Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usihukumu kwa Kutazama Sura ya Nje

Usihukumu kwa Kutazama Sura ya Nje

“Acheni kuhukumu kwa kutazama sura ya nje tu, bali hukumuni kwa uadilifu.”—YOH. 7:24.

NYIMBO: 142, 123

1. Isaya alitabiri nini kumhusu Yesu, na kwa nini unabii huo unatutia moyo?

UNABII wa Isaya kumhusu Bwana wetu Yesu Kristo unatupa uhakika na tumaini. Isaya alitabiri kwamba Yesu “hatahukumu kwa mambo anayoona kwa macho yake, wala kukaripia kulingana tu na mambo anayosikia kwa masikio yake. Atawahukumu kwa haki watu wa hali ya chini.” (Isa. 11:3, 4) Kwa nini unabii huo unatutia moyo? Kwa sababu tunaishi katika ulimwengu uliojaa ubaguzi na upendeleo. Sote tunatamani kuwa na Hakimu mkamilifu ambaye hatatuhukumu kamwe kwa kutazama sura yetu!

2. Yesu alituamuru tufanye nini, na tutachunguza nini katika makala hii?

2 Kwa kawaida, sisi huwa na maoni fulani kuwahusu watu tunaokutana nao kwa kutazama sura zao. Na kwa kuwa sisi ni wanadamu wasio wakamilifu, hatuwezi kuhukumu mambo kwa njia kamilifu kama Yesu anavyofanya. Tuna mwelekeo wa kuongozwa na mambo tunayoona kwa macho. Hata hivyo, Yesu alipokuwa duniani, aliamuru hivi: “Acheni kuhukumu kwa kutazama sura ya nje tu, bali hukumuni kwa uadilifu.” (Yoh. 7:24) Ni wazi kwamba Yesu anataka tuwe kama yeye na tusiwahukumu wengine kwa kutazama sura yao. Katika makala hii, tutachunguza mambo matatu ambayo mara nyingi huathiri maoni ya watu kuwaelekea wanadamu wenzao: rangi au jamii, vitu vya kimwili, au umri. Tutachunguza pia jinsi tunavyoweza kutii amri ya Yesu kuhusu kila moja ya mambo hayo.

USIWAHUKUMU WENGINE KWA MSINGI WA RANGI AU JAMII YAO

3, 4. (a) Ni matukio gani yaliyomfanya Petro achunguze upya maoni yake kuelekea watu wasio Wayahudi? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Yehova alimsaidia Petro kuelewa ukweli gani mpya?

3 Wazia mambo ambayo mtume Petro alikuwa akifikiria alipoombwa kwenda Kaisaria katika nyumba ya Kornelio, mtu asiye Myahudi. (Mdo. 10:17-29) Kama Wayahudi wengine wa nyakati zake, tangu utotoni Petro aliamini kwamba watu wasio Wayahudi walikuwa watu wasio safi. Hata hivyo, Petro alikuwa amejionea mambo yaliyofanya achunguze upya maoni yake. Kwa mfano, Petro alikuwa ametoka tu kupokea maono kwa njia ya kimuujiza. (Mdo. 10:9-16) Alikuwa ameona nini? Kitu kama shuka kubwa lililojaa wanyama wasio safi liliteremshwa mbele yake huku sauti nzito kutoka mbinguni ikamwamuru hivi: “Petro, simama, chinja ule!” Petro alikataa kwa uthabiti. Kisha sauti hiyo ikamwambia “[aache] kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” Alipoamka kutoka katika maono hayo, Petro alishangazwa na kile ambacho sauti hiyo ilikuwa ikimwambia. Wakati huohuo, wajumbe kutoka kwa Kornelio wakawasili. Baada ya kupokea mwongozo kupitia roho takatifu, Petro aliinuka na kuandamana na wajumbe hao hadi kwenye nyumba ya Kornelio.

