Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Nitatembea Katika Kweli Yako”

“Nitatembea Katika Kweli Yako”

“Unifundishe, Ee Yehova, kuhusu njia yako. Nitatembea katika kweli yako.”​—ZB. 86:11.

NYIMBO: 31, 72

1-3. (a) Namna gani tunapaswa kuona kweli ya Biblia? Leta mufano. (Ona picha ku mwanzo wa habari hii.) (b) Tutazungumuzia nini mu habari hii?

LEO, ni jambo la kawaida kwa watu kununua ao kuuza kitu fulani mu duka na kisha wanarudisha kitu hicho. Na watu wengi zaidi wanarudisha vitu vyenye wameuza kupitia Enternete. Pengine hawafurahie kitu chenye waliuza kama vile waliwazia, ao pengine kiko na shida fulani. Kwa hiyo, wanaamua kuomba kitu kingine pa nafasi ya kitu hicho ao kuomba warudishiwe feza zao.

2 Hatutafanya vile hata kidogo juu ya kweli ya Biblia. Wakati ‘tunanunua’ kweli, hatupendi hata kidogo ‘kuiuzisha,’ ni kusema, wakati tunajifunza kweli, hatupendi kuiacha hata kidogo. (Soma Mezali 23:23; 1 Ti. 2:4) Kama vile tuliona mu habari yenye ilitangulia, tulitumia wakati mwingi ili kujifunza kweli. Pia, pengine tuliacha kazi yenye ilikuwa inatupatia feza nyingi. Na pengine tulipaswa kubadilisha uhusiano wetu pamoja na watu fulani, kubadilisha namna yetu ya kuwaza na kutenda, ao kuacha kufanya desturi na mazoea yenye hayamupendeze Yehova. Lakini tuko hakika kama baraka zenye tunapata kwa sababu ya kujua kweli ni za maana sana kuliko mambo yote yenye tumeachana nayo.

3 Yesu alitoa mufano wa mufanyabiashara musafiri mwenye alikuwa anatafuta lulu za muzuri. Wakati mwanaume huyo alipata lulu moja ya bei sana, aliuzisha palepale kila kitu chenye alikuwa nacho ili anunue lulu hiyo. Lulu hiyo inafananisha kweli juu ya Ufalme wa Mungu. Kupitia mufano huo, Yesu alionyesha kama kweli ingekuwa ya maana sana kwa wale wenye kuitafuta. (Mt. 13:45, 46) Wakati tulijifunza kweli kwa mara ya kwanza, ni kusema, kweli juu ya Ufalme wa Mungu na kweli zingine zote za maana zenye kuwa mu Biblia, sisi pia tulikuwa tayari kuachana na kitu chochote ili kupata kweli hiyo. Kama tunaendelea kuona kweli kuwa ya maana sana, hatutaiacha hata kidogo. Lakini jambo la kuhuzunisha ni kwamba, watumishi fulani wa Mungu wameacha kuona kweli kuwa ya maana na hata wameacha kweli hiyo. Hatupendi hata kidogo kufanya vile! Tunapaswa kufuata shauri la Biblia la ‘kuendelea kutembea katika kweli.’ (Soma 3 Yohana 2-4.) Maana yake, tunatia kweli pa nafasi ya kwanza na tunaonyesha jambo hilo kupitia namna yetu ya kuishi. Lakini juu ya nini na namna gani mutu anaweza ‘kuuzisha,’ ao kuacha kweli? Ni nini inaweza kutusaidia tusifanye vile hata siku moja? Ni nini inaweza kutusaidia tuazimie kabisa ‘kuendelea kutembea katika kweli’?

JUU YA NINI NA NAMNA GANI WATU FULANI ‘WANAUZISHA’ KWELI?

