Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Mwanzo Wenye Umaskini Lakini Mwisho Wenye Utajiri

Mwanzo Wenye Umaskini Lakini Mwisho Wenye Utajiri

Nilizaliwa katika nyumba ndogo ya miti yenye ilikuwa na chumba kimoja katika muji mudogo wenye kuitwa Liberty, katika Indiana, Amerika. Tayari wazazi wangu walikuwa na watoto tatu wakati nilizaliwa, ni kusema, kaka yangu mukubwa na dada zangu wawili. Kisha, mama yangu alizaa wadogo wangu wawili wanaume na dada yangu mudogo mumoja.

Nyumba ya miti ambamo nilizaliwa

WAKATI nilikuwa ninasoma, mambo mengi hayakubadilika. Kwenye masomo yetu, watu wenye ulikuwa nao katika somo la kwanza ndio walewale wenye ulimaliza nao masomo; mutu alijua majina ya watu wengi katika muji na wao pia walijua jina lako.

Nilikuwa kati ya watoto saba na nilijifunza mambo mengi juu ya kazi ya kulima wakati nilikuwa kijana

Muji wa Liberty ulikuwa unazungukwa na mashamba madogo-madogo, na watu walizoea sana kupanda mahindi. Wakati nilizaliwa, baba yangu alikuwa anatumikia mutu mumoja wa eneo hilo mwenye alikuwa na mashamba. Wakati nilikuwa kijana, nilijifunza kutembeza motokari ya kulima na nikajua ufundi mwingine wa musingi juu ya mambo ya kulima.

Baba yangu hakukuwa kijana wakati nilizaliwa. Alikuwa na miaka 56 na mama yangu alikuwa na miaka 35. Hata hivyo baba yangu alikuwa mwembamba, mwenye afya ya muzuri, mwenye nguvu na mwenye alipenda kutumika sana na alitufundisha sisi watoto wake wote kufanya hivyo. Hakupata feza nyingi, lakini sikuzote alitutolea mahali pa kuishi, nguo za kuvaa na chakula; na sikuzote alikuwa tayari kutusaidia. Alikuwa na miaka 93 wakati alikufa. Na mama yangu alikuwa na miaka 86 wakati alikufa. Wote hawakumutumikia Yehova. Kati ya ndugu zangu, mudogo yangu mumoja amekuwa muzee wa kutaniko muaminifu tangu wakati mupango huo ulianza katika miaka ya 1970.

WAKATI NILIKUWA KIJANA

Mama yangu alikuwa anapenda sana mambo ya dini. Alikuwa anatubeba kwenye kanisa la Wabatiste kila Siku ya Yenga. Wakati nilikuwa na miaka 12, nilisikia kwa mara ya kwanza fundisho la Utatu. Kwa sababu nilipenda kujua zaidi, niliuliza mama yangu hivi: “Namna gani Yesu anaweza kuwa Mwana na Baba kwa wakati mumoja?” Ninakumbuka jibu lenye alitoa, aliniambia hivi: “Mutoto wangu, hiyo ni fumbo. Hatuwezi kuelewa jambo hilo.” Ilikuwa kabisa fumbo kwangu. Hata hivyo, wakati nilikuwa na miaka 14, nilibatizwa katika mutoni wenye ulikuwa katika eneo letu; nilitumbukizwa katika maji mara tatu kwa sababu ya fundisho la Utatu!

