Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Nizamu​—Inaonyesha Upendo wa Mungu

Nizamu​—Inaonyesha Upendo wa Mungu

‘Yeye ambaye Yehova anamupenda, anamutia nizamu.’​—EBR. 12:6.

NYIMBO: 123, 86

1. Namna gani Biblia inaeleza nizamu?

WAKATI unasikia neno ‘nizamu,’ unafikiria nini? Pengine unafikiria mara moja malipizi, lakini neno hilo linamaanisha mengi zaidi. Mara nyingi Biblia inaonyesha kama nizamu ni jambo la muzuri kwetu, wakati fulani inatajwa pamoja na ujuzi, hekima, upendo, na uzima. (Met. 1:2-7; 4:11-13) Ni kwa sababu nizamu ya Mungu inaonyesha upendo wake na tamaa yake ya kutupatia uzima wa milele. (Ebr. 12:6) Hata kama nizamu yake inaweza kutia ndani malipizi, haipite mipaka hata kidogo ao haiko yenye ukali. Kwa kweli, maana kubwa ya neno ‘nizamu’ ni kufundisha, kama vile muzazi anafundisha mutoto wake mupendwa.

2, 3. Namna gani nizamu inatia ndani mafundisho na malipizi? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

2 Fikiria mufano huu: Mutoto mudogo mwanaume mwenye kuitwa Johnny anacheza-cheza na kabumbu katika nyumba. Mama yake anamuambia hivi: “Johnny, unajua kama haupaswe kucheza na kabumbu katika nyumba! Unaweza kuvunja kitu fulani.” Lakini anazarau shauri la mama yake, na anaendelea kucheza kabumbu yake na bila kujua anavunja chombo fulani cha kuwekea maua. Namna gani mama yake atamupatia nizamu? Nizamu yake inaweza kutia ndani mafundisho na malipizi fulani. Wakati anamufundisha Johnny, anaweza kumukumbusha sababu gani tendo lenye alifanya lilikuwa la mubaya. Anapenda kumuonyesha kama ni jambo la hekima atii wazazi wake, na kumuelezea kama sheria zenye wametia ni za lazima na zinaonyesha usawaziko. Kisha, ili kukazia maneno yake, anaweza kumupatia malipizi fulani yenye kufaa. Kwa mufano, anaweza kumunyanganya kabumbu yake kwa muda fulani. Hilo linaweza kumusaidia aelewe kama kukosa kutii, kunaleta matokeo ya mubaya.

3 Kwa sababu tuko katika kutaniko la Kikristo, tuko sehemu ya nyumba ya Mungu. (1 Tim. 3:15) Kwa hiyo, tunaheshimia haki ya Yehova ya kutuwekea kanuni na kutupatia nizamu kwa upendo wakati tunavunja kanuni hizo. Zaidi ya hilo, ikiwa matendo yetu yanatuletea matokeo ya mubaya, nizamu yake inaweza kutukumbusha kama kusikiliza Baba yetu wa mbinguni ni jambo la maana sana. (Gal. 6:7) Mungu anatuhangaikia sana, na hapendi tuteseke.​—1 Pet. 5:6, 7.

4. (a) Yehova anabariki mazoezi ya namna gani? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

4 Wakati tunatoa nizamu yenye kutoka katika Maandiko, tunaweza kusaidia mutoto wetu ao mwanafunzi wetu wa Biblia afikie muradi wa kuwa mwanafunzi wa Kristo. Neno la Mungu, chombo chetu kikubwa chenye tunatumia ili kuzoeza wengine, linatusaidia ‘kutia nizamu katika uadilifu.’ Hilo linaweza kusaidia mutoto wetu ao mwanafunzi wa Biblia aelewe na ‘kushika mambo yote ambayo [Yesu] ametuamuru.’ (2 Tim. 3:16; Mt. 28:19, 20) Yehova anabariki mazoezi ya namna hiyo yenye kutusaidia kufanya zaidi wanafunzi wa Kristo. (Soma Tito 2:11-14.) Tuzungumuzie sasa maulizo tatu ya maana sana: (1) Namna gani nizamu ya Mungu inaonyesha kama anatupenda? (2) Mifano ya wale wenye Mungu alipatia nizamu zamani, inaweza kutufundisha nini, (3) Wakati tunapatia wengine nizamu, namna gani tunaweza kumuiga Yehova na Mwana wake?

