Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Songa Mbele Ukiwa Mtu wa Kiroho!

Songa Mbele Ukiwa Mtu wa Kiroho!

“Endeleeni kutembea kwa roho.”—GAL. 5:16.

NYIMBO: 22, 75

1, 2. Ndugu mmoja alitambua upungufu gani katika hali yake ya kiroho, naye alifanya marekebisho gani?

ROBERT alibatizwa akiwa na umri wa miaka 15 lakini hakuchukua kweli kwa uzito. Anasema hivi: “Sikufanya jambo lolote baya lakini nilifanya mambo kidesturi tu. Nilionekana kama mtu mwenye nguvu kiroho kwani nilihudhuria mikutano yote na kutumikia nikiwa painia msaidizi mara kadhaa kwa mwaka. Lakini jambo fulani lilikosekana.”

2 Robert hakutambua tatizo lilikuwa wapi mpaka alipofunga ndoa. Katika mazungumzo yao ya kawaida, yeye na mke wake walianza kuulizana maswali ya Biblia. Mke wake, ambaye alikuwa mwenye nguvu kiroho, hakutatizika kujibu maswali hayo lakini Robert aliaibika mara nyingi kwa sababu hakujua majibu. Anasema hivi: “Ni kana kwamba sikujua chochote. Nilijiambia hivi, ‘Ikiwa ninapaswa kuwa kichwa cha mke wangu katika mambo ya kiroho, ninahitaji kufanya marekebisho.’” Na alifanya hivyo. Anasema, “Nilianza kusoma na kujifunza Biblia kwa bidii, nami nilifanya hivyo tena na tena, na baada ya muda nikaanza kuielewa vizuri. Niliifahamu, na jambo la muhimu hata zaidi nilisitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.”

3. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Robert? (b) Tutachunguza mambo gani muhimu?

3 Tunaweza kujifunza masomo muhimu kutokana na kisa cha Robert. Huenda tuna ujuzi fulani wa Biblia na tunahudhuria mikutano kwa ukawaida lakini mambo hayo pekee hayatoshi kutufanya tuwe watu wa kiroho. Au huenda tayari tumefanya maendeleo lakini tunapojichunguza zaidi tunatambua kwamba tunaweza kuboresha hali yetu ya kiroho. (Flp. 3:16) Katika makala hii, tutajibu maswali matatu muhimu yatakayotusaidia kuendelea kufanya maendeleo: (1) Ni nini kitakachotusaidia kuchanganua jinsi hali yetu ya kiroho ilivyo kihalisi? (2) Tunaweza kusitawishaje hali nzuri ya kiroho na kuzidi kufanya maendeleo tukiwa watu wa kiroho? (3) Kuwa wenye nguvu kiroho kutatusaidiaje katika maisha yetu ya kila siku?

KUJICHUNGUZA

4. Shauri linalopatikana katika Waefeso 4:23, 24 linawahusu nani?

4 Tulipoanza kumtumikia Mungu, tulifanya mabadiliko. Mabadiliko hayo yaligusa kila sehemu ya maisha yetu. Na hatukuacha kufanya mabadiliko tulipobatizwa. Tunaambiwa “ [tuendelee] kufanywa upya katika nguvu zinazoongoza akili [zetu].” (Efe. 4:23, 24) Kwa kuwa sisi si wakamilifu, sote tunahitaji kuendelea kufanya mabadiliko. Hata wale ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu wanahitaji kuendelea kudumisha hali yao ya kiroho.—Flp. 3:12, 13.

5. Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia kujichunguza?

5 Ili kuboresha na kudumisha hali yetu ya kiroho, tunahitaji kujichunguza kwa unyoofu. Iwe sisi ni vijana au wazee, tunaweza kujiuliza maswali haya: ‘Je, kuna mabadiliko yoyote niliyofanya yanayoonyesha kwamba ninafanya maendeleo ili niwe mtu wa kiroho? Je, utu wangu umeanza kufanana na utu wa Kristo? Mtazamo na mwenendo wangu ninapokuwa kwenye mikutano unafunua nini kuhusu kina cha hali yangu ya kiroho? Mazungumzo yangu yanaonyesha nini kuhusu mambo ninayotamani? Mazoea yangu ya kujifunza, mavazi na mapambo, na jinsi ninavyoitikia shauri hufunua nini kunihusu? Mimi hutendaje ninapokabili vishawishi? Je, nimefanya maendeleo kutoka katika mambo ya msingi na kufikia ukomavu, na hivyo kuwa Mkristo aliyekomaa kabisa?’ (Efe. 4:13) Kufikiria majibu ya maswali hayo kutatusaidia kupima maendeleo yetu ya kiroho.

