Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Macho Yako Yanamtazama Nani?

Macho Yako Yanamtazama Nani?

“Nayainua macho yangu kukuelekea wewe, wewe unayeketi kwenye kiti cha ufalme mbinguni.”—ZAB. 123:1.

NYIMBO: 143, 124

1, 2. Kumtazama Yehova kunahusisha nini?

TUNAISHI katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na maisha yataendelea kuwa magumu hata zaidi kabla ya ulimwengu mpya kufika na amani ya kweli kurudishwa duniani. (2 Tim. 3:1) Hivyo, ni vema kujiuliza, ‘Macho yangu yanamtazama nani ili kupata msaada na mwongozo?’ Huenda mara moja tukajibu “Yehova,” na hilo ndilo jibu bora.

2 Kumtazama Yehova kunahusisha nini? Na tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kumkazia macho yeye peke yake tunapokabili hali ngumu maishani? Karne nyingi zilizopita, mtunga zaburi mmoja alieleza umuhimu wa kuyainua macho yetu na kumtazama Yehova ili atusaidie tunapokabili hali ngumu. (Soma Zaburi 123:1-4.) Alilinganisha kitendo cha kumtazama Yehova na jinsi mtumishi anavyomtazama bwana wake. Mtunga zaburi alimaanisha nini? Mtumishi humtazama, au humtegemea, bwana wake ampe chakula na ulinzi. Lakini pia anapaswa kuendelea kumtazama bwana wake ili ajue mambo ambayo bwana wake anataka afanye, na kisha ayatekeleze. Vivyo hivyo, tunahitaji kulichunguza Neno la Mungu kila siku ili tujue mambo ambayo Yehova anataka sisi binafsi tufanye na kisha kufuata mwongozo huo. Hiyo ndiyo njia pekee ya kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia hali ngumu zitakapotokea.—Efe. 5:17.

3. Ni nini kinachoweza kutukengeusha tushindwe kuendelea kumkazia macho Yehova?

3 Ingawa tunajua umuhimu wa kuendelea kumtazama Yehova, huenda nyakati nyingine tukakengeuka. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Martha, rafiki wa karibu wa Yesu. “Alikengeushwa na kazi nyingi.” (Luka 10:40-42) Ikiwa mtu mwaminifu kama Martha alikengeuka akiwa pamoja na Yesu, hatupaswi kushangaa kwamba hali kama hiyo inaweza kutupata hata sisi. Hivyo basi, ni nini kinachoweza kutukengeusha tushindwe kuendelea kumkazia macho Yehova? Katika makala hii, tutachunguza jinsi matendo ya wengine yanavyoweza kutukengeusha. Pia, tutajifunza jinsi tunavyoweza kuendelea kumtazama Yehova.

MWANAMUME MWAMINIFU APOTEZA PENDELEO

4. Kwa nini huenda tukashangaa kwamba Musa alipoteza pendeleo la kuingia katika Nchi ya Ahadi?

4 Bila shaka Musa alimtazama Yehova ili kupata mwelekezo na mwongozo. Kwa kweli, “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yule asiyeonekana.” (Soma Waebrania 11:24-27.) Biblia inasema kwamba “hajatokea tena nabii mwingine katika Israeli aliye kama Musa, ambaye Yehova alimjua uso kwa uso.” (Kum. 34:10) Hata hivyo, ingawa Musa alikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova, alipoteza pendeleo la kuingia katika Nchi ya Ahadi. (Hes. 20:12) Ni nini kilichomfanya Musa ajikwae?

5-7. Ni tatizo gani lililozuka muda mfupi baada ya Waisraeli kutoka Misri, na Musa alilishughulikiaje?

5 Katika kipindi kisichozidi miezi miwili tangu Waisraeli walipotoka Misri—hata kabla hawajafika kwenye Mlima Sinai—tatizo fulani kubwa lilitokea. Watu walianza kulalamika kwamba hakukuwa na maji. Walianza kumnung’unikia Musa, na hali ilizidi kuwa mbaya hivi kwamba Musa akamlilia Yehova akisema: “Nifanye nini na watu hawa? Hivi punde watanipiga mawe!” (Kut. 17:4) Yehova alimjibu Musa kwa kumpa maagizo yaliyo wazi. Alipaswa kuchukua fimbo yake na kuupiga mwamba huko Horebu, na baada ya hapo maji yangebubujika. Tunasoma hivi: “Musa akafanya hivyo mbele ya wazee wa Israeli.” Waisraeli walikunywa maji na kutosheka, na hivyo tatizo hilo likasuluhishwa.—Kut. 17:5, 6.

