Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iga Imani na Utii wa Noa, Danieli, na Ayubu

Iga Imani na Utii wa Noa, Danieli, na Ayubu

“Noa, Danieli, na Ayubu . . . wangejiokoa wao wenyewe tu kwa sababu ya uadilifu wao.”—EZE. 14:14.

NYIMBO: 89, 119

1, 2. (a) Kwa nini mfano wa Noa, Danieli, na Ayubu unaweza kutuimarisha? (b) Ezekieli aliandika maneno ya Ezekieli 14:14 chini ya hali gani?

JE, UNAKABILI hali ngumu kama vile matatizo ya afya, matatizo ya kifedha, au minyanyaso? Je, nyakati nyingine ni vigumu kwako kudumisha shangwe unapomtumikia Yehova? Ikiwa ndivyo, mfano wa Noa, Danieli, na Ayubu unaweza kukuimarisha. Walikuwa wanadamu wasio wakamilifu, nao walikabili hali ngumu kama tunazokabili leo, na baadhi ya hali hizo zilihatarisha maisha yao. Licha ya hayo, walidumisha utimilifu wao, na machoni pa Mungu wakawa vielelezo vya imani na utii.—Soma Ezekieli 14:12-14.

2 Ezekieli aliandika maneno ya andiko letu la msingi akiwa Babilonia mwaka wa 612 K.W.K. * (Eze. 1:1; 8:1) Uharibifu uliokuwa umetabiriwa wa jiji lililoasi la Yerusalemu, uliotukia mwaka wa 607 K.W.K. ulikuwa umekaribia. Ni watu wachache sana walioonyesha sifa kama za Noa, Danieli, na Ayubu, hivyo walitiwa alama ili waokolewe. (Eze. 9:1-5) Watu hao wachache walitia ndani Yeremia, Baruku, Ebed-meleki, na Warekabu.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Vivyo hivyo leo, ni wale tu ambao Yehova anawaona kuwa wasio na lawama—watu walio kama Noa, Danieli, na Ayubu—watakaotiwa alama ili waokoke mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Ufu. 7:9, 14) Hivyo basi, acheni tuchunguze kwa nini Yehova aliwatumia wanaume hao kuwa mifano ya uadilifu. Tunapozungumzia kila mmoja wao, tutakazia fikira (1) hali ngumu ambazo kila mmoja wao alikabili na (2) jinsi tunavyoweza kuiga imani na utii walioonyesha.

NOA—MWANAMUME MWAMINIFU NA MTIIFU KWA KARNE TISA

4, 5. Noa alikabili hali zipi ngumu, na kwa nini uvumilivu wake ni wa pekee sana?

4 Hali ngumu ambazo Noa alikabili. Kufikia siku za Enoko babu ya Noa, watu walikuwa wamebadilika na kuwa waovu sana. Hata walikuwa wakisema “maneno . . . yenye kushtua” kumhusu Yehova. (Yuda 14, 15) Ukatili ulikuwa ukiongezeka. Zaidi ya hilo, katika siku za Noa, “dunia ilikuwa imejaa ukatili.” Malaika waovu walijivika miili ya kibinadamu, wakajichukulia wake, na kuzaa wana wakatili waliokuwa nusu malaika na nusu binadamu. (Mwa. 6:2-4, 11, 12) Lakini Noa alikuwa mtu tofauti kabisa. “Noa [alipata] kibali machoni pa Yehova. . . . Alijithibitisha mwenyewe kuwa mtu asiye na kosa miongoni mwa watu wa siku zake. Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.”—Mwa. 6:8, 9.

