Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hivi Karibuni Mungu Atakomesha Mateso Yote

Hivi Karibuni Mungu Atakomesha Mateso Yote

“Ee Yehova, nililie msaada mpaka lini, lakini wewe hunisikii? Nitaomba msaada kwa sababu ya ukatili mpaka lini, lakini huingilii kati?” (Habakuki 1:2, 3) Hayo ni maneno ya Habakuki, mwanamume mwenye sifa nzuri aliyekuwa na kibali cha Mungu. Je, ombi lake lilionyesha kwamba hakuwa na imani? La hasha! Mungu alimhakikishia Habakuki kwamba ameweka muda hususa wa kukomesha hali hizo ngumu.—Habakuki 2:2, 3.

Mtu wako wa karibu au wewe binafsi unapopitia changamoto maishani, ni rahisi kufikiri kwamba Mungu anachelewa sana kuchukua hatua na kwamba alipaswa kuwa amefanya jambo fulani kufikia sasa. Hata hivyo, Biblia inatuhakikishia hivi: “Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake, kama watu fulani wanavyodhani, bali ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Petro 3:9.

MUNGU ATACHUKUA HATUA LINI?

Wakati wa Mungu kuchukua hatua umekaribia sana! Yesu alitaja kwamba kizazi fulani hususa kingeshuhudia mkusanyo wa matukio ya pekee ambayo yangekuwa ishara ya siku za mwisho za “mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3-42) Utimizo wa unabii wa Yesu katika siku zetu ni ishara ya wazi kwamba Mungu atachukua hatua wakati wowote kutoka sasa. *

Lakini Mungu atakomeshaje mateso yote? Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha uwezo wa Mungu wa kuondoa mateso ya wanadamu. Hebu fikiria mifano kadhaa.

Majanga ya Asili: Walipokuwa wakisafiri katika Bahari ya Galilaya, Yesu na mitume wake walipigwa na dhoruba kali ambayo ingeweza kuzamisha mashua yao. Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba yeye na Baba yake wana uwezo wa kudhibiti nguvu za asili. (Wakolosai 1:15, 16) Yesu alisema tu: “Nyamaza! Tulia!” Matokeo? “Upepo ukakoma, kukawa shwari kabisa.”—Marko 4:35-39.

Magonjwa: Yesu alifahamika sana kwa uwezo wake wa kuponya vipofu, vilema, watu waliokuwa na kifafa, ukoma, au ulemavu mwingine wowote. “[Aliwaponya] wote waliokuwa wakiteseka.”—Mathayo 4:23, 24; 8:16; 11:2-5.

Upungufu wa Chakula: Yesu alitumia nguvu alizopewa na Baba yake kutokeza chakula kingi kupitia kidogo kilichokuwepo. Wakati wa huduma yake, Biblia inasema kwamba alilisha maelfu ya watu katika visa viwili tofauti.—Mathayo 14:14-21; 15:32-38.

Kifo: Biblia inataja masimulizi matatu ya ufufuo uliofanywa na Yesu. Masimulizi hayo yanathibitisha wazi kwamba Yehova ana uwezo wa kuwarudishia uhai watu waliokufa. Mmoja wa watu ambao Yesu aliwafufua alikuwa amekufa kwa siku nne.—Marko 5:35-42; Luka 7:11-16; Yohana 11:3-44.

^ fu. 5 Ili kupata habari zaidi kuhusu siku za mwisho, soma somo la 32 kwenye kitabu Furahia Maisha Milele! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, na unachoweza kukipakua bila malipo yoyote kwenye tovuti ya www.pr418.com/sw.