4 Ikiwa Petro angehukumu mambo kwa kutazama sura ya nje tu, hangeingia katika nyumba ya Kornelio. Kwa kawaida, Wayahudi hawakuingia katika nyumba za watu wasio Wayahudi. Kwa nini Petro alienda kwa Kornelio licha ya ubaguzi uliokita sana mizizi moyoni mwake? Maoni ya Petro yalibadilika sana baada ya kuona maono hayo na kupokea uhakikisho kupitia roho takatifu. Baada ya kusikiliza mambo ambayo Kornelio alieleza, Petro alichochewa sana na akaongozwa na roho takatifu kutangaza hivi: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.” (Mdo. 10:34, 35) Huo ulikuwa uelewaji mpya na wenye kusisimua sana ambao Petro alipata, uelewaji ambao ungekuwa na matokeo kwa muda mrefu! Ukweli huo kuhusu kutokuwa na ubaguzi ungewasaidiaje Wakristo kubadili maoni yao?

5. (a) Yehova anataka Wakristo wote waelewe jambo gani? (b) Licha ya kuwa tunajua kweli, huenda bado tukawa na mielekeo gani ndani yetu?

5 Kupitia Petro, Yehova alikuwa akiwasaidia Wakristo wote kuelewa kwamba Yeye hana ubaguzi. Haoni tofauti za rangi, jamii, taifa, kabila, au lugha kuwa jambo muhimu. Mwanamume au mwanamke yeyote anayemwogopa Mungu na kufanya yaliyo sawa anakubalika kwake. (Gal. 3:26-28; Ufu. 7:9, 10) Hapana shaka unakubali kwamba hilo ni kweli. Lakini vipi ikiwa umezaliwa katika nchi au familia yenye ubaguzi? Ingawa huenda ukafikiri kwamba huna ubaguzi, ndani kabisa ya moyo wako huenda bado kukawa na hisia za ubaguzi. Hata Petro, ambaye alikuwa na pendeleo la kufunua kwamba Yehova hana ubaguzi, baadaye alionyesha kwamba alikuwa na hisia za ubaguzi. (Gal. 2:11-14) Tunaweza kumsikiliza Yesu jinsi gani na kuacha kuwahukumu wengine kwa kutazama sura yao ya nje?

6. (a) Ni nini kinachoweza kutusaidia kung’oa mielekeo yoyote ya ubaguzi kutoka moyoni mwetu? (b) Ripoti ya ndugu mmoja mwenye mapendeleo kutanikoni ilifunua nini?

6 Tunahitaji kujichunguza kwa makini kupitia Neno la Mungu ili tuone ikiwa bado tuna mawazo au hisia zozote za ubaguzi. (Zab. 119:105) Huenda pia tukahitaji msaada wenye upendo kutoka kwa wengine wanaoweza kuona mielekeo ya ubaguzi ndani yetu, hata ikiwa sisi wenyewe hatuwezi kuiona. (Gal. 2:11, 14) Inawezekana kwamba mielekeo hiyo imekita sana mizizi ndani yetu hivi kwamba hatuwezi kuitambua. Kwa mfano, fikiria ndugu mmoja mwenye mapendeleo kutanikoni ambaye aliandika ripoti kuhusu wenzi fulani wa ndoa ambao ni mfano mzuri waliokuwa kwenye utumishi wa wakati wote. Mume alikuwa ametoka katika jamii fulani yenye watu wachache na ambayo mara nyingi ilidharauliwa na watu wengine. Inaonekana ndugu aliyeandika ripoti hiyo hakujua kwamba alikuwa na hisia za ubaguzi kuelekea watu wa jamii hiyo. Katika ripoti yake, aliandika mambo mengi mazuri kuhusu mume huyo; lakini alimalizia kwa kuandika hivi: “Ingawa ametoka katika [taifa hili], tabia yake na njia yake ya maisha inawasaidia wengine kuelewa kwamba hata ikiwa mtu ametoka [katika jamii hii] haimaanishi lazima awe mchafu, mwenye tabia na viwango vya chini, ambavyo ni vya kawaida sana miongoni mwa watu wa jamii [hii].” Je, unaona tatizo liko wapi? Hata iwe tuna mapendeleo gani, lazima tujichunguze kwa makini na tuwe tayari kupokea msaada ili tutambue mielekeo yoyote ya ubaguzi iliyo moyoni mwetu. Ni nini kingine tunachoweza kufanya?

7. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunafungua mioyo yetu kabisa?

7 Ikiwa tutafungua mioyo yetu kabisa, upendo utaondoa ubaguzi. (2 Kor. 6:11-13) Je, una zoea la kushirikiana tu na watu wa rangi, jamii, taifa, kabila, au lugha yako? Ikiwa ndivyo, panuka. Kwa nini usiwaalike watu ambao wana malezi tofauti nawe ili mhubiri pamoja au uwaalike nyumbani kwako kwa ajili ya mlo au ushirika? (Mdo. 16:14, 15) Ukifanya hivyo, moyo wako utajaa upendo mwingi sana hivi kwamba hutakuwa na nafasi ya hisia zozote za ubaguzi. Lakini kuna mambo mengine ambayo hufanya tuwahukumu wengine kwa kutazama sura yao ya nje. Acheni sasa tuchunguze vitu vya kimwili.

USIWAHUKUMU WENGINE KWA MSINGI WA UTAJIRI AU UMASKINI

8. Kulingana na Mambo ya Walawi 19:15, utajiri au umaskini unaweza kuathirije jinsi tunavyowaona wengine?

8 Vitu vya kimwili ni jambo lingine linaloweza kuathiri maoni yetu kuwaelekea wengine. Andiko la Mambo ya Walawi 19:15 linasema hivi: “Usiwabague maskini au kuwapendelea matajiri. Unapaswa kumhukumu mwenzako kwa haki.” Lakini utajiri au umaskini wa mtu unaweza kuathirije maoni yetu kumhusu?

9. Sulemani aliandika ukweli gani, nao unatufundisha nini?

9 Roho takatifu ilimwongoza Sulemani kuandika jambo fulani la kweli na lenye kusikitisha kuwahusu wanadamu wasio wakamilifu. Kwenye Methali 14:20, alisema hivi: “Maskini huchukiwa hata na majirani zake, lakini tajiri ana marafiki wengi.” Methali hiyo inatufundisha nini? Ikiwa hatutakuwa waangalifu, huenda tukatamani kuwa marafiki wa ndugu ambao ni matajiri huku tukiwapuuza ndugu ambao ni maskini. Kwa nini ni hatari sana kuwaona wengine kuwa wenye thamani kwa kutegemea tu mali walizo nazo?

10. Yakobo alitaja tatizo gani?

10 Tukiwahukumu wengine kwa msingi wa mali walizo nazo, tunaweza kusababisha migawanyiko kutanikoni. Mwanafunzi Yakobo alionya kwamba tatizo hilo lilikuwa likisababisha migawanyiko kwenye baadhi ya makutaniko katika karne ya kwanza. (Soma Yakobo 2:1-4.) Lazima tuwe macho ili tusiruhusu mawazo kama hayo yaathiri makutaniko yetu leo. Tunaweza kupingaje mwelekeo wa kuwahukumu wengine kwa kutazama tu sura ya nje?

11. Vitu vya kimwili alivyo navyo mtu vina uhusiano gani na uhusiano wake na Yehova? Eleza.

11 Tunahitaji kuwaona ndugu zetu kama Yehova anavyowaona. Mtu hawi mwenye thamani machoni pa Yehova kwa sababu yeye ni tajiri au maskini. Uhusiano wetu na Yehova hautawahi kamwe kutegemea vitu vya kimwili tulivyo navyo au vitu vya kimwili ambavyo hatuna. Ingawa ni kweli kwamba Yesu alisema “itakuwa vigumu kwa tajiri kuingia katika Ufalme wa mbinguni,” hakusema kwamba haiwezekani. (Mt. 19:23) Kwa upande mwingine, Yesu alisema hivi pia: “Wenye furaha ni ninyi maskini, kwa sababu Ufalme wa Mungu ni wenu.” (Luka 6:20) Ingawa hivyo, Yesu hakumaanisha kwamba maskini wote walibarikiwa zaidi au kwamba walikubali mambo aliyofundisha. Watu wengi maskini walikataa kumsikiliza. Wazo ni, Hatuwezi kujua mtu ana uhusiano wa aina gani pamoja na Yehova kwa kutazama tu vitu vya kimwili alivyo navyo.

