Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Inamaanisha Nini Kuwa Mtu wa Kiroho?

Inamaanisha Nini Kuwa Mtu wa Kiroho?

“Mungu . . . na awawezeshe ninyi miongoni mwenu wenyewe kuwa na mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao.”—ROM. 15:5.

NYIMBO: 17, 13

1, 2. (a) Watu wengi wana maoni gani kuhusu kuwa mtu wa kiroho? (b) Tutachunguza maswali gani muhimu?

“KUWA mtu wa kiroho kumenisaidia kuwa mwenye furaha zaidi na kumenisaidia kukabiliana na changamoto za kila siku kwa mafanikio,” anasema dada mmoja kutoka Kanada. Ndugu fulani nchini Brazili anaeleza hivi: “Ndoa yetu ya miaka 23 imekuwa yenye furaha sana—na hilo limewezekana tu kwa sababu ya jitihada zetu za kuwa watu wa kiroho.” Na ndugu mwingine nchini Ufilipino anasema hivi: “Kuwa mtu wa kiroho kumenipa amani ya akili, na kumenisaidia nijue jinsi ya kushughulika vizuri zaidi na ndugu wanaotoka malezi mbalimbali.”

2 Maelezo kama hayo yanaonyesha matokeo mazuri ya kuwa mtu wa kiroho. Hivyo, huenda tukachochewa kujiuliza hivi: ‘Ninaweza kufanya nini ili niboreshe hali yangu ya kiroho na kufurahia zaidi manufaa yaliyotajwa hapo juu?’ Hata hivyo, kabla ya kujibu swali hilo tunahitaji kuelewa vizuri kile ambacho Biblia inasema kuhusu mtu wa kiroho au mtu mwenye mtazamo wa kiroho. Katika makala hii, tutajibu maswali matatu muhimu. (1) Inamaanisha nini kuwa mtu wa kiroho? (2) Ni mifano gani itakayotusaidia kufanya maendeleo ya kiroho? (3) Jitihada zetu za kuwa na “akili ya Kristo” zitatusaidiaje kuwa watu wa kiroho?

MTU WA KIROHO NI NANI?

3. Ufafanuzi wa Biblia kuhusu mtu wa kimwili unatofautianaje na ule wa mtu wa kiroho?

3 Mtume Paulo anatusaidia kuelewa mtu wa kiroho ni nani kwa kuonyesha tofauti kati ya “mtu wa kiroho” na “mtu wa kimwili.” (Soma 1 Wakorintho 2:14-16.) Wanatofautianaje? “Mtu wa kimwili” anaelezwa kuwa mtu asiyekubali “mambo ya roho ya Mungu, kwa maana hayo ni upumbavu kwake; naye hawezi kuyajua.” Kwa upande mwingine, “mtu wa kiroho” ni mtu ambaye “huchunguza mambo yote” na ana “akili ya Kristo.” Paulo anatutia moyo tuwe watu wa kiroho. Watu wa kimwili na wa kiroho wanatofautiana katika njia gani nyingine?

4, 5. Taja baadhi ya tabia za mtu wa kimwili.

4 Kwanza, fikiria mtazamo wa mtu wa kimwili. Ulimwengu umejaa watu walio na mtazamo wa kukazia sana mambo ya kimwili. Paulo anafafanua mtazamo huo kuwa “roho ambayo sasa inafanya kazi katika wana wa kutotii.” (Efe. 2:2) Roho hiyo huwasukuma watu wengi wasitawishe mtazamo ambao umeenea sana—mtazamo wa kufuata umati. Fikira na mawazo yao yote ni katika mambo ya kimwili. Hivyo, idadi kubwa ya watu hufanya mambo wanayoona kuwa sawa machoni pao wenyewe na hawafanyi jitihada zozote za kuishi kupatana na viwango vya Mungu. Mtu wa kimwili, yaani, mtu anayekazia mambo ya kimwili, mara nyingi huhangaikia sana umashuhuri na kufuatia vitu vya kimwili na kudai au kutetea mambo anayohisi ni haki yake.

5 Ni jambo gani lingine linaloweza kumtambulisha mtu wa kimwili? Watu wanaojihusisha na “matendo [yoyote] ya mwili” ni watu wa kimwili. (Gal. 5:19-21) Barua ya kwanza ya Paulo kwa kutaniko la Korintho inataja tabia nyingine za watu walio na mtazamo wa kimwili. Tabia hizo zinatia ndani kuchochea migawanyiko, mwelekeo wa kupendelea upande mmoja, kuchochea migogoro, kuwapeleka wengine mahakamani, kudharau ukichwa, na kula na kunywa kupita kiasi. Mtu wa kimwili anapokabili kishawishi fulani, yeye hushawishika kwa urahisi na kushindwa na kishawishi hicho. (Met. 7:21, 22) Yuda alizungumza kuhusu wale ambao wangedhoofika kiroho kufikia hatua ya kuwa watu “wasio na hali ya kiroho.”—Yuda 18, 19.