MUNGU ANATOA NIZAMU KWA UPENDO

5. Ni katika njia gani nizamu ya Yehova inaonyesha kama anatupenda?

5 Upendo unamuchochea Yehova aturekebishe, atufundishe, na kutuzoeza ili tubakie katika upendo wake na katika njia ya uzima. (1 Yoh. 4:16) Hatuzarau ao kututukana hata kidogo, na kutufanya tujisikie kama tuko watu wa bure. (Met. 12:18) Lakini, Yehova anatuonyesha heshima kwa kutafuta mambo ya muzuri yenye kuwa katika moyo wetu na kuheshimia uhuru wetu wa kuchagua. Je, ni hivyo unaona nizamu ya Mungu, iwe inatoka katika Neno lake Biblia, katika vichapo vyetu vyenye kutegemea Biblia, kwa wazazi Wakristo, ao wazee wa kutaniko? Kwa kweli, wakati wazee wanajikaza sana kutusaidia kwa upole na kwa upendo wakati ‘tunajikwaa katika kosa fulani,’ wanaonyesha upendo wa Yehova kwetu.​—Gal. 6:1.

6. Namna gani nizamu inaonyesha upendo wa Mungu hata kama inaweza kufanya mutu apoteze mapendeleo fulani?

6 Lakini, wakati fulani nizamu inaweza kutia ndani mambo mengi zaidi ya mashauri ao kurekebisha mutu kupitia maneno. Ikiwa mutu fulani amefanya zambi nzito, nizamu yenye anapewa inaweza kutia ndani kupoteza mapendeleo fulani katika kutaniko. Hata kama anapoteza mapendeleo fulani, nizamu hiyo inaonyesha upendo wa Mungu kwake. Kwa mufano, kupoteza mapendeleo kunaweza kusaidia mutu aelewe kama ni jambo la maana sana akaze akili yake juu ya kufanya funzo la Biblia la pekee, kutafakari, na kusali. Mambo hayo yanaweza kutia nguvu hali yake ya kiroho. (Zab. 19:7) Kisha wakati fulani anaweza kupata tena mapendeleo yake. Hata kutengwa na kutaniko kunaonyesha upendo wa Yehova kwetu, kwa sababu hilo linalinda kutaniko ili lisiambukizwe na tabia za mubaya. (1 Kor. 5:6, 7, 11) Pia, kwa sababu Mungu anatoa nizamu kwa kipimo chenye kufaa, kutengwa na kutaniko kunaweza kusaidia mutu mwenye alifanya zambi aone uzito wa zambi yake na kumuchochea atubu.​—Mdo. 3:19.

NIZAMU YA YEHOVA INATULETEA FAIDA

7. Shebna alikuwa nani, na alianza kuonyesha tabia gani ya mubaya?

7 Ili kuelewa faida ya nizamu, tuzungumuzie basi watu wawili wenye Yehova alipatia nizamu: Shebna, mwenye aliishi wakati wa Mufalme Hezekia, na Graham, ndugu wa siku zetu. Kwa sababu Shebna alikuwa musimamizi-nyumba,’ pengine wa nyumba ya Hezekia, alikuwa na mamlaka makubwa. (Isa. 22:15) Lakini, jambo la kuhuzunisha ni kwamba, akakuwa na kiburi, na kujitafutia utukufu. Alijifanyia hata kaburi la bei, na alitembea katika “magari ya utukufu”!​—Isa. 22:16-18.

