Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simulizi La Maisha

Nilikuwa Maskini​—Sasa Ni Tajiri

Nilikuwa Maskini​—Sasa Ni Tajiri

Nilizaliwa katika nyumba ya mbao yenye chumba kimoja katika mji mdogo sana unaoitwa Liberty, Indiana, Marekani. Nilipozaliwa tayari wazazi wangu walikuwa na watoto watatu—kaka yangu na dada zangu wawili. Baadaye, ndugu zangu wawili na dada yangu wakazaliwa.

Nyumba ya mbao ambamo nilizaliwa

HAKUKUWA na mabadiliko mengi nilipokuwa shuleni. Katika shule niliyosomea, wanafunzi nilioanza nao shule ndio walewale niliomaliza nao. Isitoshe, ungemjua kwa jina karibu kila mtu katika mji huo, nao pia walifahamu jina lako.

Tulikuwa familia ya watoto saba na nilijifunza mambo mengi kuhusu kilimo nilipokuwa kijana

Mji wa Liberty ulizungukwa na mashamba madogo, na zao kuu lilikuwa mahindi. Nilipozaliwa, Baba alikuwa akifanya kazi katika shamba la mkulima mmoja wa eneo hilo. Nikiwa kijana, nilijifunza kuendesha trekta na pia kufanya mambo mengine ya msingi yaliyohusu kilimo.

Baba yangu hakuwa kijana. Alikuwa na umri wa miaka 56 nilipozaliwa; Mama alikuwa na umri wa miaka 35. Hata hivyo, Baba alikuwa mwanamume mwembamba mwenye afya na nguvu nyingi, aliyependa kufanya kazi ngumu na alitufundisha sisi watoto pia tupende kazi. Hakupata pesa nyingi, lakini alihakikisha kwamba tulikuwa na mahali pa kulala, nguo, na chakula—na alitumia wakati mwingi pamoja nasi. Alikuwa na umri wa miaka 93 alipokufa. Mama alikufa akiwa na umri wa miaka 86. Wazazi wangu hawakuwa watumishi wa Yehova. Hata hivyo, mdogo wangu wa kiume ametumikia kwa uaminifu akiwa mzee wa kutaniko tangu mpango huo ulipoanza miaka ya 1970.

MIAKA YANGU YA MAPEMA

Mama yangu alipenda sana dini. Alitupeleka kwenye kanisa la Baptisti kila Jumapili. Nilisikia kuhusu Utatu kwa mara ya kwanza nilipokuwa na umri wa miaka 12. Hivyo, nikamuuliza mama yangu hivi: “Inawezekanaje kwamba Yesu awe Mwana na Baba kwa wakati uleule?” Ninakumbuka alivyonijibu: “Mwanangu, hilo ni fumbo. Hatuwezi kulielewa.” Kwa kweli, hilo lilikuwa fumbo kwangu. Ingawa hivyo, nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilibatizwa katika mto mdogo ambako nilizamishwa mara tatu kwa msingi wa fundisho hilo la Utatu!

1952—Nikiwa na umri wa miaka 17, kabla ya kuandikishwa jeshini

Nilipokuwa katika shule ya sekondari, nilikuwa na rafiki aliyekuwa mwanandondi, ambaye alinishawishi nijifunze mchezo huo. Hivyo nilianza mazoezi, na kujiunga na shirika la ndondi lililoitwa Golden Gloves. Sikufanya vizuri katika mchezo huo, hivyo baada ya mapigano kadhaa niliamua kuacha. Baadaye, niliandikishwa kwenye jeshi la Marekani na kupelekwa Ujerumani. Nikiwa huko, wakubwa wangu walinipeleka kwenye shule ya kijeshi, kwa kuwa walifikiri nilikuwa na kipawa cha kuwa kiongozi mzuri. Walitaka nitumikie nikiwa mwanajeshi maisha yangu yote. Sikuwa na nia ya kuendelea na kazi hiyo, hivyo baada ya kukamilisha miaka miwili katika utumishi huo, waliniruhusu niondoke mwaka wa 1956. Hata hivyo, muda mfupi tu baadaye, nilijiunga na jeshi tofauti kabisa.

