Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia na Wakati Wako Ujao

Biblia na Wakati Wako Ujao

JIWAZIE jioni moja ukitembea kwenye barabara yenye giza. Ingawa jua lilizama muda mrefu uliopita, hauogopi kupotea kwa sababu una tochi iliyo na mwanga mkali. Unapomulika chini unaona vizuri kila kitu kilicho karibu yako. Na unapomulika mbele, mwanga wake mkali unaangazia njia yako.

Kwa njia fulani, Biblia ni kama tochi hiyo. Kama tulivyochunguza katika makala zilizotangulia, Neno la Mungu linaweza kutusaidia kushughulika na kile kilicho karibu yetu, yaani, matatizo ya kila siku tunayokabili katika ulimwengu huu usiotabirika. Lakini zaidi ya hilo, Biblia huangazia pia wakati wetu ujao, na hivyo kutusaidia kuona na kufuata njia inayoongoza kwenye furaha ya kudumu na uradhi. (Zaburi 119:105) Jinsi gani?

Acheni tuchunguze jinsi Biblia inavyotupatia tumaini la wakati ujao katika njia mbili: 1 Inatusaidia kuwa na kusudi katika maisha yetu, na 2 hutufundisha jinsi ya kusitawisha urafiki wa kudumu pamoja na Muumba wetu.

1 KUSUDI MAISHANI

Zaidi ya kutoa ushauri wenye kutegemeka wa kukabiliana na matatizo yetu, Biblia hutusaidia kwa njia nyingine kubwa. Badala ya kutuchochea kukazia tu hali zetu binafsi, Biblia hutufundisha kufikiria pia hali za wengine. Hiyo ndiyo njia pekee ya kuwa na maisha yenye maana.

Kwa mfano, fikiria kanuni hii ya Biblia: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Je, unakumbuka wakati ambapo ulimsaidia mtu fulani mwenye uhitaji? Au, huenda ulijitoa kumsikiliza rafiki yako alipokuwa akieleza hisia zake za ndani. Je, hukuhisi uradhi wa kumsaidia mtu mwingine aboreshe maisha yake?

Tunapata furaha ya kweli tunapotoa bila kutazamia chochote. Mwandishi fulani aliandika hivi: “Karibu kila mara unapojitoa unapata zaidi ya kile ulichotoa, maadamu tu unafanya hivyo bila kutarajia malipo yoyote.” Kwa kweli, tunapojitoa kuwasaidia wengine, hasa wale wasio na uwezo wa kutupatia chochote, tunapata thawabu. Kihalisi tunakuwa tukifanya kazi pamoja na Muumba wetu ambaye huona matendo hayo ya fadhili kuwa deni analohitaji kulipa. (Methali 19:17) Anathamini sana yale tunayofanya kwa ajili ya watu wa hali ya chini, naye anaahidi kutulipa kwa kutupatia uzima wa milele katika dunia paradiso. Hilo ni tumaini lenye kusisimua sana!—Zaburi 37:29; Luka 14:12-14. *

Zaidi ya yote, Biblia hutufundisha kwamba tunaweza kuwa na kusudi halisi maishani kwa kumwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Neno Lake hutuchochea kumpa sifa, heshima, na utii anaostahili. (Mhubiri 12:13; Ufunuo 4:11) Tunapofanya hivyo, tunatimiza jambo la maana sana: Tunaufurahisha moyo wa Muumba wetu. Hiyo ndiyo sababu anatusihi hivi: “Uwe na hekima . . . na kuufanya moyo wangu ushangilie.” (Methali 27:11) Hebu fikiria jambo hilo. Tunapofanya maamuzi yanayotegemea kanuni za Biblia, tunaufanya moyo wa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo ushangilie. Kwa nini? Kwa sababu anatujali na anataka tufaidike kwa kufuata mwongozo wake. (Isaya 48:17, 18) Kwa kweli, hakuna kusudi bora zaidi kuliko kumwabudu Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima na kuishi kwa njia inayoufurahisha moyo wake.

2 URAFIKI PAMOJA NA MUUMBA WETU

Biblia pia hutuambia tusitawishe urafiki pamoja na Muumba wetu. Maandiko yanasema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Huenda nyakati nyingine tukatilia shaka uwezekano wa kuwa rafiki za Muumba mweza-yote. Lakini Biblia inatuhakikishia kwamba ‘tukimtafuta Mungu, kwa kweli tutampata,’ kwa kuwa “hayuko mbali na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Ushauri wa Biblia kuhusu kuwa rafiki za Mungu unaathiri wakati wetu ujao kwa njia kubwa sana. Jinsi gani?

Fikiria jambo hili: Hata tukijitahidi kadiri gani, hakuna yeyote kati yetu ambaye kwa uwezo wake mwenyewe anaweza kuepuka adui yetu mkubwa, kifo. (1 Wakorintho 15:26) Hata hivyo, Mungu amekuwepo kwa umilele wote. Hatawahi kufa, na anataka rafiki zake waishi milele pia. Kwa kutumia maneno haya rahisi lakini yenye kuvutia, Biblia inaeleza mapenzi ya Mungu kwa kila mtu anayemtafuta: “Na ufurahie maisha milele.”—Zaburi 22:26.

Unawezaje kusitawisha urafiki wa kudumu pamoja na Mungu? Endelea kujifunza kumhusu kupitia Neno lake, Biblia. (Yohana 17:3; 2 Timotheo 3:16) Mwombe akusaidie kuelewa Maandiko. Biblia inatuhakikishia kwamba ‘tukiendelea kumwomba Mungu’ kwa unyoofu atupatie hekima, yeye atafanya hivyo. * (Yakobo 1:5) Kisha, jitahidi kutumia yale unayojifunza, na hivyo kuruhusu Neno la Mungu liwe “taa ya mguu [wako] na nuru ya njia [yako],” sasa na milele.—Zaburi 119:105.

^ fu. 8 Ili kupata habari zaidi kuhusu ahadi ya Mungu ya uzima wa milele katika Paradiso, soma sura ya tatu ya kitabu Biblia Inatufundisha Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 13 Mashahidi wa Yehova wana programu ya kujifunza Biblia bila malipo ambayo inaweza kukusaidia uboreshe uelewaji wako wa Maandiko. Ili kuelewa jinsi programu hiyo inavyofanyika, tazama video Ni Nini Hutendeka Kwenye Funzo la Biblia? inayopatikana kwenye jw.org/sw.

Mungu amekuwepo kwa umilele wote na anataka rafiki zake waishi milele pia