6. Ni nini kinachomtambulisha mtu wa kiroho?

6 Hivyo basi, inamaanisha nini kuwa “mtu wa kiroho”? Tofauti kabisa na mtu wa kimwili, mtu wa kiroho ana mwelekeo wa kuhangaikia uhusiano wake pamoja na Mungu. Watu walio na mtazamo wa kiroho hujitahidi kuwa “waigaji wa Mungu.” (Efe. 5:1) Hilo linamaanisha kwamba wanajitahidi kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu mambo, na kuyaona kama Yehova anavyoyaona. Wanamwona Mungu akiwa halisi sana. Tofauti kabisa na watu walio na mtazamo wa kimwili, watu wa kiroho hujitahidi kuhakikisha kwamba kila jambo wanalofanya maishani mwao linapatana na viwango vya Yehova. (Zab. 119:33; 143:10) Badala ya kukazia matendo ya mwili, mtu mwenye mtazamo wa kiroho hujitahidi kuonyesha “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Ili kufafanua zaidi maana ya kuwa na “mtazamo wa kiroho,” fikiria mfano huu: Mtu ambaye ni stadi katika mambo ya kibiashara husemwa kuwa ana mtazamo au akili ya biashara. Vivyo hivyo, mtu ambaye huchukua kwa uzito mambo ya kiroho au ya kidini husemwa kuwa ana mtazamo wa kiroho.

7. Biblia inasema nini kuhusu watu walio na mtazamo wa kiroho?

7 Biblia inawasifu watu walio na mtazamo wa kiroho. Andiko la Mathayo 5:3 linasema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa Ufalme wa mbinguni ni wao.” Andiko la Waroma 8:6 linaonyesha manufaa ya kuwa na mtazamo wa kiroho linaposema hivi: “Kukaza akili kwenye mwili humaanisha kifo, lakini kukaza akili kwenye roho humaanisha uzima na amani.” Tunapokazia mambo ya kiroho, tunakuwa na amani pamoja na Mungu, tunapata amani ya akili, na tumaini la uzima wa milele.

8. Kwa nini jitihada inahitajika ili kusitawisha na kudumisha hali nzuri ya kiroho?

8 Hata hivyo, tunaishi katika mazingira hatari. Kwa kuwa tumezungukwa na watu wenye mtazamo wa kimwili tunahitaji kufanya juu chini ili tusitawishe hali nzuri ya kiroho na tuendelee kuilinda. Mtu anapopoteza hali ya kiroho, anakuwa na pengo ambalo hujazwa mara moja na “hewa” chafu ya ulimwengu huu. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusipatwe na hali hiyo? Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kukua kiroho?

MIFANO YA KUIGWA

9. (a) Ni nini kinachoweza kutusaidia kukua kiroho? (b) Tutachunguza mifano gani ya watu wa kiroho?

9 Mtoto anaweza kukomaa kwa kuwatazama wazazi wake na kuiga mfano wao mzuri. Vivyo hivyo, tunaweza kuendelea kukua kiroho kwa kuwatazama na kuwaiga watu walio na hali nzuri ya kiroho. Kinyume cha hilo, watu wenye mtazamo wa kimwili ni mifano inayotuonya. (1 Kor. 3:1-4) Biblia ina mifano ya kuigwa na mifano ya kuonya. Lakini kwa kuwa lengo letu ni kuendelea kukua kiroho, acheni tuchunguze watu kadhaa ambao tunaweza kuwaiga. Tutachunguza mfano wa Yakobo, Maria, na Yesu.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yakobo? (Tazama fungu la 10)

10. Yakobo alionyeshaje kwamba alikuwa mtu wa kiroho?

10 Kwanza, fikiria mfano wa Yakobo. Kama ilivyo kwa wengi wetu leo, maisha hayakuwa rahisi kwa Yakobo. Alilazimika kumvumilia Esau ndugu yake, aliyekuwa na mtazamo wa kimwili na aliyekusudia kumuua. Zaidi ya hilo, alilazimika kushughulika na baba mkwe wake mdanganyifu ambaye alijaribu mara kwa mara kumdhulumu. Hata hivyo, ingawa alizungukwa na watu wa “kimwili,” Yakobo alikuwa mtu wa kiroho. Alikuwa na imani katika ahadi ambayo Mungu alikuwa amempa Abrahamu na akajitoa kabisa kutunza familia ambayo ingetimiza jukumu la pekee kuhusiana na kusudi la Yehova. (Mwa. 28:10-15) Maneno na matendo ya Yakobo yanafunua kwamba alitilia maanani viwango na mapenzi ya Mungu. Kwa mfano, alipohisi kwamba Esau alitaka kumuua, Yakobo alimwambia Mungu hivi: “Nakuomba uniokoe . . . Uliniambia: ‘Hakika nitakutendea mema, nami nitaufanya uzao wako uwe mwingi kama chembe za mchanga wa bahari.’” (Mwa. 32:6-12) Ni wazi alikuwa na imani kwamba Yehova angetimiza ahadi ambazo alimpa yeye na mababu zake, na alitaka kutenda kulingana na mapenzi na kusudi la Mungu.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Maria? (Tazama fungu la 11)

