Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Macho Yako Yanaangalia Wapi?

Macho Yako Yanaangalia Wapi?

“Ninainua macho yangu kukuelekea wewe, wewe mwenye kukaa ukiwa mufalme mbinguni.”​—ZB. 123:1.

NYIMBO: 143, 124

1, 2. Kumuangalia Yehova, maana yake nini?

TUNAISHI katika “nyakati za hatari” zenye kuwa “ngumu kuvumilia.” (2 Ti. 3:1) Na mbele Yehova aharibu ulimwengu huu muovu na kuleta amani ya kweli katika dunia, maisha yatakuwa nguvu hata zaidi. Kwa hiyo, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninamuangalia nani ili kupata musaada na muongozo?’ Pengine tunaweza kujibu hivi bila kusita: “Ninamuangalia Yehova.” Na hilo ndilo jibu la muzuri zaidi.

2 Kumuangalia Yehova maana yake nini? Na namna gani tunaweza kuhakikisha kama tunaendelea kumuangalia wakati tuko na magumu? Zamani sana, muandikaji mumoja wa Biblia alieleza kama ni jambo la lazima kabisa kumuangalia Yehova wakati tuko na lazima ya musaada. (Soma Zaburi 123:1-4.) Alisema kama wakati tunamuangalia Yehova, tuko kama mutumishi mwenye anamuangalia bwana wake. Namna gani? Mutumishi anamuangalia, ao kumutegemea, bwana wake ili kupata chakula na ulinzi. Lakini anapaswa pia kumuangalia bwana wake kila mara ili kuelewa mambo yenye bwana wake anapenda afanye, na kisha anapaswa kuyafanya. Vilevile, sisi pia tunapaswa kujifunza Neno la Mungu kwa uangalifu kila siku ili kuelewa mambo yenye Yehova anapenda tufanye, na kisha tunapaswa kuyafanya. Kama tu tunafanya vile, tunaweza kuwa hakika kama Yehova atatusaidia wakati tuko na lazima ya musaada.​—Efe. 5:17.

3. Ni nini inaweza kutukengeusha ili tusiendelee kumuangalia Yehova?

3 Hata kama tunajua kwamba sikuzote tunapaswa kumuangalia Yehova, wakati fulani tunaweza kukengeushwa. Hilo ndilo jambo lenye lilimufikia Marta, rafiki wa sana wa Yesu. “Alikengeushwa na kazi nyingi.” (Lu. 10:40-42) Ikiwa mutu muaminifu kama Marta alikengeushwa wakati Yesu alikuwa tu pale pamoja naye, hatupaswe kushangaa kama jambo hilo linatufikia pia. Kwa hiyo, ni nini inaweza kutukengeusha ili tusiendelee kumuangalia Yehova? Katika habari hii, tutazungumuzia namna tunaweza kukengeushwa na matendo ya wengine. Na tutajifunza namna tunaweza kuendelea kumuangalia Yehova.

MWANAUME MUAMINIFU ALIPOTEZA PENDELEO LAKE

4. Musa alipoteza pendeleo la kuingia katika Inchi ya Ahadi. Sababu gani hilo linaweza kutushangaza?

4 Bila shaka, Musa alikuwa anamuangalia Yehova ili kupata muongozo. Biblia inasema kama “aliendelea kuwa imara kama mutu mwenye anamuona Ule mwenye haonekane.” (Soma Waebrania 11:24-27.) Inasema pia kama “hakujatokea tena nabii mwingine katika Israeli mwenye kuwa kama Musa, mwenye Yehova alijua uso kwa uso.” (Kum. 34:10) Lakini, hata kama Musa alikuwa rafiki wa sana wa Yehova, alipoteza pendeleo lake la kuingia katika Inchi ya Ahadi. (Hes. 20:12) Sababu gani?

5-7. Ni jambo gani lilitokea kisha tu Waisraeli kutoka Misri, na Musa alifanya nini?

5 Miezi mbili ilikuwa haijaenea tangu Waisraeli watoke Misri, na mbele hata wafike kwenye Mulima Sinai, jambo fulani nzito lilitokea. Watu walianza kunungunika kwa sababu walikosa maji. Walianza kumunungunikia Musa na wakakasirika sana, kwa hiyo “Musa akamulilia Yehova akisema: ‘Nifanye nini na watu hawa? Kisha wakati kidogo tu watanipiga majiwe!’” (Kut. 17:4) Yehova alimupatia Musa maagizo yenye kuwa wazi. Yehova alimuambia akamate fimbo yake na apige mwamba wenye ulikuwa katika Horebu. Biblia inasema hivi: “Musa akafanya vile mbele ya wazee wa Israeli.” Kisha maji yakatoka katika mwamba huo, Waisraeli wakapata maji mengi ya kunywa, na tatizo lao likaisha.​—Kut. 17:5, 6.