6. Ni nini kingine kinachoweza kutusaidia kuchanganua hali yetu ya kiroho?

6 Ili kuchanganua hali yetu ya kiroho, nyakati nyingine tunahitaji msaada kutoka kwa wengine. Mtume Paulo alitaja kwamba mtu wa kimwili hawezi kutambua kwamba njia yake ya maisha haimpendezi Mungu. Kwa upande mwingine, mtu wa kiroho anaelewa jinsi Mungu anavyoona mambo na vilevile anatambua kwamba njia ya maisha ya mtu wa kimwili haimpendezi Mungu. (1 Kor. 2:14-16; 3:1-3) Mara nyingi, wazee wa kutaniko walio na akili ya Kristo hutambua mapema mtu anapoanza kufikiri kwa njia ya kimwili. Ikiwa wanatujulisha kwamba wameona dalili kama hizo, je, sisi hukubali na kufuata shauri lao? Tunapokubali shauri lao, tunathibitisha kwamba tunatamani kuboresha hali yetu ya kiroho.—Mhu. 7:5, 9.

KUSITAWISHA HALI NZURI YA KIROHO

7. Kwa nini ujuzi wa Biblia pekee hautoshi kutufanya tuwe watu wa kiroho?

7 Kumbuka kwamba ujuzi wa Biblia pekee hautoshi kumfanya mtu awe wa kiroho. Mfalme Sulemani wa zamani alikuwa na ujuzi mwingi kuhusu njia za Yehova. Mambo aliyosema yaliandikwa katika Biblia. Lakini mwishowe alishindwa kuendelea kuwa mtu wa kiroho aliye mwaminifu kwa Yehova. (1 Fal. 4:29, 30; 11:4-6) Hivyo, ni nini kingine kinachohitajika zaidi ya kuifahamu Biblia? Tunahitaji kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho. (Kol. 2:6, 7) Tutafanyaje hivyo?

8, 9. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuimarisha hali yetu ya kiroho? (b) Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapojifunza na kutafakari? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

8 Paulo aliwahimiza Wakristo wa karne ya kwanza “[wasonge] mbele kuelekea ukomavu.” (Ebr. 6:1) Tunahitaji kuchukua hatua zipi ili kufuata shauri la Paulo leo? Hatua moja muhimu ni kujifunza kitabu Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu.” Kujifunza kitabu hicho hadi mwisho kutakusaidia kuona jinsi unavyoweza kutumia kanuni za Biblia maishani mwako. Ikiwa tayari umemaliza kujifunza kitabu hicho, je, unaweza kuanza kusoma machapisho mengine ya kujifunzia yanayoweza kukusaidia kuimarisha imani yako? (Kol. 1:23) Je, wewe hutafakari kuhusu mambo unayojifunza na kusali ili uone jinsi unavyoweza kutumia habari hizo maishani mwako?

9 Kumbuka kwamba tunapojifunza na kutafakari, tunapaswa kufanya hivyo tukiwa na lengo la kusitawisha tamaa ya kutoka moyoni ya kumpendeza Yehova na kutii sheria zake. (Zab. 40:8; 119:97) Wakati uleule, tunahitaji kujitahidi kukataa mambo ambayo yatazuia ukuzi wetu wa kiroho.—Tito 2:11, 12.

10. Vijana wanaweza kufanya nini ili kusitawisha hali nzuri ya kiroho?

10 Ikiwa wewe ni kijana, je, una malengo hususa ya kiroho? Ndugu mmoja anayetumikia Betheli huwa na kawaida ya kuzungumza na wale watakaobatizwa kabla ya programu kuanza anapohudhuria makusanyiko ya mzunguko. Wengi wa wale wanaotaka kubatizwa ni vijana. Ndugu huyo huwauliza kuhusu malengo ya kiroho waliyonayo. Maelezo ambayo wengi wao hutoa huonyesha kwamba wanajua kihususa mambo wanayotaka kufanya ili kumtumikia Yehova—labda kuanza aina fulani ya utumishi wa wakati wote au kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Hata hivyo, nyakati nyingine baadhi ya vijana hukosa la kusema. Je, huenda ni kwa sababu hawajafikiria kwa uzito kwamba wanapaswa kuwa na malengo hususa ya kiroho? Ikiwa wewe ni kijana jiulize hivi: ‘Je, mimi hushiriki katika utendaji wa kiroho kwa sababu tu wazazi wangu wanatarajia nifanye hivyo? Je, ninaendelea kumkaribia Mungu kwa kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja naye?’ Bila shaka shauri la kujiwekea malengo ya kiroho haliwahusu tu vijana. Kuwa na malengo kama hayo kutatusaidia sote tukiwa watumishi wa Yehova kusitawisha hali ya kiroho yenye kina.—Mhu. 12:1, 13.