11. Ni nini kinachoonyesha kwamba Maria alikuwa mtu wa kiroho?

11 Sasa fikiria mfano mwingine, ule wa Maria. Kwa nini Yehova alimchagua Maria awe mama ya Yesu? Bila shaka ni kwa sababu alikuwa mtu wa kiroho. Tunajuaje hilo? Maneno yake yenye kupendeza na ya kumsifu Yehova aliyosema wakati alipowatembelea Zekaria na Elisabeti watu wake wa ukoo, yanaonyesha wazi kwamba alikuwa mtu wa kiroho. (Soma Luka 1:46-55.) Maneno ya Maria yanaonyesha kwamba alilipenda sana Neno la Mungu na alikuwa na ufahamu wenye kina wa Maandiko ya Kiebrania. (Mwa. 30:13; 1 Sam. 2:1-10; Mal. 3:12) Ona pia kwamba Maria na Yosefu, ingawa walikuwa wameoana karibuni, waliepuka kufanya ngono hadi Yesu alipozaliwa. Hilo linaonyesha nini? Linaonyesha kwamba wote wawili walihangaikia zaidi mapenzi ya Yehova kuliko kutosheleza tamaa zao za kibinafsi. (Mt. 1:25) Kadiri wakati ulivyopita Maria alichunguza kwa uangalifu mambo yaliyokuwa yakitendeka maishani mwa Yesu, naye alisikiliza kwa makini maneno ya hekima ambayo Yesu alisema. Isitoshe, Maria ‘aliyahifadhi . . . mambo hayo yote moyoni mwake.’ (Luka 2:51) Ni wazi kwamba alipendezwa na kusudi la Mungu kumhusu Masihi. Je, si kweli kwamba mfano wa Maria unatusaidia kufikiria jinsi tunavyoweza kutanguliza mapenzi ya Mungu maishani mwetu?

12. (a) Yesu alifanana na Baba yake katika njia gani? (b) Tunaweza kuigaje mfano wa Yesu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

12 Hata hivyo, kati ya watu wote ambao wamewahi kuishi, ni mwanadamu gani aliyeweka mfano bora zaidi wa kuwa mtu wa kiroho? Bila shaka ni Yesu. Katika huduma yake na maisha yake yote, alionyesha kwamba alitaka kumwiga Yehova, Baba yake. Alifikiri, kuhisi, na kutenda kama Yehova na aliishi kupatana na mapenzi na viwango vya Mungu. (Yoh. 8:29; 14:9; 15:10) Kwa mfano, ona jinsi nabii Isaya anavyofafanua hisia za Yehova za huruma, kisha linganisha ufafanuzi huo na yale ambayo Marko mwandikaji wa Injili anaeleza kuhusu hisia za Yesu. (Soma Isaya 63:9; Marko 6:34.) Je, tunamwiga Yesu kwa kuwa tayari sikuzote kuwahangaikia kwa huruma watu wanaohitaji msaada? Isitoshe, Yesu alijitoa kabisa katika kazi ya kuhubiri na kufundisha habari njema. (Luka 4:43) Hisia hizo za huruma na matendo hayo yote ni ishara ya mtu wa kiroho.

13, 14. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya kisasa ya watu wa kiroho? (b) Toa mfano.

13 Mbali na mifano ya Kimaandiko, kuna mifano mingi ya kisasa ya watu wa kiroho ambao wamefanya maendeleo makubwa katika kuiga utu wa Kristo. Huenda umejionea bidii yao katika huduma, mfano wao mzuri wa kuwakaribisha wengine, huruma yao, au sifa zao nyingine nzuri. Kama sisi, wao pia wanapambana na udhaifu wao na hali yao ya kutokamilika huku wakijitahidi kusitawisha sifa hizo za Kikristo. Rachel, dada kutoka Brazili, anasema hivi: “Nilipenda kuiga mitindo ya mavazi ya kilimwengu. Hivyo, sikuvalia kwa kiasi. Lakini kujifunza kweli kulinichochea nifanye jitihada zilizohitajika ili niwe mtu wa kiroho. Haikuwa rahisi kwangu kufanya mabadiliko lakini furaha yangu iliongezeka na nikapata kusudi maishani.”