6 Biblia inasema kama Musa aliita mahali pale Masa, maana yake “Kujaribu,” na Meriba, maana yake “Ugomvi.” Sababu gani? “Kwa sababu ya ugomvi wa Waisraeli na kwa sababu walimujaribu Yehova kwa kusema: ‘Je, Yehova iko katikati yetu ao hapana?’”​—Kut. 17:7.

7 Namna gani Yehova aliona jambo hilo lenye lilitokea Meriba? Aliona kama Waisraeli hawakukuwa wamemuasi Musa tu, lakini walikuwa wamemuasi yeye pia na mamlaka yake. (Soma Zaburi 95:8, 9.) Jambo lenye Waisraeli walifanya lilikuwa la mubaya sana. Lakini Musa alifanya jambo la muzuri. Alimuangalia Yehova na kisha akafuata maagizo yake kwa uangalifu.

8. Ni nini ilitokea wakati Waisraeli walikaribia kumaliza safari yao katika jangwa?

8 Lakini, ni nini ilitokea katika hali kama hiyo miaka 40 hivi kisha pale? Waisraeli walikuwa wanakaribia kumaliza safari yao katika jangwa. Walifika mahali fulani karibu na Kadeshi, karibu na mupaka wa Inchi ya Ahadi. Mahali pale pakaitwa pia Meriba. * (Ona maelezo ya chini.) Sababu gani? Kwa sababu Waisraeli walinungunika tena kwamba mahali pale hapakukuwa na maji. (Hes. 20:1-5) Lakini wakati huo, Musa alifanya kosa kubwa.

9. Yehova alipatia Musa maagizo gani, lakini Musa alifanya nini? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

9 Musa alifanya nini wakati watu waliasi? Tena, alimuangalia Yehova ili kupata muongozo. Lakini wakati huo Yehova hakumuambia Musa apige mwamba. Alimuambia akamate fimbo yake, aende na watu karibu na mwamba, na kisha azungumuze na mwamba. (Hes. 20:6-8) Musa alifanya vile? Hapana. Alikuwa mwenye kuvunjika moyo na mwenye kukasirika sana mupaka akafokea watu na kusema hivi: “Musikie, sasa, ninyi waasi! Je, tunapaswa kuwatoshea maji katika mwamba huu?” Kisha akapiga mwamba huo, hapana mara moja tu, lakini mara mbili.​—Hes. 20:10, 11.

10. Yehova alijisikia namna gani kwa sababu ya jambo lenye Musa alifanya?

10 Yehova alimukasirikia sana Musa. (Kum. 1:37; 3:26) Sababu gani Yehova alijisikia vile? Sababu moja inaweza kuwa hii: Musa hakutii maagizo ya mupya yenye Yehova alikuwa amemupatia.

11. Wakati Musa alipiga mwamba, pengine alifanya Waisraeli wafikiri kama Yehova hakufanya muujiza. Sababu gani?

11 Kunaweza kuwa sababu ingine yenye ilimufanya Yehova akasirike. Miamba mikubwa ya Meriba ya kwanza ni majiwe ya nguvu-nguvu sana. Hata mutu apige majiwe hayo kwa nguvu sana, hakuna mwenye anaweza kutazamia kama maji yatatoka ndani. Lakini miamba ya Meriba ya pili iko tofauti sana. Miamba mingi kati ya miamba hiyo ni aina fulani ya miamba yenye kuitwa majiwe ya chokaa. Kwa sababu majiwe ya chokaa ni aina ya miamba yenye kuwa teketeke, mara nyingi maji kidogo-kidogo yanaingia katika miamba hiyo na kujikusanya chini ya udongo. Kisha, watu wanaweza kupata maji hayo kwa kutoboa tundu katika mwamba. Kwa hiyo, wakati Musa alipiga mwamba kuliko kusema na mwamba huo, pengine Waisraeli waliwaza kama maji yalitoka tu yenyewe. Hawakuona kama ni kwa sababu Yehova alifanya muujiza. * (Ona maelezo ya chini.) Lakini hatuwezi kuhakikisha jambo hilo.

