Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mjue Adui Yako

Mjue Adui Yako

“Hatukosi kuzijua njama [za Shetani].”​—2 KOR. 2:11, maelezo ya chini.

NYIMBO: 150, 32

1. Yehova alifunua nini kumhusu adui yetu katika bustani ya Edeni?

BILA shaka, Adamu alijua kwamba nyoka hawawezi kuzungumza. Hivyo, huenda alitambua kwamba kiumbe fulani wa roho alikuwa amezungumza na Hawa kupitia nyoka. (Mwa. 3:1-6) Adamu na Hawa hawakujua lolote kuhusu kiumbe huyo. Hata hivyo, Adamu aliamua kimakusudi kumwasi Baba yake wa mbinguni mwenye upendo na kupinga mapenzi ya Mungu kwa kumuunga mkono kiumbe huyo wasiyemjua. (1 Tim. 2:14) Mara moja, Yehova akaanza kufunua habari fulani kumhusu adui huyo aliyekuwa amewapotosha Adamu na Hawa, na kuahidi kwamba mwishowe angeangamizwa. Pia, Yehova alionya kwamba kwa kipindi fulani, kiumbe huyo aliyekuwa amezungumza kupitia nyoka angekuwa na nguvu ya kuwapinga wale wanaompenda Mungu.—Mwa. 3:15.

2, 3. Huenda ni kwa nini habari chache tu ndizo zilizofunuliwa kumhusu Shetani kabla ya Masihi kufika?

2 Kwa hekima, Yehova hajatufunulia jina la kibinafsi la malaika huyo aliyemwasi. * Pia, Mungu aliamua kutofunua hata jina linalomfafanua adui huyo hadi miaka 2,500 hivi baada ya uasi wa kwanza. (Ayu. 1:6) Isitoshe, ni vitabu vitatu tu vya Maandiko ya Kiebrania, yaani, 1 Mambo ya Nyakati, Ayubu, na Zekaria, vinavyotaja jina Shetani linalomaanisha “Mpinzani.” Kwa nini ni habari chache tu zilizofunuliwa kumhusu adui yetu kabla ya kufika kwa Masihi?

3 Inaonekana kwamba Yehova hakutaka kumpa Shetani umashuhuri asiostahili kwa sababu hakuruhusu sehemu kubwa ya Maandiko ya Kiebrania yazungumze kumhusu na kuhusu utendaji wake. Kusudi kuu lililomchochea Yehova kuwaongoza waandikaji wa Biblia kuandika sehemu hiyo ya Maandiko lilikuwa kumtambulisha Masihi na kuwaongoza watu wa Mungu kwake. (Luka 24:44; Gal. 3:24) Baada ya kutimiza kusudi hilo na Masihi kufika, Yehova alimtumia yeye pamoja na wanafunzi wake kufunua habari nyingi tunazojua kumhusu Shetani na malaika waliomuunga mkono. * Jambo hilo linafaa kwa kuwa Yehova atamtumia Yesu pamoja na watawala wenzake watiwa-mafuta kumponda Shetani na wafuasi wake.—Rom. 16:20; Ufu. 17:14; 20:10.

4. Kwa nini hatupaswi kuwa na wasiwasi mwingi kumhusu Shetani?

4 Mtume Petro anamfafanua Shetani Ibilisi kuwa “simba anayenguruma,” na Yohana anamwita “nyoka” na pia “joka.” (1 Pet. 5:8; Ufu. 12:9) Hata hivyo, hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi mwingi kumhusu Ibilisi kwa sababu nguvu zake zina mipaka. (Soma Yakobo 4:7.) Yehova, Yesu, na malaika waaminifu wako upande wetu. Kwa msaada wao, tunaweza kumpinga adui yetu. Ingawa hivyo, tunahitaji kupata majibu ya maswali haya matatu muhimu: Shetani ana nguvu au mamlaka kubwa kadiri gani? Shetani hutumiaje nguvu au mamlaka hiyo kuwapotosha wanadamu? Na nguvu zake zina mipaka gani? Tunapochunguza majibu ya maswali hayo, tutaona pia mambo tunayoweza kujifunza.

