Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kuwa Mutu wa Kiroho, Maana Yake Nini?

Kuwa Mutu wa Kiroho, Maana Yake Nini?

‘Sasa Mungu . . . awawezeshe ninyi kati yenu wenyewe kuwa na mutazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao.’ ​—ROM. 15:5.

NYIMBO: 17, 13

1, 2. (a) Ndugu na dada wengi wako na mawazo gani juu ya kuwa mutu wa kiroho? (b) Tutazungumuzia maulizo gani ya maana?

DADA mumoja katika Kanada anasema hivi: “Kuwa mutu wa kiroho kumeniletea furaha zaidi, na kumenisaidia kupambana muzuri na majaribu ya kila siku.” Ndugu mumoja katika Brazili anasema hivi: “Miaka 23 yenye tumefanya katika ndoa imekuwa yenye furaha sana kwa sababu tumejikaza kuwa watu wa kiroho.” Na ndugu mumoja katika Ufilipino anasema hivi: “Kuwa mutu wa kiroho kumenisaidia kuwa na amani ya akili na kumenisaidia kutendea muzuri zaidi ndugu wa desturi mbalimbali.”

2 Maneno kama hayo yanaonyesha kama kuwa mutu wa kiroho kunaleta faida. Kwa hiyo, tunaweza kujiuliza hivi, ‘Namna gani ninaweza kukomaa kiroho na kupata kabisa faida kama hizo?’ Lakini, mbele tujibie ulizo hilo, tunapaswa kuelewa muzuri mambo yenye Biblia inasema juu ya mutu wa kiroho ao mwenye kukaza akili yake juu ya mambo ya kiroho. Katika habari hii tutajibia maulizo tatu ya maana. (1) Kuwa mutu wa kiroho, maana yake nini? (2) Ni mifano gani yenye itatusaidia tukomae kiroho? (3) Namna gani kujikaza kuwa na “akili ya Kristo” kunatusaidia tukuwe watu wa kiroho?

MUTU WA KIROHO NI MUTU WA NAMNA GANI?

3. Biblia inatoa tofauti gani kati ya mutu wa kimwili na mutu wa kiroho?

3 Mutume Paulo anatusaidia kuelewa mutu wa kiroho ni mutu wa namna gani kwa kuonyesha tofauti kati ya ‘mutu wa kiroho’ na ‘mutu wa kimwili.’ (Soma 1 Wakorintho 2:14-16.) Wanatofautiana namna gani? Paulo anaonyesha kama ‘mutu wa kimwili’ hapokee “mambo ya roho ya Mungu, kwa maana hayo ni upumbavu kwake; naye hawezi kuyajua.” Lakini, ‘mutu wa kiroho’ ni mutu mwenye ‘kuchunguza mambo yote’ na mwenye iko na “akili ya Kristo.” Paulo anatutia moyo tukuwe watu wa kiroho. Watu wa kiroho na watu wa kimwili, wako tofauti katika njia gani zingine?

4, 5. Ni tabia gani zenye kutambulisha mutu wa kimwili?

4 Fikiria kwanza mawazo ya mutu wa kimwili. Watu wa ulimwengu huu wanakaza akili zao juu ya tamaa za mwili. Paulo anaeleza jambo hilo kuwa ‘roho ambayo sasa inatenda katika wana wa kutotii.’ (Efe. 2:2) Roho hiyo inachochea watu wengi waige mambo yenye watu wengi zaidi wanafanya. Wanakaza akili zao juu ya mwili. Kwa hiyo, wengi kati yao wanafanya mambo yenye wao wenyewe wanaona kuwa sawa na hawajikaze hata kidogo kuishi kulingana na kanuni za Mungu. Mutu wa kimwili, ao mwenye kukaza akili yake juu ya mwili, mara nyingi anahangaikia sana kusifiwa na kufuatia vitu vya kimwili ao kutetea mambo yenye anaona kuwa ni haki yake.

5 Ni mambo gani mengine yenye yanaweza kutambulisha mutu wa kimwili? Watu wenye kufanya “matendo ya mwili” ya aina yoyote, wao pia ni watu wa kimwili. (Gal. 5:19-21) Barua ya kwanza yenye Paulo aliandikia kutaniko la Korintho inataja tabia zingine zenye kutambulisha watu wa kimwili. Tabia kama vile: kuwa watu wenye kuleta migawanyiko, wenye ubaguzi, wenye hawapendi makubaliano, wenye kupelekana kwenye tribinali, wenye hawaheshimu wale wenye kuongoza, wenye wanapenda sana kula na kunywa. Wakati mutu wa kimwili anapatwa na jaribu, anakuwa zaifu na anaangukia katika jaribu hilo. (Met. 7:21, 22) Mwanafunzi Yuda alizungumuzia juu ya wale wenye wangekuwa zaifu sana mupaka wangefikia kukosa “hali ya kiroho.”​—Yuda 18, 19.

