Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ungependa Kutambuliwa na Nani?

Ungependa Kutambuliwa na Nani?

“Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—EBR. 6:10.

NYIMBO: 39, 30

1. Ni tamaa gani ya asili ambayo sisi sote tunayo, nayo inahusisha nini?

WEWE huhisije mtu fulani unayemjua na kumheshimu anaposahau jina lako au, jambo baya hata zaidi, hakukumbuki? Hilo linaweza kukuvunja moyo sana. Kwa nini? Kwa sababu kiasili kila mmoja wetu anatamani kukubaliwa na wengine. Hatutamani tu watu watujue kwa majina, bali pia tungependa wajue sisi ni watu wa namna gani na mambo tuliyotimiza.—Hes. 11:16; Ayu 31:6.

2, 3. Tamaa yetu ya kutaka wengine watuthamini inaweza kupotoka jinsi gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

2 Kama ilivyo na tamaa nyingine za asili, tamaa yetu ya kutaka wengine watuthamini inaweza kupita kiasi au kupotoka kwa sababu hatujakamilika. Inaweza kufanya tutamani wengine watutambue kwa njia isiyofaa. Ulimwengu wa Shetani unawachochea watu watamani umashuhuri na kutambuliwa ambako huwafanya wakengeuke na kuacha kumtambua yule ambaye hasa anastahili kutambuliwa na kuabudiwa, yaani, Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu.—Ufu 4:11.

3 Baadhi ya viongozi wa kidini wa siku za Yesu walikuwa na tamaa isiyofaa ya kutaka kutambuliwa na wengine. Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: “Jihadharini na waandishi wanaopenda kutembea wakiwa wamevaa kanzu na wanaopenda kusalimiwa sokoni, na viti vya mbele [“vilivyo bora,” maelezo ya chini] katika masinagogi na mahali penye heshima zaidi kwenye milo ya jioni.” Aliendelea kusema hivi: “Hao watapata hukumu kali zaidi.” (Luka 20:46, 47) Tofauti nao, Yesu alimpongeza mjane fulani maskini ambaye huenda mchango wake mdogo haukutambuliwa na wengine. (Luka 21:1-4) Ni wazi kwamba mtazamo wa Yesu kuhusu kutambuliwa ulikuwa tofauti kabisa. Makala hii itatusaidia tudumishe mtazamo unaofaa, mtazamo ambao Yehova anataka tuwe nao.

PENDELEO KUBWA LA KUTAMBULIWA NA YEHOVA

4. Ni nani hasa ambaye tungependa kutambuliwa naye, na kwa nini?

4 Ni nani hasa ambaye tungependa kutambuliwa naye? Hatuzungumzii kuhusu kutambuliwa kwa sababu ya elimu yetu, mafanikio ya kibiashara, au umashuhuri katika ulimwengu wa burudani. Badala yake tunazungumzia kuhusu kutambuliwa ambako Paulo alitaja aliposema hivi: “Lakini sasa kwa kuwa mmemjua Mungu au, kwamba sasa Mungu amewajua ninyi, kwa nini mnarudi tena kwenye mambo ya msingi yaliyo dhaifu na yasiyo na maana na kutaka kuyatumikia tena?” (Gal. 4:9) Wazia jinsi lilivyo pendeleo kubwa kwelikweli ‘kujulikana na Mungu,’ Mtawala Mkuu Zaidi wa ulimwengu wote! Yuko tayari kuwa na uhusiano wa karibu pamoja nasi. Kama msomi mmoja alivyosema, “tunakuwa vitu ambavyo anapenda kuvikazia uangalifu.” Tunapotambuliwa na Yehova kuwa marafiki wake, tunatimiza kusudi hasa lililofanya tuumbwe.—Mhu. 12:13, 14.

5. Tunaweza kufanya nini ili tujulikane au tutambuliwe na Mungu?

5 Musa alipata pendeleo la kuwa rafiki ya Yehova. Alipomsihi Yehova amruhusu kufahamu vizuri zaidi njia Zake, Yehova alijibu hivi: “Nitafanya pia jambo hilo unaloomba, kwa sababu umepata kibali machoni pangu nami nakujua wewe kwa jina.” (Kut. 33:12-17) Sisi pia tunaweza kupata baraka tele Yehova anapotujua kibinafsi. Lakini tunaweza kufanya nini ili tujulikane au tutambuliwe na Yehova? Tutajulikana naye tunapoanza kumpenda na tunapojiweka wakfu kwake.—Soma 1 Wakorintho 8:3.

6, 7. Ni nini kinachoweza kufanya tupoteze uhusiano wetu pamoja na Yehova?

