Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Subira​—Kuvumilia Ukiwa na Kusudi

Subira​—Kuvumilia Ukiwa na Kusudi

KWA SABABU ya kuongezeka kwa mikazo katika “siku za mwisho,” watu wa Yehova wanahitaji sifa ya subira sasa kuliko wakati mwingine wowote. (2 Tim. 3:1-5) Tunaishi katika ulimwengu uliojaa watu wenye kujipenda wenyewe, wasiotaka makubaliano yoyote, na wasiojizuia. Kwa kawaida, watu wenye tabia hizo hawana subira hata kidogo. Hivyo, kila Mkristo anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, nimeathiriwa na mtazamo wa ulimwengu wa kukosa subira? Inamaanisha nini hasa kuwa mwenye subira? Na ninaweza kufanya nini ili sifa hii ya Kikristo inayovutia iwe sehemu ya kudumu ya utu wangu?’

MAANA YA KUWA MWENYE SUBIRA

Katika Biblia, neno subira lina maana kubwa zaidi ya kuvumilia tu hali ngumu. Mtu mwenye subira inayotoka kwa Mungu huvumilia akiwa na kusudi. Hakazii fikira mahitaji yake tu, bali anazingatia pia faida za yule anayesababisha hali ya kutoelewana. Hivyo, mtu mwenye subira anapokosewa au kukasirishwa, hakati tamaa kamwe kwamba uhusiano ulioharibika unaweza kuwa mzuri tena. Hivyo basi, haishangazi kwamba Biblia inataja sifa ya “subira” kuwa ya kwanza kati ya sifa nyingi nzuri zinazotokana na sifa ya upendo. * (1 Kor. 13:4) Pia, Neno la Mungu linataja sifa ya “subira” ikiwa mojawapo ya sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Lakini ni nini kinachohitajiwa ili tusitawishe sifa hii inayotoka kwa Mungu?

JINSI YA KUSITAWISHA SIFA YA SUBIRA

Ili kusitawisha sifa ya subira, ni lazima tusali ili tupate msaada wa roho ya Yehova, ambayo anawapa wale wanaomwamini na kumtegemea. (Luka 11:13) Hata hivyo, ingawa roho ya Mungu ina nguvu, tunahitaji kufanya sehemu yetu na kutenda kupatana na sala zetu. (Zab. 86:10, 11) Hilo linamaanisha kwamba ni lazima tufanye yote tuwezayo kuonyesha sifa ya subira kila siku ili sifa hii itie mizizi moyoni mwetu. Na hata baada ya kufanya hivyo, huenda tukahitaji kufanya mengi zaidi ili kufanya sifa ya subira iwe sehemu ya kudumu ya utu wetu. Ni nini kingine kinachoweza kutusaidia?

Tunaweza kusitawisha sifa ya subira kwa kuchunguza na kuiga mfano mkamilifu wa Yesu. Kupatana na mfano wa Yesu, mtume Paulo aliongozwa na roho kufafanua “utu mpya,” ambao unatia ndani sifa ya “subira,” kisha akatuhimiza “[tuache] amani ya Kristo itawale mioyoni [mwetu].” (Kol. 3:10, 12, 15) Tunaweza kuacha amani hiyo “itawale” mioyoni mwetu kwa kuiga imani thabiti ya Yesu kwamba kwa wakati Wake, Mungu atarekebisha mambo yote yanayotuhangaisha. Tunapofuata mfano wa Yesu, hatutakasirika kufikia hatua ya kukosa subira, hata hali gani itupate.—Yoh. 14:27; 16:33.

Ingawa tunatamani sana kuona ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu, tunajifunza kuwa wenye subira zaidi tunapotafakari jinsi Yehova anavyotuonyesha subira. Maandiko yanatuhakikishia hivi: “Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake, kama watu fulani wanavyodhani, bali ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9) Tunapotafakari subira ya Yehova kutuelekea, je, hatuchochewi kuwa na subira zaidi kuwaelekea wengine? (Rom. 2:4) Hivyo basi, unahitaji kuonyesha sifa ya subira katika hali gani?