6. Ni mambo gani yenye kutambulisha mutu wa kiroho?

6 Sasa, kuwa ‘mutu wa kiroho,’ maana yake nini? Tofauti na mutu wa kimwili, mutu wa kiroho anahangaikia sana urafiki wake pamoja na Yehova. Watu wa kiroho wanajikaza kuwa “waigaji wa Mungu.” (Efe. 5:1) Hilo linamaanisha kama wanajikaza kuwa na mawazo ya Yehova juu ya mambo mbalimbali na kuona mambo namna anayaona. Wanaona kuwa Mungu ni mutu wa kweli kabisa. Tofauti na watu wa kimwili, watu wa kiroho wanajikaza kupatanisha njia zao zote na kanuni za Yehova. (Zab. 119:33; 143:10) Kuliko kukaza akili yake juu ya matendo ya mwili, mutu wa kiroho anajikaza kuonyesha sifa za ‘tunda la roho.’ (Gal. 5:22, 23) Ili kueleza zaidi maana ya ‘mutu wa kiroho,’ fikiria ulinganifu huu: Mutu mwenye kujua muzuri kufanya biashara anaweza kuitwa mufanyabiashara, vilevile mutu mwenye kukaza akili yake juu ya mambo ya kiroho anaweza kuitwa mutu wa kiroho.

7. Biblia inasema nini juu ya watu wa kiroho?

7 Biblia inasema kama watu wa kiroho wako na furaha. Andiko la Mathayo 5:3 linasema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” Pia andiko la Waroma 8:6 linaonyesha faida ya kuwa mutu wa kiroho, linasema hivi: ‘Kukaza akili juu ya mwili kunamaanisha kifo, bali kukaza akili juu ya roho kunamaanisha uzima na amani.’ Wakati tunakaza akili yetu juu ya mambo ya kiroho, tunakuwa na amani ya akili na amani pamoja na Mungu sasa na tumaini la kupata uzima wa milele wakati wenye kuja.

8. Sababu gani tunapaswa kujikaza kukomaa kiroho na kulinda hali hiyo?

8 Lakini, tunaishi katika ulimwengu muovu. Kwa sababu tunazungukwa na watu wenye kukazia tamaa za mwili, tunapaswa kujikaza sana ili kuwa watu wa kiroho na kulinda hali hiyo. Ikiwa hatujaze akili zetu mawazo ya Yehova, ulimwengu utajaza akili na mawazo yetu tamaa za kimwili. Ni nini inaweza kutusaidia tuepuke jambo hilo? Namna gani tunaweza kukomaa kiroho?

MIFANO YA KUTUFUNDISHA

9. (a) Ni nini inaweza kutusaidia kukomaa kiroho? (b) Tutazungumuzia mifano gani ya watu wa kiroho?

9 Mutoto anaweza kujifunza mambo mengi kwa kuangalia na kuiga mufano wa wazazi wake. Vilevile, tunaweza kukomaa kiroho kwa kuangalia na kuiga mifano wa watu wenye kuwa nguvu kiroho. Lakini, mifano ya watu wenye kukaza akili juu ya mwili, inapaswa kuwa onyo kwetu. (1 Kor. 3:1-4) Biblia inazungumuzia mifano ya watu wa aina hizo mbili. Lakini, kwa sababu muradi wetu ni kuwa watu wenye kukomaa kiroho, tuzungumuzie basi mifano fulani ya watu wazuri wenye tunaweza kuiga. Tutazungumuzia mufano wa Yakobo, Maria, na Yesu.

Mufano wa Yakobo unaweza kutufundisha nini? (Picha hizi zinapatana na fungu la 10)

10. Namna gani Yakobo alionyesha kama alikuwa mutu wa kiroho?

10 Tufikirie kwanza mufano wa Yakobo. Kama wengi wetu leo, Yakobo alikuwa na maisha magumu. Alipaswa kuvumilia ndugu yake Esau, mwenye alipenda vitu vya kimwili na mwenye alitaka kumuua. Zaidi ya hilo, alipaswa kuvumilia baba-mukwe wake mudanganyifu mwenye alimutumikisha na kujaribu mara kwa mara kupata faida. Lakini, hata kama alizungukwa na watu wa “kimwili,” Yakobo alikuwa mutu wa kiroho. Alikuwa na imani katika ahadi yenye Mungu alitolea Abrahamu na akajitoa sana ili kuhangaikia familia yake yenye ingekuwa na daraka la pekee katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. (Mwa. 28:10-15) Maneno na matendo ya Yakobo yanaonyesha kama alikuwa anajua kanuni za Mungu na kusudi lake. Kwa mufano, wakati aliogopa kwa sababu ya Esau, Yakobo aliambia Mungu hivi: “Nakuomba, unikomboe . . . Umesema, ‘Bila shaka nitakutendea vema nami nitaufanya uzao wako ukuwe kama chembe za muchanga wa baharini.’” (Mwa. 32:6-12) Kwa kweli, alikuwa na imani katika ahadi zenye Yehova alimuahidi yeye na Abrahamu na Isaka, na alipenda kutenda kulingana na mapenzi na kusudi la Mungu.