1954-1956—Nilitumikia katika Jeshi la Marekani kwa miaka miwili

NAANZA MAISHA MAPYA

Kufikia wakati huu, nilikuwa nimejifunza kuwa mwanamume mshupavu. Niliathiriwa sana na maoni ya jamii na yale yaliyowasilishwa katika sinema kuhusu maana ya kuwa mwanamume halisi. Kulingana na maoni yangu, wanaume waliofanya kazi ya kuhubiri walikuwa dhaifu. Hata hivyo, nilianza kujifunza mambo fulani yaliyofanya maisha yangu yabadilike kabisa. Siku moja, nilipokuwa nikiendesha gari langu jekundu la kifahari katikati ya mji, wasichana wawili walinisimamisha. Niliwafahamu. Walikuwa wadogo wa kike wa mwanamume aliyekuwa amemwoa dada yangu. Kwa ufupi, wasichana hao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Hapo awali walikuwa wamenipa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, lakini kwa ujumla nilihisi kwamba gazeti la Mnara wa Mlinzi lilikuwa gumu sana kwangu kueleweka. Hata hivyo, wakati huu walinialika nihudhurie mkutano wa Funzo la Kitabu la Kutaniko, ambao ulikuwa mkutano mdogo wa kujifunza na kuzungumzia Biblia uliofanywa nyumbani kwao. Niliwaambia nitafikiria kuhusu jambo hilo. Wakatabasamu na kuniuliza, “Unaahidi?” Nikawaambia “Ndiyo, ninaahidi.”

Nilijutia kiasi fulani kutoa ahadi hiyo, lakini nilihisi kwamba siwezi kuivunja. Hivyo, usiku huo nikahudhuria mkutano, na watoto ndio walionishangaza sana. Nilistaajabu kuona jinsi walivyokuwa na ujuzi mwingi kuhusu Biblia! Licha ya kwenda kanisani Jumapili hizo zote pamoja na mama yangu, bado ujuzi wangu wa Biblia ulikuwa mdogo sana. Sasa niliazimia kujifunza zaidi. Nikakubali kujifunza rasmi Biblia. Mapema nilipoanza kujifunza nilifundishwa kwamba jina la Mungu Mweza Yote ni Yehova. Miaka mingi mapema nilipomuuliza Mama kuhusu Mashahidi wa Yehova, alinijibu hivi: “Ah, hao wanamwabudu mzee fulani anayeitwa Yehova.” Lakini sasa nilianza kuhisi kwamba macho yangu yalikuwa yakifunguliwa!

Nilifanya maendeleo haraka sana kwa sababu nilijua kwamba nimeipata kweli. Haikupita miezi tisa tangu nilipohudhuria mkutano wangu wa kwanza, nami nikabatizwa mwezi wa Machi, 1957. Mtazamo wangu kuhusu maisha ulibadilika. Ninapokumbuka maoni niliyokuwa nayo kuhusu jinsi mwanamume halisi anavyopaswa kuwa, ninafurahi kwamba nilijifunza yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu sifa za mwanamume halisi. Yesu alikuwa mwanamume mkamilifu. Alikuwa na uwezo na nguvu nyingi za kimwili na hakuna mwanamume yeyote anayeweza kulingana naye. Hata hivyo, hakuwahi kupigana, bali “alikubali kuteswa,” kama ilivyotabiriwa. (Isa. 53:2, 7) Nilijifunza kwamba mfuasi wa kweli wa Yesu “anahitaji kuwa mpole kwa wote.”—2 Tim. 2:24.

Mwaka uliofuata, yaani, mwaka wa 1958 nilianza upainia. Hata hivyo, muda mrefu haukupita nikalazimika kuacha upainia kwa muda mfupi. Kwa nini? Niliamua kumwoa Gloria, mmoja wa wale wasichana waliokuwa wamenialika kwenye funzo la kitabu! Sijawahi kamwe kujutia uamuzi huo. Kwangu, Gloria alikuwa kama jiwe la thamani wakati huo, na angali hivyo hadi leo. Yeye ni kama ile almasi maarufu yenye thamani kubwa ijulikanayo kama Hope Diamond, na ninafurahi sana kwamba nilimwoa! Acheni awaeleze mambo machache kujihusu:

