Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Na Tuwe na Umoja Kama Yehova na Yesu Walivyo na Umoja

Na Tuwe na Umoja Kama Yehova na Yesu Walivyo na Umoja

“Ninaomba . . . wote wawe kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe Baba umo katika muungano nami.”—YOH. 17:20, 21.

NYIMBO: 24, 99

1, 2. (a) Yesu alitaja ombi gani katika sala yake ya mwisho pamoja na mitume wake? (b) Ni sababu gani ambayo huenda ilimfanya Yesu asisitize sana umuhimu wa kuwa na umoja?

KATIKA mlo wa mwisho wa jioni pamoja na mitume wake, Yesu alisisitiza umuhimu wa kuwa na umoja. Alipokuwa akisali pamoja nao, alieleza kwamba alitamani wanafunzi wake wawe kitu kimoja, kama ambavyo yeye na Baba yake walivyo kitu kimoja. (Soma Yohana 17:20, 21.) Umoja wao ungetoa ushuhuda wenye nguvu na kuthibitisha wazi kwamba Yesu alitumwa na Yehova duniani ili kufanya mapenzi ya Mungu. Upendo ungekuwa alama inayowatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu, nao ungewasaidia wawe na umoja.​—Yoh. 13:34, 35.

2 Tunaweza kuelewa kwa nini Yesu alikazia umuhimu wa kuwa na umoja. Alikuwa ametambua kwamba kulikuwa na ukosefu wa umoja na upatano miongoni mwa mitume, kama hali ilivyokuwa wakati wa mlo wa mwisho pamoja nao. Kama ilivyokuwa imetukia hapo awali, mitume walibishana kuhusu “ni nani aliyekuwa mkuu zaidi kati yao.” (Luka 22:24-27; Marko 9:33, 34) Katika pindi nyingine, Yakobo na Yohana walimwomba Yesu waketi mahali penye kuheshimika kando yake katika Ufalme wake.—Marko 10:35-40.

3. Ni mambo gani ambayo huenda yalisababisha ukosefu wa umoja miongoni mwa wanafunzi wa Kristo, na tutachunguza maswali gani?

3 Hata hivyo, mbali na tamaa ya umashuhuri, kuna mambo mengine yaliyohatarisha umoja miongoni mwa wanafunzi wa Kristo. Kulikuwa na migawanyiko miongoni mwa watu kwa sababu ya chuki na ubaguzi. Wanafunzi wa Yesu walihitaji kushinda hisia hizo. Katika makala hii, tutachunguza maswali yafuatayo: Yesu alishughulikaje na ubaguzi? Aliwasaidiaje wafuasi wake kujifunza jinsi ya kuwatendea wengine bila ubaguzi na kuwa na umoja wa kweli? Na mafundisho yake yatatusaidiaje kuendelea kuwa na umoja?

UBAGUZI AMBAO YESU NA WAFUASI WAKE WALIKABILI

4. Yesu alikabili ubaguzi wa aina gani?

4 Yesu mwenyewe alibaguliwa. Filipo alipomwambia Nathanaeli kwamba amempata Masihi, Nathanaeli alijibu hivi: “Je, kitu chochote kizuri kinaweza kutoka Nazareti?” (Yoh. 1:46) Inaonekana kwamba Nathanaeli alijua kuhusu unabii unaopatikana kwenye Mika 5:2, na kwa maoni yake mji wa Nazareti ulikuwa duni sana usiweze kumtokeza Masihi. Pia, Wayudea mashuhuri walimdharau Yesu kwa sababu alikuwa Mgalilaya. (Yoh. 7:52) Wayudea wengi waliwaona Wagalilaya kuwa duni. Wayahudi wengine walimtukana Yesu kwa kumwita Msamaria. (Yoh. 8:48) Wasamaria walitofautiana sana na Wayahudi kidesturi na kidini. Wayudea na Wagalilaya waliwadharau Wasamaria, na waliwaepuka kabisa.​—Yoh. 4:9.