11. (a) Ili tufanye maendeleo halisi ya kiroho, tunahitaji kufanya nini? (b) Tunaweza kuiga mfano gani ulio katika Biblia?

11 Baada ya kutambua mambo tunayohitaji kuboresha, tunapaswa kuchukua hatua zitakazotusaidia kufanya maendeleo. Kuwa mtu wa kiroho ni jambo muhimu sana. Ukweli ni kwamba kuwa mtu wa kiroho ni jambo litakaloamua ikiwa tutaishi ama tutakufa. (Rom. 8:6-8) Hata hivyo, kuwa mtu mkomavu kiroho hakumaanishi kuwa mkamilifu. Roho ya Yehova inaweza kutusaidia kufanya maendeleo yanayohitajika. Lakini bado tunahitaji kutia jitihada. Akizungumzia andiko la Luka 13:24, John Barr, ambaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema hivi miaka kadhaa iliyopita: “Wengi wanashindwa kwa sababu hawajitahidi kuwa wenye nguvu kiroho.” Tunahitaji kuwa kama Yakobo ambaye hakuacha kupigana mweleka na malaika hadi alipobarikiwa. (Mwa. 32:26-28) Ingawa tunaweza kufurahia kujifunza Biblia, hatupaswi kutazamia Biblia iwe kama kitabu cha riwaya kilichokusudiwa kutuburudisha tu. Tunahitaji kutia jitihada nyingi kutafuta hazina za kiroho zitakazotusaidia.

12, 13. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuwa na “mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao”? (b) Shauri la mtume Petro na mfano aliotuwekea unaweza kutusaidiaje? (c) Tunaweza kufanya nini ili kusitawisha hali nzuri ya kiroho? (Tazama sanduku “ Mambo Yanayoweza Kukusaidia Kufanya Maendeleo ya Kiroho.”)

12 Tunapoendelea kujitahidi kusitawisha hali nzuri ya kiroho, roho takatifu itatupatia nguvu za kubadili akili zetu. Kwa msaada wa roho hiyo, hatua kwa hatua njia yetu ya kufikiri itazidi kuwa kama ya Kristo. (Rom. 15:5) Isitoshe, itatusaidia kung’oa kabisa tamaa za kimwili na kusitawisha sifa zinazomfurahisha Mungu. (Gal. 5:16, 22, 23) Ikiwa tunatambua kwamba akili yetu inatuchochea tuanze kupenda vitu vya kimwili au kufuata tamaa za kimwili, hatupaswi kuacha kujitahidi kung’oa tamaa hizo. Endelea kumwomba Yehova akupe roho takatifu, naye atakusaidia ubadili mtazamo wako wa kiakili ili ukazie mambo yanayofaa. (Luka 11:13) Mkumbuke mtume Petro. Mara kadhaa maishani mwake hakutenda kama mtu wa kiroho. (Mt. 16:22, 23; Luka 22:34, 54-62; Gal. 2:11-14) Lakini hakukata tamaa. Kwa msaada wa Yehova, hatua kwa hatua Petro alisitawisha njia ya Kristo ya kufikiri. Tunaweza kufanya vivyo hivyo pia.

13 Kwa kweli, Petro hata alitaja mambo hususa tunayoweza kufanyia kazi. (Soma 2 Petro 1:5-8.) ‘Kujitahidi kabisa’ kusitawisha sifa kama vile kujizuia, uvumilivu, na upendo wa kindugu, kutatusaidia kuendelea kufanya maendeleo tukiwa watu wa kiroho. Kwa nini usijiulize hivi kila siku, ‛Ni jambo gani ninaloweza kufanyia kazi leo ili nifanye maendeleo ya kiroho?’

KUTUMIA KANUNI ZA BIBLIA KATIKA MAISHA YA KILA SIKU

14. Kuwa mtu wa kiroho kutakuwa na matokeo gani maishani mwetu?

14 Kufikiri kama Kristo kutatuchochea tuwe na mwenendo mzuri tukiwa kazini au shuleni, kutaboresha mazungumzo yetu na pia maamuzi tunayofanya kila siku. Maamuzi hayo yataonyesha kwamba tunajitahidi kuwa wafuasi wa Kristo. Tukiwa watu wa kiroho, hatungependa kuruhusu chochote kihatarishe uhusiano wetu na Baba yetu wa mbinguni. Tunapokabili vishawishi, mtazamo wetu wa akili ulio kama wa Kristo utatuchochea tuvipinge kabisa. Tunapofanya maamuzi, tutatua na kufikiri kwa uzito kuhusu maswali haya: ‘Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kunisaidia kufanya uamuzi mzuri? Kristo angetendaje chini ya hali hii? Ni uamuzi upi utakaomfurahisha Yehova?’ Ili tujizoeze kufikiri kwa njia hiyo, acheni tuchunguze mifano michache. Katika kila mfano, tutaona kanuni ya Kimaandiko itakayotusaidia kufanya uamuzi wa hekima.