6 Biblia inasema kwamba Musa “[alipaita] mahali hapo Masa na Meriba, kwa sababu ya ugomvi wa Waisraeli na kwa sababu walimjaribu Yehova kwa kusema: ‘Je, Yehova yuko katikati yetu au la?’” (Kut. 17:7) Majina hayo yalifaa kwa sababu yanamaanisha “Kujaribu” na “Kugombana.”

7 Tukio hilo la Meriba lilimfanya Yehova ahisije? Yehova aliona kwamba Waisraeli walikuwa wakimwasi yeye, akiwa Mungu wao, na kupinga mamlaka yake; hawakuwa wakimpinga Musa tu. (Soma Zaburi 95:8, 9.) Walikuwa wamekosea sana. Wakati huo, Musa alitenda kwa njia inayofaa alipomtazama Yehova na kufuata mwongozo wake kwa makini.

8. Ni tatizo gani lililozuka Waisraeli walipokaribia mwisho wa safari yao ya miaka 40 nyikani?

8 Lakini ni nini kilichotendeka tatizo hilohilo lilipozuka miaka 40 hivi baadaye, Waisraeli walipokuwa wakikaribia mwisho wa safari yao nyikani? Waisraeli walifika kwenye eneo ambalo baadaye lilikuja kujulikana kuwa Meriba. Lakini eneo hili lilikuwa eneo tofauti na lile la kwanza, nalo lilikuwa karibu na Kadeshi, karibu na mpaka wa Nchi ya Ahadi. * Kwa mara nyingine tena Waisraeli walinung’unika kwamba hawakuwa na maji. (Hes. 20:1-5) Lakini wakati huu, Musa alitenda tofauti kabisa.

9. Musa alipokea maagizo gani, lakini alitendaje? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

9 Musa alitendaje uasi huo ulipotokea? Kwa mara nyingine tena alimtazama Yehova ili ampe mwongozo. Lakini wakati huu Yehova hakumwambia aupige mwamba. Alimwambia Musa achukue fimbo, awakusanye watu mbele ya mwamba, na kisha azungumze na mwamba. (Hes. 20:6-8) Hata hivyo, Musa hakuzungumza na mwamba huo. Badala yake, aliwaka hasira na kuwakemea watu waliokuwa wamekusanyika kwa kusema hivi: “Sikilizeni sasa, enyi waasi! Je, ni lazima tuwatolee maji katika mwamba huu?” Kisha akaupiga mwamba huo si mara moja tu, bali akaupiga mara mbili.—Hes. 20:10, 11.

10. Yehova alitendaje Musa alipokosa kufuata mwongozo?

10 Yehova alimkasirikia Musa vikali. (Kum. 1:37; 3:26) Kwa nini Yehova alitenda hivyo? Huenda mambo kadhaa yalihusika. Kama tulivyoona, huenda Yehova alimkasirikia Musa vikali kwa sababu hakufuata mwongozo mpya aliokuwa amepokea.

11. Kwa nini huenda Musa alipoupiga mwamba Waisraeli wangefikiri kwamba huo haukuwa muujiza wa Yehova?

11 Kuna uwezekano mwingine. Miamba iliyo karibu na eneo la Meriba ya kwanza ilikuwa imefanyizwa na mawe magumu ya matale au graniti. Mwamba wa graniti hauwezi kwa vyovyote kutoa maji hata upigwe kwa nguvu kadiri gani. Hata hivyo, miamba iliyo katika eneo la Meriba ya pili ni tofauti kabisa, na mara nyingi ni ya chokaa nyepesi. Kwa sababu chokaa huwa na matundu-matundu, mara nyingi maeneo yenye miamba ya chokaa huwa na maji chini ya ardhi, hivyo mtu anaweza kuchimba na kupata maji. Je, inawezekana kwamba Musa alipoupiga mwamba huo mara mbili, aliwapa watu sababu ya kufikiri kwamba maji yalitokea tu yenyewe kiasili na si Yehova aliyeyatokeza? Musa alipoupiga mwamba badala ya kuzungumza nao, je, aliwafanya watu waone kana kwamba huo haukuwa muujiza? * Hatuwezi kuwa na uhakika kuhusu hilo.