5. Wafuasi wa Yesu walikabili ubaguzi wa aina gani?

5 Viongozi wa Kiyahudi waliwadharau pia wafuasi wa Yesu. Mafarisayo waliwajumlisha katika kundi la “watu waliolaaniwa.” (Yoh. 7:47-49) Naam, kulingana na maoni yao, mtu yeyote ambaye hakuwa amesomea katika shule za kirabi au ambaye hakushika desturi zao alikuwa mwenye kudharaulika na wa hali ya chini. (Mdo. 4:13, maelezo ya chini) Yesu na wanafunzi wake walibaguliwa kwa misingi ya kidini, kijamii, na kitamaduni. Wanafunzi wa Yesu pia waliathiriwa na hisia za ubaguzi. Ili wawe na umoja, walihitaji kubadili mtazamo wao.

6. Toa mifano inayoonyesha jinsi ubaguzi unavyoweza kutuathiri.

6 Leo, wengi wetu tumezungukwa na ubaguzi. Huenda sisi wenyewe tunabaguliwa, au tunawabagua wengine kwa njia fulani. Dada mmoja kutoka Australia ambaye sasa ni painia anasema hivi: “Chuki niliyokuwa nayo kuelekea watu weupe iliongezeka nilipofikiria jinsi wenyeji wa asili wa Australia walivyodhulumiwa zamani na wanavyoendelea kudhulumiwa hadi leo. Na mambo mabaya niliyotendewa zamani yalifanya nizidi kuwachukia.” Ndugu mmoja kutoka Kanada alitaja jinsi ambavyo hapo awali aliwabagua watu kwa msingi wa lugha waliyozungumza. Anakiri hivi: “Kwa maoni yangu watu waliozungumza Kifaransa walikuwa bora. Nami niliwachukia watu waliozungumza Kiingereza.”

7. Yesu alishughulikaje na ubaguzi?

7 Kama ilivyokuwa katika siku za Yesu, hisia za ubaguzi zimekita mizizi mioyoni mwa watu wengi leo. Yesu alishughulikaje na hali hiyo? Kwanza, alipinga kabisa ubaguzi; aliepuka kabisa upendeleo wa aina yoyote. Aliwahubiria matajiri kwa maskini, Mafarisayo na Wasamaria, na hata wakusanya kodi na watenda dhambi. Pili, kupitia mafundisho na mfano wake, Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake kwamba lazima waepuke kuwashuku wengine au kuwabagua.

UPENDO NA UNYENYEKEVU HUTUSAIDIA KUSHINDA UBAGUZI

8. Ni kanuni gani ya msingi ambayo ndiyo nguzo ya umoja wa Kikristo? Eleza.

8 Yesu aliwafundisha wafuasi wake kanuni ya msingi ambayo ndiyo nguzo ya umoja wetu. Alisema hivi: “Nyote ni ndugu.” (Soma Mathayo 23:8, 9.) Bila shaka, sisi sote ni “ndugu” katika maana ya kwamba sote ni wazao wa Adamu. (Mdo. 17:26) Lakini kuna zaidi. Yesu alieleza kwamba wanafunzi wake ni ndugu na dada kwa sababu walitambua kwamba Yehova ndiye Baba yao wa mbinguni. (Mt. 12:50) Zaidi ya hilo, tayari walikuwa washiriki wa familia moja kubwa ya kiroho iliyounganishwa kwa upendo na imani. Ndiyo sababu katika barua walizoandika, mara nyingi mitume waliwarejelea wanafunzi wenzao kuwa ‘ndugu na dada.’—Rom. 1:13; 1 Pet. 2:17; 1 Yoh. 3:13. *

9, 10. (a) Kwa nini Wayahudi hawakuwa na sababu ya kuona jamii yao kuwa bora kuliko nyingine? (b) Yesu alitumia mfano gani kufundisha somo kuhusu jinsi ya kushinda ubaguzi wa kijamii? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

9 Baada ya kutaja waziwazi kwamba tunapaswa kuwaona waabudu wenzetu kuwa ndugu na dada zetu, Yesu alikazia umuhimu wa kuwa wanyenyekevu. (Soma Mathayo 23:11, 12.) Kama tulivyoona, kiburi kiliwafanya mitume wake wapoteze umoja wao kwa kiasi fulani. Jambo lingine ambalo huenda lilichangia tatizo hilo ni kujiona kuwa bora zaidi kuliko watu wa jamii nyingine. Je, Wayahudi walikuwa na sababu ya kujiona kuwa bora kuliko wengine kwa sababu walikuwa wazao wa Abrahamu? Ndani kabisa ya mioyo yao Wayahudi wengi waliamini hivyo. Lakini Yohana Mbatizaji aliwaambia hivi: “Mungu anaweza kumwinulia Abrahamu watoto kutoka kwenye mawe haya.”—Luka 3:8.