5 Maneno hayo yanafunua nini kuhusu mwanamume huyo mwadilifu? Ona kwamba Noa hakutembea pamoja na Mungu katika ulimwengu huo mwovu wa kabla ya gharika kwa miaka 70 au 80 tu—urefu wa maisha ya wanadamu wengi leo. Aliishi katika ulimwengu huo mwovu kwa miaka 600 hivi! (Mwa. 7:11) Pia, tofauti nasi leo, hakukuwa na kutaniko ambalo angeshirikiana nalo na kupata utegemezo wa kiroho, na inaonekana pia kwamba hata ndugu na dada zake wa kimwili hawakumwabudu Yehova. *

6. Noa alionyesha ujasiri mkubwa jinsi gani?

6 Noa hakuridhika tu kuwa mtu mzuri. Alikuwa pia “mhubiri wa uadilifu” mwenye ujasiri aliyetangaza hadharani imani yake kwa Yehova. (2 Pet. 2:5) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia imani hiyo aliuhukumu ulimwengu.” (Ebr. 11:7) Hivyo, tunaweza kufikia mkataa kwamba Noa alidhihakiwa na kupingwa, na huenda hata alikabili vitisho vya kutendewa kwa ukatili. Lakini ‘hakuwaogopa wanadamu.’ (Met. 29:25) Badala yake, alikuwa na ujasiri ambao Yehova huwapa watumishi wake waaminifu.

7. Noa alikabili changamoto gani alipokuwa akijenga safina?

7 Baada ya Noa kutembea na Mungu kwa zaidi ya karne tano, Yehova alimwambia ajenge safina ambayo ingetumiwa kuwaokoa wanadamu na wanyama. (Mwa. 5:32; 6:14) Hapana shaka kwamba Noa aliona mradi huo kuwa mgumu kwelikweli kwani mengi zaidi yalihusika mbali na kazi ya ujenzi! Kwa hakika Noa alijua kwamba kazi hiyo ingefanya adhihakiwe na kupingwa hata zaidi. Lakini licha ya hayo, kwa imani alisonga mbele na kuitimiza. “Hivyo ndivyo alivyofanya.”—Mwa. 6:22.

8. Noa alimtegemea Yehova Mwandalizi wake katika njia zipi?

8 Hali nyingine ngumu ambayo Noa alikabili ni kumwandalia mke na watoto wake mahitaji yao ya kimwili. Kabla ya Gharika, watu walihitaji kufanya kazi kwa bidii sana shambani ili wapate chakula, na hapana shaka kwamba Noa alifanya vivyo hivyo pia. (Mwa. 5:28, 29) Ingawa hivyo, hakuhangaikia kutafuta vitu vya kimwili, bali alimtanguliza Mungu maishani mwake. Hata alipokuwa akijenga safina—kazi ambayo huenda ilichukua miaka 40 au 50 hivi—Noa aliendelea kukazia mambo ya kiroho. Na aliendelea kukazia mambo ya kiroho kwa miaka 350 baada ya Gharika. (Mwa. 9:28) Alikuwa mfano bora sana wa imani na utii!

9, 10. (a) Tunaweza kuigaje imani na utii wa Noa? (b) Mungu anawaonaje wale wote wanaounga mkono viwango vyake?

9 Jinsi tunavyoweza kuiga imani na utii wa Noa. Tunafanya hivyo kwa kutetea uadilifu wa Mungu, kwa kuepuka kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani, na kwa kutanguliza masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:33; Yoh. 15:19) Ukweli ni kwamba njia yetu ya maisha hufanya ulimwengu utuchukie. Kwa hakika, hata sasa katika nchi fulani, tunasemwa vibaya kwa sababu ya msimamo wetu imara kuhusu sheria za Mungu, kama vile sheria zinazohusu ndoa na maadili kuhusu ngono. (Soma Malaki 3:17, 18.) Hata hivyo, kama Noa, tunamwogopa Yehova si wanadamu. Tunajua kwamba ni Yehova pekee anayewapa watu uzima wa milele.—Luka 12:4, 5.

10 Lakini vipi wewe binafsi? Je, utaendelea ‘kutembea pamoja na Mungu,’ hata wengine wanapokudhihaki au kukuchambua au unapokabili mikazo ya kiuchumi inayojaribu imani yako katika Mwandalizi wako? Ukiiga imani na utii wa Noa, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakutunza.—Flp. 4:6, 7.