JINSI MUSA ALIVYOASI

12. Huenda ni sababu gani nyingine iliyomfanya Yehova awakasirikie vikali Musa na Haruni?

12 Kuna sababu nyingine ambayo huenda ilimfanya Yehova awakasirikie vikali Musa na Haruni. Ona jinsi Musa alivyowaambia watu: “Je, ni lazima tuwatolee maji katika mwamba huu?” Aliposema “tuwatolee,” huenda Musa alikuwa akimaanisha yeye na Haruni. Maneno hayo yalionyesha ukosefu mkubwa wa heshima kwa Yehova akiwa Chanzo halisi cha muujiza huo. Ukweli wa kwamba huenda Musa hakuonyesha heshima unathibitishwa na maneno ya Zaburi 106:32, 33: “Walimkasirisha kwenye maji ya Meriba, na mambo yakamwendea Musa vibaya kwa sababu yao. Waliitia uchungu roho yake, naye akaongea bila kufikiri kwa midomo yake.” * (Hes. 27:14) Vyovyote vile, kupitia matendo yake, Musa hakumwelekezea Yehova heshima aliyostahili. Yehova aliwaambia hivi Musa na Haruni: “Ninyi wawili mliasi agizo nililowapa.” (Hes. 20:24) Hiyo ilikuwa dhambi kubwa sana!

13. Kwa nini hukumu ambayo Yehova alitoa dhidi ya Musa ilikuwa ya haki na isiyo na upendeleo?

13 Wakiwa viongozi wa watu wa Yehova, Musa na Haruni waliwajibika zaidi mbele za Yehova. (Luka 12:48) Hapo awali, Yehova alikataa kizazi kizima cha Waisraeli kiingie katika nchi ya Kanaani kwa sababu ya uasi wao. (Hes. 14:26-30, 34) Hivyo, Yehova alitenda kwa haki na bila upendeleo kwa kutoa hukumu ileile dhidi ya Musa kwa sababu ya uasi wake. Na kama tu ilivyokuwa kwa Waisraeli wengine walioasi, Musa hakuruhusiwa kuingia katika Nchi ya Ahadi.

CHANZO CHA TATIZO

14, 15. Ni nini kilichomfanya Musa aasi?

14 Ni nini kilichomfanya Musa asitawishe mtazamo wa uasi? Tazama tena Zaburi 106:32, 33: “Walimkasirisha [Yehova] kwenye maji ya Meriba, na mambo yakamwendea Musa vibaya kwa sababu yao. Waliitia uchungu roho yake, naye akaongea bila kufikiri kwa midomo yake.” Ingawa Waisraeli walimkasirisha Yehova, Musa ndiye aliyetiwa uchungu. Alikosa sifa ya kujizuia naye akazungumza bila kufikiria matokeo ya maneno yake.

15 Musa aliruhusu matendo ya wengine yamkengeushe na kuacha kumkazia macho Yehova. Musa alishughulikia vizuri kisa cha kwanza. (Kut. 7:6) Hata hivyo, inawezekana kwamba baada ya kushughulika kwa miaka mingi na Waisraeli waasi, alianza kuchoka na kuvunjika moyo. Je, Musa alikuwa akifikiria tu hisia zake badala ya kukazia fikira jinsi ambavyo angeweza kumtukuza Yehova?

16. Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito mambo ambayo Musa alifanya?

16 Ikiwa nabii mwaminifu kama Musa alikengeuka na kujikwaa, ni rahisi kwetu pia kujikuta katika hali kama hiyo. Kama Musa, sisi pia tumekaribia kuingia katika Nchi ya mfano ya Ahadi, yaani, ulimwengu mpya ambao Yehova ametuahidi. (2 Pet. 3:13) Hakuna yeyote kati yetu ambaye angependa kukosa pendeleo hilo la pekee. Hata hivyo, ili tufikie lengo letu, tunahitaji kuendelea kumkazia macho Yehova, sikuzote tukijitahidi kufanya mapenzi yake. (1 Yoh. 2:17) Tunapaswa kujifunza somo gani kutokana na kosa ambalo Musa alifanya?