1952 Wakati nilikuwa na miaka 17, mbele niandikishwe katika jeshi

Wakati nilikuwa kwenye masomo ya segondere, nilikuwa na rafiki fulani mwenye alikuwa anacheza muchezo wa kupigana ngumi ili kupata feza, na alinisadikisha nianze kucheza muchezo huo. Kwa hiyo, nilianza kufanya mazoezi na nilijiandikisha katika kikundi fulani cha wapiganaji wa ngumi chenye kuitwa Golden Gloves. Sikuweza muchezo huo; kwa hiyo, kisha michezo fulani, niliacha. Kisha niliandikishwa katika Jeshi la Amerika na nilitumwa Ujerumani. Wakati nilikuwa ninatumikia huko, wakubwa wangu walinituma kwenye Masomo ya Maofisa kwa sababu waliwaza kama nilikuwa na uwezo wa kizalikio wa kuongoza. Walipenda nifanye kazi ya jeshi katika maisha yangu yote. Sikukuwa ninapenda kubakia katika jeshi; kwa hiyo, kisha kumaliza miaka yangu mbili ya kutumika katika jeshi, niliruhusiwa kuondoka katika jeshi kwa heshima katika mwaka wa 1956. Lakini kisha muda mufupi nilijiunga na jeshi lingine lenye kuwa tofauti kabisa.

1954-1956 Nilifanya miaka mbili katika Jeshi la Amerika

MAISHA MAPYA YANAANZA

Kufikia wakati huo katika maisha yangu, nilikuwa na mawazo ya mubaya juu ya namna mwanaume anapaswa kuwa kabisa. Nilichochewa sana na mawazo yenye yalionyeshwa katika filme na mawazo ya watu wengi juu ya namna mwanaume anapaswa kuwa. Nilikuwa ninawaza kama, wale wenye kuzungumuza juu ya Biblia hawakukuwa wanaume kabisa. Lakini nilianza kujifunza mambo fulani yenye yalibadilisha maisha yangu. Siku moja, wakati nilikuwa ninatembeza katika muji motokari yangu ya mwekundu, vijana wawili wanawake walinipepea. Nilikuwa ninawajua, walikuwa dada wadogo wa mwanaume mwenye alikuwa ameoa dada yangu kubwa. Vijana hao wawili wanawake walikuwa Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa nimekubali magazeti ya Munara wa Mulinzi na Amuka! yenye walikuwa wamenipatia mbele ya hapo, hata hivyo, niliwaza kama ilikuwa vigumu kwangu kuelewa Munara wa Mulinzi. Lakini sasa, walinialika kufika kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko, mukutano mudogo wa kujifunza Biblia na mazungumuzo wenye ulifanywa katika nyumba yao. Niliwaambia kama ningefikiria jambo hilo. Vijana hao wanawake waliniuliza hivi kwa sura ya kicheko: “Utafikiria kabisa jambo hilo?” Niliwajibia hivi: “Nitalifikiria kabisa.”

Nilijuta kidogo juu ya ahadi hiyo yenye nilitoa, lakini nilijisikia kama nilipaswa kuitimiza. Kwa hiyo, usiku huo nilienda kwenye mukutano huo. Watoto walinishangaza sana. Sikuweza kuamini kuona namna wanajua mambo mengi sana juu ya Biblia! Hata kama zamani nilikuwa ninaenda kwenye kanisa kila Siku ya Yenga pamoja na mama yangu, nilijua tu mambo madogo sana juu ya Biblia. Sasa nilikuwa nimeazimia kujifunza mambo mengi zaidi. Nilikubali kujifunza Biblia. Mwanzoni nilijifunza kama jina la pekee la Mungu Mweza Yote ni Yehova. Miaka fulani mbele ya hapo, wakati niliuliza mama yangu juu ya Mashahidi wa Yehova, aliniambia tu hivi: “Oh, wanaabudu mwanaume fulani mwenye kuzeeka mwenye kuitwa Yehova.” Lakini sasa nilijisikia kama macho yangu yalikuwa yanafunguliwa!

Nilifanya maendeleo haraka, kwa sababu nilijua kama nimepata kweli. Miezi kenda kisha kuhuzuria mukutano wa kwanza, nilibatizwa katika Mwezi wa 3, 1957. Mawazo yangu juu ya maisha yalibadilika. Wakati ninakumbuka mawazo yenye nilikuwa nayo juu ya kuwa mwanaume, ninafurahi kwa sababu nilijifunza mambo yenye Biblia inafundisha juu ya maana ya kuwa mwanaume kabisa. Yesu alikuwa mwanaume mukamilifu. Alikuwa na nguvu na uwezo wa kimwili wenye ungefanya mutu yeyote mwenye kujiona kuwa ‘mwanaume kabisa’ aonekane kuwa wa bure mbele yake. Hata hivyo, hakujiingiza katika mapigano, lakini “alijiachilia ateswe,” kama vile tu ilikuwa imetabiriwa. (Isa. 53:2, 7) Nilijifunza kama mwanafunzi wa kweli wa Yesu ‘anahitaji kuwa mupole kwa wote.’​—2 Tim. 2:24.