SHETANI ANA NGUVU AU MAMLAKA KUBWA KADIRI GANI?

5, 6. Kwa nini serikali za wanadamu haziwezi kuleta mabadiliko ambayo wanadamu wanahitaji hasa?

5 Idadi kubwa ya malaika walimuunga mkono Shetani katika kumwasi Mungu. Kabla ya Gharika, Shetani alifanikiwa kuwashawishi angalau baadhi ya malaika hao kufanya ngono na mabinti wa wanadamu. Biblia inafunua ukweli huo inapomwonyesha kwa njia ya mfano akikokota theluthi moja ya nyota za mbinguni. (Mwa. 6:1-4; Yuda 6; Ufu. 12:3, 4) Malaika hao walipojitenga na familia ya Mungu, walijiruhusu waongozwe na Shetani. Hata hivyo, waasi hao si kundi tu la wafanya ghasia. Shetani amesimamisha ufalme wake mwenyewe akijaribu kuiga Ufalme wa Mungu, na kujiweka kuwa mfalme wa ufalme huo. Katika ulimwengu wa roho, Shetani amewapanga roho waovu katika serikali mbalimbali, amewapa mamlaka, na kuwafanya kuwa watawala wa ulimwengu.—Efe. 6:12.

6 Kupitia tengenezo lake la viumbe wa roho, Shetani ana mamlaka juu ya serikali zote za wanadamu. Ukweli huo ulionekana wazi Shetani alipomwonyesha Yesu “falme zote za dunia inayokaliwa” na kumwambia: “Nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wake, kwa sababu nimepewa, nami humpa yeyote ninayetaka.” (Luka 4:5, 6) Licha ya uovu unaoendelezwa na Shetani, serikali nyingi huwatendea raia wake mambo fulani mazuri. Na huenda watawala fulani wakawa na nia nzuri. Lakini hakuna serikali yoyote ya wanadamu au mtawala yeyote mwenye uwezo wa kuleta mabadiliko ambayo wanadamu wanahitaji hasa.—Zab. 146:3, 4; Ufu. 12:12.

7. Mbali na kutumia serikali mbalimbali, Shetani anatumiaje pia dini ya uwongo na mfumo wa kibiashara? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Shetani na roho wake waovu hawatumii tu serikali mbalimbali kuipotosha “dunia nzima inayokaliwa,” bali pia hutumia dini ya uwongo na mfumo wa kibiashara. (Ufu. 12:9) Shetani anatumia dini ya uwongo kuendeleza uwongo kumhusu Yehova. Zaidi ya hilo, Ibilisi ameazimia kuwafanya watu wengi kadiri iwezekanavyo walisahau jina la Mungu. (Yer. 23:26, 27) Hivyo, watu wanyoofu wamepotoshwa kwa kufikiri kwamba wanamwabudu Mungu lakini kumbe wanaabudu roho waovu. (1 Kor. 10:20; 2 Kor. 11:13-15) Pia, Shetani anaendeleza uwongo kupitia mfumo wa kibiashara. Kwa mfano, kupitia mfumo huo anawafundisha watu kwamba njia bora ya kupata furaha ni kufuatia pesa na kujikusanyia mali. (Met. 18:11) Wale wanaoamini uwongo huo hutumia maisha yao kutumikia “Utajiri” badala ya kumtumikia Mungu. (Mt. 6:24) Hatimaye, upendo walio nao kuelekea vitu vya kimwili unaweza kufanya upendo wowote walio nao kumwelekea Mungu utokomee.—Mt. 13:22; 1 Yoh. 2:15, 16.

8, 9. (a) Tunajifunza mambo gani mawili kutokana na simulizi la Adamu, Hawa, na malaika waasi? (b) Tunanufaikaje kwa kujua kiwango cha mamlaka au nguvu ambazo Shetani anazo?