Mufano wa Maria unaweza kutufundisha nini? (Picha hizi zinapatana na fungu la 11)

11. Ni nini inaonyesha kama Maria alikuwa mutu wa kiroho?

11 Sasa, tufikirie mufano wa Maria. Sababu gani Yehova alimuchagua Maria akuwe mama ya Yesu? Kwa kweli, ni kwa sababu alikuwa mutu wa kiroho. Namna gani tunajua jambo hilo? Alionyesha wazi kama alikuwa mutu wa kiroho kupitia maneno ya muzuri ya kumusifu Mungu yenye alisema wakati alitembelea Zekaria na Elizabethi, watu wa jamaa yake. (Soma Luka 1:46-55.) Maneno ya Maria yanaonyesha kama alipenda sana Neno la Mungu na alijua muzuri sana Maandiko ya Kiebrania. (Mwa. 30:13; 1 Sam. 2:1-10; Mal. 3:12) Kwa kweli, hata kama yeye na Yosefu walikuwa wametoka tu kuoana, walijizuia kufanya kitendo cha ndoa mupaka wakati Yesu alizaliwa. Hilo linaonyesha nini? Linaonyesha kama wote wawili walihangaikia zaidi mapenzi ya Yehova kuliko kutimiza tamaa zao. (Mt. 1:25) Kadiri wakati ulipita, Maria aliona mambo yenye yalikuwa yanatendeka katika maisha ya Yesu na alisikiliza kwa uangalifu maneno yenye hekima yenye alisema. Zaidi ya hilo, ‘aliweka kwa uangalifu maneno yote hayo moyoni mwake.’ (Lu. 2:51) Ni wazi kama alipendezwa na kusudi la Mungu juu ya Masiya. Kwa kweli, mufano wa Maria unatusaidia kufikiria namna tunaweza kutia mapenzi ya Mungu pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu.

12. (a) Yesu alifanana na Baba yake katika njia gani? (b) Namna gani tunaweza kuiga mufano wa Yesu? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

12 Hata hivyo, kati ya watu wote wenye wameishi, ni Yesu ndiye mufano muzuri zaidi wa mutu wa kiroho. Katika maisha yake na utumishi wake wote, alionyesha kama alipenda kumuiga Baba yake, Yehova. Mawazo na matendo yake yalionyesha hivyo. Pia, alionyesha sifa kama za Yehova na aliishi kulingana na mapenzi na kanuni za Mungu. (Yoh. 8:29; 14:9; 15:10) Kwa mufano, ona namna nabii Isaya anaeleza sifa ya Mungu ya huruma, na ulinganishe jambo hilo na mambo yenye Marko muandikaji wa Injili anaeleza juu ya namna Yesu alionyesha sifa hiyo. (Soma Isaya 63:9; Marko 6:34.) Kama Yesu, sikuzote tuko tayari kuonyesha huruma wakati tunakutana na watu wenye kuwa na lazima ya musaada? Zaidi ya hilo, Yesu alijitoa kabisa katika kazi ya kuhubiri na kufundisha habari njema. (Lu. 4:43) Sifa zake na matendo yake vinaonyesha kama alikuwa mutu wa kiroho.

13, 14. (a) Mifano ya watu wa kiroho wa wakati wetu inaweza kutufundisha nini? (b) Toa mufano.

13 Zaidi ya mifano yenye kuwa katika Maandiko, kuko pia mifano ya watu wa kiroho wa wakati wetu wenye wamefanya maendeleo makubwa katika kuonyesha sifa kama za Yesu. Pengine umeona bidii yao katika kazi ya kuhubiri, namna wanaonyesha ukarimu mwingi, huruma yao, ao sifa zingine za muzuri. Kama sisi, wamepiganisha uzaifu na hali ya kukosa kukamilika ili kujikaza kukomalisha sifa hizo za muzuri. Rachel, dada mumoja katika Brazili, anasema hivi: “Nilipenda kufuata namna ya kuvaa ya watu wa ulimwengu. Kwa hiyo, sikuvaa kwa kiasi kabisa. Lakini, kujifunza kweli kulinichochea kujikaza ili nikuwe mutu wa kiroho. Haikukuwa vyepesi kufanya mabadiliko, lakini nikakuwa na furaha zaidi na nikapata kusudi la kweli katika maisha.”