4. Mu siku za Yesu, juu ya nini watu fulani hawakuendelea kutembea katika kweli?

4 Mu siku za Yesu, watu fulani wenye walikubali kweli mwanzoni hawakuendelea kutembea katika kweli hiyo. Kwa mufano, kisha Yesu kufanya muujiza na kukulisha watu wengi sana, watu hao walimufuata kwenye upande mwingine wa Bahari ya Galilaya. Kisha Yesu alisema jambo fulani lenye liliwakwaza. Alisema hivi: “Kama hamukule mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamuna uzima ndani yenu wenyewe.” Kuliko kumuomba Yesu awafasirie maana ya maneno hayo, walisema hivi: “Maneno hayo ni yenye kuchukiza; ni nani mwenye anaweza kuyasikiliza?” Kwa hiyo, “wengi kati ya wanafunzi wake wakaenda kwenye mambo yenye yalikuwa nyuma na hawakutembea tena pamoja naye.”​—Yoh. 6:53-66.

5, 6. (a) Leo, juu ya nini watu fulani wameacha kweli? (b) Namna gani mutu anaweza kupeperushwa mbali na kweli?

5 Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, leo watu fulani wameacha pia kweli. Juu ya nini? Wamoja walikwazika kwa sababu ya mafasirio fulani ya mupya juu ya andiko fulani la Biblia ao kwa sababu ya jambo lenye ndugu fulani mwenye kujulikana sana alisema ao kufanya. Wengine hawakufurahia wakati mutu fulani aliwapatia mashauri kutoka mu Biblia, ao walikuwa na tatizo kubwa la kukosa kupatana na ndugu ao dada fulani mu kutaniko. Na wengine walifuata mafundisho ya uongo ya waasi-imani na wengine wenye kusema mambo ya uongo juu yetu. Hizo ni sababu fulani kati ya sababu zenye zimefanya watu fulani wamuache Yehova na kutaniko kwa makusudi. (Ebr. 3:12-14) Ingekuwa muzuri zaidi kama wangemutumainia Yesu kama vile Petro alifanya! Wakati watu wengine walikwazika kwa sababu ya maneno ya Yesu, Yesu aliuliza mitume wake ikiwa wao pia walipenda kuenda. Petro alijibu hivi: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe uko na maneno ya uzima wa milele.”​—Yoh. 6:67-69.

6 Wengine wamepeperushwa mbali na kweli pole kwa pole, pengine bila hata kutambua jambo hilo. Mutu mwenye anaacha kweli pole kwa pole iko kama mashua yenye inapeperushwa polepole kutoka kwenye inchi kavu. Biblia inatuonya tukuwe waangalifu ili “tusipeperushwe mbali hata kidogo.” (Ebr. 2:1) Mara nyingi mutu mwenye anapeperushwa mbali na kweli hafanye vile kwa makusudi. Lakini anaacha urafiki wake pamoja na Yehova ukuwe zaifu, na kisha wakati fulani anaweza kupoteza urafiki huo. Tunaweza kufanya nini ili jambo hilo lisitufikie hata kidogo?

TUNAWEZA KUFANYA NINI ILI TUSIUZISHE KWELI HATA KIDOGO?

7. Ni nini itatusaidia ili tusiuzishe kweli hata kidogo?

7 Ili tuendelee kutembea katika kweli, tunapaswa kukubali na kutii kila jambo lenye Yehova anasema. Tunapaswa kufanya kweli kuwa jambo la maana zaidi katika maisha yetu na kufuata kanuni za Biblia katika mambo yote yenye tunafanya. Katika sala, Mufalme Daudi alimuahidi Yehova hivi: “Nitatembea katika kweli yako.” (Zb. 86:11) Daudi aliazimia kuendelea kutembea katika kweli, na sisi pia tunapaswa kufanya vile. Ikiwa hatufanye vile, tunaweza kuanza kuwaza juu ya mambo yenye tumeachana nayo kwa ajili ya kweli na tunaweza hata kupenda kurudilia mambo fulani kati ya mambo hayo. Lakini hatuwezi kuchagua kweli za Biblia zenye tutaitika na zenye tutakataa. Tunapaswa kutembea katika “kweli yote.” (Yoh. 16:13) Mu habari yenye ilitangulia, tulizungumuzia mambo tano yenye pengine tuliachana nayo ili kujifunza kweli na kuitumia mu maisha yetu. Sasa tutazungumuzia mambo yenye tunapaswa kufanya ili tusirudilie hata kidogo mambo hayo yenye tumeacha nyuma.​—Mt. 6:19.