12. Maandiko yanatoa maagizo gani kwa matajiri na maskini?

12 Tumebarikiwa sana kuwa na ndugu na dada wengi, matajiri na maskini, ambao wanampenda na kumtumikia Yehova kwa moyo kamili. Maandiko yanawaagiza wale ambao ni matajiri “wasiutumaini utajiri usiotegemeka, bali wamtumaini Mungu.” (Soma 1 Timotheo 6:17-19.) Wakati huohuo, Neno la Mungu linawahimiza watu wa Mungu wawe waangalifu ili wasipende pesa, iwe wao ni matajiri au maskini. (1 Tim. 6:9, 10) Kwa kweli, tunapofungua macho yetu na kuwaona ndugu zetu kama Yehova anavyowaona, hatutashawishiwa kuwahukumu kwa kutegemea tu vitu vya kimwili ambavyo wanavyo au hawana. Lakini vipi kuhusu umri wa mtu? Je, huo ni msingi mzuri wa kuwahukumu wengine? Acheni tuone.

USIWAHUKUMU WENGINE KWA MSINGI WA UMRI

13. Maandiko yanatufundisha nini kuhusu kuwaheshimu watu wenye umri mkubwa?

13 Maandiko hutuagiza mara nyingi tuwaheshimu watu wenye umri mkubwa. Andiko la Mambo ya Walawi 19:32 linasema hivi: “Unapaswa kuinuka mbele ya kichwa chenye mvi, na ni lazima umheshimu mzee, nawe lazima umwogope Mungu wako.” Vivyo hivyo, andiko la Methali 16:31 linatufundisha kwamba “mvi ni taji la umaridadi zinapopatikana katika njia ya uadilifu.” Kisha, Paulo pia alimhimiza Timotheo asimkosoe kwa ukali mwanamume mzee bali amwone ndugu huyo kama baba. (1 Tim. 5:1, 2) Ingawa Timotheo alikuwa na mamlaka ya kadiri fulani juu ya ndugu kama hao, alipaswa kuwatendea kwa huruma na heshima.

14. Ni katika hali gani huenda tukahitaji kumshauri au kumtia nidhamu mtu aliye na umri mkubwa kuliko sisi?

14 Hata hivyo, je, kanuni hiyo inatumika nyakati zote? Kwa mfano, je, tunapaswa kuhisi kwamba hatuwezi kumkosoa ndugu aliye na umri mkubwa ikiwa anatenda dhambi kimakusudi au anaunga mkono jambo lisilompendeza Yehova? Yehova hatawahukumu watu kwa kutazama sura yao ya nje na hatakosa kumwadhibu mtenda dhambi aliyekusudia eti kwa sababu tu ni mwenye umri mkubwa. Ona kanuni inayopatikana kwenye andiko la Isaya 65:20: “Mtenda dhambi atalaaniwa, hata ingawa ana umri wa miaka mia moja.” Kanuni inayofanana na hiyo inapatikana kwenye maono ambayo Ezekieli aliona. (Eze. 9:5-7) Hivyo, sikuzote hangaiko letu kuu linapaswa kuwa kumheshimu yule Mzee wa Siku, Yehova Mungu. (Dan. 7:9, 10, 13, 14) Tukifanya hivyo, hatutaogopa kumrekebisha mtu yeyote anayehitaji shauri, hata iwe ana umri gani.—Gal. 6:1.