“Nilizaliwa katika familia yenye watoto 17. Mama yangu alikuwa Shahidi mwaminifu wa Yehova. Alikufa nilipokuwa na umri wa miaka 14. Wakati huo ndipo Baba alipoanza kujifunza Biblia. Kwa kuwa mama hakuwepo, Baba alifanya mpango fulani na mwalimu mkuu wa shule tuliyosomea. Wakati huo dada yangu alikuwa katika mwaka wake wa mwisho kwenye shule hiyo ya sekondari, hivyo Baba alimwomba mwalimu mkuu ikiwa mimi na dada yangu tungeenda shuleni kwa zamu. Tulifanya hivyo ili angalau mmoja wetu abaki nyumbani kuwatunza wadogo zetu na kutayarisha chakula cha usiku kabla Baba hajarudi kutoka kazini. Mwalimu mkuu alikubali kufanya hivyo, na mpango huo uliendelea hadi dada yangu alipohitimu shule. Familia mbili za Mashahidi zilijifunza Biblia pamoja nasi, na watoto 11 katika familia yetu tukawa Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia sana utumishi wa shambani ingawa mimi ni mwenye haya sana. Kwa miaka hiyo yote, mume wangu Sam amenisaidia kukabiliana na hali hiyo.”

Mimi na Gloria tulifunga ndoa mwezi wa Februari, 1959. Tulifurahia kufanya upainia pamoja. Mwezi wa Julai mwaka huo, tulijaza fomu ya utumishi wa Betheli, kwa sababu tulitamani sana kutumikia katika makao makuu ya ulimwenguni pote. Ndugu mpendwa anayeitwa, Simon Kraker, alituhoji. Alituambia kwamba kwa wakati huo Betheli haikuwa ikiwapokea wenzi wa ndoa. Tamaa yetu ya kutumikia Betheli haikufifia lakini tulihitaji kusubiri kwa muda mrefu!

Tuliandika barua kwa makao makuu ya ulimwenguni pote, tukiomba watupatie mgawo wa kwenda kutumikia katika eneo lenye uhitaji. Walitupatia chaguo moja tu: Pine Bluff, Arkansas. Siku hizo kulikuwa na makutaniko mawili tu huko Pine Bluff—moja la ndugu weupe na lingine la ndugu weusi. Tulitumwa kwenye kutaniko la ndugu weusi, lililokuwa na wahubiri 14 tu.

KUKABILIANA NA UBAGUZI WA RANGI

Huenda ukashangaa ni kwa nini hata akina ndugu weusi na weupe katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova hawakuwa wakichangamana. Kwa ufupi, hakukuwa na namna nyingine siku hizo isipokuwa kufanya hivyo. Kulikuwa na sheria zilizowakataza watu wa jamii hizo mbili kuchangamana, na kulikuwa pia na tishio la kutendewa kikatili ikiwa sheria hizo zingekiukwa. Katika maeneo mengi, akina ndugu walikuwa na sababu nzuri ya kuogopa kwamba Jumba lao la Ufalme lingeharibiwa ikiwa ndugu wa jamii hizo mbili wangekutanika pamoja kwa ajili ya ibada. Visa kama hivyo vilitokea. Ikiwa Mashahidi weusi wangehubiri nyumba kwa nyumba katika eneo la watu weupe, wangekamatwa na hata labda kupigwa. Hivyo, ili kazi ya kuhubiri isonge mbele, tulitii sheria hizo tukitumaini kwamba mambo yangebadilika.

Tulikabili changamoto mbalimbali katika huduma yetu. Nyakati nyingine tulipokuwa tukihubiri katika eneo la watu weusi, bila kutarajia tulibisha hodi kwenye nyumba ya familia ya watu weupe. Mara moja tulihitaji kufanya uamuzi ikiwa tungezungumzia kifupi andiko moja au tungekiri kosa letu na kuondoka. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa katika maeneo mengine siku hizo.