6 Hata hivyo, tunahitaji kudumisha uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Kama ambavyo Paulo aliwaandikia Wakristo Wagalatia, sisi pia tunapaswa kuepuka kutumikia “mambo ya msingi yaliyo dhaifu na yasiyo na maana” ya ulimwengu huu, kutia ndani tamaa ya kutambuliwa na ulimwengu. (Gal. 4:9) Wakristo hao wa karne ya kwanza walikuwa wamefanya maendeleo kufikia hatua ya kujulikana na Mungu. Hata hivyo, Paulo alisema kwamba ndugu haohao walikuwa ‘wakirudi tena’ kwenye mambo yasiyofaa kitu. Kwa maneno mengine Paulo alikuwa akisema: “Baada ya kufanya maendeleo makubwa hivyo, kwa nini mrudi tena kwenye mambo ya kipumbavu na yasiyo na thamani yoyote mliyoacha nyuma?”

7 Je, tunaweza kujikuta katika hali kama hiyo leo? Ndiyo, inawezekana. Tulipoanza kumjua Yehova, kama Paulo huenda tuliacha kutafuta umashuhuri katika ulimwengu wa Shetani. (Soma Wafilipi 3:7, 8.) Huenda tuliacha fursa za kupata elimu ya juu, au ya kupandishwa cheo kazini, au ya kupata pesa nyingi katika ulimwengu wa biashara. Huenda tungekuwa mashuhuri au matajiri sana kwa sababu ya vipawa vyetu vya muziki au michezo, lakini tuliacha mambo hayo yote. (Ebr. 11:24-27) Lingekuwa jambo la kipumbavu sana kuanza kuona hatua tuliyochukua ya kuacha mambo hayo kuwa ‘fursa zilizopotea’! Mawazo hayo yanaweza kufanya tuanze kufuatilia tena mambo ya ulimwengu huu ambayo hapo awali tulifikia uamuzi kwamba ni “dhaifu na yasiyo na maana.” *

IMARISHA AZIMIO LAKO

8. Ni nini kitakachotusaidia kuimarisha azimio letu la kutaka kutambuliwa na Yehova?

8 Tunaweza kuimarishaje azimio letu la kutambuliwa na Yehova badala ya kutambuliwa na ulimwengu? Ili tufaulu kufanya hivyo, tunahitaji kukumbuka mambo mawili muhimu. Kwanza, sikuzote Yehova huwatambua wale wanaomtumikia kwa uaminifu. (Soma Waebrania 6:10; 11:6) Anamthamini sana kila mmoja wa watumishi wake, na machoni pake kuwapuuza watu walio waaminifu kwake ni sawa na ‘ukosefu wa uadilifu.’ Sikuzote Yehova “anawajua walio wake.” (2 Tim. 2:19) “Anaijua njia ya waadilifu” na anajua jinsi ya kuwakomboa kutoka kwenye jaribu.—Zab. 1:6; 2 Pet. 2:9.

9. Toa mifano ya jinsi Yehova alivyoonyesha kwamba watu wake wana kibali chake.

9 Nyakati nyingine, Yehova ameonyesha kwa njia za pekee sana kwamba watu wake wana kibali chake. (2 Nya. 20:20, 29) Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyowaokoa watu wake kwenye Bahari Nyekundu walipokuwa wakifuatiliwa na jeshi lenye nguvu la Farao. (Kut. 14:21-30; Zab. 106:9-11) Tukio hilo lilikuwa lenye kustaajabisha sana hivi kwamba hata baada ya miaka 40 kupita, bado watu wa mataifa jirani walikuwa wakizungumza kulihusu. (Yos. 2:9-11) Ni jambo lenye kutia moyo sana kwetu kukumbuka jinsi Yehova alivyoonyesha upendo na nguvu zake, kwa kuwa hivi karibuni tutakabili shambulizi la Gogu wa Magogu lililotabiriwa miaka mingi iliyopita! (Eze. 38:8-12) Wakati huo, tutafurahi sana kwamba tulijitahidi kutambuliwa na Mungu badala ya kutambuliwa na ulimwengu.

10. Tunapaswa kuzingatia jambo gani akilini kuhusu jinsi Yehova anavyowatambua watu wake?

10 Pia, tunapaswa kuzingatia akilini jambo hili la pili muhimu: Yehova anaweza kuonyesha kwamba anatutambua katika njia ambazo hatukutazamia hata kidogo. Watu wanaofanya matendo mema wakiwa na lengo hasa la kuonekana na wanadamu hawatapata thawabu yoyote kutoka kwa Yehova. Kwa nini? Tayari wamepokea thawabu kamili ya matendo yao wanaposifiwa na wanadamu. (Soma Mathayo 6:1-5.) Hata hivyo, Yesu alisema kwamba Baba yake ‘huwatazama akiwa mahali pa siri’ wale ambao hawatambuliwi kwa mambo mema wanayowafanyia wengine. Anayaona matendo hayo na kumlipa kila mtu kulingana na matendo yake. Hata hivyo, nyakati nyingine Yehova hututhawabisha katika njia ambazo hatukutazamia. Acheni tuchunguze mifano kadhaa.