DANIELI—MWANAMUME MWAMINIFU NA MTIIFU KATIKA JIJI LENYE UOVU

11. Danieli na rafiki zake watatu walikabili changamoto zipi kubwa huko Babiloni? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

11 Hali ngumu ambazo Danieli alikabili. Danieli aliishi akiwa mateka huko Babiloni, jiji lililojaa ibada ya sanamu na mazoea ya kuwasiliana na roho. Zaidi ya hilo, Wababiloni waliwadharau Wayahudi, na waliwadhihaki wao pamoja na Mungu wao, Yehova. (Zab. 137:1, 3) Hapana shaka jambo hilo liliwaumiza sana Wayahudi waaminifu kama vile Danieli! Pia, watu walikuwa wakiwatazama kwa ukaribu Danieli pamoja na rafiki zake watatu Hanania, Mishaeli, na Azaria kwa sababu walikuwa wakizoezwa ili watumikie katika makao ya mfalme. Hata walipangiwa chakula walichopaswa kula. Isitoshe, baada ya muda mfupi suala la chakula na vinywaji lilizua utata kwa sababu Danieli hakutaka “[kujichafua] kwa vyakula bora vya mfalme.”—Dan. 1:5-8, 14-17.

12. (a) Danieli alikuwa na sifa zipi zenye kuvutia? (b) Yehova alikuwa na maoni gani kumhusu Danieli?

12 Changamoto nyingine isiyo ya moja kwa moja ambayo Danieli alikabili huenda ilihusiana na uwezo wake wa pekee ambao ulimfanya apate madaraka makubwa. (Dan. 1:19, 20) Lakini badala ya kuingiwa na kiburi na kushikilia maoni yake, aliendelea kuwa mnyenyekevu na mwenye kiasi, sikuzote akimwelekezea Yehova sifa. (Dan. 2:30) Zaidi ya hilo, Danieli alikuwa angali kijana Yehova alipomtaja kuwa mfano bora wa uadilifu, pamoja na Noa na Ayubu. Je, Mungu alikuwa amekosea alipoonyesha uhakika huo kumhusu Danieli? La, hasha! Danieli aliendelea kuwa mwaminifu na mtiifu mpaka mwisho wa maisha yake. Kwa kweli, inaonekana alikuwa akikaribia miaka 100 malaika wa Yehova alipomwambia hivi kwa upendo: “Ee Danieli, wewe mtu mwenye thamani sana.”—Dan. 10:11.

13. Huenda Danieli alikuwa baraka kwa Wayahudi wenzake jinsi gani?

13 Kwa kuwa Danieli alikuwa na kibali cha Mungu, aliwekwa kuwa ofisa mkuu katika utawala wa Babiloni na pia katika Milki ya Umedi na Uajemi. (Dan. 1:21; 6:1, 2) Huenda Yehova aliongoza mambo kwa njia hiyo ili Danieli atumiwe kuwabariki watu wake, kama ilivyokuwa kwa Yosefu nchini Misri na Esta na Mordekai katika Milki ya Uajemi. * (Dan. 2:48) Wazia jinsi Wayahudi waliokuwa wamechukuliwa mateka, kutia ndani Ezekieli, walivyofarijika kuona mkono wa Yehova ukiongoza mambo kwa njia hiyo!

Yehova anawaona wale wanaodumisha utimilifu kuwa wenye thamani (Tazama fungu la 14 na 15)

14, 15. (a) Hali zetu zinafananaje na zile za Danieli? (b) Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na wazazi wa Danieli?

14 Jinsi tunavyoweza kuiga imani na utii wa Danieli. Leo, sisi ni kama wageni katika ulimwengu ambao umepotoshwa kiadili na kiroho na Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo, “makao ya roho waovu.” (Ufu. 18:2) Hivyo, sisi pia ni tofauti kabisa na nyakati nyingine tunadhihakiwa. (Marko 13:13) Kwa hiyo, kama Danieli, acheni tumkaribie Yehova Mungu wetu. Tunapomtegemea Yehova kwa unyenyekevu na kwa utiifu, sisi pia tutakuwa wenye thamani machoni pake.—Hag. 2:7.