Bila shaka tulihitaji kufanya kazi kwa bidii ili tujitegemeze tukiwa mapainia. Malipo tuliyopokea kwa kazi mbalimbali tulizofanya yalikuwa dola tatu kwa siku. Gloria alifanya kazi ya kuwasafishia watu nyumba. Familia moja iliniruhusu nimsaidie ili tumalize kazi mapema. Tulipewa chakula cha mchana kilichokusudiwa kiwe cha mtu mmoja, lakini mimi na Gloria tuligawana na kula kabla ya kuondoka. Na kila juma Gloria alipiga pasi nguo za familia fulani. Nilifanya kazi ya kutunza bustani, kusafisha madirisha, na kazi nyingine za mikono. Katika familia moja ya watu weupe, Gloria alisafisha madirisha upande wa ndani, nami upande wa nje. Tulifanya kazi hiyo kwa siku nzima, hivyo tulipewa chakula cha mchana. Gloria alikula chakula chake ndani ya nyumba lakini hakuketi pamoja na familia hiyo, nami nililia chakula changu nje kwenye banda la kuegeshea gari. Sikujali. Kilikuwa chakula kitamu sana. Familia hiyo ilikuwa yenye urafiki ingawa walikuwa wameathiriwa na mfumo huo na njia hiyo ya kufikiri. Ninakumbuka wakati mmoja tulipokwenda kwenye kituo kimoja cha mafuta. Baada ya kujaza gari letu mafuta, nilimwomba mhudumu amruhusu Gloria atumie choo chao. Alinitazama kwa ukali na kusema, “Kimefungwa.”

MATENDO YA FADHILI AMBAYO HATUTASAHAU

Kwa upande mwingine, tulikuwa na pindi zenye kufurahisha pamoja na akina ndugu, na tulifurahia huduma yetu! Tulipowasili kwa mara ya kwanza huko Pine Bluff, tulikaa kwa ndugu mmoja ambaye alikuwa mtumishi wa kutaniko wakati huo. Mke wake hakuwa Shahidi, hivyo Gloria akaanza kujifunza Biblia pamoja naye. Wakati huohuo, nilianza kujifunza Biblia na binti yao pamoja na mume wake. Binti huyo pamoja na mama yake wakaamua kuwa watumishi wa Yehova na kubatizwa.

Tulikuwa na marafiki tuliowapenda katika kutaniko la ndugu weupe. Walizoea kutukaribisha kwa ajili ya chakula cha jioni, lakini walilazimika kufanya hivyo giza lilipoingia. Kundi la KKK (Ku Klux Klan) linalochochea ubaguzi wa rangi na ukatili, lilikuwa lenye nguvu sana wakati huo. Ninakumbuka nikimwona mwanamume mmoja akiwa ameketi nje barazani usiku wa Halloween akiwa amevaa mavazi meupe na kofia iliyomfunika hadi usoni, kama wafuasi wa KKK walivyovalia. Ingawa hali zilikuwa hivyo, akina ndugu hawakuacha kuonyesha ukarimu. Pindi moja wakati wa majira ya kiangazi, tulihitaji pesa ili tusafiri kwenda kwenye kusanyiko, na ndugu mmoja alikubali kununua gari letu aina ya Ford la mwaka wa 1950 ili tupate nauli. Siku moja, mwezi mmoja baadaye, tulikuwa tumechoka sana baada ya kuhubiri nyumba kwa nyumba kwenye joto kali la kiangazi na kuongoza mafunzo ya Biblia. Lakini tulipofika nyumbani tulikuta jambo lililotufurahisha sana. Gari letu lilikuwa limeegeshwa mbele ya nyumba yetu! Kulikuwa na karatasi kwenye kioo cha gari iliyokuwa na ujumbe huu: “Nimewarudishia gari lenu ikiwa zawadi kutoka kwangu. Ni mimi ndugu yenu.”

Kuna tendo lingine la fadhili ambalo siwezi kamwe kusahau. Mwaka wa 1962, nilialikwa kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme huko South Lansing, New York. Ilikuwa shule iliyofanywa kwa mwezi mzima ambayo iliwapa mazoezi wale waliosimamia makutaniko, mizunguko, na wilaya. Hata hivyo nilipopokea mwaliko, sikuwa na kazi wala pesa. Lakini kampuni moja ya simu huko Pine Bluff ilikuwa imenihoji kwa ajili ya kazi. Ikiwa wangeniajiri, ningekuwa mtu wa kwanza mweusi kufanya kazi katika kampuni hiyo. Hatimaye waliniambia kwamba wataniajiri. Ningefanyaje? Sikuwa na pesa za kwenda New York. Nilikuwa karibu kukubali kazi hiyo na kukataa mwaliko wa kuhudhuria shule. Hata nilikuwa nikijiandaa kuandika barua ya kukataa mwaliko huo, jambo fulani ambalo sitawahi kusahau lilipotokea.