HALI AMBAZO TUNAHITAJI KUONYESHA SIFA YA SUBIRA

Hali nyingi tunazokabili kila siku zinaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuonyesha sifa ya subira. Kwa mfano, unapohisi kwamba una jambo fulani muhimu la kusema, huenda ukahitaji kuonyesha subira ili uepuke kuwakatiza wengine wanapozungumza. (Yak. 1:19) Huenda pia ukahitaji kuonyesha sifa ya subira unaposhirikiana na waamini wenzako ambao mazoea yao yanakuudhi. Badala ya kukasirika kupita kiasi, ni jambo la hekima kukumbuka jinsi Yehova na Yesu wanavyotenda tunapokosea. Hawatuchambui wala kukazia fikira makosa yetu madogo-madogo. Badala yake, wao huona sifa zetu nzuri, na huonyesha subira tunapojitahidi kuboresha sifa zetu.—1 Tim. 1:16; 1 Pet. 3:12.

Hali nyingine inayoweza kufanya iwe vigumu kwetu kuonyesha sifa ya subira ni wakati mtu fulani anapodai kwamba tumesema au kutenda jambo lisilofaa. Kwa kawaida, huenda tukakasirika haraka na kuanza kujitetea. Hata hivyo, Neno la Mungu hupendekeza tufanye jambo tofauti. Linasema hivi: “Ni bora kuwa na subira kuliko kuwa na roho ya kiburi. Usikasirike haraka, kwa maana hasira hukaa katika kifua cha wajinga.” (Mhu. 7:8, 9) Hivyo, hata kama mambo yaliyosemwa ni ya uwongo, tunapaswa kuchanganua kwa subira jinsi tutakavyosema au kutenda. Yesu alifuata kanuni hiyo wengine walipomdhihaki isivyo haki.—Mt. 11:19.

Wazazi hasa wanapaswa kuonyesha sifa ya subira wanapohitaji kuzungumzia mitazamo, tamaa, na mielekeo yoyote mibaya ambayo huenda ikaanza kusitawi ndani ya watoto wao. Fikiria kisa cha Mattias, ambaye anatumikia akiwa mshiriki wa familia ya Betheli ya Skandinavia. Alipokuwa tineja, Mattias alivumilia dhihaka za muda mrefu shuleni kwa sababu ya mambo aliyoamini. Mwanzoni, wazazi wake hawakujua alikuwa akipitia hali hiyo. Hata hivyo, walilazimika kukabili matokeo ya upinzani ambao mwana wao alikuwa akikabili, jambo lililofanya aanze kutilia shaka ikiwa mambo aliyokuwa amejifunza yalikuwa kweli. Anapokumbuka kipindi hicho, Gillis, baba ya Mattias anasema hivi: “Hali hiyo ilihitaji tuwe na subira nyingi. Mattias angeuliza hivi: ‘Mungu ni nani? Vipi ikiwa Biblia si Neno la Mungu? Tunajuaje ikiwa kwa kweli Mungu ndiye anayetaka tutimize jambo hili au lile?’” Pia, angemuuliza hivi baba yake: “Kwa nini nihukumiwe ikiwa sihisi kama mnavyohisi au kuamini mambo mnayoamini?”