14 Reylene, kutoka nchini Ufilipino, alikuwa na changamoto tofauti. Alikazia fikira kupata elimu ya juu na kazi nzuri ili awe na maisha bora. Anasema hivi: “Nilianza kupuuza malengo yangu ya kiroho. Lakini nilianza kuhisi kwamba ninakosa kitu fulani maishani, kitu muhimu zaidi kuliko kazi yangu. Hivyo, nilielekeza fikira zangu katika utumishi wangu kwa Yehova.” Tangu wakati huo, Reylene amekuwa mfano mzuri wa mtu ambaye anaamini ahadi ya Yehova iliyo katika Mathayo 6:33, 34. Anasema, “Ninajua kwa hakika kwamba Yehova atanitunza!” Huenda unawajua ndugu na dada katika kutaniko lenu walio kama Reylene. Je, hatuchochewi kuwaiga ndugu na dada hao waaminifu wanapoendelea kumfuata Kristo?—1 Kor. 11:1; 2 The. 3:7.

UWE NA “AKILI YA KRISTO”

15, 16. (a) Tunahitaji kufanya nini ili tuwe kama Kristo? (b) Tunaweza kufanya nini ili turuhusu akili yetu iwe kama “akili ya Kristo”?

15 Sisi binafsi tunawezaje kumwiga Kristo? Kwenye andiko la 1 Wakorintho 2:16, Biblia inazungumza kuhusu kuwa na “akili ya Kristo.” Na andiko la Waroma 15:5 linazungumza kuhusu kuwa na “mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao.” Kwa hiyo, ili tuwe kama Kristo, tunahitaji kujua njia yake ya kufikiri na kufahamu utu wake kikamili. Kisha tunahitaji kufuata hatua zake. Yesu alikazia akilini mwake uhusiano wake na Mungu. Hivyo, tunapomwiga Yesu tunakuwa kama Yehova. Sababu hizo zinatusaidia kuona wazi jinsi ilivyo muhimu kwetu kujifunza kufikiri kama Yesu.

16 Tunaweza kufanya nini ili tufikiri kama Yesu? Wanafunzi wa Yesu walijionea miujiza yake, walisikiliza hotuba zake, waliona jinsi alivyoshughulika na watu wa namna zote, na jinsi alivyotumia kanuni za Mungu maishani mwake. Walisema hivi: “[Sisi] ni mashahidi wa mambo yote aliyofanya.” (Mdo. 10:39) Hata hivyo, leo Yesu hawezi kuonekana kwa macho. Lakini kwa upendo Yehova ametupatia masimulizi ya Injili yanayoweza kutusaidia kupiga picha akilini na kuona jinsi utu wa Yesu ulivyokuwa. Tunaposoma na kutafakari vitabu vya Biblia kama vile Mathayo, Marko, Luka, na Yohana, tunaruhusu akili yetu iwe kama akili ya Kristo. Kufanya hivyo kutatusaidia “[kufuata] hatua zake kwa ukaribu “na “[kujiimarisha] kwa mwelekeo uleule wa akili” ambao Kristo alikuwa nao.—1 Pet. 2:21; 4:1.

17. Kufikiri kama Kristo hutunufaishaje?

17 Kujifunza kufikiri kama Kristo kutatunufaishaje? Kama tu ambavyo chakula chenye lishe huimarisha mwili wetu, kulisha akili yetu mawazo ya Kristo hutuimarisha kiroho. Hatua kwa hatua, tunajifunza jinsi ambavyo Kristo angetenda katika hali yoyote ile. Kisha kufanya hivyo hutusaidia kufanya maamuzi yatakayotuacha tukiwa na dhamiri safi na kibali cha Mungu. Je, hukubali kwamba manufaa tunayopata yanatupatia sababu nzuri za “[kumvaa] Bwana Yesu Kristo”?—Rom. 13:14.

18. Mazungumzo haya yamekufundisha nini kuhusu kuwa mtu wa kiroho?

18 Tumechunguza kile kinachohusika ili kuwa mtu wa kiroho. Tumeona pia mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mifano mizuri ya watu wa kiroho. Mwishowe tumejifunza jinsi kuwa na “akili ya Kristo” kunavyotusaidia kuendelea kukua kiroho. Hata hivyo, kuna mambo mengine yanayohusu hali yetu ya kiroho tunayopaswa kuchunguza. Kwa mfano, ni mambo gani yatakayotusaidia kuchanganua uthabiti wa hali yetu ya kiroho? Ni mambo gani mengine tunayoweza kufanya ili kusitawisha hali nzuri ya kiroho? Na hali yetu ya kiroho ina matokeo gani katika maisha yetu ya kila siku? Makala inayofuata itatusaidia kujibu maswali hayo.