Je, unawaheshimu ndugu vijana? (Tazama fungu la 15)

15. Tunajifunza somo gani kutoka kwa mtume Paulo kuhusu kuwaheshimu ndugu vijana?

15 Namna gani kuhusu ndugu vijana kutanikoni? Una maoni gani kuwahusu? Mtume Paulo alimwandikia hivi kijana Timotheo: “Usiruhusu kamwe mtu yeyote audharau ujana wako. Badala yake, uwe mfano mzuri kwa waaminifu katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, na katika usafi wa kiadili.” (1 Tim. 4:12) Huenda Timotheo alikuwa na umri wa miaka thelathini hivi mtume Paulo alipoandika maneno hayo. Hata hivyo, Paulo alikuwa amempa mgawo wa kushughulikia majukumu mazito. Hata iwe Paulo alikuwa na sababu gani ya kutoa shauri hilo, wazo kuu liko wazi. Hatupaswi kuwahukumu ndugu vijana kwa kutegemea tu umri wao. Tunahitaji kukumbuka kwamba hata Bwana wetu Yesu alitimiza huduma yake yote hapa duniani akiwa na umri wa miaka thelathini hivi.

16, 17. (a) Wazee wanapaswa kutegemea nini wanapoamua ikiwa ndugu fulani anastahili kupendekezwa awe mtumishi wa huduma au mzee? (b) Maoni ya kibinafsi au ya kitamaduni yanaweza kutofautiana na Maandiko jinsi gani?

16 Huenda tumelelewa katika utamaduni unaowafanya watu wawe na mwelekeo wa kuwadharau vijana. Ikiwa ndivyo, huenda wazee wa kutaniko wakasita kuwapendekeza vijana wanaostahili wawe watumishi wa huduma au wazee. Wazee wote wanahitaji kukumbuka kwamba Maandiko hayasemi umri hususa ambao kijana anapaswa kufikisha ili apendekezwe kuwa mtumishi wa huduma au mzee. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Ikiwa mzee anaweka amri fulani kwa kutegemea utamaduni, hatendi kupatana na Maandiko. Wanaume vijana wanapaswa kuchunguzwa kwa kutegemea viwango vya Neno la Mungu, si viwango vya mtu binafsi au vya kitamaduni.—2 Tim. 3:16, 17.

17 Fikiria jinsi maoni hayo ya kitamaduni na yasiyo ya Kimaandiko yanavyoweza kuwazuia ndugu wanaostahili kufikia mapendeleo. Katika nchi moja, mtumishi mmoja wa huduma alipewa majukumu fulani mazito. Wazee wa kutaniko lake walikubali kwamba ndugu huyo alitimiza kwa kadiri inayofaa matakwa ya Kimaandiko ya kuwa mzee wa kutaniko, lakini hakupendekezwa. Wazee fulani wenye umri mkubwa walisisitiza kwamba ndugu huyo alionekana kuwa kijana sana. Kwa kusikitisha, ndugu huyo hakupendekezwa kwa sababu tu ya jinsi alivyoonekana. Ingawa hilo ni jambo moja tu lililoonwa, ripoti zinaonyesha kwamba njia hiyo ya kufikiri imeathiri watu wengi katika sehemu mbalimbali za ulimwengu. Ni muhimu sana kwetu kutegemea Maandiko badala ya utamaduni wetu au maoni yetu binafsi! Hiyo ndiyo njia pekee ya kumtii Yesu na kuacha kuwahukumu wengine kwa kutazama sura ya nje.

HUKUMU KWA UADILIFU

18, 19. Tunahitaji kufanya nini ili tuwaone wengine kama Yehova anavyowaona?

18 Licha ya kutokamilika kwa kibinadamu, tunaweza kujifunza kutowabagua wengine kwa kumwiga Yehova. (Mdo. 10:34, 35) Lakini hilo linahitaji tuendelee kujitahidi na kutumia vikumbusho tunavyopokea kwa ukawaida kutoka katika Neno la Mungu. Kwa kutumia vikumbusho hivyo, tutaendelea kutii amri ya Yesu ya kuacha kuwahukumu wengine kwa kutazama sura ya nje.—Yoh. 7:24.

19 Hivi karibuni, Mfalme wetu Yesu Kristo, atawahukumu wanadamu, si kwa kutegemea mambo anayoona kwa macho yake au anayosikia kwa masikio yake, bali kwa uadilifu. (Isa. 11:3, 4) Hilo litakuwa jambo lenye kufurahisha sana!