Gillis anaeleza hivi: “Nyakati nyingine mwana wetu angezungumza kwa hasira, si kwamba alikuwa amenikasirikia mimi au mama yake, bali alikuwa ameikasirikia kweli—kweli ambayo alihisi ilifanya maisha yake yawe magumu sana.” Gillis alishughulikiaje hali hiyo? Anasema hivi: “Pindi fulani mimi na mwanangu tungeketi na kuzungumza kwa saa nyingi. Mara nyingi nilimsikiliza tu na kumuuliza maswali mara chache ili nipate picha kamili ya jinsi alivyohisi na kuona mambo. Nyakati nyingine ningempa ufafanuzi fulani ambao angeufikiria kwa siku moja au mbili kabla ya kuendeleza mazungumzo yetu. Na nyakati nyingine, ningemwambia kwamba nilihitaji siku kadhaa ili nifikirie wazo fulani alilotoa. Kupitia mazungumzo hayo ya kawaida, hatua kwa hatua Mattias alianza kuelewa na kukubali mafundisho kuhusu mambo kama vile fidia, enzi kuu ya Mungu, na upendo wa Yehova. Mabadiliko hayo yalichukua muda, na hali haikuwa rahisi, lakini pole kwa pole, alianza kumpenda Yehova kutoka moyoni. Mimi na mke wangu tunafurahi sana kwamba jitihada tulizofanya za kumsaidia mwana wetu kwa subira alipokuwa tineja zilikuwa na matokeo mazuri na zikafikia moyo wake.”

Gillis na mke wake walitegemea msaada wa Yehova walipokuwa wakijitahidi kumsaidia mwana wao kwa subira. Anapokumbuka wakati huo, Gillis anasema hivi: “Mara nyingi nilimwambia Mattias kwamba kwa kuwa tulimpenda sana, mimi na mama yake tulichochewa kusali kwa Yehova kwa bidii hata zaidi ili Yehova amsaidie kuelewa.” Wazazi hao wanafurahi sana kwamba waliendelea kuonyesha sifa hiyo muhimu ya subira!

Zaidi ya kuwasaidia kiroho, Wakristo wa kweli wanahitaji kuchochewa na upendo kusitawisha sifa ya subira wanapowasaidia washiriki wa familia au marafiki ambao wana ugonjwa wa kudumu. Mfikirie Ellen, * anayeishi Skandinavia.

Miaka minane hivi iliyopita, mume wa Ellen alipatwa na kiharusi mara mbili na kuathiri ubongo wake. Matokeo ni kwamba hana tena hisia za huruma, furaha, au huzuni. Ni vigumu sana kwa Ellen kushughulika na hali hiyo. Anasema hivi: “Nimehitaji kuonyesha subira nyingi na kusali mara nyingi.” Anaongeza hivi: “Andiko ninalolipenda zaidi na linalonifariji ni Wafilipi 4:13, linalosema, ‘Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.’” Kwa sababu ya nguvu hizo, Ellen anaendelea kuvumilia kwa subira akiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova anamtegemeza.—Zab. 62:5, 6.

IGA SUBIRA YA YEHOVA

Bila shaka inapohusu kuonyesha subira, Yehova ndiye mfano bora zaidi tunaopaswa kuiga. (2 Pet. 3:15) Kuna masimulizi mengi katika Neno la Mungu yanayoonyesha pindi ambazo Yehova alionyesha subira nyingi. (Neh. 9:30; Isa. 30:18) Kwa mfano, Yehova alitendaje Abrahamu alipotilia shaka uamuzi Wake wa kuharibu jiji la Sodoma? Kwanza kabisa, Yehova hakumkatiza Abrahamu alipokuwa akizungumza. Badala yake, Yehova alisikiliza kwa subira kila mara Abrahamu alipouliza swali au kueleza jambo fulani lililomhangaisha. Kisha, Yehova alionyesha kwamba alikuwa anamsikiliza kwa kutaja tena mambo yaliyomhangaisha Abrahamu na akamhakikishia kwamba hangeharibu jiji la Sodoma ikiwa hata watu kumi tu waadilifu wangepatikana katika jiji hilo. (Mwa. 18:22-33) Huo ni mfano mzuri sana wa kusikiliza kwa subira na wa kuepuka kukasirika!

Kwa hakika, sifa ya subira inayotoka kwa Mungu ni sehemu muhimu ya utu mpya ambao Wakristo wote wanapaswa kujivika. Tukitia bidii kusitawisha sifa hiyo yenye thamani na itakayodumu milele, tutamheshimu Baba yetu mwenye subira na upendo, na tutahesabiwa kuwa miongoni mwa “wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Ebr. 6:10-12.