Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini ‘Tunaendelea Kuzaa Matunda Mengi’?

Kwa Nini ‘Tunaendelea Kuzaa Matunda Mengi’?

“Baba yangu hutukuzwa kwa jambo hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi na kujithibitisha kuwa wanafunzi wangu.”​—YOH. 15:8.

NYIMBO: 53, 60

1, 2. (a) Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia nini wanafunzi wake? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kwa nini ni muhimu tuzingatie akilini sababu zinazotufanya tuendelee kuhubiri? (c) Tutachunguza mambo gani?

KATIKA jioni ya mwisho kabla ya kifo chake, Yesu alikuwa na mazungumzo marefu pamoja na mitume wake ambapo aliwahakikishia kwamba anawapenda sana. Pia, aliwasimulia mfano wa mzabibu kama tulivyoona katika makala iliyotangulia. Yesu alitumia mfano huo kuwatia moyo wanafunzi wake “[waendelee] kuzaa matunda mengi,” naam, waendelee kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa uvumilivu.—Yoh. 15:8.

2 Isitoshe, Yesu aliwaambia wanafunzi wake mambo waliyopaswa kufanya na sababu ya kuyafanya. Aliwapa sababu za kuendelea kufanya kazi ya kuhubiri. Kwa nini ni muhimu tuchunguze sababu hizo? Tunapozingatia akilini sababu zinazotufanya tuendelee kuhubiri, tunachochewa kutoa “ushahidi kwa mataifa yote” kwa uvumilivu. (Mt. 24:13, 14) Hivyo basi, acheni tuchunguze sababu nne za Kimaandiko zinazotufanya tuhubiri. Pia, tutachunguza zawadi nne kutoka kwa Yehova zinazotusaidia kuendelea kuzaa matunda kwa uvumilivu.

TUNAMTUKUZA YEHOVA

3. (a) Andiko la Yohana 15:8 linatupatia sababu gani ya kuendelea kuhubiri? (b) Zabibu zinazotajwa katika mfano wa Yesu zinawakilisha nini, na kwa nini ulinganifu huo unafaa sana?

3 Sababu muhimu zaidi inayotufanya tushiriki katika kazi ya kuhubiri ni kumtukuza Yehova na kulitakasa jina lake miongoni mwa wanadamu. (Soma Yohana 15:1, 8.) Ona kwamba Yesu alimlinganisha Yehova, Baba yake, na mkulima au mtunza-bustani anayetunza mizabibu. Yesu alijilinganisha na mzabibu, au shina la mzabibu, na kuwalinganisha wafuasi wake na matawi. (Yoh. 15:5) Hivyo, inafaa sana kulinganisha zabibu na matunda ya Ufalme ambayo wafuasi wa Kristo hutokeza. Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Baba yangu hutukuzwa kwa jambo hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi.” Kama tu ambavyo mizabibu inayozaa zabibu nzuri humletea heshima mkulima, vivyo hivyo sisi humletea Yehova heshima, au utukufu, tunapojitahidi kadiri tuwezavyo kutangaza ujumbe wa Ufalme.—Mt. 25:20-23.

4. (a) Tunalitakasa jina la Mungu katika njia zipi? (b) Unahisije kuhusu pendeleo ulilonalo la kulitakasa jina la Mungu?

