Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ahadi Zenye Zitatimia

Ahadi Zenye Zitatimia

Habari njema ya Ufalme wa Mungu iko inahubiriwa katika dunia yote, kama tu vile Yesu alitabiri. (Mathayo 24:14) Katika kitabu cha Danieli, Biblia inatuambia kama Ufalme huo ni serikali ya Mungu. Katika sura ya 2 ya kitabu hicho munapatikana unabii wenye kuonyesha namna serikali fulani zenye nguvu za wanadamu, ao falme, zinafuatana kuanzia Babiloni mupaka siku zetu. Kuhusu mambo ya wakati wenye kuja, mustari wa 44 unatabiri hivi:

‘Na katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mupaka wakati usio na kipimo.’

Unabii huo na unabii mwengine mbalimbali wa Biblia unaonyesha kama Ufalme wa Mungu utachukua nafasi ya utawala wote wa wanadamu na kuletea watu wenye kuwa duniani amani na utaratibu. Maisha yatakuwa namna gani chini ya Ufalme? Tuone ahadi za muzuri zaidi zenye zitatimia hivi karibuni.

  • HAKUTAKUWA TENA VITA

    Zaburi 46:9: ‘[Mungu] anakomesha vita mupaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mukuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza [katika] moto.’

    Wazia namna ulimwengu ungekuwa ikiwa feza zote na ufundi wenye unatumiwa leo ili kutengeneza silaha ungetumiwa katika mambo yenye yangeletea watu faida kuliko kuwaua! Ahadi hiyo itatimia chini ya Ufalme wa Mungu.

  • HAKUTAKUWA TENA MAGONJWA

    Isaya 33:24: “Hakuna mukaaji atakayesema: ‘Mimi ni mugonjwa.’”

    Fikiria ulimwengu wenye hakuna tena mutu mwenye atakuwa na ugonjwa wa moyo, kansere, malaria, ao magonjwa mengine yoyote. Watu hawatakuwa tena na lazima ya kuenda kwenye hospitali na kutumia dawa. Watakuwa na afya kamilifu​—ni hivyo mambo yatakuwa wakati wenye kuja kwa wale wenye wataishi katika dunia.

  • HAKUTAKUWA TENA UPUNGUFU WA CHAKULA

    Zaburi 72:16: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”

    Udongo utazaa chakula ya mingi kwa ajili ya kila mutu, na watu wote hawatakuwa na magumu ya kupata chakula. Njaa na utapiamulo havitakuwa tena.

  • HAKUTAKUWA TENA MAUMIVU, HUZUNI, NA KIFO

    Ufunuo 21:4: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

    Hilo linamaanisha kama watu wataishi milele wakiwa wakamilifu katika dunia paradiso! Hiyo ndiyo ahadi kutoka kwa Muumbaji wetu mwenye upendo, Yehova Mungu.

“HAKIKA LITAFANIKIWA”

Tunaweza kusema kama mambo hayo yote ni ndoto tu? Watu wengi watakubali bila kusita kwamba maisha kama vile yameahidiwa na kuzungumuziwa katika Biblia ni maisha yenye wangependa kuwa nayo. Lakini juu ya sababu mbalimbali, watu wengi wanaona kuwa ni nguvu kuelewa wazo la kuishi milele. Hilo haliwezi kushangaza, kwa sababu hakuna mwanadamu kama sisi mwenye amekwisha kuishi milele ili kutuelezea juu ya jambo hilo.

Wanadamu wamefanywa kuwa watumwa wa zambi na kifo na wamelemewa sana na maumivu, mateso, na magumu kwa miaka mingi hivi kwamba wamefikia kuanza kuona maisha kama hayo kuwa ya kawaida. Lakini haiko ndiyo maisha yenye Muumbaji wetu, Yehova Mungu alipenda wanadamu wakuwe nayo.

Ili kutusaidia tukuwe hakika kama ahadi zake zote zitatimia, Mungu alisema kwa uhakika maneno haya kuhusu neno lake: “Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”​—Isaya 55:11.

Biblia inasema kama Yehova ni Mungu mwenye ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Kwa sababu ametoa ahadi hizo za muzuri zaidi kwa ajili ya wakati wenye kuja, ni jambo lenye hekima kujiuliza: Inawezekana kabisa wanadamu waishi milele katika dunia Paradiso yenye iliahidiwa? Tunapaswa kufanya nini ili kufaidika na ahadi za Mungu? Habari zenye kufuata za gazeti hili, zitakusaidia kupata majibu ya maulizo hayo.