8. Namna gani kutumia wakati mubaya kunaweza kumufanya Mukristo apeperushwe mbali na kweli? Leta mufano.

8 Wakati. Ili tusipeperushwe mbali na kweli hata kidogo, tunapaswa kuendelea kutumia wakati wetu kwa hekima. Kama hatuko waangalifu, tunaweza kutumia wakati mwingi sana mu mambo ya kujifurahisha, mu mambo yenye tunafurahia kufanya ili kupitisha tu wakati, juu ya kutafuta-tafuta habari kwenye Enternete, ao kuangalia televizyo. Haiko mubaya kufanya mambo hayo. Lakini pengine tumeanza kutumia mu mambo hayo wakati wenye zamani tulikuwa tunatumia ili kujifunza na kuhubiri. Jambo kama hilo lilimufikia dada mumoja mwenye kuitwa Emma. * (Ona maelezo ya chini.) Tangu wakati alikuwa mudogo, alikuwa anapenda farasi na alikuwa anatembeza farasi wakati wowote alipata nafasi ya kufanya vile. Lakini zamiri yake ilianza kumusumbua juu ya wakati wenye alikuwa anapitisha ili kutembeza farasi, na akaamua kufanya mabadiliko juu ya mambo yenye alikuwa anatia pa nafasi ya kwanza. Pia, Emma alijifunza mambo fulani kupitia mufano wa dada Cory Wells, mwenye alikuwa anafanya mashindano ya kutembeza farasi. * (Ona maelezo ya chini.) Sasa, Emma anatumia wakati mwingi ili kumutumikia Yehova, na anatumia wakati mwingi pamoja na familia yake na marafiki wake wenye wanamutumikia Yehova pia. Anajisikia kuwa karibu zaidi na Mungu na anafurahi kujua kama anatumia wakati wake kwa hekima.

9. Namna gani tunaweza kuanza kuona vitu vya kimwili kuwa vya maana sana?

9 Vitu vya kimwili. Ili tuendelee kutembea katika kweli, hatupaswe kuruhusu vitu vya kimwili vikuwe vya maana sana kwetu. Wakati tulijifunza kweli, tulitambua kama kumutumikia Yehova ni jambo la maana sana kupita vitu vya kimwili, na tulifurahia kuachana na kitu chochote kwa ajili ya kweli. Lakini kadiri wakati unapita, tunaweza kuona wengine wanauza vitu vya kielektroniki vya sasa ao kufurahia vitu vingine vya kimwili. Tunaweza kuanza kuona kama tunakosa jambo fulani. Pengine hatutatosheka tena na vitu vyenye tuko navyo na tunaweza kuanza kukaza zaidi akili yetu juu ya kupata vitu vya kimwili kuliko kukaza akili yetu juu ya kumutumikia Yehova. Hilo linatukumbusha jambo lenye lilimufikia Dema. “Alipenda [sana] mupangilio wa mambo wa sasa,” mupaka akaacha mugao wenye alikuwa anafanya pamoja na mutume Paulo. (2 Ti. 4:10) Pengine Dema alipenda sana vitu vya kimwili kupita namna alipenda kumutumikia Mungu. Ao pengine hakupenda tena kujitoa ili kutumika pamoja na mutume Paulo. Mufano huo unatufundisha jambo gani? Pengine zamani tulipenda sana vitu vya kimwili. Kama hatuko waangalifu, upendo huo unaweza kukomaa tena ndani yetu na kuwa wenye nguvu kupita upendo wetu juu ya kweli.