Nilianza kufanya kazi ya upainia mwaka wenye ulifuata, katika mwaka wa 1958. Lakini, kisha muda mufupi, nilipaswa kusimamisha upainia kwa muda mufupi. Sababu gani? Nilikuwa nimeamua kuoa Gloria, mumoja kati ya vijana hao wanawake wenye walinialika kwenye funzo la kitabu! Sijajuta hata kidogo juu ya uamuzi huo. Gloria alikuwa mutu wa maana sana wakati huo, na anaendelea kuwa wa maana sana hata leo. Ninamuona kuwa wa maana sana kuliko almasi, na ninafurahi sana kwa sababu nilimuoa. Muache yeye mwenyewe awaelezee mambo fulani juu yake:

“Nilikuwa kati ya watoto 17. Mama yangu alikuwa Shahidi muaminifu. Alikufa wakati nilikuwa na miaka 14. Huo ndio wakati baba yangu alianza kujifunza. Kwa sababu Mama yangu alikuwa amekufa, Baba yangu alifanya mipango pamoja na musimamizi wa masomo. Dada yangu mukubwa alikuwa katika darasa la mwisho la masomo ya segondere na Baba aliomba ikiwa mimi naye tunaweza kuenda kwenye masomo katika siku tofauti. Tulikuwa tunabadilishana siku ya kuenda kwenye masomo ili mumoja wetu achunge watoto wadogo na kutayarisha chakula cha mangaribi kwa ajili ya familia ili kikuwe tayari wakati Baba atatoka kwenye kazi. Musimamizi wa masomo alikubali, na mupango huo uliendelea mupaka wakati dada yangu alimaliza masomo. Familia mbili za Mashahidi zilijifunza pamoja na sisi, na watoto 11 kati yetu tulifikia kuwa Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia kazi ya kuhubiri, hata kama sikuzote nimekuwa na tatizo la kusikia haya. Kwa miaka mingi, Sam amenisaidia juu ya jambo hilo.”

Mimi na Gloria tulioana katika Mwezi wa 2, mwaka wa 1959. Tulifurahia kufanya pamoja kazi ya upainia. Katika Mwezi wa 7 mwaka huo, tulijaza ombi la kutumika kwenye Beteli, kwa sababu tulikuwa tunapenda kutumikia kwenye makao yetu makubwa. Ndugu mupendwa, Simon Kraker, alizungumuza na sisi. Alituambia kama wakati huo wale wenye wamekwisha kuoana hawakukuwa wanakubaliwa kwenye Beteli. Hatukupoteza hata kidogo tamaa yetu ya kutumikia kwenye Beteli, lakini kulipita miaka mingi mbele tuingie kwenye Beteli!

Tuliandikia makao yetu makubwa na kuomba tutumwe ili kutumikia mahali kwenye kulikuwa lazima kubwa ya wahubiri. Tulipata jibu la kuenda kutumikia tu katika Pine Bluff, Arkansas. Katika siku hizo, kulikuwa makutaniko mbili katika Pine Bluff, ni kusema, moja la wazungu na lingine la weusi. Tulitumwa katika kutaniko la watu weusi, lenye lilikuwa tu na wahubiri 14 hivi.