4 Kazi yetu ya kuhubiri hulitakasa jina la Mungu jinsi gani? Hatuwezi kulifanya jina la Mungu liwe takatifu zaidi. Tayari jina hilo ni takatifu katika maana kamili. Lakini ona maneno haya ya nabii Isaya: “Yehova wa majeshi—Yeye ndiye mnayepaswa kumwona kuwa mtakatifu.” (Isa. 8:13) Mojawapo ya njia tunazotakasa jina la Mungu ni kwa kuliona kuwa tofauti na majina mengine na kuwasaidia wengine walione kuwa takatifu. (Mt. 6:9, maelezo ya chini) Kwa mfano, tunapowatangazia wengine ukweli kuhusu sifa za Yehova zenye kuvutia na kusudi lake lisilobadilika kuelekea wanadamu, tunatetea jina la Mungu dhidi ya uwongo wa Shetani na uchongezi wake. (Mwa. 3:1-5) Pia, tunalitakasa jina la Mungu tunapojitahidi kuwasaidia watu katika eneo letu waone kwamba Yehova anastahili “kupokea utukufu na heshima na nguvu.” (Ufu. 4:11) Rune, ndugu ambaye amekuwa painia kwa miaka 16 anasema hivi: “Kujua kwamba nina fursa ya kuwa shahidi wa Muumba wa ulimwengu wote hufanya moyo wangu ujawe na shukrani, na kunifanya niwe na tamaa ya kuendelea kuhubiri.”

TUNAMPENDA YEHOVA NA MWANA WAKE

5. (a) Andiko la Yohana 15:9, 10 linatupatia sababu gani ya kuendelea kuhubiri? (b) Yesu alisisitizaje umuhimu wa kuendelea kuhubiri kwa uvumilivu?

5 Soma Yohana 15:9, 10. Kumpenda Yehova na Yesu kutoka moyoni ni sababu nyingine muhimu inayotufanya tuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Marko 12:30; Yoh. 14:15) Yesu hakuwaambia wafuasi wake wawe tu katika upendo wake, bali pia ‘wakae katika upendo wake.’ Kwa nini? Kwa sababu kuwa mwanafunzi wa kweli wa Kristo mwaka baada ya mwaka kunahitaji uvumilivu. Katika mistari michache ya Yohana 15:4-10, Yesu alisisitiza uhitaji wa kuvumilia kwa kurudia tena na tena neno ‘kukaa.’

6. Tunaonyeshaje kwamba tunataka kukaa katika upendo wa Kristo?

6 Tunaonyeshaje kwamba tunataka kukaa katika upendo wa Kristo na kuendelea kuwa na kibali chake? Kwa kushika amri za Yesu. Kwa maneno rahisi Yesu anatuambia, ‘Nitiini.’ Isitoshe, Yesu alituambia tufanye mambo ambayo yeye mwenyewe alifanya, kwa kuwa alisema, “nimeshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.” Yesu anatuwekea kielelezo kizuri.—Yoh. 13:15.

7. Kuna uhusiano gani kati ya sifa ya utii na upendo?

7 Awali katika mazungumzo yake, Yesu alionyesha uhusiano uliopo kati ya sifa ya utii na upendo alipowaambia hivi mitume wake: “Yeyote aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye anayenipenda.” (Yoh. 14:21) Zaidi ya hilo, tunapotii amri ya Yesu ya kwenda kuhubiri tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa sababu amri za Yesu zinafunua mawazo ya Yehova mwenyewe. (Mt. 17:5; Yoh. 8:28) Tunapoendelea kuwaonyesha Yehova na Yesu upendo kwa njia hiyo, wao pia wataendelea kututunza katika upendo wao.

TUNAWAONYA WATU

8, 9. (a) Tuna sababu gani nyingine ya kuendelea kuhubiri? (b) Maneno ya Yehova kwenye Ezekieli 3:18, 19 na 18:23 yanatuchocheaje kuendelea kuhubiri?

8 Kuna sababu nyingine inayotufanya tuendelee kuhubiri. Tunahubiri ili kuwaonya watu. Biblia inasema kwamba Noa alikuwa “mhubiri.” (Soma 2 Petro 2:5.) Ni wazi kwamba kazi ya kuhubiri aliyofanya kabla ya Gharika ilihusisha pia kuwaonya watu kuhusu maangamizi yaliyokuwa yakikaribia. Kwa nini tunaweza kufikia mkataa huo? Ona maneno haya ya Yesu: “Kwa maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya Gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina, nao hawakujali mpaka Gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mt. 24:38, 39) Licha ya kwamba watu hawakuitikia vizuri ujumbe wake, Noa aliendelea kwa uaminifu kuwatangazia onyo alilokuwa amepewa.

