Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ushahidi wa Kimya-Kimya Wenye Kuonyesha Kama Unabii wa Biblia Ni wa Kweli

Ushahidi wa Kimya-Kimya Wenye Kuonyesha Kama Unabii wa Biblia Ni wa Kweli

KATIKA ROMA YA KATI, ITALIA, MUNAPATIKANA MULANGO WA USHINDI WENYE UNAVUTIA WAGENI WENYE KUTOKA SEHEMU ZOTE ZA DUNIA. MULANGO HUO WENYE KUWA KAMA UPINDE ULIJENGWA ILI KUMUPATIA HESHIMA MUTAWALA MUMOJA MUROMA MWENYE KUPENDWA SANA, NI KUSEMA, TITO.

Mulango wa Tito uko na michongo mbili kubwa yenye kuonyesha tukio lenye kujulikana katika historia. Hata kama haujulikane na watu wengi, mulango huo unapatana kwa njia ya ajabu na mambo yenye Biblia inasema​—Mulango wa Tito unatoa ushahidi wa kimya-kimya kwamba unabii wa Biblia ni wa kweli kabisa.

MUJI WENYE ULIHUKUMIWA

Mwanzoni mwa karne ya kwanza wakati wetu, Utawala wa Roma ulichukua eneo la Uingereza na Gaul (leo Ufaransa) mupaka Misri, na eneo hilo lilikuwa kabisa tajiri na lenye usalama. Lakini kulikuwa eneo moja la mbali lenye halikuwa kila mara katika amani na Roma. Eneo hilo ni jimbo la Yudea.

Kitabu Encyclopedia of Ancient Rome kinasema hivi: “Ni maeneo kidogo sana yenye yalikuwa chini ya utawala wa Roma ndiyo yalikuwa na chuki kubwa kama hiyo, pande zote mbili, kama Yudea. Wayahudi walichukia wakubwa wenye hawakuwa Wayahudi ambao hawakuhangaikia desturi zao, na Waroma waliona kama hawakupaswa kuvumilia Wayahudi wenye vichwa vigumu.” Wayahudi wengi walitumaini kuwa kiongozi mumoja angewaokoa na kufukuza Waroma hao wenye walichukia na kurudishia Waisraeli utukufu wao wa zamani. Lakini katika mwaka wa 33 wakati wetu, Yesu Kristo alisema kama muji wa Yerusalemu ulikuwa karibu kupatwa na musiba.

Yesu alisema hivi: “Siku zitakuja juu yako wakati adui zako watakapojenga kukuzunguka ngome yenye miti iliyochongoka nao watakuzunguka na kukutaabisha kutoka kila upande, nao watakuangusha chini wewe na watoto wako walio ndani yako, nao hawataacha jiwe juu ya jiwe ndani yako.”​Luka 19:43, 44.

Bila shaka maneno ya Yesu yalivuruga wanafunzi wake. Siku mbili kisha, wakati waliona hekalu la Yerusalemu, mumoja wao alisema hivi: ‘Mwalimu, ona! jinsi yalivyo majiwe haya na majengo haya!’ Kwa kweli, inasemekana kuwa majiwe fulani yalikuwa na urefu wa metre 11, upana wa metre 5, na kimo (hauteur) cha metre 3! Lakini, Yesu alijibu hivi: ‘Vitu hivi ambavyo ninyi munaviona, siku zitakuja ambapo hakuna jiwe litakaloachwa hapa juu ya jiwe nalo lisiangushwe chini.’​Marko 13:1; Luka 21:6.

Kisha, Yesu aliwaambia hivi: ‘Mutakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia. Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke, nao wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani.’ (Luka 21:20, 21) Je, maneno ya Yesu yalitimia?

KUHARIBIWA KWA MUJI

Miaka 33 ilipita, na Yudea ilikuwa ingali inachukia kutawaliwa na Roma. Lakini katika mwaka wa 66 wakati wetu, wakati mutawala Muroma wa jimbo la Yudea, Gessius Florus, alichukua kwa nguvu feza zenye zilikuwa katika hazina takatifu la hekalu, Wayahudi walikasirika na kuona kuwa hawawezi tena kuvumilia jambo hilo. Kisha tu muda mufupi, wapiganaji Wayahudi walikutana wengi katika Yerusalemu, wakaua kikundi cha maaskari Waroma wenye walikuwa wanachunga muji, na wakatangaza uhuru kuwa hawako tena chini ya utawala wa Roma.

