Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Habari Kamili?

Je, Una Habari Kamili?

“Yeyote anayejibu kabla ya kusikia ukweli wa mambo, huo ni upumbavu na aibu kwake.”—MET. 18:13.

NYIMBO: 126, 95

1, 2. (a) Ni uwezo gani muhimu tunaopaswa kusitawisha, na kwa nini? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

TUKIWA Wakristo wa kweli, tunapaswa kusitawisha uwezo wa kuchanganua habari na kufikia mkataa au uamuzi ulio sahihi. (Met. 3:21-23; 8:4, 5) Tusipositawisha uwezo huo, itakuwa rahisi zaidi kwa Shetani na ulimwengu wake kupotosha akili zetu. (Efe. 5:6; Kol. 2:8) Ukweli ni kwamba hatuwezi kufikia uamuzi ulio sahihi ikiwa hatuna habari kamili. Andiko la Methali 18:13 linasema hivi: “Yeyote anayejibu kabla ya kusikia ukweli wa mambo, huo ni upumbavu na aibu kwake.”

2 Katika makala hii, tutachunguza changamoto mbalimbali zinazofanya iwe vigumu kupata habari za kweli zitakazotusaidia kufikia uamuzi ulio sahihi. Pia, tutachunguza kanuni na mifano mbalimbali katika Biblia inayoweza kutusaidia kuboresha uwezo wetu wa kuchanganua habari kwa usahihi.

USIAMINI “KILA NENO”

3. Kwa nini tunahitaji kutumia kanuni ya Biblia iliyo kwenye Methali 14:15? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Leo, watu wamezungukwa na habari nyingi sana. Vituo vya Intaneti, televisheni, na vyombo vingine vya habari husambaza habari chungu nzima kuhusu mambo mbalimbali. Pia, watu wengi hupokea barua-pepe, jumbe fupi, na ripoti mbalimbali kutoka kwa marafiki na watu wanaowafahamu. Kwa kuwa zoea la kusambaza kimakusudi habari zisizo za kweli na kupotosha ukweli wa mambo limeenea sana, tuna sababu nzuri ya kuwa waangalifu na kuchanganua kwa makini mambo tunayosikia. Ni kanuni gani ya Biblia inayoweza kutusaidia? Andiko la Methali 14:15 linasema hivi: “Mjinga huamini kila neno, lakini mwerevu hutafakari kila hatua.”

4. Andiko la Wafilipi 4:8, 9 linatusaidiaje inapohusu kuchagua habari tutakazosoma, na kwa nini ni muhimu sana kupata habari sahihi? (Tazama pia sanduku “ Maandalizi ya Kutusaidia Kupata Habari Kamili.”)

4 Ili kufanya maamuzi mazuri, tunahitaji habari zinazotegemeka. Hivyo, tunahitaji kuwa wateuzi sana na kuchagua kwa makini ni habari gani tutakayosoma. (Soma Wafilipi 4:8, 9.) Hatupaswi kupoteza muda wetu kutazama vituo vya habari vya Intaneti visivyotegemeka au kusoma ripoti ambazo hazijathibitishwa zinazosambazwa kupitia barua-pepe. Na ni jambo la muhimu hasa kuepuka tovuti za waasi imani. Kusudi lao kuu ni kudhoofisha imani ya watu wa Mungu na kupotosha ukweli. Habari zisizotegemeka zitasababisha ufanye maamuzi yasiyo sahihi. Usipuuze kamwe jinsi akili na moyo wako unavyoweza kuathiriwa sana na habari zenye kupotosha.—1 Tim. 6:20, 21.