NAMNA MUSA ALIASI

12. Pengine ni sababu gani ingine yenye ilimufanya Yehova amukasirikie Musa na Haruni?

12 Kunaweza kuwa sababu ingine yenye ilifanya Yehova amukasirikie sana Musa na Haruni. Musa aliambia watu hivi: “Je, tunapaswa kuwatoshea maji katika mwamba huu?” Wakati Musa alisema “tunapaswa,” pengine alimaanisha yeye na Haruni. Maneno ya Musa yalimukosea Yehova heshima sana kwa sababu hakuonyesha kama ni Yehova ndiye alifanya muujiza huo. Zaburi 106:32, 33 inasema hivi: “Walimukasirisha kwenye maji ya Meriba, na mambo yakamuendea Musa mubaya kwa sababu yao. Walitia uchungu roho yake, naye akaongea bila kufikiri kupitia midomo yake.” * (Ona maelezo ya chini.) (Hes. 27:14) Musa hakumupatia Yehova utukufu wenye anastahili. Yehova alimuambia hivi Musa na Haruni: “Ninyi wawili muliasi agizo langu.” (Hes. 20:24) Hiyo ilikuwa zambi nzito sana!

13. Sababu gani namna yenye Yehova alimuazibu Musa ilikuwa ya haki?

13 Yehova alitazamia Musa na Haruni wafanye mengi zaidi, kwa sababu walikuwa wanaongoza watu wake. (Lu. 12:48) Mbele ya Musa kuasi, Yehova alikuwa amekatalia kizazi chote cha Waisraeli kuingia katika Inchi ya Ahadi kwa sababu walikuwa wamemuasi. (Hes. 14:26-30, 34) Kwa hiyo, wakati Musa aliasi, Yehova alitenda kwa haki kwa kumuazibu kwa njia ileile. Kama tu waasi hao wengine, Musa hakuruhusiwa kuingia katika Inchi ya Ahadi.

JAMBO LENYE LILIFANYA MUSA AMUASI YEHOVA

14, 15. Ni nini ilifanya Musa amuasi Yehova?

14 Ni nini ilifanya Musa amuasi Yehova? Ona tena Zaburi 106:32, 33. Inasema hivi: “Walimukasirisha kwenye maji ya Meriba, na mambo yakamuendea Musa mubaya kwa sababu yao. Walitia uchungu roho yake, naye akaongea bila kufikiri kupitia midomo yake.” Kwa hiyo, hata kama ni Yehova ndiye Waisraeli waliasi, Musa ndiye alitiwa uchungu, ao kukasirika. Hakuonyesha sifa ya kujizuia lakini alisema bila kufikiria matokeo ya jambo hilo.

15 Musa aliacha kumuangalia Yehova kwa sababu aliruhusu matendo ya wengine yamukengeushe. Wakati watu walinungunika juu ya maji kwa mara ya kwanza, Musa alifanya jambo la muzuri. (Kut. 7:6) Lakini pengine alichoka na kukasirika kwa sababu Waisraeli walikuwa wamemuasi Yehova kwa miaka mingi. Pengine Musa alianza sasa kufikiria tu namna alikuwa anajisikia kuliko kufikiria namna angeweza kumuletea Yehova utukufu.

16. Sababu gani tunapaswa kufikiria jambo lenye Musa alifanya?

16 Ikiwa nabii muaminifu kama Musa alikengeushwa na kufanya zambi, jambo hilo linaweza pia kutufikia kwa vyepesi. Musa alikuwa karibu kuingia katika Inchi ya Ahadi, na sisi pia tuko karibu kuingia katika dunia mupya. (2 Pe. 3:13) Kwa kweli, hatupendi kupoteza pendeleo hilo la pekee. Lakini, ili tuingie katika dunia mupya, tunapaswa kuendelee kumuangalia Yehova na kumutii sikuzote. (1 Yo. 2:17) Kosa lenye Musa alifanya linaweza kutufundisha nini?