KUPAMBANA NA MUGAWANYIKO NA UBAGUZI WA RANGI YA NGOZI

Unaweza kujiuliza sababu gani kulikuwa mugawanyiko katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Kwa kifupi, jibu ni kwamba, hakukuwa namna ingine ya kufanya wakati huo. Wakati huo kulikuwa sheria zenye zilikataza watu wa rangi tofauti ya ngozi kukusanyika pamoja mahali pa watu wengi kama vile katika nafasi za kufanyia ibada, na kulikuwa pia hatari kabisa ya kutendewa kwa jeuri. Katika mahali mbalimbali, ndugu walikuwa na sababu za muzuri za kuogopa kama ikiwa watu wa rangi tofauti ya ngozi wangekusanyika pamoja ili kuabudu, Jumba lao la Ufalme lingeharibiwa. Mambo hayo yalitokea kabisa. Ikiwa Mashahidi weusi wangehubiri nyumba kwa nyumba katika eneo la wazungu, wangefungwa na pengine kupigwa. Kwa hiyo, ili tuendelee kufanya kazi ya kuhubiri, tulitii sheria hizo, na kutumaini kama mambo yangebadilika na kuwa muzuri zaidi.

Tulipata magumu fulani katika kazi ya kuhubiri. Wakati tulikuwa tunahubiri katika eneo la watu weusi, wakati fulani tuligonga bila kujua kwenye milango ya familia za wazungu. Tulipaswa kuamua ikiwa tungejaribu kuzungumuza nao kwa kifupi juu ya Maandiko ao kuomba musamaha na kuondoka. Katika mahali fulani, mambo yalikuwa hivyo katika siku hizo.

Kwa kweli, tulipaswa kutumika sana ili kutimiza mahitaji yetu ya kimwili wakati tulikuwa tunafanya kazi yetu ya upainia. Kwenye kazi nyingi zenye tulifanya, tulilipwa dola tatu kwa siku. Gloria alitumika katika nyumba fulani za watu. Nilikuwa ninaruhusiwa kumusaidia kwenye nyumba fulani ili amalize kazi mbele ya wakati. Tulipewa chakula cha muchana chenye tulikula mimi na Gloria mbele tuondoke. Kila juma, Gloria alikuwa anafanya kazi ya kupiga manguo pasi kwa ajili ya familia moja. Mimi nilitumika katika bustani, nilisafisha madirisha, na kufanya kazi zingine za inje ya nyumba. Katika nyumba ya familia moja ya wazungu, tulisafisha madirisha; Gloria alisafisha madirisha kwa ndani, na mimi niliyasafisha kwa inje. Tulifanya kazi hiyo muchana muzima, kwa hiyo, tulipewa chakula cha muchana. Gloria alikulia katika nyumba, lakini hapana pamoja na familia hiyo, na miye nilikulia katika nafasi ya kuwekea motokari. Jambo hilo halikunihangaisha. Kilikuwa chakula kizuri sana. Familia hiyo ilikuwa ya muzuri; walikuwa tu wamefungwa na mupango huo, namna hiyo ya kufikiri. Ninakumbuka wakati fulani tulisimama mahali pa kuuzia mafuta ya motokari. Kisha kujaza mafuta tanki ya motokari yetu, niliuliza mutu mwenye alikuwa anatumika hapo ikiwa Gloria angeweza kutumia choo ao W.C yenye ilikuwa hapo. Aliniangalia tu na kusema, “Inafungwa.”

MATENDO YA MUZURI YENYE TUNAENDELEA KUKUMBUKA

Kwa upande mwingine, tulipitisha wakati muzuri sana pamoja na ndugu zetu, na tulipenda sana kazi yetu ya kuhubiri! Wakati tulifika kwa mara ya kwanza katika Pine Bluff, tuliishi kwa ndugu mumoja mwenye alikuwa mutumishi wa kutaniko wakati huo. Wakati huo, bibi yake hakukuwa Shahidi, na Gloria alianza kujifunza Biblia pamoja naye. Wakati huohuo, nilianza kujifunza na mutoto wao mwanamuke pamoja na bwana yake. Mama na mutoto wake mwanamuke waliamua kumutumikia Yehova na wakabatizwa.