5. Waisraeli walisikiliza habari gani ya uwongo, nayo iliwaathirije?

5 Kuamini habari za uwongo kunaweza kusababisha matatizo makubwa. Kwa mfano, fikiria yale yaliyotokea katika siku za Musa, wakati wapelelezi 10 kati ya wapelelezi 12 waliokuwa wametumwa wakapeleleze Nchi ya Ahadi walipoleta habari mbaya. (Hes. 13:25-33) Maelezo yao yaliyotiwa chumvi na yenye kushtua yaliwafanya watu wa Yehova wavunjike moyo kabisa. (Hes. 14:1-4) Kwa nini walivunjika moyo? Huenda walifikiri kwamba kwa kuwa idadi kubwa ya wapelelezi walileta habari mbaya, basi zilikuwa za kweli. Walikataa kusikiliza habari nzuri zilizokuwa zimeletwa na Yoshua na Kalebu, wanaume waliotegemeka. (Hes. 14:6-10) Badala ya kutafuta ukweli wa mambo na kumtumaini Yehova, waliamua kuamini habari mbaya waliyoletewa. Upumbavu ulioje!

6. Kwa nini hatupaswi kushangaa tunaposikia habari zenye kushtua kuhusu watu wa Yehova?

6 Tunahitaji kuwa waangalifu hasa tunaposikia habari fulani kuhusu watu wa Yehova. Usisahau kamwe kwamba Shetani ni mshtaki wa watumishi waaminifu wa Mungu. (Ufu. 12:10) Hivyo, Yesu alituonya kwamba wale wanaotupinga “[wangetusingizia] kila aina ya uovu.” (Mt. 5:11) Tukizingatia kwa uzito onyo hilo, hatutashangaa tunaposikia habari zenye kushtua kuhusu watu wa Yehova.

7. Kabla ya kuwatumia wengine barua-pepe au ujumbe mfupi, tunapaswa kujiuliza nini?

7 Je, wewe unapenda kuwatumia rafiki zako na watu unaowafahamu barua-pepe au ujumbe mfupi? Ikiwa ndivyo, mara tu unapopata habari mpya au kusikia jambo fulani, huenda ukahisi kama mwandishi wa habari ambaye hutamani sana kuwa wa kwanza kuripoti kuhusu habari fulani mpya yenye kusisimua. Hata hivyo, kabla ya kutuma ujumbe huo au barua-pepe hiyo, jiulize hivi: ‘Je, nina hakika kwamba habari ninayotaka kueneza ni ya kweli? Je, kweli nina habari kamili?’ Ikiwa huna uhakika, basi huenda bila kutambua ukasambaza habari zisizo za kweli miongoni mwa akina ndugu. Ukiwa na shaka kuhusu habari ulizopata, zifute mara moja, usizitume.

8. Katika nchi fulani, wapinzani wetu wamefanya nini, na ni kwa njia gani tunaweza kushirikiana nao bila kujua?

8 Kuna hatari nyingine ya kuwatumia wengine bila kufikiri barua-pepe au jumbe fupi tulizopokea. Katika baadhi ya nchi, kazi yetu imewekewa vizuizi au hata imepigwa marufuku. Katika nchi hizo, wapinzani huenda wakaeneza kimakusudi habari zilizokusudiwa kutuogopesha au kufanya tuache kuaminiana. Fikiria mambo yaliyotukia chini ya utawala wa Muungano wa Sovieti. Polisi wa siri, wanaojulikana kama KGB, walieneza uvumi kwamba ndugu kadhaa wenye mapendeleo walikuwa wamewasaliti watu wa Yehova. * Ndugu wengi waliamini habari hizo za uwongo na wakaacha kushirikiana na tengenezo la Yehova. Inasikitisha sana! Inafurahisha kwamba baadaye wengi wao walirudi kwenye tengenezo. Hata hivyo, wengine hawakurudi. Imani yao ilivunjika. (1 Tim. 1:19) Tunaweza kufanya nini ili tusipatwe na msiba kama huo? Usieneze habari zisizofaa au habari ambazo hazijathibitishwa. Usiwe mwepesi wa kuamini kila jambo unalosikia. Hakikisha kwamba una habari kamili.

