Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fundisha Kweli

Fundisha Kweli

“Ee Yehova, . . . kiini hasa cha neno lako ni kweli.”—ZAB. 119:159, 160.

NYIMBO: 29, 53

1, 2. (a) Ni kazi gani ambayo Yesu aliiona kuwa jambo kuu maishani mwake, na kwa nini? (b) Tunapaswa kufanya nini ili tupate mafanikio tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu”?

YESU KRISTO alikuwa seremala na mhudumu wa habari njema. (Marko 6:3; Rom. 15:8) Alikuwa stadi katika mambo hayo yote mawili. Akiwa seremala, alijifunza jinsi ya kutumia vifaa vya useremala kutengeneza vitu mbalimbali kwa kutumia mbao. Akiwa mwalimu wa habari njema, alitumia kwa ustadi ujuzi wake wenye kina wa Maandiko ili kuwasaidia watu kuelewa kweli za Neno la Mungu. (Mt. 7:28; Luka 24:32, 45) Alipofikisha umri wa miaka 30, Yesu aliacha kazi ya useremala kwa sababu alijua kwamba kuwa mhudumu wa habari njema ndiyo kazi muhimu zaidi. Alisema kwamba sababu moja iliyomfanya Mungu amtume duniani ni ili afanye kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 20:28; Luka 3:23; 4:43) Yesu aliiona huduma kuwa jambo kuu maishani mwake, naye alitaka wengine wajiunge naye katika kazi hiyo.—Mt. 9:35-38.

2 Huenda sisi si maseremala, lakini bila shaka sisi sote ni wahudumu wa habari njema. Kazi hiyo ni muhimu sana hivi kwamba Mungu anahusika katika kuifanya; sisi ni “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9; 2 Kor. 6:4) Tunatambua kwamba “kiini hasa cha neno [la Yehova] ni kweli.” (Zab. 119:159, 160) Hiyo ndiyo sababu tungependa kuhakikisha kuwa “[tunalitumia] sawasawa neno la kweli” katika huduma yetu. (Soma 2 Timotheo 2:15.) Hivyo, sisi huendelea kunoa ustadi wetu wa kutumia Biblia, kifaa kikuu tunachotumia kufundisha kweli kumhusu Yehova, Yesu, na Ufalme. Ili kutusaidia tupate mafanikio katika huduma yetu, tengenezo la Yehova limetuandalia vifaa vingine vya msingi tunavyohitaji kujua jinsi ya kuvitumia vizuri. Vifaa hivyo vimo katika Sanduku la Vifaa vya Kufundishia.

3. Tunapaswa kukazia fikira nini katika kipindi kifupi kilichobaki cha kuhubiri, na andiko la Matendo 13:48 linatusaidiaje kufanya hivyo?

3 Huenda unajiuliza kwa nini linaitwa Sanduku la Vifaa vya Kufundishia na si Sanduku la Vifaa vya Kuhubiri. “Kuhubiri” kunamaanisha kutangaza ujumbe; lakini “kufundisha” kunamaanisha kueleza ujumbe kwa njia ambayo ujumbe huo utafika akilini na moyoni mwa mtu, hivi kwamba atachochewa kutenda kulingana na mambo anayojifunza. Katika kipindi kifupi kilichobaki cha kufanya kazi ya kuhubiri, tunapaswa kukazia fikira kuanzisha mafunzo ya Biblia na kuwafundisha watu kweli. Hilo linamaanisha kuwatafuta kwa bidii wale walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” na kuwasaidia waanze kumtumikia Yehova.—Soma Matendo 13:44-48.

4. Tunaweza kuwatambuaje watu walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele,” na tunaweza kuwapataje?

4 Tunaweza kuwatambuaje watu walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele”? Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, njia pekee ya kuwatambua watu hao ni kwa kufanya kazi ya kuhubiri. Hivyo, tunahitaji kufanya sawasawa kabisa na jinsi Yesu alivyoagiza, kwamba: “Mtakapoingia katika jiji au kijiji chochote, tafuteni humo mtu anayestahili.” (Mt. 10:11) Hatutarajii kwamba watu wasio wanyoofu, wenye kiburi, au wasiopenda mambo ya kiroho watasikiliza ujumbe wa habari njema. Tunawatafuta watu wanyoofu, wanyenyekevu, na walio na njaa ya kweli. Tunaweza kulinganisha jambo hilo na yale ambayo Yesu, akiwa seremala, angefanya alipokuwa akitafuta mbao zinazofaa kwa ajili ya kutengeneza fanicha, milango, nira, na vitu vingine. Baada ya kupata mbao nzuri, angetumia sanduku lake la vifaa na ustadi wake kutengeneza kitu alichokusudia. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo tunapoendelea kujitahidi kuwasaidia watu walio na moyo mnyoofu kuwa wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.