9 Leo, sisi huhubiri ujumbe wa Ufalme ili kuwapa watu fursa ya kujifunza kuhusu mapenzi ya Mungu kwa wanadamu. Kama Yehova, tunatamani sana watu waitikie ujumbe huo ili ‘waendelee kuishi.’ (Eze. 18:23) Wakati huohuo, tunapohubiri nyumba kwa nyumba na katika maeneo ya umma, tunawaonya watu wengi iwezekanavyo kwamba Ufalme wa Mungu utakuja na kukomesha ulimwengu huu usiomwogopa Mungu.—Eze. 3:18, 19; Dan. 2:44; Ufu. 14:6, 7.

TUNAWAPENDA JIRANI ZETU

10. (a) Andiko la Mathayo 22:39 linatupatia sababu gani ya kuendelea kuhubiri? (b) Simulia jinsi Paulo na Sila walivyomsaidia mlinzi fulani wa jela huko Filipi.

10 Sababu nyingine muhimu inayotufanya tuendelee kuhubiri ni hii: Tunahubiri kwa sababu tunawapenda jirani zetu. (Mt. 22:39) Upendo huo hutusukuma tuendelee kufanya kazi hiyo kwa uvumilivu, kwa sababu tunatambua kwamba watu wanaweza kubadili mtazamo wao hali zao zinapobadilika. Fikiria mambo yaliyompata mtume Paulo na mwandamani wake, Sila. Walipokuwa katika jiji la Filipi, wapinzani waliwatupa gerezani. Kisha, katikati ya usiku, tetemeko la ardhi likatikisa gereza na kufanya milango yake ifunguke. Mlinzi wa jela alikuwa karibu kujiua akifikiri kwamba wafungwa walikuwa wametoroka. Lakini Paulo akapaza sauti na kumwambia: “Usijiumize!” Mlinzi huyo aliyekuwa amefadhaika akauliza: “Nifanye nini ili niokolewe?” Wakamwambia hivi: “Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa.”—Mdo. 16:25-34.

Kumpenda Yehova, Yesu, na jirani hutuchochea kuhubiri (Tazama fungu la 5 na 10)

11, 12. (a) Simulizi la mlinzi wa jela linahusianaje na kazi yetu ya kuhubiri? (b) Tungependa kuwa tayari kufanya nini?

11 Simulizi hilo la mlinzi wa jela linahusianaje na kazi yetu ya kuhubiri? Ona kwamba mlinzi wa jela alibadili mtazamo wake na kuomba msaada baada ya tetemeko kutokea. Vivyo hivyo, baadhi ya watu ambao hawakuitikia vizuri ujumbe wa Biblia wanaweza kubadili mtazamo wao na kuomba msaada wanapokumbwa na badiliko la ghafla maishani mwao lililo kama tetemeko. Kwa mfano, huenda baadhi ya watu tunaowahubiria katika eneo letu wamepoteza ghafla kazi ambayo wamekuwa wakifanya kwa muda mrefu nao wamepigwa na butwaa. Huenda wengine wanahuzunika baada ya ndoa yao kuvunjika hivi karibuni. Na huenda wengine hawajui la kufanya baada ya kuambiwa kwamba wana ugonjwa mbaya sana, au wengine wamevunjika moyo baada ya kufiwa na mpendwa. Huenda baadhi ya watu wanaokabili hali kama hizo wakauliza maswali kuhusu kusudi la maisha, maswali ambayo mwanzoni waliyapuuza. Labda hata wanajiuliza, ‘Nifanye nini ili niokolewe?’ Tunapokutana nao huenda wakasikiliza ujumbe wetu wa tumaini kwa mara ya kwanza maishani mwao.