HABARI ZISIZO KAMILI

9. Ni jambo gani lingine linaloweza kufanya iwe vigumu kupata habari sahihi?

9 Habari zisizo kamili au ambazo kwa sehemu si za kweli zinaweza pia kufanya iwe vigumu kwetu kujua ukweli wa mambo. Habari ambayo ina ukweli kwa asilimia 10 tu, ni habari isiyoweza kutegemeka hata kidogo. Tunaweza kufanya nini ili tusipotoshwe na habari zenye hila ambazo huenda zikawa na mambo fulani ya kweli?—Efe. 4:14.

10. Kwa nini Waisraeli walikuwa karibu kupigana na ndugu zao, na ni nini kilichowasaidia wasipigane nao?

10 Fikiria jinsi ilivyokuwa kwa Waisraeli waliokuwa wakiishi upande wa magharibi wa Mto Yordani katika siku za Yoshua. (Yos. 22:9-34) Walipokea habari kwamba Waisraeli waliokuwa wakiishi upande wa mashariki wa Mto Yordani (kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase) walikuwa wamejenga madhabahu kubwa inayovutia karibu na mto huo. Habari hiyo ilikuwa ya kweli, lakini haikuwa kamili. Wakitegemea habari hizo ambazo hazikuwa kamili, Waisraeli waliokuwa wakiishi upande wa magharibi walifikia mkataa kwamba ndugu zao walikuwa wamemwasi Yehova, hivyo wakakusanyika ili wapigane vita na ndugu zao waliokuwa upande wa mashariki. (Soma Yoshua 22:9-12.) Hata hivyo, kabla ya kuwashambulia, Waisraeli hao waliwatuma wanaume fulani wenye kutegemeka ili wapate habari kamili. Waligundua nini? Waligundua kwamba Waisraeli wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase walikuwa wamejenga madhabahu hiyo ili itumiwe si kwa ajili ya dhabihu, bali iwe ishara ya ukumbusho. Ilijengwa ili wakati ujao kila mtu afahamu kwamba wao pia walikuwa watumishi waaminifu wa Yehova. Hapana shaka Waisraeli hao walifurahi sana kwamba hawakuwaangamiza ndugu zao kwa msingi wa habari ambazo hazikuwa kamili, na badala yake walitumia wakati ili wapate habari kamili!

11. (a) Mefiboshethi alipatwa na madhara gani kwa sababu ya kutendewa isivyo haki? (b) Daudi angeepukaje kumtendea Mefiboshethi isivyo haki?

11 Tukiwa mtu mmoja-mmoja, sisi pia tunaweza kupatwa na madhara kwa sababu ya habari zilizopotoshwa au zisizo kamili ambazo huenda zikaenezwa kutuhusu. Fikiria mfano wa Mfalme Daudi na Mefiboshethi. Daudi alimwonyesha Mefiboshethi ukarimu na fadhili kwa kumrudishia ardhi yote iliyokuwa ya Sauli, babu yake. (2 Sam. 9:6, 7) Hata hivyo, baadaye Daudi alipata habari fulani mbaya kumhusu Mefiboshethi. Bila kuchunguza ikiwa habari hizo zilikuwa za kweli, Daudi alimnyang’anya Mefiboshethi mali zake zote. (2 Sam. 16:1-4) Hatimaye Daudi alipozungumza na Mefiboshethi, alitambua kosa lake na kumrudishia sehemu ya mali aliyomnyang’anya. (2 Sam. 19:24-29) Lakini Daudi angeepuka kutenda isivyo haki ikiwa angetumia wakati ili kupata habari kamili, badala ya kufanya uamuzi haraka-haraka kwa kutegemea habari zisizo kamili.

12, 13. (a) Yesu alishughulikaje na habari zenye uchongezi? (b) Tunaweza kufanya nini mtu fulani anapoeneza habari zisizo za kweli kutuhusu?