5. Tunahitaji kujua nini kuhusu vifaa vilivyo katika Sanduku letu la Kufundishia? Toa mfano. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

5 Kama ilivyo na sanduku lolote lile la vifaa, kila kifaa huwa na kazi au matumizi hususa. Kwa mfano, fikiria vifaa vya useremala ambavyo huenda Yesu alitumia. * Alihitaji vifaa vya kupimia na kuweka alama kwenye mbao; vifaa vya kukata, vya kutoboa mashimo, vya kuchonga; vya kusawazisha, na vya kuunganisha mbao. Vivyo hivyo, kila kifaa katika Sanduku letu la Vifaa vya Kufundishia kina kazi au matumizi hususa. Sasa acheni tuone jinsi tunavyoweza kutumia vifaa hivyo muhimu ambavyo tumeandaliwa.

VIFAA TUNAVYOTUMIA KUJITAMBULISHA

6, 7. (a) Umetumiaje kadi za mawasiliano? (b) Mwaliko wa kuhudhuria mikutano hutimiza malengo gani mawili?

6 Kadi ya Mawasiliano. Sisi hutumia kifaa hicho kidogo lakini chenye matokeo kujitambulisha na kuwaelekeza watu kwenye Tovuti yetu, ambapo wanaweza kujifunza mengi zaidi kutuhusu au hata kuomba wafundishwe Biblia. Kufikia sasa, zaidi ya maombi 400,000 ya kujifunza Biblia yamepokelewa kupitia Tovuti ya jw.org, na maombi mengine mengi zaidi hufanywa kila siku! Unaweza kubeba kadi chache ili utumie vizuri fursa za kuhubiri zinazojitokeza unapokuwa katika shughuli zako za kila siku.

7 Mialiko. Mwaliko tunaowapa watu ili wahudhurie mikutano hutimiza malengo mawili. Mwaliko huo unasema hivi: “Unakaribishwa kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.” Kisha mwaliko huo unampa mtu anayetaka kujifunza Biblia fursa ya kuchagua kujifunza Biblia “kwenye mikutano yetu” “au pamoja na mwalimu [wake] binafsi.” Hivyo, hatukitumii kifaa hicho kujitambulisha tu, bali pia tunakitumia kuwaalika wale “wanaotambua uhitaji wao wa kiroho” wajifunze Biblia pamoja nasi. (Mt. 5:3) Bila shaka, watu wote wanakaribishwa kuhudhuria mikutano yetu iwe watakubali kujifunza Biblia rasmi au la. Wanapohudhuria wanaweza kujionea na kusikia kuhusu elimu tunayotoa ya kweli za Biblia.

8. Kwa nini ni muhimu watu wahudhurie angalau mojawapo ya mikutano yetu? Toa mfano.

8 Ni muhimu tuendelee kuwaalika watu waje kwenye mikutano yetu angalau mara moja. Kwa nini? Watajionea tofauti kubwa iliyopo kati ya ufanisi wa kiroho ulio kwenye mikutano yetu na hali ya kiroho iliyozorota ya Babiloni Mkubwa. (Isa. 65:13) Miaka kadhaa iliyopita, Ray na Linda, wenzi fulani wa ndoa nchini Marekani walijionea jambo hilo. Walifikia uamuzi kwamba walihitaji kuanza kwenda kanisani. Waliamini kwamba Mungu yupo na walitambua kwamba walihitaji kutosheleza uhitaji wao wa kiroho, hivyo walianza kushirikiana na makanisa yaliyokuwa katika jiji lao, moja baada ya lingine. Kulikuwa na makanisa mbalimbali na vikundi vingi vya kidini. Tangu mwanzoni, wenzi hao waliamua kwamba ili wajiunge na kanisa fulani, lazima kanisa hilo litimize masharti mawili. Kwanza, ni lazima wajifunze jambo jipya katika ibada ya kanisa hilo, na pili, ni lazima washiriki wa kanisa hilo waonekane kama watu wanaodai kumwakilisha Mungu. Baada ya miaka kadhaa, wenzi hao walikuwa wametembelea kila kanisa katika eneo lao, lakini walikuwa wametamaushwa sana. Hawakuwa wamejifunza chochote, na washiriki wa makanisa hayo hawakuvalia kwa njia ya heshima hata kidogo. Baada ya kuhudhuria ibada ya kanisa la mwisho kwenye orodha yao ya makanisa, Linda alielekea kazini na Ray akarudi nyumbani. Akiwa njiani, Ray alipita karibu na Jumba la Ufalme na akawaza, ‘Ni nini huendelea humu ndani? Hebu niingie nione.’ Na kwa kweli, hakujuta kufanya hivyo! Kila mtu katika Jumba la Ufalme alikuwa mchangamfu na mwenye urafiki na alivalia mavazi yenye heshima sana. Ray aliketi kwenye kiti cha mbele na alifurahia sana mambo aliyojifunza! Ilikuwa kama mtume Paulo alivyosema kuhusu mtu anayehudhuria mkutano kwa mara ya kwanza na kusema: “Kwa kweli Mungu yupo kati yenu.” (1 Kor. 14:23-25) Baada ya hapo, Ray alianza kuhudhuria mikutano kila Jumapili; kisha akaanza kuhudhuria kila mkutano wa katikati ya juma. Linda pia alianza kuhudhuria mikutano, na ingawa wote wawili walikuwa na umri wa miaka 70 hivi, walianza kujifunza Biblia na wakabatizwa.