8 Mfano wa Adamu, Hawa, na malaika waasi unatufundisha angalau mambo mawili muhimu. Kwanza, kuna pande mbili tu, na ni lazima tuchague upande mmoja. Tunaweza kuchagua kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova au kujiunga na upande wa Shetani. (Mt. 7:13) Pili, wale wanaojiunga na Shetani hupata manufaa ya kadiri fulani tu. Adamu na Hawa walipata fursa ya kujiamulia viwango vyao vya mema na mabaya, na roho waovu walipata mamlaka fulani juu ya serikali za wanadamu. (Mwa. 3:22) Hata hivyo, sikuzote hasara ambayo mtu anapata huzidi mambo yoyote yanayoonekana kuwa faida ambayo Shetani anaweza kuahidi.—Ayu. 21:7-17; Gal. 6:7, 8.

9 Tunanufaikaje kwa kujua kiwango cha mamlaka au nguvu ambazo Shetani anazo? Kujua jambo hilo hutusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu mamlaka za serikali na hutuchochea katika kazi yetu ya kuhubiri. Tunajua kwamba Yehova anataka tuheshimu mamlaka za serikali. (1 Pet. 2:17) Na anatarajia tutii sheria za serikali za wanadamu maadamu sheria hizo hazipingi viwango vyake. (Rom. 13:1-4) Lakini tunatambua kwamba hatupaswi kuunga mkono upande wowote wa kisiasa; hatupaswi kamwe kuona chama fulani cha kisiasa au kiongozi fulani kuwa bora kuliko mwingine. (Yoh. 17:15, 16; 18:36) Kwa kuwa tunajionea jinsi Shetani anavyojaribu kuwafanya watu wasilijue jina la Yehova na kumchafulia sifa yake, tunachochewa hata zaidi kuwafundisha wengine ukweli kumhusu Mungu wetu. Tunajivunia kulibeba na kulitumia jina lake tukijua kwamba kumpenda yeye hutuletea thawabu nyingi zaidi kuliko kupenda pesa au vitu vya kimwili.—Isa. 43:10; 1 Tim. 6:6-10.

SHETANI HUWAPOTOSHA WANADAMU JINSI GANI?

10-12. (a) Huenda Shetani alitumiaje chambo kuwanasa malaika wenzake? (b) Kisa cha malaika wengi walioanguka katika kishawishi kinatufundisha nini?

10 Shetani hutumia mbinu zenye mafanikio kuwapotosha watu. Kwa mfano, yeye hutumia chambo ili kuwashawishi watu wafanye mambo kwa njia yake. Pia, yeye hujaribu kuwashinikiza ili wajitiishe kwake.

11 Fikiria jinsi Shetani alivyotumia chambo ili kushawishi na kunasa idadi kubwa ya malaika wenzake. Inaonekana kwamba aliwachunguza kwa muda mrefu kabla ya kuwashawishi wajiunge naye. Baadhi ya malaika hao waliponaswa katika mtego wa kufanya ngono na wanawake, walizaa watoto waliokuwa nusu malaika na nusu wanadamu ambao waliwakandamiza wanadamu. (Mwa. 6:1-4) Shetani hakuwashawishi tu malaika hao wasio washikamanifu wafanye ngono, bali pia huenda aliwaahidi kuwapa mamlaka ya kuwatawala wanadamu. Huenda alikusudia kuvuruga mpango ambao ungetokeza ‘uzao wa mwanamke’ uliokuwa umeahidiwa. (Mwa. 3:15) Vyovyote vile, Yehova alikomesha njama hizo zote kwa kuleta Gharika—hatua ambayo ilivuruga jitihada za Shetani na malaika hao waasi.