12 Lakini vipi ikiwa mtu fulani anaeneza mashtaka yenye uchongezi dhidi yako? Yesu na Yohana Mbatizaji walikabili hali kama hiyo. (Soma Mathayo 11:18, 19.) Yesu alishughulikaje na habari zisizo za kweli? Hakutumia wakati wake wote na nguvu zake kujitetea. Badala yake aliwatia watu moyo wachunguze ukweli wa mambo, yaani, mambo aliyofanya na kufundisha. Naye alisema hivi: “Hekima hutetewa kuwa yenye uadilifu kupitia kazi zake.”—Mt. 11:19; maelezo ya chini.

13 Kuna jambo fulani muhimu ambalo Yesu anatufundisha. Nyakati nyingine, huenda watu wakasema mambo fulani yasiyo ya kweli kutuhusu au wakatuchambua. Huenda tukatamani sana haki itendeke au tukatamani kufanya jambo fulani ili kurudisha sifa yetu nzuri. Je, kuna jambo fulani tunaloweza kufanya? Mtu anapoeneza habari fulani ya uwongo kutuhusu, tunaweza kuthibitisha kwamba habari hiyo si ya kweli kupitia jinsi tunavyoishi. Kwa kweli, kama tu mfano wa Yesu unavyoonyesha, maisha yetu ya unyoofu ya Kikristo yatathibitisha wazi kwamba mashtaka hayo si ya kweli.

JE, WEWE HUJIAMINI KUPITA KIASI?

14, 15. Kutegemea uelewaji wetu wenyewe kunaweza kuwa mtego jinsi gani?

14 Tumeona kwamba mojawapo ya mambo yanayoweza kufanya tushindwe kufikia uamuzi ulio sahihi ni kutokuwa na habari kamili. Hata hivyo, kuna changamoto nyingine kubwa; sisi si wakamilifu. Vipi ikiwa tumekuwa tukimtumikia Yehova kwa miaka mingi? Huenda tumesitawisha uwezo mzuri wa kufikiri na pia utambuzi. Huenda ndugu na dada wanatuheshimu sana kwa sababu sisi hufanya maamuzi mazuri. Lakini, je, hilo linaweza kuwa mtego pia?

15 Ndiyo, kutegemea sana uelewaji wetu wenyewe kunaweza kuwa mtego. Hisia na maoni yetu wenyewe yanaweza kuanza kuongoza fikira zetu. Huenda tukaanza kuhisi kwamba tuna uwezo wa kuchanganua hali fulani na kuielewa hata ingawa hatuna habari zote zinazohusika. Jambo hilo ni hatari sana! Biblia inatuonya waziwazi tusitegemee uelewaji wetu wenyewe.—Met. 3:5, 6; 28:26.

16. Kama kisa hiki cha kuwaziwa kinavyoonyesha, ni jambo gani lililotokea kwenye mkahawa fulani, na Tom alifikia mkataa gani haraka-haraka?

16 Fikiria kisa hiki cha kuwaziwa. Jioni moja, Tom, mzee mwenye uzoefu, alienda kwenye mkahawa. Akiwa huko alishtuka kumwona mzee mwenzake anayeitwa John, akiwa ameketi na mwanamke fulani ambaye hakuwa mke wake. Tom aliwaona wakicheka pamoja huku wakifurahia sana mazungumzo yao, na hata walikumbatiana. Jambo hilo lilizidi kumhangaisha sana. Je, sasa John na mke wake watatalikiana? Hali itakuwaje kwa mke wa John? Namna gani watoto wao? Hapo awali Tom alikuwa amejionea ndugu na dada wengine wakipitia hali kama hizo zenye kuvunja moyo. Wewe ungehisije ikiwa ungeona mambo hayo?