MWANAMKE MNYENYEKEVU ATAMBULIWA BILA KUTAZAMIA

11. Yehova alionyeshaje kwamba alimtambua mwanamke kijana aliyeitwa Maria?

11 Wakati ulipofika wa Mwana wa Mungu kuzaliwa hapa duniani akiwa mwanadamu, Yehova alimchagua Maria, bikira mnyenyekevu, awe mama ya mtoto huyo wa pekee. Maria aliishi Nazareti, jiji dogo lisilo maarufu lililokuwa mbali na jiji la Yerusalemu na hekalu lake la kifahari. (Soma Luka 1:26-33.) Kwa nini Yehova alimchagua Maria na kumpa pendeleo hilo? Malaika Gabrieli alimwambia kwamba “amepata kibali cha Mungu.” Mazungumzo yake pamoja na Elisabeti, mtu wake wa ukoo, yalionyesha kwamba alikuwa mtu wa kiroho sana. (Luka 1:46-55) Naam, Yehova alikuwa akimtazama Maria, na kwa sababu alikuwa mwaminifu, alimpa pendeleo hilo ambalo hakutazamia.

12, 13. Yehova alionyeshaje kwamba anamtambua Yesu wakati alipozaliwa, na wakati Maria alipompeleka hekaluni siku 40 baadaye?

12 Maria alipomzaa Yesu, Yehova hakuwapa maafisa maarufu na watawala jijini Yerusalemu na Bethlehemu pendeleo la kujua kwamba Yesu amezaliwa. Malaika waliwatokea wachungaji wa hali ya chini waliokuwa wakichunga kondoo nje ya jiji la Bethlehemu. (Luka 2:8-14) Kisha wachungaji hao wakaenda kumwona mtoto huyo. (Luka 2:15-17) Hapana shaka kwamba Maria na Yosefu walishangaa na kufurahi kuona jinsi Yesu alivyoonyeshwa heshima! Fikiria tofauti iliyopo kati ya njia ya Yehova ya kufanya mambo na njia ya Ibilisi ya kufanya mambo. Shetani alipowatuma wanajimu wakamtembelee Yesu na wazazi wake, watu wote huko Yerusalemu walifadhaika walipopata habari kwamba Yesu amezaliwa. (Mt. 2:3) Habari hizo kuhusu kuzaliwa kwa Yesu zilienea kotekote, jambo lililosababisha watoto wengi wasio na hatia wauawe.—Mt. 2:16.

13 Siku 40 baada ya Yesu kuzaliwa, Maria alipaswa kumtolea Yehova dhabihu kwenye hekalu la Yerusalemu, ambalo lilikuwa kilomita 9 kutoka Bethlehemu. (Luka 2:22-24) Yosefu, Maria, na mtoto wao Yesu walipokuwa njiani kuelekea huko, huenda Maria alijiuliza ikiwa kuhani aliyekuwa akihudumu angefanya jambo fulani la pekee kuonyesha kwamba anatambua jukumu ambalo Yesu angekuwa nalo wakati ujao. Kwa kweli jukumu la Yesu lilitambuliwa, lakini katika njia ambayo huenda Maria hakutazamia. Yehova alimtumia Simeoni, mwanamume ‘mwadilifu na aliyemwogopa Mungu,’ na mjane Ana, nabii wa kike mwenye umri wa miaka 84, ili kutangaza kwamba mtoto huyo ndiye angekuwa Masihi aliyekuwa ameahidiwa, au Kristo.—Luka 2:25-38.

14. Maria alipokea baraka zipi kutoka kwa Yehova?

14 Namna gani Maria? Je, Yehova aliendelea kuonyesha kwamba anamtambua kwa sababu ya jukumu lake la kumtunza kwa uaminifu na kumlea Mwana wa Mungu? Ndiyo. Mungu alihakikisha kwamba maneno na matendo yake yaliandikwa katika Biblia. Inaonekana kwamba Maria hangeweza kusafiri pamoja na Yesu wakati wa huduma yake ya miaka mitatu na nusu. Huenda alikuwa mjane, na kwa hiyo alilazimika kubaki Nazareti. Hata hivyo, ingawa hakupata fursa ya kufurahia mambo mengi mazuri, alikuwepo pamoja na Yesu alipokuwa akifa. (Yoh. 19:26) Baadaye, Maria alikuwa Yerusalemu pamoja na wanafunzi wengine siku chache kabla ya Pentekoste, wakati ambapo roho takatifu ilimiminwa. (Mdo. 1:13, 14) Hivyo, kuna uwezekano mkubwa alitiwa mafuta pamoja na wanafunzi wengine waliokuwepo. Na ikiwa ndivyo, hilo linamaanisha kwamba alipata fursa ya kuwa pamoja na Yesu mbinguni kwa umilele wote. Alipokea thawabu nzuri ajabu kwa sababu ya utumishi wake wa uaminifu!