Shetani hujaribu kutushawishi akitumia uasherati, kiburi, na uchawi (Tazama fungu la 12 na 13)

12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa hicho? Usifikiri kamwe kwamba huwezi kunaswa na kishawishi cha kufanya uasherati au kusitawisha kiburi. Malaika waliojiunga na Shetani walikuwa wametumikia mbele za Mungu mwenyewe kwa mamilioni ya miaka. Lakini licha ya kwamba walitumikia katika mazingira hayo mazuri, waliruhusu tamaa mbaya itie mizizi na kusitawi ndani yao. Vivyo hivyo, huenda sisi pia tumetumikia kwa miaka mingi katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Mungu. Lakini hata katika mazingira hayo safi kiroho, tamaa zisizofaa zinaweza kusitawi ndani yetu. (1 Kor. 10:12) Hivyo ni muhimu sana kwetu tuendelee kuuchunguza moyo wetu, tukatae mawazo yaliyopotoka kiadili, na tusiruhusu kiburi kisitawi ndani yetu!—Gal. 5:26; soma Wakolosai 3:5.

13. Ni chambo kipi kingine ambacho Shetani anatumia kwa mafanikio, na tunaweza kuepukaje kunaswa na mtego huo?

13 Chambo kingine ambacho Shetani hutumia kwa mafanikio ni kuwachochea watu wadadisi mambo ya kichawi. Leo, Shetani hatumii tu dini ya uwongo kuwachochea watu wavutiwe na roho waovu, bali pia anatumia ulimwengu wa burudani. Sinema, michezo ya kompyuta, na burudani nyinginezo hufanya zoea la kuwasiliana na roho waovu lionekane kuwa lenye kusisimua. Tunaweza kuepukaje kunaswa na mtego huo? Hatupaswi kutarajia tengenezo la Mungu litupatie orodha ya burudani zinazokubalika na zisizokubalika. Kila mmoja wetu anahitaji kuzoeza dhamiri yake mwenyewe ipatane na viwango vya Mungu. (Ebr. 5:14) Pamoja na hilo, tutafanya maamuzi ya hekima ikiwa tutafuata ushauri huu wa Paulo ulioongozwa na roho kwamba upendo wetu kwa Mungu “uwe bila unafiki.” (Rom. 12:9) Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, burudani ninayochagua itafanya nionekane kuwa mnafiki? Ikiwa watu ninaojifunza nao Biblia au watu ninaowarudia ili kuzungumzia Biblia pamoja nao wangeona burudani ninazochagua, je, wangefikia mkataa kwamba ninaishi kulingana na mambo ninayohubiri?’ Tunapojitahidi kupatanisha mambo tunayosema na mambo tunayotenda, hatutanaswa kwa urahisi na mitego ya Shetani.—1 Yoh. 3:18.

Shetani hujaribu kutushinikiza kupitia marufuku za serikali, kushinikizwa na wanafunzi wenzetu, na upinzani kutoka kwa familia (Tazama fungu la 14)

14. Shetani anaweza kutumia nini ili kutushinikiza, na tunaweza kukabilianaje na hali hizo?

14 Zaidi ya kutumia chambo, Shetani hujaribu kutushinikiza tuvunje ushikamanifu wetu kwa Yehova. Kwa mfano, anaweza kuongoza mambo ili serikali zipige marufuku kazi yetu ya kuhubiri. Au anaweza kuwachochea wafanyakazi au wanafunzi wenzetu watudhihaki kwa sababu tunaishi kulingana na viwango vya Biblia vya maadili. (1 Pet. 4:4) Pia, anaweza kuwachochea watu wa familia walio na nia nzuri watuvunje moyo ili tuache kuhudhuria mikutano. (Mt. 10:36) Tunaweza kukabilianaje na hali hizo? Kwanza, tunapaswa kutarajia kwamba Shetani atatushambulia kwa njia ya moja kwa moja kwa kuwa anapigana vita dhidi yetu. (Ufu. 2:10; 12:17) Kisha, tunapaswa kutambua suala kuu linalohusika—Shetani anadai kwamba sisi humtumikia Yehova ikiwa tu hali ni nzuri. Anasema ikiwa tutashinikizwa, tutamwacha Mungu. (Ayu. 1:9-11; 2:4, 5) Na mwishowe, tunahitaji kumtegemea Yehova ili atupe nguvu tunazohitaji. Kumbuka, hatatuacha kamwe.—Ebr. 13:5.