VIFAA TUNAVYOTUMIA KUANZISHA MAZUNGUMZO

9, 10. (a) Kwa nini ni rahisi kutumia trakti zetu? (b) Eleza jinsi ya kutumia trakti yenye kichwa Ufalme wa Mungu Ni Nini?

9 Trakti. Tuna trakti nane ambazo ni rahisi kutumia na ni vifaa bora sana vya kuanzisha mazungumzo. Tangu trakti hizo zilipoanza kuchapishwa mwaka wa 2013, nakala bilioni tano hivi zimechapishwa! Uzuri wa trakti hizo ni kwamba unapojifunza kutumia moja ya trakti hizo, utakuwa na uwezo wa kutumia trakti nyingine zote, kwa sababu zote zina mpangilio uleule. Unaweza kutumiaje trakti kuanzisha mazungumzo?

10 Huenda ukachagua kutumia trakti yenye kichwa Ufalme wa Mungu Ni Nini? Mwonyeshe mtu unayezungumza naye swali lililo juu ya trakti hiyo, kisha umuulize: “Je, umewahi kujiuliza Ufalme wa Mungu ni nini? Unafikiri ni . . . ?” Halafu muulize angechagua jibu gani kati ya majibu matatu yaliyopo. Bila kumwambia ikiwa jibu lake ni sahihi au la, fungua upande wa ndani wenye kichwa “Biblia Husema Hivi,” na usome pamoja naye maandiko mawili yaliyoonyeshwa, yaani, Danieli 2:44 na Isaya 9:6. Ikiwa hali zinaruhusu, endeleza mazungumzo. Mwishowe, mwonyeshe swali mtakalozungumzia mtakapokutana tena, linalopatikana upande wa nyuma chini ya kichwa “Jambo la Kufikiria”: “Maisha yatakuwaje chini ya Ufalme wa Mungu?” Swali hilo litakuwa msingi wa kuendeleza mazungumzo pamoja na mtu huyo kwenye ziara itakayofuata. Mtakapokutana tena, unaweza kurejelea somo la 7 katika broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu!, ambayo ni mojawapo ya vifaa tunavyotumia kuanzisha mafunzo ya Biblia.

VIFAA VYA KUWASAIDIA WATU WAIAMINI BIBLIA

11. Magazeti yetu yamekusudiwa yatimize lengo gani, lakini tunapaswa kujua nini kuyahusu?

11 Magazeti. Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ndiyo magazeti yanayochapishwa kwa wingi na kutafsiriwa katika lugha nyingi zaidi ulimwenguni! Kwa kuwa magazeti hayo husomwa na watu kutoka nchi mbalimbali kote ulimwenguni, habari kuu zinazozungumziwa zimetayarishwa ili ziwavutie watu wa namna zote. Tunapaswa kuyatumia magazeti hayo kama vifaa vya kuwasaidia watu wakazie masuala yaliyo muhimu zaidi maishani leo. Hata hivyo, ili tuwape watu magazeti yanayowafaa, tunahitaji kujua habari zilizo katika kila gazeti zimeandikwa kwa ajili ya watu wa aina gani.