10. Tunapaswa kupinga kishawishi gani?

10 Uhusiano pamoja na wengine. Ili tuendelee kutembea katika kweli, hatupaswe kuacha wale wenye hawamutumikie Yehova watushawishi. Wakati tulijifunza kweli, uhusiano wetu pamoja na marafiki na watu wa familia yetu wenye hawako Mashahidi ulibadilika. Pengine wamoja waliheshimia mambo ya mupya yenye tunaamini, lakini pengine wengine walipinga mambo hayo. (1 Pe. 4:4) Kwa kweli, tunajikaza kuelewana na watu wa familia yetu na kuwatendea kwa heshima. Lakini hatuwezi kuvunja kanuni za Yehova ili kuwafurahisha. Na kama vile andiko la 1 Wakorinto 15:33 linaonyesha, marafiki wetu wa sana wanapaswa kuwa watu wenye kumupenda Yehova.

11. Tunaweza kufanya nini ili kuepuka mawazo na matendo machafu?

11 Mawazo na matendo machafu. Ili tutembee katika kweli, tunapaswa kuwa watakatifu, ao safi, mbele za Yehova. (Isa. 35:8; soma 1 Petro 1:14-16.) Wakati tulijifunza kweli, tulifanya mabadiliko katika maisha yetu ili kufuata kanuni za Biblia. Wamoja walifanya mabadiliko makubwa. Lakini, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusiache maisha yetu yenye kuwa safi na kuanza kuishi maisha machafu. Ni nini inaweza kutusaidia ili tushinde kishawishi cha kufanya jambo lolote la mubaya? Fikiria jambo lenye Yehova alitoa ili tukuwe watakatifu. Alitoa uzima wa maana sana wa Mwana wake mupendwa, Yesu Kristo! (1 Pe. 1:18, 19) Ili kuendelea kuwa safi mbele za Yehova, sikuzote tunapaswa kukumbuka kama zabihu ya bei ya ukombozi ya Yesu ni ya maana sana.

12, 13. (a) Juu ya nini tunapaswa kuona sikukuu namna Yehova anaziona? (b) Tutazungumuzia nini sasa?

12 Desturi na mazoea yenye hayamupendeze Mungu. Watu wa familia yetu, wafanyakazi wenzetu, na wanafunzi wenzetu wanaweza kutuchochea tujiunge nao ili kufanya sikukuu mbalimbali. Ni nini inaweza kutusaidia kupinga mukazo wa kufanya desturi na sikukuu zenye hazimupendeze Yehova? Tunapaswa kuendelea kukumbuka sababu zenye zinafanya Yehova asikubali sikukuu hizo. Tunaweza kutafuta habari katika vichapo vyetu na kujikumbusha namna sikukuu fulani zilianza. Wakati tunafikiri sana juu ya sababu zenye kutegemea Maandiko zenye kutuchochea tusifanye sikukuu hizo, tunakuwa hakika kama tunatembea katika njia yenye “kukubaliwa kwa Bwana.” (Efe. 5:10) Kama tunamutumainia Yehova na Neno lake, hatutaogopa mambo yenye watu wengine wanawaza juu yetu.​—Mez. 29:25.

13 Tunatumaini kama tutaendelea kutembea katika kweli milele. Ni nini inaweza kutusaidia tuazimie hata zaidi kuendelea kutembea katika kweli? Tuone mambo tatu yenye tunaweza kufanya.

AZIMIA ZAIDI KUTEMBEA KATIKA KWELI

14. (a) Juu ya nini kuendelea kujifunza Biblia kunatusaidia tuazimie zaidi kubakia katika kweli? (b) Juu ya nini tuko na lazima ya hekima, nizamu, na uelewaji?

