Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wanaotoa kwa Ukarimu Ni Watu Wenye Furaha

Watu Wanaotoa kwa Ukarimu Ni Watu Wenye Furaha

“Kuna furaha . . . katika kutoa.”—MDO. 20:35.

NYIMBO: 76, 110

1. Uumbaji unatoa uthibitisho gani kwamba Yehova ni mkarimu?

HATA ingawa Yehova alikuwa peke yake kabla ya kuumba kitu chochote, hakuwa akijifikiria yeye tu. Badala yake, aliwapa zawadi ya uhai viumbe wenye akili, yaani, viumbe wa roho na wanadamu. “Mungu mwenye furaha,” Yehova, anapenda kuwapa wengine vitu vizuri. (1 Tim. 1:11; Yak. 1:17) Na kwa kuwa anataka sisi pia tuwe na furaha, anatufundisha kuwa wakarimu.—Rom. 1:20.

2, 3. (a) Kwa nini kuwa wakarimu hutufanya tuwe na furaha? (b) Tutachunguza nini?

2 Mungu alimuumba mwanadamu kwa mfano wake. (Mwa. 1:27) Hilo linamaanisha kwamba tuliumbwa tukiwa na uwezo wa kuiga sifa za utu wake. Hivyo, ili tuwe na furaha na turidhike, tunahitaji kumwiga Yehova kwa kuwafikiria wengine na pia kuwa watoaji wakarimu. (Flp. 2:3, 4; Yak. 1:5) Kwa nini? Jibu rahisi ni kwamba Yehova alichochewa na upendo kuwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuonyesha sifa ya ukarimu. Licha ya kuwa sisi si wakamilifu, tunaweza kufaulu kuiga sifa ya Yehova ya ukarimu.

3 Biblia hutuambia jinsi tunavyoweza kuwa watoaji wakarimu. Acheni tuchunguze baadhi ya mambo ambayo Maandiko hufundisha kuhusu ukarimu. Tutaona jinsi kuwa wakarimu hutusaidia tupate kibali cha Mungu na jinsi kusitawisha sifa hiyo hutusaidia kutimiza jukumu ambalo Mungu ametupatia. Pia, tutachunguza jinsi kuonyesha sifa ya ukarimu kunavyohusiana na kuwa wenye furaha na kwa nini tunahitaji kuendelea kuisitawisha.

JINSI TUNAVYOWEZA KUPATA KIBALI CHA MUNGU

4, 5. Yehova na Yesu wametuwekea mfano gani kuhusu ukarimu?

4 Yehova anataka viumbe wake wa kibinadamu wamwige, hivyo yeye hufurahi tunapokuwa wakarimu. (Efe. 5:1) Tunapotazama jinsi tulivyoumbwa na umaridadi na ubora wa mazingira ya asili yanayotuzunguka, tunaona wazi kabisa kwamba Mungu anataka wanadamu wawe na furaha. (Zab. 104:24; 139:13-16) Hivyo, tunamheshimu tunapojitahidi kuwafanya wengine wawe na furaha.

5 Wakristo wa kweli humwiga Kristo, ambaye aliweka kielelezo kikamilifu cha jinsi wanadamu wanavyoweza kuwa wakarimu. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mwana wa binadamu [alikuja], si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa uhai wake uwe fidia badala ya wengi.” (Mt. 20:28) Hivyo, mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo: “Iweni na mtazamo huu wa akili ambao pia Kristo Yesu alikuwa nao . . . Alijiondolea hali yake na kuchukua umbo la mtumwa.” (Flp. 2:5, 7) Ni vizuri kila mmoja wetu ajiulize hivi: ‘Je, ninaweza kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu hata zaidi kuliko ninavyofanya sasa?’—Soma 1 Petro 2:21.