Kukubali kwa unyenyekevu kubadilisha mawazo yetu kunaleta baraka za Mungu (Picha hizi zinapatana na fungu la 8-10)

8. Namna gani Yehova alimupatia Shebna nizamu, na hilo lilikuwa na matokeo gani?

8 Kwa sababu Shebna alijitafutia utukufu, Mungu ‘alimuondoa katika cheo chake’ na akatia Eliakimu pa nafasi yake. (Isa. 22:19-21) Mabadiliko hayo yalitokea wakati Senakeribu mufalme wa Asiria alikuwa anapanga kushambulia Yerusalemu. Kisha wakati fulani, mufalme huyo alituma wakubwa wake Yerusalemu, pamoja na maaskari wengi ili kuvunja moyo Wayahudi na kumuogopesha Hezekia ili akubali kushindwa. (2 Fal. 18:17-25) Eliakimu alitumwa ili kuzungumuza na wakubwa hao, lakini hakukuwa yeye mwenyewe. Alisindikizwa na watu wengine wawili, kati yao kulikuwa Shebna; mwenye wakati huo alikuwa mwandishi. Kwa kweli, hilo linaweza kutuonyesha kama pengine Shebna hakuweka kinyongo ao kusikia uchungu lakini alikubali kwa unyenyekevu cheo cha hali ya chini. Ikiwa ni hivyo, mufano wake unaweza kutufundisha nini? Tuzungumuzie mambo tatu.

9-11. (a) Mufano wa Shebna unaweza kutufundisha mambo gani ya maana? (b) Ni nini inakutia moyo kuhusu namna Yehova alimutendea Shebna?

9 Kwanza, Shebna alipoteza cheo chake. Mufano wake unatoa onyo kwamba ‘kiburi kinatangulia kuanguka, na roho ya majivuno inatangulia kujikwaa.’ (Met. 16:18) Ikiwa uko na mapendeleo katika kutaniko, na pengine watu wanakuona kuwa wa maana, utajikaza kuendelea kuonyesha unyenyekevu? Utamupatia Yehova utukufu juu ya uwezo wowote wenye uko nao ao juu ya mambo yenye umetimiza? (1 Kor. 4:7) Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Ninamuambia kila mutu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali kufikiri ili akuwe na akili timamu [akili nzuri].’​—Rom. 12:3.

10 Pili, shauri nzito lenye Yehova alimutolea Shebna, pengine lilionyesha kama aliamini kuwa Shebna angeweza kufanya mabadiliko. (Met. 3:11, 12) Wale wenye wamepoteza mapendeleo ya utumishi katika tengenezo la Mungu wanaweza kujifunza mambo mengi kupitia mufano huo! Kuliko kuwa na hasira na kinyongo, waendelee basi kumutumikia Mungu kwa bidii katika hali zao za mupya, na kuendelea kuona kwamba nizamu inaonyesha upendo wa Yehova. Kumbuka kwamba, Baba yetu wa mbinguni hatatuona kama watu wenye hawawezi kubadilika ikiwa tunajinyenyekeza kabisa mbele yake. (Soma 1 Petro 5:6, 7.) Mungu anaweza kutufinyanga kupitia nizamu yake yenye kuonyesha upendo; kwa hiyo, tuendelee basi kuwa kama udongo wa teketeke katika mikono yake.

11 Wale wenye kuwa na madaraka ya kutoa nizamu kama vile wazazi na waangalizi Wakristo, wanaweza kujifunza mambo mengi ya maana kupitia namna Yehova alimutendea Shebna. Wanaweza kujifunza mambo gani? Nizamu ya Yehova inaonyesha kama anachukia zambi, lakini inaonyesha pia kama anahangaikia mutu mwenye alifanya zambi. Ikiwa wewe muzazi ao mwangalizi katika kutaniko unapaswa kutoa nizamu, utamuiga Yehova kwa kuchukia zambi na wakati huohuo kuona mambo ya muzuri yenye kuwa katika mutoto wako ao Mukristo mwenzako?​—Yuda 22, 23.

12-14. (a) Watu fulani wanatenda namna gani wakati Mungu anawapatia nizamu? (b) Namna gani Neno la Mungu lilisaidia ndugu mumoja abadilishe mawazo yake, na alipata matokeo gani?