10 Yesu alishutumu mtazamo wa kuona jamii moja kuwa bora kuliko nyingine. Alifanya hivyo pindi moja mwandishi fulani alipomuuliza, “Kwa kweli jirani yangu ni nani?” Yesu alimjibu kwa kutoa mfano wa Msamaria aliyeonyesha fadhili kwa kumtunza msafiri fulani, Myahudi, aliyekuwa amepigwa na wezi. Wayahudi waliokuwa wakipitia njia hiyo walimpuuza mwanamume huyo aliyekuwa ameumizwa, lakini Msamaria huyo alimwonyesha huruma. Yesu alimalizia simulizi hilo kwa kumwambia mwandishi huyo awe kama Msamaria huyo. (Luka 10:25-37) Yesu alionyesha kwamba hata Msamaria anaweza kuwafundisha Wayahudi maana ya kumpenda jirani kikweli.

11. Kwa nini wanafunzi wa Kristo hawakupaswa kuwabagua watu wasio Wayahudi, na Yesu aliwasaidiaje wawe na maoni yanayofaa?

11 Ili kutimiza utume wao, wanafunzi wa Yesu walihitaji kushinda kiburi na ubaguzi waliokuwa nao. Kabla ya kurudi mbinguni, Yesu aliwaagiza watoe ushahidi “katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Awali, Yesu alikuwa amewatayarisha kwa ajili ya mgawo huo mzito kwa kuwasaidia watambue sifa nzuri za watu ambao hawakuwa Wayahudi. Alimpongeza ofisa mmoja wa jeshi asiye Myahudi kwa sababu ya imani yake ya pekee. (Mt. 8:5-10) Alipokuwa Nazareti mji wa nyumbani kwao, Yesu alizungumzia jinsi Yehova alivyokuwa amewaonyesha kibali watu wasio Wayahudi, kama vile mjane fulani Mfoinike kutoka Sarefathi na pia Naamani, mwanamume Msiria aliyekuwa na ukoma. (Luka 4:25-27) Yesu hakumhubiria mwanamke Msamaria tu, bali pia alikaa katika mji wa Samaria kwa siku mbili kwa sababu watu walipendezwa na ujumbe wake.—Yoh. 4:21-24, 40.

KUPAMBANA NA UBAGUZI KATIKA KARNE YA KWANZA

12, 13. (a) Mitume waliitikiaje Yesu alipomfundisha mwanamke Msamaria? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yakobo na Yohana hawakuelewa vizuri jambo ambalo Yesu alikuwa akijaribu kuwafundisha?

12 Haikuwa rahisi kwa mitume kushinda hisia za ubaguzi. Walistaajabu kuona kwamba Yesu alikuwa tayari kumfundisha mwanamke Msamaria. (Yoh. 4:9, 27) Viongozi wa dini ya Kiyahudi hawangezungumza na mwanamke hadharani, sembuse mwanamke Msamaria aliyekuwa na sifa mbaya. Mitume walimhimiza Yesu ale. Lakini jibu lake lilionyesha kwamba alikuwa amezama kabisa katika mazungumzo ya mambo ya kiroho hivi kwamba njaa aliyokuwa nayo haikuwa jambo la muhimu sana. Kuwahubiria wengine—hata mwanamke Msamaria—yalikuwa mapenzi ya Baba yake, naye aliiona kazi hiyo kuwa kama chakula.​—Yoh. 4:31-34.