15 Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa wazazi wa Danieli? Ingawa uovu ulikuwa umeenea nchini Yuda wakati Danieli alipokuwa mtoto, mvulana huyo alimpenda Mungu. Bila shaka jambo hilo halikujitokeza lenyewe tu. Lilionyesha kwamba Danieli alizoezwa vizuri na wazazi wake. (Met. 22:6) Hata jina Danieli linalomaanisha “Mwamuzi Wangu Ni Mungu,” linaonyesha kwamba wazazi wake walikuwa watu waliomwogopa Mungu. (Dan. 1:6, maelezo ya chini) Hivyo wazazi msiache kamwe kuwazoeza watoto wenu, bali wafundisheni kwa subira. (Efe. 6:4) Pia, salini pamoja nao na kwa ajili yao. Mnapojitahidi kukazia kweli ya Biblia mioyoni mwao, Yehova atawabariki sana.—Zab. 37:5.

AYUBU—MWANAMUME MWAMINIFU NA MTIIFU ALIPOKUWA TAJIRI NA MASKINI

16, 17. Ayubu alipitia hali gani zilizotofautiana sana?

16 Hali ngumu ambazo Ayubu alikabili. Ayubu alipitia hali mbili zilizotofautiana kabisa. Kabla ya kupatwa na majaribu, alikuwa “mkuu kuliko watu wote wa Mashariki.” (Ayu. 1:3) Alikuwa mtu tajiri aliyejulikana sana na kuheshimiwa na watu wengi. (Ayu. 29:7-16) Lakini licha ya mambo hayo yote, Ayubu hakujiona kuwa bora au kuhisi kwamba hamhitaji Mungu. Hata Yehova alimwita, “mtumishi wangu,” na akaongeza hivi: “Yeye ni mtu mnyoofu na mtimilifu, anayemwogopa Mungu na kuepuka uovu.”—Ayu. 1:8.

17 Hata hivyo, katika kipindi kifupi cha wakati maisha ya Ayubu yalibadilika kabisa! Alijikuta katika umaskini mkubwa na hali ya kukata tamaa. Tunajua aliyesababisha hali hiyo ni mchongezi Shetani ambaye alimshtaki Ayubu kwa uwongo kwamba anamwabudu Mungu kwa sababu ya ubinafsi. (Soma Ayubu 1:9, 10.) Yehova hakupuuza mashtaka hayo maovu. Badala yake, alimpa Ayubu fursa ya kuonyesha utimilifu wake—fursa ya kuonyesha kwamba ibada yake ilichochewa na moyo safi usio na ubinafsi wowote.

18. (a) Ni nini kinachokuvutia kuhusu utimilifu wa Ayubu? (b) Tunajifunza nini kumhusu Yehova kupitia jinsi alivyoshughulika na Ayubu?

18 Shetani alimpiga Ayubu kwa mfululizo wa mashambulizi ya kikatili yaliyomfanya Ayubu afikiri kwamba Mungu ndiye aliyeyasababisha. (Ayu. 1:13-21) Kisha wafariji watatu wa uwongo wakaja na kumshambulia Ayubu kwa maneno makali sana, wakidokeza kwamba Mungu alikuwa akimlipa alichostahili! (Ayu. 2:11; 22:1, 5-10) Licha ya hayo, Ayubu aliendelea kuwa mtimilifu. Ni kweli kwamba nyakati nyingine alizungumza bila kufikiri, lakini Yehova alielewa maumivu yake. (Ayu. 6:1-3) Mungu alimwona mwanamume aliyekuwa ameshuka moyo lakini aliyeendelea kuwa mtimilifu Kwake, jambo lililofanya Shetani amshambulie Ayubu na kumpiga kwa maneno makali na mashtaka ya uwongo. Majaribu hayo yalipokwisha, Yehova alimpa Ayubu maradufu ya vitu alivyokuwa navyo awali na akamwongezea miaka 140 ya kuishi. (Yak. 5:11) Ayubu aliendelea kujitoa kikamili kwa Yehova hata katika kipindi hicho. Tunajuaje? Ayubu alikuwa amekufa kwa karne nyingi Ezekieli alipoandika maneno ya andiko letu la msingi.