Dada mmoja kutanikoni, ambaye mume wake hakuwa Shahidi, alibisha hodi mlangoni kwetu mapema asubuhi moja na kunikabidhi bahasha. Ilikuwa imejaa pesa. Yeye pamoja na watoto wake kadhaa wadogo walikuwa wakiamka mapema sana asubuhi na kwenda kung’oa magugu kwenye mashamba ya pamba ili wapate pesa za kutosha kugharimia nauli yangu ya kwenda New York. Aliniambia hivi: “Nenda kwenye shule hiyo, ujifunze kadiri uwezavyo, kisha uje utufundishe!” Baadaye, niliiomba kampuni hiyo ya simu waniruhusu nianze kazi baada ya majuma matano, tofauti na walivyotaka. Walinijibu moja kwa moja, “Hapana!” Lakini sikujali. Nilikuwa nimefanya uamuzi tayari. Ninafurahi sana kwamba sikukubali kazi hiyo!

Gloria anasema hivi kuhusu wakati tuliokuwa pamoja huko Pine Bluff: “Nilipenda sana kuhubiri katika eneo hilo! Niliongoza mafunzo 15 hadi 20 ya Biblia. Tungeenda nyumba kwa nyumba asubuhi, kisha tungeongoza mafunzo ya Biblia mchana, na nyakati nyingine tulifanya hivyo hadi saa 5 usiku. Utumishi ulikuwa wenye kufurahisha sana! Nilitamani sana kuendelea kuhubiri katika eneo hilo. Lazima nikiri kwamba sikutaka kubadili mgawo huo na kuingia katika kazi ya kuzungukia makutaniko, lakini Yehova alikuwa na mpango mwingine.” Na hilo ni kweli kabisa.

MAISHA NIKIWA MWANGALIZI WA MZUNGUKO

Tulipokuwa mapainia huko Pine Bluff, tuliomba kutumikia tukiwa mapainia wa pekee. Tulikuwa na matumaini makubwa ya kuwa mapainia wa pekee kwa sababu mwangalizi wetu wa wilaya alitaka tusaidie kutaniko fulani huko Texas tukiwa mapainia wa pekee. Wazo la kuwa mapainia wa pekee lilitufurahisha sana. Hivyo tuliendelea kusubiri na kusubiri, tukitumaini kupata jibu kutoka kwa Sosaiti, lakini hatukupokea barua yoyote. Hatimaye, barua ilikuja—tulipokea mgawo wa kutumikia katika kazi ya kuzungukia makutaniko! Ilikuwa Januari mwaka wa 1965. Ndugu Leon Weaver, ambaye sasa anatumikia akiwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, aliwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko wakati huohuo pia.

Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kuwa mwangalizi wa mzunguko. Mwaka mmoja hivi mapema, mwangalizi wa wilaya, James A. Thompson, Jr., alichunguza ikiwa nilikuwa na sifa za kustahili. Alinionyesha kwa fadhili mambo ambayo nilihitaji kufanyia kazi na akataja sifa ambazo mwangalizi mzuri wa mzunguko anahitaji kuwa nazo. Nilikuwa nimetumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko kwa muda mfupi tu nilipotambua kwamba kwa kweli nilihitaji kutumia shauri lake. Nilipowekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko, Ndugu Thompson ndiye aliyekuwa mwangalizi wa kwanza wa wilaya niliyefanya kazi naye. Nilijifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu huyo mwaminifu na wa kiroho.

Ninathamini msaada niliopokea kutoka kwa ndugu waaminifu wa kiroho

Siku hizo mwangalizi wa mzunguko hakupata mazoezi mengi. Nilitazama kwa juma moja jinsi mwangalizi wa mzunguko alivyokuwa akifanya ziara alipotembelea kutaniko. Kisha juma lililofuata alitazama jinsi nilivyofanya ziara katika kutaniko lililofuata. Alinipa mwongozo na mapendekezo. Lakini baada ya hapo tuliachwa peke yetu. Ninakumbuka nikimwambia Gloria, “Kwani ni lazima atuache sasa hivi?” Hata hivyo, baada ya muda nilitambua jambo fulani muhimu. Sikuzote kutakuwa na ndugu wazuri wanaoweza kukusaidia—ikiwa utawaruhusu wakusaidie. Ningali nathamini sana msaada niliopokea kutoka kwa ndugu wazoefu kama J. R. Brown, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko wakati huo, na Fred Rusk wa familia ya Betheli.