Tulikuwa na marafiki wapendwa katika kutaniko la wazungu. Walikuwa wanatualika ili tukule pamoja nao chakula cha mangaribi, lakini walipaswa kufanya hivyo bila watu kujua. Kikundi cha Ku Klux Klan (KKK), chenye kilichochea ubaguzi wa rangi ya ngozi na jeuri kilikuwa kinatumika sana wakati huo. Ninakumbuka siku moja ya Halowini, mwanaume mumoja alikuwa anakaa mbele ya veranda yake, na alijivunia kuvaa kitambaa ya mweupe na kofia ya kikundi hicho cha KKK. Hata hivyo, mambo kama hayo hayakuzuia ndugu kuonyeshana wema. Wakati fulani, tulikuwa na lazima ya feza za kutusaidia kufanya safari ya kuenda kwenye mukusanyiko, na ndugu fulani alikubali kuuza motokari yetu ili tuweze kufanya safari hiyo. Kisha kupita mwezi moja, siku moja tulikuwa wenye kuchoka kisha kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuongoza mafunzo ya Biblia wakati wa kipindi cha joto. Kisha tulirudia nyumbani kwetu na tuliona jambo lenye lilitushangaza. Motokari yetu ilikuwa hapo, mbele ya nyumba yetu! Kulikuwa barua kwenye kioo cha mbele yenye kusema hivi: “Ninawarudishia motokari yenu, ni zawadi yenye ninawapatia. Ndugu yenu.”

Siwezi kusahau tendo lingine la wema lenye niliona. Katika mwaka wa 1962, nilialikwa ili kusoma Masomo ya Huduma ya Ufalme katika South Lansing, New York. Ilikuwa masomo ya mwezi muzima wa mazoezi kwa ajili ya wale wenye kusimamia makutaniko, mizunguko, na wilaya. Lakini, wakati nilipata mualiko, sikukuwa na kazi na nilikuwa na magumu ya kupata feza. Hata hivyo, kompanyi moja ya telefone katika Pine Bluff ilikuwa imezungumuza na mimi ili kunipatia kazi. Ikiwa wangenipatia kazi hiyo, ningekuwa mutu mweusi wa kwanza kutumika katika kompanyi hiyo. Mwishowe waliniambia kama watanipatia kazi. Ningefanya nini? Sikukuwa na feza za kulipa safari ya kuenda New York. Nilifikiria sana juu ya kukubali kazi hiyo na kukataa mualiko wa masomo hayo. Kwa kweli, nilikuwa karibu kuandika barua ya kukataa mualiko huo wakati jambo fulani lilitokea, jambo lenye siwezi kusahau hata kidogo.

Siku moja asubui sana dada mumoja wa kutaniko letu, mwenye alikuwa na bwana mwenye hakukuwa Shahidi, aligonga kwenye mulango wetu na kunipatia bahasha (enveloppe) moja. Ilikuwa inajaa feza. Yeye na watoto wake walikuwa wanaamuka kila asubui sana ili kuenda kutumika katika mashamba ya pamba, walikuwa wanaongoa majani yenye kuota katikati ya miti ya pamba ili wapate feza za kutosha za kunisaidia kufanya safari ya kuenda New York. Alisema hivi: “Uende kwenye masomo na ujifunze mambo mengi, na urudie na kutufundisha!” Kisha, niliomba kompanyi hiyo ya telefone ikiwa ninaweza kuanza kutumika kisha juma tano kuliko namna ilikuwa imepangwa. Jibu lao lilikuwa “Hapana!” walikataa kabisa-kabisa. Lakini jambo hilo halikunihangaisha. Nilikuwa nimekamata uamuzi wangu. Ninafurahi sana kwa sababu sikukubali kazi hiyo!