12 Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, kisha kupewa nizamu, watu fulani wanakasirika sana na hata wanamuacha Mungu na watu wake. (Ebr. 3:12, 13) Lakini, hilo linamaanisha kama watu hao hawawezi tena kufanya mabadiliko? Fikiria mufano wa Graham, mwenye alitengwa na kutaniko, na kisha muda fulani alirudishwa. Lakini, akaacha kuhubiri na kukusanyika. Kisha miaka fulani, aliomba muzee mwenye alikuwa anamusaidia ajifunze Biblia pamoja naye.

13 Muzee huyo anakumbuka hivi: “Kiburi ndilo lilikuwa tatizo la Graham. Alikuwa anasema mubaya wazee wenye walikuwa katika halmashauri ya hukumu yenye ilimutenga na kutaniko. Kwa hiyo, katika funzo fulani zenye zilifuata, tulizungumuzia maandiko yenye kuzungumuzia kiburi na matokeo yake. Graham alianza kujiona muzuri zaidi katika kioo cha Neno la Mungu, na hakufurahia mambo yenye aliona! Matokeo yalikuwa ya muzuri sana! Kisha kukubali kama alikuwa amefungwa macho na ‘boriti’ (kipande kikubwa cha muti) lenye kufananishwa na kiburi na kama tabia ya kusema mubaya juu ya wazee ndiyo ilikuwa tatizo lake, alianza kufanya mabadiliko ya muzuri bila kukawia. Alianza kuhuzuria mikutano ya Kikristo kwa ukawadia, kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, na kuwa na zoea la kusali kila siku. Alitimiza pia madaraka yake ya kiroho ya kichwa cha familia, na hilo lilifurahisha sana bibi yake na watoto wake.”​—Lu. 6:41, 42; Yak. 1:23-25.

14 Muzee huyo anaendelea kusema hivi: “Siku moja, Graham aliniambia jambo fulani lenye lilinigusa moyo. Alisema hivi: ‘Kumepita miaka mingi tangu wakati nilijua kweli, na hata nimekuwa painia. Lakini, kusema kweli, ni wakati huu tu ndio ninaweza kusema kama ninamupenda Yehova.’ Kisha wakati fulani, aliombwa aanze kupitisha mikrofone katika Jumba la Ufalme; alifurahia sana pendeleo hilo. Mufano wake ulinifundisha kama wakati mutu anajinyenyekeza mbele za Mungu kwa kukubali nizamu, anapata baraka nyingi sana!”

UIGE MUNGU NA KRISTO WAKATI UNATOA NIZAMU

15. Ikiwa tunapenda nizamu yenye tunatoa iguse moyo, tunapaswa kufanya nini?

15 Ili tukuwe walimu wazuri, tunapaswa kwanza kuwa wanafunzi wazuri. (1 Tim. 4:15, 16) Vilevile, wale wenye Mungu amepatia daraka la kutoa nizamu wanapaswa kuendelea kutii kwa unyenyekevu muongozo wa Yehova. Wakati wengine wanaona kama uko munyenyekevu watakuheshimia na itakuwa vyepesi wakubali wakati unawashauria ao kuwarekebisha. Fikiria mufano wa Yesu.

16. Mufano wa Yesu unaweza kutufundisha nini juu ya nizamu na mafundisho yenye matokeo mazuri?

16 Yesu alisikiliza na kutii Baba yake sikuzote, hata wakati ilikuwa vigumu sana kufanya hivyo. (Mt. 26:39) Na alimupatia Baba yake utukufu juu ya mafundisho na hekima yenye alikuwa nayo. (Yoh. 5:19, 30) Unyenyekevu na utii wa Yesu vilichochea watu wenye kuwa na moyo muzuri wamukaribie na vilimusaidia akuwe mwalimu muzuri na mwenye huruma. (Soma Luka 4:22.) Maneno yake yenye upendo yalitia moyo wale wenye walikuwa wamevunjika moyo na wenye walikuwa zaifu. (Mt. 12:20) Hata wakati uvumilivu wake ulijaribiwa, Yesu aliendelea kuonyesha upole na upendo. Hilo lilionekana wazi wakati alirekebisha mitume wake kwa sababu walionyesha roho ya kutafuta makubwa.​—Mk. 9:33-37; Lu. 22:24-27.