Ubaguzi wa rangi ulikuwa umeenea sana siku hizo. Wakati fulani, kundi la KKK lilifanya maandamano katika mji tuliokuwa tukizuru huko Tennessee. Ninakumbuka siku moja wakati kikundi chetu cha utumishi kilipoenda kwenye mkahawa fulani. Nilipokuwa nikienda chooni, nilitambua kwamba mwanamume mmoja mwenye sura ya kutisha alikuwa akinifuata. Alikuwa amechanjwa chale kama mfuasi wa kikundi kilichoendeleza sera zilizotukuza watu weupe. Lakini ndugu mmoja mweupe aliyekuwa na umbo kubwa kuliko mimi na aliyemzidi pia kwa umbo yule mwanamume, alitufuata. Kisha akaniuliza, “Uko sawa Ndugu Herd?” Mwanamume huyo aliondoka mara moja bila kutumia choo. Kadiri miaka ilivyopita, nimekuja kutambua kwamba chanzo cha ubaguzi si rangi ya ngozi, bali ni dhambi, yaani, dhambi ya Adamu inayotuathiri sisi sote. Na nimejifunza kwamba ndugu ni ndugu tu haijalishi rangi ya ngozi yake, na anaweza kufa kwa ajili yako hali ikilazimu.

MWISHO WENYE UTAJIRI

Tulizungukia makutaniko kwa miaka 33, na 21 kati ya hiyo nikiwa mwangalizi wa wilaya. Ilikuwa miaka iliyojaa baraka na thawabu nyingi, na mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo. Hata hivyo, thawabu nyingine ilikuwa njiani. Mwezi wa Agosti 1997, ndoto yetu ya muda mrefu ilitimia. Tulialikwa kutumikia katika Betheli ya Marekani—miaka 38 hivi tangu tulipojaza ombi letu la kwanza. Mwezi uliofuata tulianza utumishi wetu wa Betheli. Nilidhani kwamba ndugu waliosimamia kazi Betheli walitaka nisaidie kazi kwa muda mfupi tu, lakini mambo hayakwenda hivyo.

Gloria alikuwa kama jiwe la thamani wakati huo, na angali hivyo hadi leo

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa kwenye Idara ya Utumishi. Nilijifunza mambo mengi. Akina ndugu katika idara hiyo hushughulikia maswali magumu na yenye kutatanisha kutoka kwa mabaraza ya wazee na waangalizi wa mzunguko nchini pote. Nilithamini jinsi ndugu hao walivyonisaidia na kuonyesha sifa ya subira walipokuwa wakinizoeza. Ingawa hivyo, ninahisi kwamba ikiwa ningepewa mgawo huo tena bado ningehitaji kujifunza mengi.

Mimi na Gloria tunapenda maisha ya Betheli. Sikuzote tumekuwa na zoea la kuamka mapema, na hilo ni zoea zuri sana katika maisha ya Betheli. Mwaka mmoja hivi baadaye, nilianza kutumikia nikiwa msaidizi wa Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Kisha katika mwaka wa 1999, niliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Mgawo huo umenifunza mambo mengi, lakini jambo muhimu zaidi nililojifunza ni kujionea waziwazi kwamba Yesu Kristo—na si mwanadamu yeyote—ndiye kichwa cha kutaniko la Kikristo.

Tangu mwaka wa 1999, nimepata pendeleo la kutumikia kwenye Baraza Linaloongoza

Ninapotafakari kuhusu maisha yangu, nyakati nyingine mimi huhisi kama nabii Amosi. Yehova alimwona mchungaji huyo wa hali ya chini aliyefanya kazi duni ya kuchanja tini za mikuyu—chakula kilichoonwa kuwa cha watu maskini. Mungu alimweka Amosi kuwa nabii, mgawo wenye kutajirisha kiroho. (Amo. 7:14, 15, maelezo ya chini) Vivyo hivyo, Yehova aliniona mimi, mwana wa mkulima maskini kutoka mji wa Liberty, Indiana, naye akanimiminia baraka zake zenye kutajirisha—nyingi sana hivi kwamba siwezi kuziorodhesha zote! (Met. 10:22) Ingawa nilikuwa maskini, sasa mimi ni tajiri kiroho, nimetajirika kuliko jinsi ambavyo ningeliweza kuwazia!