Karibu miezi tatu kisha, maaskari Waroma zaidi ya 30 000, wenye kuongozwa na Cestius Gallus, walienda katika Yerusalemu ili kumaliza kabisa uasi huo. Waroma waliingia haraka katika muji na kuregeza ukuta wa inje wenye ulikuwa upande wa hekalu. Kisha, kwa sababu yenye hatujue, walitoka katika muji. Wayahudi waasi walifurahi na wakawafuatilia haraka. Kwa sababu maaskari Waroma na Wayahudi waasi walikuwa wametoka katika muji, Wakristo wenye walisikia onyo la Yesu, walitoka katika Yerusalemu na kukimbia kuenda kwenye milima ngambo ya Muto Yordani.​—Mathayo 24:15, 16.

Mwaka wenye ulifuata, Roma ilipanga tena kupigana na Yudea. Wapiganaji Waroma waliongozwa na Jenerali Vespasien na mutoto wake Tito. Lakini, kisha tu kufa kwa Mutawala Nero katika mwaka wa 68 wakati wetu, Vespasien alirudia Roma ili kuwa mutawala, na akaachia mutoto wake, Tito, daraka la kuendelea na vita akiongoza jeshi la maaskari 60 000 hivi.

Katika Mwezi wa 6, mwaka wa 70 wakati wetu, Tito aliamuru maaskari wake wakate miti yenye ilikuwa katika Yudea, yenye ilitumiwa ili kujenga ukuta wa kilometre 7 wa miti yenye kuchongoka kuzunguka Yerusalemu. Kufikia Mwezi wa 9, walikuwa wamepora na kuunguza muji na hekalu lake na wakaongoa jiwe kwa jiwe, kama vile tu Yesu alikuwa ametabiri. (Luka 19:43, 44) Imekadiriwa kwa kiasi kwamba “watu karibu 500 000 walikufa katika Yerusalemu na katika sehemu ingine ya inchi.”

USHINDI MUKUBWA

Katika mwaka wa 71 wakati wetu, Tito alirudia katika Italia akikaribishwa kwa furaha kubwa na raia wa Roma. Watu wote katika muji walifurahia kuona moja ya matembezi makubwa zaidi ya ushindi yenye hayajafanyikaka katika muji huo mukubwa.

Watu walishangaa sana wakati walikuwa wanaangalia utajiri mukubwa wenye ulionyeshwa katika barabara za Roma. Walifurahi sana kuangalia mashua zenye zilinyanganywa, magari makubwa ya vita yenye kuonyesha namna walipigana vita, na vitu vyenye walikamata katika hekalu la Yerusalemu.

Tito alikuwa mutawala pa nafasi ya baba yake Vespasien katika mwaka wa 79 wakati wetu. Lakini miaka mbili tu kisha, Tito alipatwa na kifo cha kushtukia. Domitiani, ndugu yake, alichukua kiti cha ufalme na bila kukawia akajenga mulango wa ushindi kwa heshima ya Tito.

MULANGO HUO LEO

Mulango wa Tito katika Roma leo

Leo, Mulango wa Tito unavutia mamia ya maelfu ya watu wenye wanakuja kutembelea Roma kila mwaka. Watu fulani wanaona mulango huo kuwa chombo cha sanaa (œuvre d’art) cha hali ya juu, wengine wanaona kuwa mulango huo unaonyesha nguvu kubwa ya Utawala wa Roma, lakini wengine wanauona kuwa kitu chenye kuwakumbusha namna Yerusalemu na hekalu lake viliharibiwa.

Lakini wasomaji wa Biblia wenye kuwa waangalifu wanaona kuwa Mulango wa Tito uko hata na maana kubwa zaidi. Ni ushahidi wa kimya-kimya wenye kuonyesha kama unabii mbalimbali wa Biblia ni wa kweli na wenye kutegemeka, na ni ushuhuda kuwa unabii huo uliongozwa na roho ya Mungu.​—2 Petro 1:19-21.