YEHOVA AONYESHA KWAMBA ANAMTAMBUA MWANA WAKE

15. Yesu alipokuwa duniani, Yehova alionyeshaje kwamba Mwana wake ana kibali chake?

15 Yesu hakutamani hata kidogo kutukuzwa na viongozi wa kidini au wa kisiasa wa siku zake. Bila shaka alitiwa moyo sana wakati ambapo Yehova katika pindi tatu tofauti alizungumza moja kwa moja kutoka mbinguni na kuonyesha kwamba anamtambua. Muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa kwenye Mto Yordani, Yehova alisema hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mt. 3:17) Inaonekana kwamba Yohana Mbatizaji pia alisikia maneno hayo. Kisha mwaka mmoja hivi kabla ya kifo cha Yesu, mitume wake watatu walimsikia Yehova akisema hivi kumhusu Yesu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali. Msikilizeni.” (Mt. 17:5) Mwishowe, siku chache tu kabla ya kifo cha Yesu, Yehova alizungumza tena na Mwana wake kutoka mbinguni.—Yoh. 12:28.

Unajifunza nini kutokana na jinsi ambavyo Yehova alionyesha kwamba anamtambua Mwana wake? (Tazama fungu la 15 hadi 17)

16, 17. Yehova alionyeshaje kwa njia ambayo haikutazamiwa kwamba alimtambua Yesu?

16 Ingawa Yesu alijua kwamba angekufa kifo cha aibu na angeitwa mkufuru, alisali kwamba mapenzi ya Yehova yatendeke, si yake mwenyewe. (Mt. 26:39, 42) “Alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu,” kwa sababu alitaka kutambuliwa na Baba yake, si na ulimwengu. (Ebr. 12:2) Yehova alionyeshaje kwamba anamtambua Mwana wake?

17 Alipokuwa duniani Yesu alimwomba Baba yake amrudishie utukufu aliokuwa nao mbinguni. (Yoh. 17:5) Hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba Yesu alitazamia kwamba angepewa mengi zaidi ya utukufu aliokuwa nao hapo awali. Hakutarajia kwamba sasa, baada ya kurudi mbinguni, “angepandishwa cheo.” Lakini Yehova alifanya nini? Alionyesha kwamba anamtambua Yesu katika njia ambayo haikutazamiwa alipomfufua na kumpa “cheo cha juu zaidi” na pia kitu ambacho hakuna yeyote mwingine aliyekuwa amewahi kupewa, yaani, mwili wa roho usioweza kufa! * (Flp. 2:9; 1 Tim. 6:16) Yehova alionyesha kwa njia ya pekee sana kwamba alitambua utumishi wake wa uaminifu!

18. Ni nini kitakachotusaidia tuepuke kutamani kutambuliwa na ulimwengu huu?

18 Ni nini kitakachotusaidia tuepuke kutamani kutambuliwa na ulimwengu huu? Zingatia akilini kwamba sikuzote Yehova huwatambua watumishi wake waaminifu na kwamba mara nyingi yeye hufanya hivyo katika njia ambazo hawatazamii. Kwa kweli hatuwezi kujua baraka zote tutakazopata wakati ujao! Lakini kwa sasa, tunapoendelea kuvumilia hali ngumu na majaribu ya ulimwengu huu mwovu, acheni sikuzote tukumbuke kwamba ulimwengu huu, pamoja na fursa zozote za kutambuliwa nao, zitapitilia mbali. (1 Yoh. 2:17) Baba yetu mwenye upendo, Yehova, “hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi [yetu] na upendo [tulioonyesha] kwa ajili ya jina lake.” (Ebr. 6:10) Naam, atatuonyesha kibali chake, na huenda akafanya hivyo katika njia ambazo hatuwezi kuwazia kwa sasa!

^ fu. 7 Katika tafsiri nyingine za Biblia, maneno “yasiyo na maana” yametafsiriwa kuwa “yenye upungufu” na “maskini.”

^ fu. 17 Huenda zawadi hiyo ya mwili wa roho usioweza kufa ilikuwa baraka ambayo haikutazamiwa kwa kuwa uhai usioweza kufa hautajwi popote katika Maandiko ya Kiebrania.