14 Kwanza, uendelee kujifunza Biblia na kufikiri sana juu ya mambo yenye unajifunza. Upange wakati wa kufanya vile kwa ukawaida. Kama unaendelea kujifunza, utapenda kweli zaidi na utaazimia zaidi kubakia katika kweli. Mezali 23:23 inasema ‘tununue kweli’ na tununue pia “hekima na nizamu na uelewaji.” Haitoshe tu kujua kweli ya Biblia. Tunapaswa kuitumia katika maisha yetu. Wakati tunapata uelewaji, tunatia pamoja mambo yenye tumejifunza na mambo yenye tayari tunajua. Hekima inatuchochea kutenda kulingana na mambo yenye tunajua. Wakati fulani kweli inatupatia nizamu kwa kutuonyesha mambo yenye tunapaswa kufanyia mabadiliko. Tunapaswa kutenda haraka wakati tunapewa nizamu hiyo, yenye Biblia inasema kama ni ya maana sana kuliko feza.​—Mez. 8:10.

15. Namna gani kweli inatulinda kama vile mukaba?

15 Pili, uazimie kutumia kweli katika maisha yako ya kila siku. Biblia inalinganisha kweli na mukaba ao mushipi wa askari. (Efe. 6:14) Wakati wa zamani, mukaba ulikuwa unamulinda askari wakati wa vita ikiwa tu ulikuwa unakaza. Kama mukaba huo haukukuwa unakaza kabisa, haungemusaidia. Namna gani kweli inatulinda kama vile mukaba? Kama tunaendelea kukumbuka kweli ya Biblia kila wakati, itatulinda ili tusikuwe na mawazo ya mubaya na itatusaidia kukamata maamuzi ya muzuri. Wakati tuko na tatizo kubwa ao wakati tunashawishiwa kufanya jambo fulani la mubaya, kweli ya Biblia itatusaidia tuazimie zaidi kufanya mambo yenye kuwa sawa. Kama vile askari hangeenda kwenye vita hata siku moja bila kuwa na mukaba wake, hatutaacha kweli hata siku moja. Tunajikaza kutumia kweli ya Biblia katika kila sehemu ya maisha yetu. Askari angeweza kubeba pia upanga kwenye mukaba wake. Tuone basi namna sisi pia tunaweza kufanya vile.

16. Namna gani kufundisha kweli kunatusaidia tuendelee kutembea katika kweli?

16 Tatu, ujikaze kabisa kufundisha wengine kweli ya Biblia kwa kadiri unaweza. Biblia inafananishwa na upanga. Kama vile askari muzuri alishika kwa nguvu sana upanga wake, tunapaswa kuendelea kushika kwa nguvu sana Neno la Mungu. (Efe. 6:17) Sisi wote tunaweza kuwa walimu wazuri zaidi, wenye ‘kutumia sawasawa neno la kweli.’ (2 Ti. 2:15) Wakati tunatumia Biblia ili kufundisha wengine, tunafikia kujua kweli zaidi na kuipenda zaidi. Na tunaazimia zaidi kuendelea kutembea katika kweli.

17. Juu ya nini unaona kweli kuwa ya maana sana?

17 Kweli ni zawadi ya maana sana kutoka kwa Yehova. Inatusaidia kuwa na urafiki wa sana pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Hilo ndilo jambo la maana zaidi lenye tuko nalo. Tayari Yehova ametufundisha mambo mengi sana, lakini huo ni mwanzo tu! Anatuahidi kama ataendelea kutufundisha milele. Kwa hiyo, uone kweli kuwa ya maana sana kama vile unaweza kuona lulu ya samani. Uendelee ‘kununua kweli na usiiuzishe hata kidogo.’ Kisha, kama Daudi, utatimiza ahadi hii kwa Yehova: “Nitatembea katika kweli yako.”​—Zb. 86:11.

^ fu. 8 Jina limebadilishwa.

^ fu. 8 Fungua JW Télédiffusion, kwenye sehemu yenye kichwa KUULIZWA MAULIZO NA USHUHUDA > KWELI INABADILISHA MAISHA.