12. (a) Gazeti la Amkeni! limekusudiwa nani hasa, nalo hutimiza lengo gani? (b) Umepata matokeo gani mazuri hivi karibuni kwa kutumia kifaa hicho?

12 Gazeti la Amkeni! limekusudiwa kuwasaidia wasomaji walio na ujuzi mdogo kuhusu Biblia au watu wasioifahamu hata kidogo. Huenda hawajui mafundisho yoyote ya Kikristo, hawana imani na dini, au hawajui kwamba Biblia inaweza kuwasaidia. Lengo kuu la gazeti la Amkeni! ni kumsadikisha msomaji kwamba Mungu yupo. (Rom. 1:20; Ebr. 11:6) Limekusudiwa pia kumsaidia msomaji ajenge imani kwamba Biblia ‘kwa kweli ni neno la Mungu.’ (1 The. 2:13) Habari kuu za matoleo matatu ya mwaka wa 2018 ya gazeti la Amkeni! ni: “Njia ya Maisha Inayoleta Furaha,” “Siri 12 za Mafanikio Katika Familia,” na “Kukabiliana na Huzuni ya Kufiwa.”

13. (a) Gazeti la Mnara wa Mlinzi toleo la watu wote limekusudiwa nani hasa? (b) Umepata matokeo gani mazuri hivi karibuni kwa kutumia kifaa hicho?

13 Gazeti la Mnara wa Mlinzi toleo la watu wote, limekusudiwa kuwasaidia kiroho wale wanaomheshimu Mungu na Neno lake angalau kwa kadiri fulani. Ingawa huenda watu hao wana ujuzi fulani kuhusu Biblia, hawana ujuzi sahihi kuhusu mafundisho yake. (Rom. 10:2; 1 Tim. 2:3, 4) Habari kuu za matoleo matatu ya mwaka wa 2018 ya gazeti la watu wote la Mnara wa Mlinzi ni: “Biblia—Kitabu Kisichopitwa na Wakati!,” “Maisha Yatakuwaje Wakati Ujao?,” na “Je, Mungu Anakujali?

VIFAA VYA KUWACHOCHEA WATU WAJIFUNZE BIBLIA

14. (a) Video nne zilizo kwenye Sanduku letu la Vifaa vya Kufundishia hutimiza lengo gani? (b) Umepata matokeo gani mazuri kwa kuwaonyesha watu video hizo?

14 Video. Katika siku za Yesu, seremala alitumia vifaa vilivyomlazimu atumie nguvu zake. Hata hivyo, siku hizi maseremala hutumia vifaa vinavyotumia umeme, kama vile misumeno, kekee, msasa, mashine ya kupigilia misumari, na vifaa vingine. Zaidi ya machapisho ya kusoma, sasa tuna video maridadi tunazoonyesha watu—na nne kati ya hizo zinapatikana kwenye Sanduku letu la Vifaa vya Kufundishia. Video hizo ni: Kwa Nini Ujifunze Biblia?, Ni Nini Hutendeka Kwenye Funzo la Biblia?, Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme?, na Mashahidi wa Yehova Ni Nani? Video zenye urefu usiozidi dakika mbili zinafaa sana kwenye ziara ya kwanza. Video ndefu zaidi zinaweza kutumiwa tunapofanya ziara za kurudia au kwa wale wanaoturuhusu tuzungumze nao kwa muda mrefu zaidi. Vifaa hivyo maridadi vinaweza kuwachochea watu wajifunze Biblia na kuhudhuria mikutano yetu.

15. Toa mfano unaoonyesha jinsi watu wanavyochochewa wanapotazama video zetu katika lugha zao.

15 Kwa mfano, dada mmoja alipokutana na mwanamke mmoja aliyehama kutoka Mikronesia ambaye lugha yake ya mama ni Kiyape, alimwonyesha video Kwa Nini Ujifunze Biblia? katika lugha yake. Video hiyo ilipoanza, mwanamke huyo alisema: “Hii ni lugha yangu. Siamini! Lafudhi yake imefanya nitambue mara moja kwamba ametoka kisiwa nilichotoka. Anazungumza lugha yangu!” Baada ya hapo alisema kwamba atasoma na kutazama video zote za lugha yake zinazopatikana kwenye Tovuti ya jw.org. (Linganisha Matendo 2:8, 11.) Fikiria jambo lingine lililoonwa. Dada mmoja kutoka Marekani alimtumia mpwa wake kiunganishi cha video hiyohiyo katika lugha ambayo mpwa wake alizungumza. Aliitazama na kumwandikia ujumbe huu wa barua pepe: “Sehemu hasa iliyonivutia ni ile inayotaja kwamba ulimwengu unatawaliwa na kiumbe fulani mwovu. Nilijaza ombi la kujifunza Biblia.” Anaishi katika nchi ambayo kazi yetu imewekewa vizuizi!