6. Yesu alitufundisha somo gani katika mfano wa Msamaria mwema? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

6 Tunaweza kupata kibali cha Mungu kwa kuiga mfano mkamilifu wa Yehova na Kristo, kwa kufikiria hali njema ya wengine na kwa kutafuta njia za kuwatimizia mahitaji yao. Kwa kweli, katika mfano wake wa Msamaria mwema, Yesu alionyesha wazi kwamba aliwatazamia wafuasi wake wajidhabihu ili wawasaidie wengine, hata wale wanaotoka katika malezi tofauti nao. (Soma Luka 10:29-37.) Je, unakumbuka swali ambalo lilimfanya Yesu asimulie mfano wa Msamaria mwema? Myahudi fulani alimuuliza hivi: “Kwa kweli jirani yangu ni nani?” Jibu la Yesu linaonyesha kwamba, kama Msamaria huyo, lazima tuwe tayari kutoa kwa ukarimu ikiwa tunataka kupata kibali cha Mungu.

7. Kuna uhusiano gani kati ya suala la enzi kuu na kuwa mbinafsi au mkarimu?

7 Wakristo wana sababu nyingi nzuri za kuwa wakarimu. Kwa mfano, sifa hiyo inahusiana na suala lililozushwa na Shetani katika bustani ya Edeni. Jinsi gani? Shetani alidai kwamba Adamu na Hawa—na wanadamu wote kwa ujumla—wangekuwa na maisha bora ikiwa wangejifikiria tu wenyewe na kutanguliza mapendezi yao badala ya kumtii Mungu. Hawa aliongozwa na ubinafsi alipotamani kuwa kama Mungu. Adamu alionyesha ubinafsi alipochagua kumpendeza Hawa badala ya kumtii Mungu. (Mwa. 3:4-6) Tunajionea wazi matokeo ya maamuzi yao. Kwa kweli, ubinafsi hauwezi kamwe kutuletea furaha. Tunapokuwa wakarimu, tunaonyesha kuwa tunasadiki kwamba njia ya Mungu ya kufanya mambo ndio njia bora.

KUTIMIZA JUKUMU AMBALO MUNGU AMEWAPA WATU WAKE

8. Kwa nini wenzi wa kwanza wa ndoa walipaswa kuzingatia sifa ya ukarimu?

8 Mungu aliwapa wenzi wa kwanza wa ndoa maagizo ambayo yangewafanya wafikirie hali njema ya wengine, ingawa walikuwa peke yao katika bustani ya Edeni. Yehova aliwabariki Adamu na Hawa na kuwatia moyo wazaane, waijaze dunia, na kuitiisha. (Mwa. 1:28) Kama tu ambavyo Muumba alihangaikia sana hali njema ya viumbe wake, wazazi wetu wa kwanza walipaswa kuhangaikia furaha ya watoto wao ambao hawakuwa wamezaliwa. Walipaswa kuifanya dunia yote kuwa paradiso kwa faida ya wazao wa Adamu. Mradi huo mkubwa ungehitaji wote katika familia hiyo iliyozidi kuongezeka washirikiane.

9. Kwa nini kupanua Paradiso kungewaletea wanadamu furaha?

9 Ili wanaume na wanawake wakamilifu wafaulu kutimiza kazi ya kupanua Paradiso, wangehitaji kushirikiana kikamili na Yehova ili kutimiza mambo aliyokusudia kufanya, na hivyo kuingia katika pumziko lake. (Ebr. 4:11) Wazia jinsi ambavyo mradi huo ungekuwa wenye kuthawabisha na kuridhisha! Kujitoa kwa ajili ya manufaa ya wengine kungewaletea baraka tele na furaha nyingi.

10, 11. Tunaweza kutimizaje utume wa kuhubiri na kufanya wanafunzi?

10 Leo, Yehova amewapa watu wake kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Ili kutimiza utume huo, tunahitaji kupendezwa kutoka moyoni na hali njema ya wengine. Tutafaulu kuendelea kufanya kazi hiyo ikiwa tu tutachochewa na mambo yanayofaa, yaani, upendo kwa Mungu na jirani yetu.

11 Katika karne ya kwanza W.K., Paulo alijirejelea yeye na baadhi ya watu waliofanya kazi pamoja naye kwa ukaribu kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” kwa sababu ya jukumu lao la kupanda na kutia maji mbegu za kweli ya Ufalme. (1 Kor. 3:6, 9) Leo, sisi pia tunaweza kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” kwa kutoa kwa ukarimu wakati, mali, na nguvu zetu ili kufanya kazi tuliyopewa na Mungu ya kuhubiri. Hilo ni pendeleo kubwa sana!