12 Hivyo, tunapoendelea kuhubiri kwa uaminifu, tunakuwa tayari sikuzote kuwapa watu faraja wakati barabara wanapohitaji faraja hiyo. (Isa. 61:1) Charlotte, ambaye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 38, anasema hivi: “Leo watu wamechanganyikiwa. Wanahitaji kusikia habari njema.” Ejvor, dada ambaye amekuwa painia kwa miaka 34, anaeleza hivi: “Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu wamevunjika moyo. Ninatamani sana kuwasaidia. Hilo hunichochea kuhubiri.” Naam, kuwapenda jirani zetu ni sababu nzuri sana ya kuendelea kutimiza huduma yetu!

ZAWADI ZINAZOTUSAIDIA KUVUMILIA

13, 14. (a) Ni zawadi gani inayotajwa katika Yohana 15:11? (b) Shangwe ya Yesu itakuwa yetu jinsi gani? (c) Kuwa na shangwe huwa na matokeo gani katika huduma yetu?

13 Jioni ya mwisho kabla ya kifo chake, Yesu alitaja pia zawadi kadhaa ambazo zingewasaidia mitume wake kuendelea kuzaa matunda kwa uvumilivu. Zawadi hizo ni nini, na zinatunufaishaje?

14 Zawadi ya shangwe. Je, lingekuwa jambo gumu kutii amri ya Yesu ya kuhubiri? Sivyo hata kidogo. Baada ya kutoa mfano wa mzabibu, Yesu alisema kwamba wahubiri wa Ufalme watakuwa na shangwe. (Soma Yohana 15:11.) Isitoshe alituhakikishia kwamba shangwe yake itakuwa shangwe yetu pia. Jinsi gani? Kama tulivyoona awali, Yesu alijilinganisha na mzabibu na wanafunzi wake na matawi. Mzabibu hutegemeza matawi yake. Maadamu matawi hayo yameunganika kwenye shina la mzabibu, matawi hayo yataendelea kupata maji na lishe kutoka kwenye mzabibu. Vivyo hivyo, maadamu tunakaa katika muungano na Kristo kwa kufuata hatua zake kwa ukaribu, sisi pia tutakuwa na shangwe ambayo Yesu anayo kwa kufanya mapenzi ya Baba yake. (Yoh. 4:34; 17:13; 1 Pet. 2:21) Hanne, dada ambaye amekuwa painia kwa zaidi ya miaka 40 anasema hivi: “Shangwe ambayo mimi huhisi baada ya kushiriki katika huduma, hunichochea niendelee kumtumikia Yehova.” Kwa kweli, shangwe ya kutoka moyoni hutupatia nguvu za kuendelea kuhubiri hata katika maeneo ambayo watu hawapendezwi sana na ujumbe wetu.—Mt. 5:10-12.

15. (a) Ni zawadi gani inayotajwa katika Yohana 14:27? (b) Ni kwa njia gani amani hutusaidia kuendelea kuzaa matunda?

15 Zawadi ya amani. (Soma Yohana 14:27.) Mapema jioni hiyo kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Ninawapa amani yangu.” Zawadi hiyo, yaani, amani ya Yesu, inatusaidiaje kuzaa matunda? Tunapoendelea kuvumilia tunapata amani ya kudumu mioyoni mwetu, amani ambayo tunapata kwa kujua kwamba tuna kibali cha Yehova na Yesu. (Zab. 149:4; Rom. 5:3, 4; Kol. 3:15) Ulf, ndugu ambaye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 45, anasema hivi: “Mimi huchoka ninapofanya kazi ya kuhubiri, lakini kazi hiyo hunipa furaha ya kweli na kusudi maishani.” Tunafurahi sana kwamba Yehova ametubariki kwa kutupatia amani ya kudumu!

16. (a) Ni zawadi gani inayotajwa katika Yohana 15:15? (b) Mitume walihitaji kufanya nini ili waendelee kuwa rafiki za Yesu?