13 Yakobo na Yohana hawakuelewa vizuri jambo hilo. Walipokuwa wakisafiri pamoja na Yesu katika eneo la Samaria, wanafunzi walitafuta mahali pa kulala katika kijiji fulani cha Wasamaria. Hata hivyo, Wasamaria walikataa kuwakaribisha. Jambo hilo liliwakasirisha sana Yakobo na Yohana nao wakapendekeza wapewe ruhusa ya kuamuru moto ushuke kutoka mbinguni na kuangamiza kijiji kizima. Yesu akawakemea kwa uthabiti. (Luka 9:51-56) Huenda tukajiuliza ikiwa kweli Yakobo na Yohana wangesema maneno hayo ikiwa kijiji hicho kingekuwa Galilaya, eneo la nyumbani kwao. Inawezekana kwamba chuki waliyokuwa nayo ilichochewa na ubaguzi. Huenda mtume Yohana aliaibikia kitendo hicho cha kulipuka kwa hasira kwani baadaye alifurahia kampeni ya kuwahubiria Wasamaria iliyokuwa na matokeo mazuri.​—Mdo. 8:14, 25.

14. Tatizo ambalo huenda lilisababishwa na tofauti za lugha lilishughulikiwaje?

14 Muda mfupi baada ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., suala la ubaguzi lilizuka. Wajane wenye uhitaji walipokuwa wakigawiwa chakula, wajane waliozungumza Kigiriki walipuuzwa. (Mdo. 6:1) Huenda walibaguliwa kwa sababu ya lugha waliyozungumza. Mitume walirekebisha mambo bila kukawia kwa kuwaweka rasmi wanaume wenye sifa za kustahili ili wasimamie kazi ya ugawaji wa chakula. Wanaume hao wote waliokuwa na sifa za kustahili kiroho walikuwa na majina ya Kigiriki. Huenda hilo liliwafariji sana wajane hao waliokuwa wameumia moyoni.

15. Petro alifanya mabadiliko gani kuhusiana na kutowabagua wengine? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

15 Katika mwaka wa 36 W.K., kazi ya kufanya wanafunzi ilihusisha kuwahubiria watu wa mataifa mengine. Mtume Petro alikuwa na desturi ya kushirikiana na Wayahudi tu. Lakini Mungu alipoweka mambo wazi kwamba Wakristo hawapaswi kuwa na ubaguzi, Petro alimhubiria Kornelio, mwanajeshi Mroma. (Soma Matendo 10:28, 34, 35.) Baada ya hapo, Petro alifurahia kushirikiana na waamini wasio Wayahudi na kula pamoja nao. Hata hivyo, miaka kadhaa baadaye, Petro aliacha kula pamoja na Wakristo wasio Wayahudi katika jiji la Antiokia. (Gal. 2:11-14) Hivyo, Paulo alimpa karipio lililofaa, naye Petro alikubali karipio hilo. Petro alipoandika barua yake ya kwanza kwa Wakristo Wayahudi na wasio Wayahudi huko Asia Ndogo, alizungumzia mambo mazuri kuhusu ushirika mzima wa akina ndugu.​—1 Pet. 1:1; 2:17.

16. Wakristo wa mapema walijulikana kwa sifa gani?

16 Ni wazi kwamba mitume walijifunza kutokana na mfano wa Yesu wa kuwapenda “watu wa namna zote.” (Yoh. 12:32; 1 Tim. 4:10) Ingawa walichukua muda mrefu kufanya mabadiliko hayo, mwishowe walirekebisha njia yao ya kufikiri. Wakristo wa mapema walijulikana kuwa watu waliopendana. Tertullian, mwandishi wa karne ya pili, alinukuu maneno haya yaliyosemwa na watu wasio Wakristo: “Wanapendana . . . Hata wako tayari kufa kwa ajili ya wenzao.” Baada ya kuvaa “utu mpya,” Wakristo wa mapema walikuja kuwaona watu wote kuwa sawa machoni pa Mungu.​—Kol. 3:10, 11.