19, 20. (a) Tunaweza kuigaje imani na utii wa Ayubu? (b) Tunaposhughulika na wengine, tunaweza kuonyeshaje huruma kama Mungu?

19 Jinsi tunavyoweza kuiga imani na utii wa Ayubu. Hata iwe tunakabili hali gani, acheni sikuzote tuendelee kumtanguliza Yehova maishani mwetu, tumtegemee kabisa na kumtii kwa moyo kamili. Kwa kweli, tunapojilinganisha na Ayubu, tuna sababu nyingi zaidi za kufanya hivyo! Fikiria hili: Sisi tunajua mambo mengi kuhusu Shetani na mbinu zake. (2 Kor. 2:11) Tunashukuru kwamba kitabu cha Ayubu kinatusaidia kujua kwa kadiri fulani kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke. Unabii wa Danieli unatusaidia kuelewa kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali itakayotawala ulimwengu wote chini ya uongozi wa Kristo Yesu. (Dan. 7:13, 14) Na tunajua kwamba hivi karibuni Ufalme huo utakomesha kabisa mateso yote.

20 Kisa cha Ayubu kinakazia pia kwamba tunahitaji kuwaonyesha huruma Wakristo wenzetu ambao huenda wanavumilia hali ngumu. Kama Ayubu huenda nyakati nyingine baadhi yao wakazungumza bila kufikiri. (Mhu. 7:7) Lakini badala ya kuwahukumu, acheni tuwaelewe na kuwaonyesha huruma. Tunapofanya hivyo, tunamwiga Yehova, Baba yetu mwenye upendo na rehema.—Zab. 103:8.

YEHOVA ‘ATAKUTIA NGUVU’

21. Maneno ya 1 Petro 5:10 yanatukumbusha nini kuhusu maisha ya Noa, Danieli, na Ayubu?

21 Ingawa Noa, Danieli, na Ayubu waliishi vipindi tofauti na chini ya hali zilizotofautiana sana, walivumilia hali ngumu walizokabili. Masimulizi ya maisha yao yanatukumbusha maneno ya mtume Petro aliyeandika hivi: “Baada ya kuteseka kwa muda mfupi, Mungu wa fadhili zote zisizostahiliwa . . . yeye mwenyewe atamaliza mazoezi yenu. Atawafanya muwe imara, atawatia nguvu, atawapa msingi imara.”—1 Pet. 5:10.

22. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

22 Kupitia maneno ya Petro yaliyoongozwa na roho, Yehova anatuhakikishia kwamba atawafanya watumishi wake wawe imara na wenye nguvu. Maneno hayo yanawahusu pia watu wa Mungu leo. Sisi sote tunatamani kuimarishwa na Yehova na kuendelea kumwabudu bila kuyumbayumba. Hivyo, tungependa kuiga imani na utii wa Noa, Danieli, na Ayubu! Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, wanaume hao walidumisha utimilifu kwa sababu walimjua Yehova vizuri. Kwa kweli, ‘walielewa mambo yote’ ambayo Mungu alitaka wafanye. (Met. 28:5) Na inaweza kuwa hivyo kwetu pia.

^ fu. 2 Ezekieli alipelekwa uhamishoni mwaka wa 617 K.W.K. Ezekieli 8:1–19:14 iliandikwa mwaka wa 612 K.W.K. ambao ulikuwa “mwaka wa sita” wa uhamisho huo.

^ fu. 5 Baba ya Noa, aliyeitwa Lameki, alimwogopa Mungu, na alikufa miaka mitano hivi kabla ya Gharika. Ikiwa mama na ndugu za Noa walikuwa hai Gharika ilipoanza, basi hawakuokoka.

^ fu. 13 Huenda pia Yehova aliongoza mambo ilipohusu rafiki watatu wa Danieli, ambao pia walipewa vyeo vikubwa.—Dan. 2:49.