USIACHE MATENDO YA WENGINE YAKUKENGEUSHE

17. Tunapaswa kufanya nini ili tuepuke kupoteza sifa ya kujizuia wakati wengine wanatukasirisha?

17 Usipoteze sifa yako ya kujizuia wakati wengine wanakukasirisha. Wakati fulani, tunapatwa na magumu yaleyale tena na tena. Lakini Biblia inasema hivi: “Tusiache kufanya mema, kwa maana kwa wakati wenye kufaa tutavuna kama hatuchoke kabisa.” (Gal. 6:9; 2 Te. 3:13) Wakati jambo fulani ao mutu fulani anatukasirisha tena na tena, je tunawaza mbele ya kusema? Je, tunazuia kasirani yetu? (Mez. 10:19; 17:27; Mt. 5:22) Wakati wengine wanatuchokoza, tunapaswa kujifunza ‘kuachia kasirani kali nafasi,’ ao kumuachia Yehova nafasi ya kuonyesha kasirani yake. (Soma Waroma 12:17-21.) Hilo linamaanisha nini? Kuliko kukasirika, tunamungojea Yehova kwa uvumilivu ili afanye jambo fulani juu ya magumu yetu wakati yeye mwenyewe anaona kuwa ni lazima kufanya vile. Kama tunajaribu kujilipizia kisasi kuliko kumuangalia Yehova, kufanya vile itakuwa kumukosea heshima.

18. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu kufuata maagizo?

18 Fuata kwa uangalifu maagizo ya mupya. Je, tunafuata kwa uaminifu maagizo ya mupya yenye Yehova ametupatia? Hatupaswe kuendelea kufanya mambo namna tumeyafanya sikuzote kwa sababu tu tumezoea kufanya vile. Lakini, tunapaswa kuwa tayari kufuata maagizo yote ya mupya yenye Yehova anatupatia kupitia tengenezo lake. (Ebr. 13:17) Pia, tunapaswa kuwa waangalifu ili ‘tusipite mambo yenye yaliandikwa.’ (1 Ko. 4:6) Wakati tunafuata kwa uangalifu maagizo ya Yehova, tunaendelea kumuangalia.

Namna Musa alitenda wakati wengine walifanya makosa, inaweza kutufundisha nini? (Picha hii inapatana na fungu la 19)

19. Tunaweza kufanya nini ili tusiruhusu makosa ya wengine yaharibu urafiki wetu pamoja na Yehova?

19 Usiruhusu makosa ya wengine yaharibu urafiki wako pamoja na Yehova. Kama tunaendelea kumuangalia Yehova, hatutaharibu urafiki wetu pamoja naye wala kukasirika kwa sababu ya matendo ya wengine. Hilo ni jambo la maana, zaidi sana kama tuko na madaraka fulani katika tengenezo la Mungu, kama vile Musa. Kwa kweli, kila mumoja wetu anapaswa kujikaza sana na kumutii Yehova ili aokolewe. (Flp. 2:12) Hata hivyo, kama tuko na madaraka mengi, Yehova anatuomba pia tufanye mengi zaidi. (Lu. 12:48) Lakini, kama tunamupenda Yehova kabisa, hakuna jambo lolote lenye litafanya tujikwae ao kututenganisha na upendo wake.​—Zb. 119:165; Ro. 8:37-39.

20. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Tunaishi katika wakati wenye magumu mengi. Kwa hiyo, ni jambo la maana sana tuendelee kumuangalia Yehova, mwenye ‘kukaa akiwa mufalme mbinguni,’ ili tuelewe mambo yenye anapenda tufanye. Hatupaswe kuruhusu hata kidogo matendo ya wengine yaharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. Jambo lenye lilimufikia Musa linatufundisha jambo hilo la maana sana. Kuliko kutenda kwa kasirani wakati wengine wanafanya makosa, tuazimie ‘kumuangalia Yehova Mungu wetu mupaka wakati atatuonyesha wema.’​—Zb. 123:1, 2.

^ fu. 8 Meriba hii iko tofauti na Meriba ya karibu na Refidimu yenye iliitwa pia Masa. Lakini, mahali hizo mbili ziliitwa Meriba kwa sababu Waisraeli walinungunika pale.​—Ona karte katika Nyongeza B3 ya Biblia​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya.

^ fu. 11 Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia anasema kama, kulingana na hadisi fulani ya Wayahudi, waasi hao walisema kama hakuna muujiza wenye ulifanyika kwa sababu Musa alijua kama kulikuwa maji ndani ya mwamba huo. Kwa hiyo, walimuomba afanye muujiza huo kwenye mwamba mwingine. Lakini, hiyo ni hadisi tu.

^ fu. 12 Ona habari yenye kichwa “Maswali Kutoka kwa Wasomaji Wetu” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 10, 1987.