Kuwasaidia watu wanaothamini kweli za kiroho waelewe kweli hizo ni miongoni mwa mambo machache sana yanayoridhisha (Tazama fungu la 12)

12, 13. Unaweza kusema kazi ya kufanya wanafunzi ina thawabu zipi?

12 Kutumia wakati na nguvu zetu kwa ukarimu katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi hutuletea shangwe kubwa. Wengi ambao wamepata pendeleo la kuwafundisha wanafunzi wa Biblia wanaofanya maendeleo watakwambia kwamba kufanya hivyo ni miongoni mwa mambo machache sana yanayoridhisha. Tunafurahi sana tunapoona nyuso za wanafunzi wenye kuthamini kweli ziking’aa wanapoelewa kweli za Biblia, imani yao inapokua, wanapofanya mabadiliko, na kuanza kuwaambia wengine kweli hizo. Yesu pia alifurahi sana wakati wale wahubiri 70 aliokuwa amewatuma kuhubiri ‘waliporudi wakiwa na shangwe’ kwa sababu ya matokeo mazuri waliyokuwa wamepata.—Luka 10:17-21.

13 Ndugu na dada zetu ulimwenguni pote hushangilia kuona ujumbe wa habari njema ukiwasaidia watu kubadili maisha yao. Fikiria mfano wa Anna, dada kijana aliye mseja, ambaye alipanua utumishi wake kwa kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri lililo Mashariki mwa Ulaya. * Anaandika hivi: “Hapa, kuna fursa nyingi za kuwafundisha watu Biblia, jambo linalonifurahisha sana. Utumishi wangu hunipa shangwe nyingi sana. Ninaporudi nyumbani, sina muda wa kujifikiria sana. Mimi huwafikiria wale ninaojifunza nao—matatizo yao na mahangaiko yao. Mimi hutafuta njia za kuwatia moyo na kuwasaidia. Na sasa nimesadiki kwamba ‘kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’”—Mdo. 20:35.

Tunapotembelea kila nyumba katika eneo letu, tunawapa watu fursa ya kukubali au kukataa ujumbe wa Ufalme (Tazama fungu la 14)

14. Hata ikiwa ni watu wachache tu wanaokubali kusikiliza habari njema, unaweza kupata furaha jinsi gani katika huduma yako?

14 Tutakuwa na furaha kwa kuwapa watu fursa ya kuamua watakavyoitikia ujumbe wa habari njema, iwe watasikiliza au la. Kwa kweli, utume wetu leo unafanana na utume wa nabii Ezekieli, ambaye Yehova alimwambia hivi: “Ni lazima uwaambie maneno yangu, iwe watasikiliza au la.” (Eze. 2:7; Isa. 43:10) Iwe watu hawatathamini ujumbe wetu Yehova anathamini jitihada zetu. (Soma Waebrania 6:10.) Mhubiri mmoja alionyesha mtazamo mzuri sana kuhusiana na jambo hilo. Aliandika hivi kuhusu huduma yake: “Tumepanda, tumetia maji, na tumesali tukitumaini kwamba Yehova atachochea hamu yao ya kujifunza iendelee kukua.”—1 Kor. 3:6.

JINSI YA KUWA NA FURAHA

15. Watu wengi hutendaje wanapoonyeshwa ukarimu, na je, itikio lao linapaswa kuathiri jinsi tunavyotenda?

15 Yesu anataka tupate furaha kwa kuwa wakarimu. Kwa kawaida, watu huthamini wanapoonyeshwa ukarimu. Yesu alihimiza hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, nanyi mtapewa. Watawamwagia kwenye mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa, na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachowapimia watu, ndicho watakachowapimia.” (Luka 6:38) Ni kweli kwamba si wote wanaothamini ukarimu tunaowaonyesha, lakini baadhi yao wanapouthamini, ukarimu wetu unaweza kuwachochea wawaonyeshe wengine ukarimu pia. Hivyo, uwe na zoea la kuwaonyesha watu ukarimu iwe watathamini au la. Huwezi kujua utatimiza mambo gani mazuri kwa tendo moja tu la ukarimu.

