya iwe vigumu kujizoeza imani.” Kisha nyongeza hiyo inatoa mapendekezo kadhaa kuhusu jinsi mzazi Mkristo anavyoweza kumsaidia kijana ambaye imani yake inayumbayumba.

19. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao ili wawe na “hekima kwa ajili ya wokovu”?

19 Ukiwa mzazi una jukumu zito sana na pendeleo kubwa la kuwalea watoto wako “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Kama tulivyoona, kufanya hivyo hakuhusishi tu kuwafundisha mambo ambayo Biblia inasema, bali pia kuwasaidia kusitawisha usadikisho kuhusu mambo wanayojifunza. Naam, wanahitaji kuwa na usadikisho wenye nguvu sana utakaowachochea wajiweke wakfu kwa Yehova na kumtumikia kwa moyo wote. Acha Neno la Yehova, roho yake, na jitihada zako ukiwa mzazi ziwasaidie watoto wako wawe na “hekima kwa ajili ya wokovu.”

^ fu. 9 Miongozo ya kujifunza yenye kichwa “Biblia Inafundisha Nini?” ni vifaa bora vya kuwasaidia vijana na watu wazima kuelewa na kufafanua kweli za Biblia. Miongozo hiyo inapatikana katika lugha nyingi kwenye Tovuti ya jw.org. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > VIFAA VYA KUJIFUNZIA BIBLIA.