Gloria anakumbuka mambo haya juu ya wakati wenye tulifanya katika Pine Bluff: “Nilipenda sana eneo hilo! Nilikuwa na mafunzo ya Biblia 15 mupaka 20. Tulikuwa tunaenda katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba asubui na kisha tuliongoza mafunzo ya Biblia katika saa zenye kubakia katika siku, wakati fulani mupaka saa 5 kamili ya usiku. Kazi ya kuhubiri ilikuwa yenye kufurahisha sana! Ningefurahia kubakia katika kazi hiyo. Ninapaswa kukubali kama sikupenda kabisa kubadilisha mugawo wangu ili kuanza kufanya kazi ya muzunguko, lakini Yehova alikuwa na jambo lingine katika mawazo yake.” Bila shaka alikuwa na mawazo mengine.

MAISHA KATIKA KAZI YA KUSAFIRI

Wakati tulikuwa tunafanya kazi ya upainia katika Pine Bluff, tulijaza ombi la kuwa mapainia wa pekee. Tulitumainia sana jambo hilo kwa sababu mwangalizi wetu wa wilaya alipenda tusaidie katika kutaniko moja katika Texas, na alipenda tuende huko tukiwa mapainia wa pekee. Tulifurahia sana kufanya mabadiliko hayo. Kwa hiyo, tulingojea sana jibu kutoka kwenye makao yetu makubwa, lakini kila wakati hatukupata barua katika kisanduku cha barua. Mwishowe, siku moja barua ilifika, tulitumwa katika kazi ya kusafiri! Ilikuwa katika Mwezi wa 1 mwaka wa 1965. Ndugu Leon Weaver, mwenye kuwa sasa muratibu wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika, aliwekwa pia kuwa mwangalizi wa muzunguko wakati huohuo.

Niliogopa kuwa mwangalizi wa muzunguko. Mwaka moja hivi mbele ya hapo, mwangalizi wa wilaya, James A. Thompson, alikuwa amenichunguza ili kuona ikiwa ninastahili. Alinionyesha kwa upole mambo mbalimbali yenye nilipaswa kufanyia maendeleo, alitaja ufundi wenye mwangalizi muzuri wa muzunguko anapaswa kuwa nao. Kisha kufanya muda mufupi tu katika kazi ya muzunguko, nilielewa kama nilikuwa kabisa na lazima ya mashauri hayo. Kisha kuwekwa kuwa mwangalizi wa muzunguko, Ndugu Thompson alikuwa mwangalizi wa kwanza wa wilaya mwenye nilitumika naye. Nilijifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu huyo muaminifu.

Ninafurahia musaada wenye ndugu wenye uzoefu walinitolea

Katika siku hizo, mwangalizi wa muzunguko alikuwa anapata mazoezi kidogo. Kwa juma moja niliangalia namna mwangalizi wa muzunguko anatembelea kutaniko moja. Kisha juma lenye kufuata aliniangalia namna ninatembelea kutaniko lingine. Alinipatia mapendekezo na muongozo. Lakini kisha hapo alituacha sisi wenyewe tuendelee na kazi. Ninakumbuka siku moja nilimuambia Gloria hivi: “Anapaswa kuondoka tu sasa?” Lakini, kisha wakati fulani, nilitambua jambo fulani la maana. Sikuzote kutakuwa ndugu wazuri wenye wanaweza kukusaidia, ikiwa unawaacha wakusaidie. Ningali ninafurahia musaada wenye nilipata kutoka kwa ndugu hao wenye uzoefu kama vile J. R. Brown, mwenye wakati huo alikuwa mwangalizi mwenye kusafiri, na Fred Rusk mwenye alikuwa wa familia ya Beteli.