17. Tunaweza kung’oa hisia za ubaguzi kutoka moyoni mwetu jinsi gani? Toa mifano.

17 Leo, huenda sisi pia tukachukua muda kung’oa hisia za ubaguzi kutoka moyoni mwetu. Dada mmoja kutoka Ufaransa anaeleza hivi kuhusu pambano lake: “Yehova amenifundisha maana ya upendo, maana ya kuwa mkarimu, na maana ya kuwapenda watu wa namna zote. Lakini bado ninaendelea kujifunza jinsi ya kushinda hisia za ubaguzi, na si rahisi nyakati zote. Hiyo ndiyo sababu ninaendelea kusali kuhusu jambo hilo.” Dada mwingine kutoka Hispania anakabili pambano kama hilo: “Nyakati nyingine mimi hupambana na hisia za chuki kuelekea watu wa jamii fulani, na mara nyingi ninafaulu kushinda hisia hizo. Lakini ninajua kwamba ninahitaji kuendelea kupambana. Ninamshukuru Yehova kwamba nimo katika familia iliyo na umoja.” Kila mmoja wetu anaweza kujichunguza kwa unyoofu. Je, huenda sisi binafsi tunahitaji kushinda hisia za ubaguzi kama dada hao wawili?

UBAGUZI HUFIFIA KADIRI UPENDO UNAVYOKUA

18, 19. (a) Tuna sababu zipi za kuwakubali watu wa namna zote? (b) Tutaonyeshaje kwamba tunawakubali?

18 Ni vizuri kukumbuka kwamba wakati mmoja sisi sote tulikuwa “wageni,” hatukuwa karibu na Mungu. (Efe. 2:12) Lakini Yehova alituvuta kwake “kwa kamba za upendo.” (Hos. 11:4; Yoh. 6:44) Na Kristo akatukaribisha. Ni kana kwamba alitufungulia mlango, ili tuwe sehemu ya familia ya Mungu. (Soma Waroma 15:7.) Kwa kuwa Yesu ametukubali kwa fadhili licha ya kuwa sisi si wakamilifu, hatupaswi kamwe kumwona mtu yeyote kuwa hafai!

Watumishi wa Yehova hutumia hekima kutoka juu na wameunganishwa kwa upendo (Tazama fungu la 19)

19 Hapana shaka kwamba migawanyiko, ubaguzi, na chuki, vitaendelea kuongezeka duniani kadiri tunavyokaribia mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo. (Gal. 5:19-21; 2 Tim. 3:13) Hata hivyo, tukiwa watumishi wa Yehova, tunatumia hekima inayotoka juu, ambayo haina ubaguzi na huchochea amani. (Yak. 3:17, 18) Tunashangilia tunapositawisha urafiki pamoja na watu wa nchi nyingine, tunapokubali tamaduni zao au hata kujifunza lugha zao. Tunapofanya hivyo, amani hutiririka kama mto, na haki kama mawimbi ya bahari.​—Isa. 48:17, 18.

20. Ni nini hutendeka upendo unapofinyanga akili na mioyo yetu?

20 Dada kutoka Australia aliyetajwa awali, anasema hivi: “Mabubujiko ya ujuzi wa kweli yalifunguliwa.” Anaeleza kwa unyoofu jinsi funzo la Biblia lilivyobadili mtazamo wake: “Nilifinyangwa na kupata moyo mpya na akili mpya. Hivyo, ubaguzi na chuki yote iliyokuwa imekita mizizi moyoni mwangu ikatokomea.” Na yule ndugu kutoka Kanada sasa anatambua kwamba “kwa kawaida ukosefu wa ujuzi ndio chanzo cha ubaguzi na kwamba sifa ambazo watu wanazo hazitegemei mahali walipozaliwa.” Alioa dada anayezungumza Kiingereza! Mabadiliko kama hayo ni ushahidi ulio wazi kwamba sikuzote upendo wa Kikristo hushinda ubaguzi. Upendo hutuunganisha katika kifungo kisichoweza kuvunjwa.​—Kol. 3:14.

^ fu. 8 Neno “ndugu” linaweza kutia ndani pia washiriki wa kike wa kutaniko. Paulo aliandika barua yake kwa “akina ndugu” huko Roma. Ni wazi kwamba aliwahusisha akina dada kwa kuwa aliwataja baadhi yao kwa majina. (Rom. 16:3, 6, 12) Kwa muda mrefu, gazeti la Mnara wa Mlinzi limekuwa likiwaita waamini Wakristo kuwa ‘ndugu na dada.’