17. Ni sifa gani zenye zitasaidia wazee wakuwe wachungaji wazuri wa kundi la Mungu?

17 Wale wote wenye Mungu amepatia daraka la kutoa nizamu kupitia Maandiko wanaonyesha kama wako na hekima wakati wanaiga mufano wa Kristo. Kwa kweli, wakati wanafanya hivyo wanaonyesha kama wanapenda wafinyangwe na Mungu na Mwana wake. Mutume Petro aliandika hivi: ‘Mulichunge kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni uriti wa Mungu, bali kuwa vielelezo [mifano] kwa kundi.’ (1 Pet. 5:2-4) Ili kuhakikisha jambo hilo, waangalizi wanajitiisha kwa furaha kwa Mungu na Kristo, kichwa cha kutaniko, na hilo linawaletea faida wao na wale wenye kuwa chini ya ulinzi wao.​—Isa. 32:1, 2, 17, 18.

18. (a) Yehova anaomba wazazi wafanye nini? (b) Namna gani Mungu anasaidia wazazi watimize madaraka yao?

18 Kanuni hizo za musingi zinatumika pia katika familia. Biblia inaambia hivi vichwa vya familia: ‘Musiwe mukiwakasirisha watoto wenu, bali muendelee kuwalea katika nizamu na muongozo wa akilini wa Yehova.’ (Efe. 6:4) Hilo ni jambo nzito kwa kadiri gani? Methali 19:18 inasema kama kupatia watoto nizamu kunaweza kuwasaidia wapate uzima. Kwa kweli, wazazi watatoa hesabu mbele za Yehova ikiwa wanashindwa kumupatia mutoto wao nizamu! (1 Sam. 3:12-14) Hata hivyo, Yehova anapatia wazazi hekima na nguvu yenye wako nayo lazima wakati wanamuomba kwa unyenyekevu katika sala na kutegemea muongozo wa Neno lake na roho yake takatifu.​—Soma Yakobo 1:5.

UJIFUNZE NAMNA YA KUISHI MILELE KATIKA AMANI

19, 20. (a) Tunapata baraka gani wakati tunakubali nizamu ya Mungu? (b) Tutazungumuzia nini katika habari yenye kufuata?

19 Inaweza kuwa vigumu kutaja baraka zote zenye tunapata ikiwa tunakubali nizamu ya Yehova na ikiwa tunamuiga yeye na Yesu wakati tunapatia wengine nizamu. Familia zetu na makutaniko yetu yanakuwa mahali penye kuwa amani na utulivu. Pia watu wanajisikia kuwa wanapendwa, wenye kuwa wa maana, na wenye kuwa salama; hayo ni mambo madogo yenye kuonyesha baraka zenye tutapata wakati wenye kuja. (Zab. 72:7) Kwa kweli, haiko kutia chumvi kusema kama nizamu ya Yehova inatufundisha namna ya kuishi milele pamoja katika amani na umoja kama familia moja ya Baba yetu, Yehova. (Soma Isaya 11:9.) Wakati tunakuwa na mawazo kama hayo juu ya nizamu ya Yehova, inawezekana kabisa kama tutapendezwa na nizamu hiyo yenye kuonyesha upendo mwingi wenye Mungu iko nao kwetu.

20 Katika habari yenye kufuata, tutazungumuzia mengi zaidi juu ya nizamu katika familia na katika kutaniko. Tutazungumuzia pia kujitia nizamu na pia jambo fulani lenye linaweza kuwa mubaya zaidi kuliko maumivu yoyote ya muda yenye tunaweza kupata wakati tunapewa nizamu.