Ubaguzi wa rangi ya ngozi ulikuwa unaendelea sana katika siku hizo. Wakati fulani, watu wa kikundi cha KKK walifanya maandamano katika muji moja wenye tulikuwa tunatembelea katika Tennessee. Ninakumbuka wakati mwingine tulikuwa katika mahubiri tukiwa kikundi na tulipumuzikia mahali pa kuuzishia chakula chepesi. Nilienda kwenye choo ya wanaume, na niliona kama mwanaume mumoja mwenye kuwa na hasira na mwenye kuwa na chanjo kama za wazungu wenye kuona kama wao ndio watu wa maana zaidi, alisimama na kunifuata. Lakini ndugu mumoja muzungu mwenye alikuwa munene na murefu kuliko mimi na mwanaume huyo alitufuata. Aliniuliza hivi: “Ndugu Herd, mambo yote ni sawa?” Mwanaume huyo akaondoka mara moja bila kuingia katika choo. Kwa miaka mingi, nimeona kama jambo lenye kuchochea ubaguzi haiko rangi ya ngozi ya mutu, lakini ni zambi yenye sisi wote tuliriti kutoka kwa Adamu. Na nimejifunza kama ndugu ni ndugu hata kama iko na rangi gani ya ngozi, na atakufa kwa ajili yako ikiwa ni lazima.

MWISHO WENYE UTAJIRI

Tulifanya miaka 12 katika kazi ya muzunguko, na miaka 21 katika kazi ya wilaya. Ilikuwa miaka yenye utajiri, yenye baraka, na tulijionea mambo mengi. Hata hivyo, tulikuwa karibu kupata baraka ingine. Katika Mwezi wa 8 mwaka wa 1997, tamaa yetu ya muda murefu ilitimizwa. Tulialikwa kutumikia kwenye Beteli ya Amerika kisha kupita miaka 38 hivi tangu wakati tulijaza ombi la kwanza. Mwezi wenye ulifuata, tulianza kutumika kwenye Beteli. Niliwaza kama ndugu wenye kuongoza kazi kwenye Beteli walipenda tu nisaidie kwa muda fulani, lakini mambo hayakukuwa hivyo.

Gloria alikuwa mutu wa maana sana wakati nilimuoa, na anaendelea kuwa wa maana sana hata leo

Nilipewa kwanza mugawo wa kutumika katika Idara ya Utumishi. Mugawo huo ulinisaidia kujifunza mambo mengi. Katika idara hiyo, ndugu wanashugulikia maulizo mengi mazito kutoka kwa mabaraza ya wazee na waangalizi wa mizunguko katika inchi yote. Nilifurahia namna ndugu walinisaidia na kunizoeza kwa uvumilivu. Lakini, ninajisikia kama ikiwa ninapewa tena mugawo wa kutumika katika idara hiyo, nitakuwa tena na lazima ya kujifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu hao.

Mimi na Gloria tunapenda maisha ya Beteli. Tangu zamani tumekuwa na tabia ya kuamuka asubui sana, na tabia hiyo inatusaidia kabisa kwenye Beteli. Kisha mwaka moja hivi, nilianza kutumika kama musaidizi katika Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Lenye Kuongoza la Mashahidi wa Yehova. Kisha katika mwaka wa 1999, niliwekwa kuwa kati ya ndugu wa Baraza Lenye Kuongoza. Nimejifunza mambo mengi katika mugawo huo, lakini jambo la maana zaidi lenye nimejifunza ni kwamba ni Yesu Kristo ndiye kichwa cha kutaniko la Kikristo, hapana mwanadamu.

Tangu mwaka wa 1999, nimepata pendeleo la kutumika katika Baraza Lenye Kuongoza

Wakati ninakumbuka maisha yangu ya zamani, wakati fulani ninajisikia kwa kadiri fulani kama nabii Amosi. Yehova aliona muchungaji huyo munyenyekevu mwenye alikuwa anafanya kazi ya hali ya chini ya kutunza miti ya tini za mikuyu, chakula chenye kilionwa kuwa ni cha watu maskini tu. Mungu aliweka Amosi kuwa nabii, kwa kweli mugawo huo ulikuwa tajiri kiroho. (Amo. 7:14, 15) Vilevile, Yehova aliniona mimi, mutoto wa mwanaume mulimaji maskini katika Liberty, Indiana, na alinimuangia baraka nyingi, nyingi sana zenye ninashindwa kutaja! (Met. 10:22) Kwa kweli, ninajisikia kama mwanzoni nilikuwa maskini kimwili, lakini mwishowe nimekuwa tajiri kiroho, tajiri zaidi kuliko namna ningewazia!