17. Kama tulivyoona katika kisa hicho cha kuwaziwa, Tom alijifunza nini, nasi tunajifunza nini?

17 Lakini hebu tua kidogo. Ingawa Tom alifikia mkataa haraka kwamba John hakuwa mwaminifu kwa mke wake, je, kweli alikuwa na habari kamili? Baadaye jioni hiyo, Tom alimpigia John simu. Wazia jinsi Tom alivyohisi alipogundua kwamba mwanamke huyo alikuwa dada wa kimwili wa John ambaye alikuwa amemtembelea kutoka eneo lingine. John na dada yake hawakuwa wameonana kwa miaka mingi. Kwa kuwa dada yake alikuwa katika eneo hilo kwa muda mfupi tu, fursa pekee waliyopata ilikuwa kukutana kwenye mkahawa kwa ajili ya chakula. Mke wa John hakuweza kujiunga nao. Jambo zuri ni kwamba Tom hakuwa amemweleza yeyote maoni yake yasiyo sahihi. Tunajifunza nini? Hata iwe tumemtumikia Yehova kwa miaka mingi kadiri gani, bado tunahitaji kuwa na habari kamili kabla ya kufikia mkataa kuhusu jambo lolote.

18. Migongano ya utu inaweza kuathirije maoni yetu kuhusu ndugu zetu?

18 Jambo lingine linaloweza kufanya iwe vigumu kuchanganua mambo kwa usahihi ni wakati kunapokuwa na migongano ya utu baina yetu na ndugu mwingine kutanikoni. Ikiwa tutakazia fikira tofauti zetu, huenda tukaanza kumshuku ndugu yetu. Hivyo, tunaposikia habari zisizofaa kumhusu ndugu huyo, huenda ikawa rahisi kwetu kuziamini. Tunajifunza nini? Tunapokuwa na maoni yasiyofaa kumwelekea ndugu yetu, inaweza kuwa rahisi kwetu kufikia mkataa usiofaa unaotegemea habari ambazo si kamili. (1 Tim. 6:4, 5) Tunaweza kuepuka hali hiyo kwa kuondolea mbali wivu kutoka mioyoni mwetu. Badala ya kuruhusu hisia hizo mbaya zituathiri, acheni tutambue wajibu tulionao wa kuwapenda ndugu zetu na kuwasamehe kwa hiari kutoka moyoni.—Soma Wakolosai 3:12-14.

KANUNI ZA BIBLIA ZITATULINDA

19, 20. (a) Ni kanuni gani za Biblia zitakazotusaidia kuchanganua habari kwa usahihi? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

19 Leo, ni vigumu kujua ukweli wa mambo na kuchanganua habari kwa usahihi kwa sababu tumezungukwa na habari nyingi zisizo za kweli, habari ambazo si kamili, na sisi pia si wakamilifu. Ni nini kitakachotusaidia kukabiliana na changamoto hiyo? Ni lazima tujue kanuni za Biblia na tuzitumie. Mojawapo ya kanuni hizo inasema kwamba ni upumbavu na aibu kujibu kabla ya kusikia ukweli wa mambo. (Met. 18:13) Kanuni nyingine ya Biblia inatukumbusha kwamba hatupaswi kuamini kila neno bila kuthibitisha ikiwa habari hiyo ni ya kweli. (Met. 14:15) Na mwishowe, hata iwe tumemtumikia Yehova kwa miaka mingi kadiri gani, ni lazima tuwe waangalifu na kuepuka kutegemea uelewaji wetu wenyewe. (Met. 3:5, 6) Kanuni za Biblia zitatulinda ikiwa tutahakikisha kwamba tuna habari kamili kutoka kwenye chanzo kinachotegemeka, zitakazotusaidia kufikia mkataa unaofaa na kufanya maamuzi yenye hekima.

20 Hata hivyo, kuna changamoto nyingine. Changamoto hiyo ni mwelekeo wa kuwahukumu wengine kwa kutazama sura ya nje. Katika makala inayofuata, tutachunguza baadhi ya mambo yanayoweza kufanya tunaswe na mtego huo, na jinsi tunavyoweza kuyaepuka.

^ fu. 8 Tazama Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2004, uku. 111-112, na Kitabu cha Mwaka cha 2008, uku. 133-135.