16 Zawadi ya kuwa na urafiki na Yesu. Baada ya Yesu kueleza kwamba alitamani shangwe ya mitume wake “ijae,” aliwaeleza umuhimu wa kuonyesha upendo wa kujidhabihu. (Yoh. 15:11-13) Kisha akasema: “Nimewaita rafiki.” Ni zawadi nzuri ajabu kuwa rafiki ya Yesu! Mitume walihitaji kufanya nini ili waendelee kuwa rafiki za Yesu? Walipaswa “[kwenda] na kuendelea kuzaa matunda.” (Soma Yohana 15:14-16.) Miaka miwili hivi mapema, Yesu alikuwa amewaagiza hivi mitume wake: “Mnapoenda, hubirini mkisema: ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:7) Hivyo jioni hiyo ya mwisho, Yesu aliwatia moyo waendelee kwa uvumilivu kufanya kazi waliyokuwa wameanza. (Mt. 24:13; Marko 3:14) Ingawa kutii amri ya Yesu kungetokeza changamoto mbalimbali, bado mitume wangefaulu kutimiza kazi hiyo na hivyo kuendelea kuwa rafiki zake. Jinsi gani? Kuna zawadi nyingine tena ambayo ingewasaidia.

17, 18. (a) Ni zawadi gani inayotajwa katika Yohana 15:16? (b) Zawadi hiyo ingewasaidiaje wanafunzi wa Yesu? (c) Ni zawadi zipi zinazotutia nguvu leo?

17 Zawadi ya kuona sala zikijibiwa. Yesu alisema hivi: “Mkimwomba Baba jambo lolote katika jina langu, [atawapa].” (Yoh. 15:16) Lazima mitume waliimarishwa sana na ahadi hiyo! * Ingawa hawakuelewa vizuri kwamba baada ya muda mfupi maisha ya Kiongozi wao hapa duniani yangefikia mwisho, hawangeachwa bila msaada. Yehova alikuwa tayari kujibu sala zao na kuwapa msaada wowote ambao wangehitaji ili kutii amri ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Na kwa kweli, muda mfupi baadaye walijionea jinsi Yehova alivyojibu sala zao.—Mdo. 4:29, 31.

Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hujibu sala zetu za kuomba msaada (Tazama fungu la 18)

18 Hali iko hivyo leo pia. Tunapoendelea kuzaa matunda kwa uvumilivu, tunafurahia urafiki pamoja na Yesu. Isitoshe, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova yuko tayari kujibu sala zetu tunapomwomba atusaidie kushinda vizuizi ambavyo huenda tukakabili tunapohubiri habari njema ya Ufalme. (Flp. 4:13) Tunafurahi sana kwamba Yehova anatubariki kwa kujibu sala zetu na kwamba tuna urafiki pamoja na Yesu! Zawadi hizo tunazopokea kutoka kwa Yehova hututia nguvu tuendelee kuzaa matunda.—Yak. 1:17.

19. (a) Kwa nini sisi huendelea kufanya kazi ya kuhubiri? (b) Ni mambo gani yanayotusaidia kukamilisha kazi tuliyoagizwa na Mungu?

19 Kama tulivyochunguza katika makala hii, tunaendelea kufanya kazi ya kuhubiri ili kumtukuza Yehova na kulitakasa jina lake, ili tuonyeshe kwamba tunampenda Yehova na Yesu, ili kutoa onyo, na kuonyesha kwamba tunawapenda jirani zetu. Zaidi ya hilo, zawadi ya shangwe, amani, urafiki pamoja na Yesu, na kuona sala zetu zikijibiwa hututia nguvu ili tukamilishe kazi ambayo Mungu alituagiza. Yehova atafurahi sana kuona tukijitahidi kwa nafsi yote “[kuendelea] kuzaa matunda mengi”!

^ fu. 17 Alipokuwa akizungumza na mitume wake, Yesu aliwahakikishia tena na tena kwamba sala zao zingejibiwa.—Yoh. 14:13; 15:7, 16; 16:23.