14 Reylene, wa inchi ya Ufilipino, alikuwa na magumu tofauti. Alikaza akili yake juu ya kufuatia masomo ya juu na kupata kazi ya muzuri ili akuwe na maisha ya muzuri sana. Anasema hivi: “Sikukaza tena akili juu ya miradi yangu ya kiroho. Lakini nilianza kutambua kama nilikuwa ninakosa jambo fulani katika maisha yangu, jambo la maana sana kuliko kazi yangu. Kwa hiyo, nilikaza tena akili yangu juu ya utumishi wangu kwa Yehova.” Tangu wakati huo, Reylene iko na imani katika ahadi ya Yehova yenye kuwa katika Mathayo 6:33, 34. Anasema hivi: “Ninajua kabisa kama Yehova atanihangaikia!” Pengine unajua watu wenye kuonyesha mifano kama hiyo katika kutaniko lenu. Kwa kweli, tunachochewa kuiga watu waaminifu kama hao wenye kumufuata Kristo.​—1 Kor. 11:1; 2 Tes. 3:7.

UKUWE NA “AKILI YA KRISTO”

15, 16. (a) Ili tukuwe kama Kristo, tunapaswa kufanya nini? (b) Namna gani tunaweza kujua muzuri “akili ya Kristo”?

15 Namna gani unaweza kuiga Kristo? Andiko la 1 Wakorintho 2:16 linasema kama tunapaswa kuwa na “akili ya Kristo.” Na Waroma 15:5 inasema kama tunapaswa kuwa na ‘mutazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao.’ Kwa hiyo, ili tukuwe kama Kristo tunapaswa kujua namna anafikiri na sifa zake zote. Kisha tunapaswa kufuata mufano wake. Yesu alikaza akili yake juu ya urafiki wake pamoja na Mungu. Kwa hiyo, kuwa kama Yesu kunafanya tukuwe zaidi kama Yehova. Kwa hiyo, tunaona kuwa ni jambo la maana sana tujifunze kufikiri kama Yesu.

16 Tunaweza kufanya hivyo namna gani? Wanafunzi wa Yesu waliona miujiza yake, walisikiliza mafundisho yake, waliona namna alitendea watu wa namna mbalimbali, na waliona namna alitumikisha kanuni za Mungu. Walisema hivi: “Nasi ni mashahidi wa mambo yote aliyoyafanya.” (Mdo. 10:39) Lakini sisi hatuwezi kumuona moja kwa moja. Hata hivyo, kwa upendo, Yehova ametutolea vitabu vya Injili vyenye vinaweza kutusaidia kujua muzuri zaidi sifa za Yesu. Wakati tunasoma na kutafakari juu ya kitabu cha Mathayo, Marko, Luka, na Yohana tunajua muzuri zaidi mawazo ya Kristo. Kwa hiyo, tunaweza ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu’ na ‘kujivika [kuvaa] silaha ya mwelekeo uleule wa akili’ kama ya Kristo.​—1 Pet. 2:21; 4:1.

17. Namna gani kufikiri kama Kristo kutatusaidia?

17 Namna gani kujifunza kufikiri kama Kristo kunaweza kutusaidia? Kama vile tu chakula chenye kujenga kinatia nguvu mwili wetu, vilevile kujaza mawazo ya Kristo katika akili yetu kunatia nguvu hali yetu ya kiroho. Hatua kwa hatua, tunafikia kujua namna Kristo angetenda katika hali yoyote. Na hilo linatusaidia kukamata maamuzi yenye kutusaidia tuendelee kuwa na zamiri safi na tukubaliwe na Mungu. Kwa kweli, faida hizo zinatupatia sababu ya muzuri ya ‘kuvaa Bwana Yesu Kristo.’​—Rom. 13:14.

18. Umejifunza nini juu ya kuwa mutu wa kiroho?

18 Tumezungumuzia maana ya kuwa mutu wa kiroho. Tumeona pia kama mifano ya muzuri ya watu wa kiroho inaweza kutufundisha mambo fulani. Mwishowe, tumejifunza namna kuwa na “akili ya Kristo” kunatusaidia kukomaa kiroho. Lakini, kuko mambo mengine yenye kuhusu hali yetu ya kiroho yenye tunapaswa kufikiria. Kwa mufano, namna gani tunaweza kuchunguza ikiwa tuko nguvu kiroho? Tunaweza kufanya mambo gani mengine ili kukomaa kiroho? Na hali yetu ya kiroho itakuwa na matokeo gani katika maisha yetu ya kila siku? Habari yenye kufuata itatusaidia kujibia maulizo hayo.