VIFAA VINAVYOTUSAIDIA KUFUNDISHA KWELI

16. Eleza lengo hususa la broshua zifuatazo: (a) Msikilize Mungu Uishi Milele. (b) Habari Njema Kutoka kwa Mungu! (c) Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?

16 Broshua. Unaweza kutumia nini kumfundisha mtu ambaye hajui kusoma vizuri au ambaye machapisho ya Biblia hayapatikani katika lugha yake? Tuna kifaa hususa kwa ajili ya watu wa namna hiyo—broshua Msikilize Mungu Uishi Milele. * Kifaa bora sana cha kuanzisha mafunzo ni broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu! Unaweza kumwonyesha mtu vichwa 14 vilivyoorodheshwa upande wa nyuma, halafu umruhusu achague kichwa kinachomvutia zaidi. Kisha anza kujifunza naye habari aliyochagua. Je, umejaribu kutumia mbinu hiyo unapowarudia watu? Broshua ya tatu inayopatikana kwenye Sanduku letu la Vifaa vya Kufundishia ni Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo? Lengo la broshua hiyo ni kuwaelekeza wanafunzi wa Biblia kwenye tengenezo. Ili ujue jinsi ya kuitumia kila mara unapojifunza na mwanafunzi, tazama Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo toleo la Machi 2017.

17. (a) Kila kitabu tunachotumia kuwafundisha watu Biblia kina lengo gani hususa? (b) Baada ya kubatizwa, ndugu na dada wapya wanatarajiwa wafanye nini, na kwa nini?

17 Vitabu. Baada ya kuanzisha funzo kwa kutumia broshua, unaweza kuacha kutumia broshua na kuanza kutumia kitabu Biblia Inatufundisha Nini? wakati wowote unapoona kwamba inafaa. Kifaa hicho kitamsaidia mwanafunzi aongeze ujuzi wake wa mafundisho ya msingi ya Biblia. Baada ya kukamilisha kitabu hicho na ikiwa mwanafunzi anafanya maendeleo ya kiroho, endeleza funzo kwa kutumia kitabu Dumu Katika Upendo wa Mungu. Kifaa hicho kitamfundisha mwanafunzi jinsi ya kutumia kanuni za Biblia kila siku maishani. Kumbuka kwamba hata baada ya kubatizwa, ndugu na dada wapya waliobatizwa wanahitaji kuendelea kujifunza mpaka watakapokamilisha vitabu vyote viwili. Kufanya hivyo kutawasaidia kuwa na msingi imara katika kweli.—Soma Wakolosai 2:6, 7.

18. (a) Andiko la 1 Timotheo 4:16 linatutia moyo tufanye nini tukiwa walimu wa kweli za Biblia, na matokeo yatakuwa nini? (b) Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapotumia Sanduku la Vifaa vya Kufundishia?

18 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tumekabidhiwa “ujumbe wa kweli ya habari njema” ambao unaweza kuwasaidia watu wapate uzima wa milele. (Kol. 1:5; soma 1 Timotheo 4:16.) Hiyo ndiyo sababu tumeandaliwa Sanduku la Vifaa vya Kufundishia lililojaa vifaa hususa tunavyohitaji. (Tazama, “ Sanduku la Vifaa vya Kufundishia.”) Acheni tujitahidi kadiri tuwezavyo kutumia vifaa hivyo kwa ustadi. Kila mhubiri anaweza kuamua ni chapisho lipi katika Sanduku la Vifaa vya Kufundishia atakalotumia na wakati wa kulitumia. Lakini lengo letu halipaswi tu kuwa kuwaachia watu machapisho; wala hatupaswi kuwaachia machapisho watu wasiopendezwa na ujumbe wetu. Lengo letu ni kuwasaidia watu wanyoofu, wanyenyekevu, na walio na njaa ya kiroho wawe wanafunzi—watu walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.”—Mdo. 13:48; Mt. 28:19, 20.

^ fu. 5 Tazama makala yenye kichwa, “Seremala” na sanduku lenye kichwa “Sanduku la Vifaa vya Seremala” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2010.

^ fu. 16 Ikiwa mtu hajui kusoma, unaweza kumwomba aambatane nawe kwa kutumia broshua Msikilize Mungu, ambayo haina maandishi mengi.