16. Ni nini kinachopaswa kutuchochea kuwaonyesha wengine ukarimu?

16 Watu wakarimu kikweli hawawaonyeshi wengine ukarimu ili wapate faida fulani. Yesu alikuwa na wazo hilo akilini alipofundisha hivi: “Unapoandaa karamu, waalike maskini, viwete, vilema, na vipofu; nawe utakuwa mwenye furaha, kwa sababu hawana kitu cha kukulipa.” (Luka 14:13, 14) Mwandikaji mmoja aliyeongozwa na roho takatifu aliandika hivi: “Mtu mkarimu atabarikiwa.” Mwingine aliandika hivi: “Mwenye furaha ni mtu yeyote anayemjali mtu wa hali ya chini.” (Met. 22:9; Zab. 41:1) Kwa hakika, tunapaswa kuwa wakarimu kwa sababu tunapata furaha kwa kuwasaidia wengine.

17. Ni kutoa kwa aina gani ambako kutakufanya uwe na furaha?

17 Paulo aliponukuu maneno ya Yesu kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea,” hakuwa akirejelea tu kuwapa watu vitu vya kimwili, bali pia kuwatia wengine moyo, kuwapa mwongozo, na msaada wale wanaouhitaji. (Mdo. 20:31-35) Kupitia maneno na mfano wake, mtume huyo alitufundisha tuwe tukijitoa, yaani, tutoe muda wetu, nguvu zetu, fikira zetu, na upendo wetu.

18. Waandishi wengi wamefikia mkataa gani kuhusu ukarimu?

18 Pia, watafiti katika nyanja za sayansi ya jamii wametambua kwamba kuwa wakarimu huwafanya watu wawe na furaha. Kulingana na makala moja, “watu huripoti kwamba wanapata furaha nyingi zaidi baada ya kuwatendea wengine matendo ya fadhili.” Watafiti wanasema kwamba kuwasaidia wengine ni jambo muhimu ambalo huwasaidia watu wawe na maisha yenye ‘kusudi zaidi kwa sababu kufanya hivyo hutimiza uhitaji wa msingi wa mwanadamu.’ Hivyo, mara nyingi wataalamu hupendekeza kwamba watu wajitolee kufanya utumishi wa umma ili kuboresha afya zao na kuwafanya wawe na furaha zaidi. Hilo haliwashangazi wale wanaokubali kwamba Biblia ni Neno kutoka kwa Yehova, Muumba mwenye upendo wa wanadamu.—2 Tim. 3:16, 17.

ENDELEA KUSITAWISHA SIFA YA UKARIMU

19, 20. Una sababu zipi zinazokuchochea utamani kuwa mkarimu?

19 Inaweza kuwa changamoto kudumisha roho ya ukarimu ikiwa tumezungukwa na watu wanaotanguliza mapendezi yao badala ya mapendezi ya wengine. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba amri mbili kuu ni kumpenda Yehova kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zetu zote na kumpenda jirani yetu kama tunavyojipenda. (Marko 12:28-31) Kama tulivyoona katika makala hii, wale wanaompenda Yehova humwiga. Yehova huonyesha ukarimu, na Yesu pia hufanya vivyo hivyo. Wanapendekeza tuwaige kwa sababu tutakuwa na furaha kikweli kwa kufanya hivyo. Tukijitahidi kuonyesha roho hiyo ya ukarimu tunapomtumikia Mungu au kushughulika na jirani zetu, tutamletea Yehova heshima, tutawanufaisha wengine, nasi pia tutanufaika.

20 Hapana shaka kwamba tayari unajitahidi kujitoa ili uwasaidie wengine, hasa waamini wenzako. (Gal. 6:10) Ukiendelea kufanya hivyo, kwa hakika utapendwa na kuthaminiwa na wengine, na hilo litakufanya uwe na furaha. Andiko la Methali 11:25 linasema hivi: “Mtu mkarimu atapata ufanisi, na yule anayewaburudisha wengine yeye mwenyewe ataburudishwa.” Bila shaka, kutoa bila ubinafsi, kuonyesha fadhili, na ukarimu kunaweza kuonyeshwa katika njia mbalimbali na katika nyanja mbalimbali za maisha na huduma ya Kikristo, na kufanya hivyo huleta thawabu nyingi. Makala inayofuata itazungumzia baadhi ya njia na nyanja hizo.

^ fu. 13 Jina limebadilishwa.