15, 16. Toa mifano ya jinsi kufikiri kama Kristo kunavyoweza kutusaidia tunapofanya maamuzi kuhusu (a) kuchagua mwenzi wa ndoa. (b) kuchagua marafiki.

15 Kuchagua mwenzi wa ndoa. Kanuni ya Kimaandiko inayohusu jambo hilo inapatikana katika 2 Wakorintho 6:14, 15. (Soma.) Maneno ya Paulo yanaonyesha wazi kwamba mtu wa kiroho na mtu wa kimwili hawawezi kuwa na upatano kamili. Kanuni hiyo inahusikaje tunapochagua mwenzi wa ndoa?

16 Marafiki. Ona kanuni ya Kimaandiko iliyo katika 1 Wakorintho 15:33. (Soma.) Mtu anayemwogopa Mungu hatashirikiana na watu wanaoweza kuhatarisha hali yake ya kiroho. Ni maswali gani yanayoweza kukusaidia kuona jinsi kanuni hiyo inavyotumika? Kwa mfano, kanuni hiyo inaweza kutumikaje kuhusiana na matumizi ya mitandao ya kijamii? Au unapaswa kufanya nini ikiwa watu usiowafahamu wanakualika kucheza michezo ya kompyuta mtandaoni?

Je, maamuzi yangu yatanisaidia kukua kiroho? (Tazama fungu la 17)

17-19. Kuwa na mtazamo wa kiroho kutakusaidiaje (a) kuepuka kufuatia miradi ya ubatili? (b) kujiwekea malengo maishani? (c) kushughulika na hali za kutoelewana?

17 Mambo yanayoweza kuzuia ukuzi wa kiroho. Maneno ambayo Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake yanahusisha onyo fulani. (Soma Waebrania 6:1.) “Matendo yaliyokufa” tunayopaswa kuepuka ni gani? Ni miradi yoyote isiyo ya kiroho, ya ubatili, na isiyo na faida. Kanuni hii inaweza kutusaidia kujibu maswali mengi yanayoweza kuzuka maishani, kama vile: ‘Je, utendaji huu ni mojawapo ya matendo ya mwili? Je, nijihusishe na mradi huu wa kutafuta pesa? Kwa nini nisijiunge na vikundi vya ulimwengu huu vya wanaharakati wa kuleta mabadiliko?’’

Je, maamuzi yangu yatanisaidia kujiwekea malengo ya kiroho? (Tazama fungu la 18)

18 Malengo ya kiroho. Maneno ya Yesu kwenye Mahubiri ya Mlimani yanatupatia mwongozo ulio wazi kuhusu kujiwekea malengo. (Mt. 6:33) Mtu wa kiroho hufuatia malengo ya kiroho. Kuzingatia kanuni hiyo akilini mwetu kutatusaidia kujibu maswali kama vile: ‘Je, nifuatie elimu ya juu? Je, nikubali kazi hii?’

Je, maamuzi yangu yatanisaidia “kufanya amani”? (Tazama fungu la 19)

19 Hali za kutoelewana. Shauri la Paulo kwa Wakristo huko Roma linatusaidiaje kushughulika na hali za kutoelewana? (Rom. 12:18) Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunajitahidi kabisa “[kufanya] amani na watu wote.” Hali za kutoelewana zinapotokea, sisi hutendaje? Je, ni vigumu kwetu kukubali maoni ya wengine, au je, tunajulikana kuwa watu “wanaofanya amani”?—Yak. 3:18.

20. Kwa nini ungependa kufanya maendeleo ya kiroho?

20 Hiyo ni baadhi tu ya mifano ya jinsi ambavyo kutafakari kanuni za Mungu kunaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayoonyesha kwamba sisi ni watu wa kiroho. Kuwa mtu wa kiroho kunaweza kufanya maisha yetu ya kila siku yawe yenye furaha zaidi na yenye kuridhisha zaidi. Robert, ambaye tulichunguza kisa chake mwanzoni mwa makala hii, anasema hivi: “Nilianza kuwa mume mzuri zaidi na baba mzuri zaidi baada ya kusitawisha uhusiano halisi pamoja na Yehova. Niliridhika maishani na kuwa na furaha.” Tunaweza kufurahia baraka kama hizo ikiwa jambo kuu maishani mwetu litakuwa kufanya maendeleo ya kiroho. Tukiwa watu wa kiroho, tutafurahia maisha yenye kuridhisha sasa na “uzima ulio wa kweli” wakati ujao.—1 Tim. 6:19.