NGUVU ZA SHETANI ZINA MIPAKA GANI?

15. Je, Shetani anaweza kutulazimisha kufanya mambo kinyume cha mapenzi yetu? Eleza.

15 Shetani hawezi kuwalazimisha watu watende kinyume cha mapenzi yao. (Yak. 1:14) Hata hivyo, watu wengi huunga mkono kusudi la Shetani bila kujua. Lakini baada ya kujifunza kweli, kila mmoja huamua ikiwa atamtumikia Mungu au Shetani. (Mdo. 3:17; 17:30) Ikiwa tumeazimia kufanya mapenzi ya Mungu, hakuna jambo lolote ambalo Shetani anaweza kufanya ili kuvunja utimilifu wetu.—Ayu. 2:3; 27:5.

16, 17. (a) Ni mambo gani mengine ambayo Shetani na roho waovu hawawezi kufanya? (b) Kwa nini hatupaswi kuogopa kusali kwa Yehova kwa sauti?

16 Kuna mambo mengine pia ambayo Shetani na roho waovu hawawezi kufanya. Kwa mfano, hakuna Andiko lolote linaloonyesha kwamba wanaweza kusoma akili na moyo wa mtu. Ni Yehova na Yesu pekee wanaotajwa kuwa na uwezo huo. (1 Sam. 16:7; Marko 2:8) Vipi kuhusu kuzungumza au kusali kwa sauti? Je, tunapaswa kuogopa kwamba Ibilisi au roho waovu wanaweza kusikia sala zetu na kutumia habari hizo dhidi yetu? Jibu ni la. Kwa nini? Kwa kawaida, hatuogopi kutenda matendo mema katika utumishi wa Yehova eti kwa sababu Ibilisi atatuona. Vivyo hivyo, hatupaswi kuogopa kusali kwa sauti eti kwa sababu Shetani atatusikia. Ukweli ni kwamba Biblia ina mifano mingi ya watumishi wa Mungu waliosali kwa sauti, na hakuna jambo lolote linalodokeza kwamba waliogopa kuwa Ibilisi atawasikia. (1 Fal. 8:22, 23; Yoh. 11:41, 42; Mdo. 4:23, 24) Ikiwa tutafanya yote tuwezayo kusema na kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hatamruhusu Ibilisi atusababishie madhara yoyote ya kudumu.—Soma Zaburi 34:7.

17 Tunahitaji kumjua adui yetu, lakini hatupaswi kumwogopa. Kwa msaada wa Yehova, hata wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kumshinda Shetani. (1 Yoh. 2:14) Tukimpinga, atatukimbia. (Yak. 4:7; 1 Pet. 5:9) Inaonekana kwamba vijana ndio hasa wanaolengwa na Shetani. Ni jambo gani hususa wanaloweza kufanya ili wampinge Ibilisi kwa uthabiti? Tutazungumzia swali hilo katika makala inayofuata.

^ fu. 2 Biblia inafunua majina ya kibinafsi ya baadhi ya malaika. (Amu. 13:18; Dan. 8:16; Luka 1:19; Ufu. 12:7) Kwa kuwa Yehova ameipa kila nyota jina lake (Zab. 147:4), tunaweza kufikia mkataa kwamba wana wote wa Mungu walio mbinguni, yaani, malaika, kutia ndani Shetani, wana majina ya kibinafsi.

^ fu. 3 Katika Maandiko ya Kiebrania, jina Shetani linapatikana mara 18 tu lakini linapatikana zaidi ya mara 30 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.