USIKENGEUSHWE NA MATENDO YA WENGINE

17. Ni nini kitakachotusaidia tusichokozeke wengine wanapotuudhi?

17 Usichokozeke kwa sababu ya matendo ya wengine. Hata tukilazimika kupambana na matatizo yaleyale tena na tena, “tusife moyo katika kufanya mema, kwa maana kwa wakati unaofaa tutavuna ikiwa hatutachoka kabisa.” (Gal. 6:9; 2 The. 3:13) Tunapokabili hali zinazotuchosha kihisia au tunapopatwa na matatizo yaleyale kwa sababu ya migongano ya utu, je, tunazuia midomo yetu na kudhibiti hasira yetu? (Met. 10:19; 17:27; Mt. 5:22) Wengine wanapotuudhi, tunapaswa kujifunza ‘kuiachia ghadhabu nafasi.’ Ghadhabu ya nani? Ghadhabu ya Yehova. (Soma Waroma 12:17-21.) Tukiendelea kumtazama Yehova, tutampa heshima anayostahili kwa kuiachia nafasi ghadhabu yake, tukingoja kwa subira achukue hatua wakati anapoona kuwa inafaa kufanya hivyo. Kutenda kinyume na hilo kwa kujilipizia kisasi kwa njia yoyote ile ni sawa na kumvunjia Yehova heshima.

18. Tunahitaji kukumbuka nini inapohusu kutii miongozo?

18 Fuata kwa makini miongozo mipya. Je, tunafuata kwa uaminifu miongozo mipya ambayo Yehova ametupatia? Ikiwa ndivyo, hatutafanya mambo kama tulivyozoea kufanya awali. Badala yake, tutatii bila kukawia miongozo yoyote mipya inayotolewa na Yehova kupitia tengenezo lake. (Ebr. 13:17) Wakati huohuo tutakuwa waangalifu kwamba “[tusipite] mambo yaliyoandikwa.” (1 Kor. 4:6) Tukifanya hivyo, tutaendelea kumkazia macho Yehova.

Tunajifunza somo gani kutokana na jinsi Musa alivyotenda wengine walipokosea? (Tazama fungu la 19)

19. Tunaweza kufanya nini ili tusiharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova hata ingawa huenda wengine wametukosea?

19 Usiruhusu makosa ya wengine yaharibu uhusiano wako pamoja na Yehova. Ikiwa tutaendelea kumkazia Yehova macho yetu ya mfano, hatutaruhusu matendo ya wengine yatutie uchungu au yaharibu uhusiano wetu pamoja naye. Ni muhimu hata zaidi kuzingatia jambo hilo ikiwa, kama Musa, tuna mapendeleo fulani katika tengenezo la Mungu. Ingawa ni kweli kwamba kila mmoja wetu anahitaji ‘kuendelea kuufanyia kazi wokovu wake mwenyewe kwa kuogopa na kutetemeka,’ tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova humhukumu mtu mmoja-mmoja ikitegemea hali na mapendeleo aliyo nayo. (Flp. 2:12) Kadiri tulivyo na mapendeleo mengi zaidi, ndivyo tunavyowajibika zaidi mbele za Yehova. (Luka 12:48) Lakini ikiwa tunampenda Yehova kikweli, hakuna jambo litakalotukwaza au kututenganisha na upendo wake.—Zab. 119:165; Rom. 8:37-39.

20. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Katika nyakati hizi zenye changamoto nyingi, acheni tuendelee kuyainua macho yetu kumwelekea Yule “[anayeketi] kwenye kiti cha ufalme mbinguni,” ili tuweze kutambua mapenzi yake. Tusiruhusu kamwe uhusiano wetu pamoja na Yehova uathiriwe na matendo ya wengine. Mambo yaliyompata Musa yanakazia akilini na moyoni mwetu somo hilo muhimu. Badala ya kuchokozeka kwa sababu ya makosa ya wengine yanayosababishwa na hali ya kutokamilika, na tuazimie kuacha ‘macho yetu yamtazame Yehova Mungu wetu mpaka atakapotuonyesha kibali.’—Zab. 123:1, 2.

^ fu. 8 Eneo hili la Meriba lilikuwa tofauti na eneo la Meriba lililokuwa karibu na Refidimu. Tofauti na eneo la kwanza, eneo hili la pili lilihusianishwa na eneo la Kadeshi, si Masa. Hata hivyo, maeneo yote mawili yalipewa jina Meriba kwa sababu ya ugomvi uliotokea huko.—Tazama ramani iliyo kwenye Nyongeza ya B3 kwenye Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

^ fu. 11 Profesa John A. Beck anaeleza hivi kuhusu simulizi hilo: “Kulingana na mapokeo ya Kiyahudi, waasi wanamdhihaki Musa kwa kusema hivi: ‘Musa anajua vizuri mwamba huu ni wa aina gani! Ikiwa angependa kuonyesha nguvu zake za kimuujiza, acha atutolee maji kutoka kwenye mwamba huu mwingine.’” Lakini hayo ni mapokeo tu.

^ fu. 12 Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Oktoba 15, 1987, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji.”