Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Vijana, Munaweza Kuwa na Maisha Yenye Furaha

Vijana, Munaweza Kuwa na Maisha Yenye Furaha

“Unanijulisha njia ya uzima.”​—ZB. 16:11.

NYIMBO: 133, 89

1, 2. Namna gani mufano wa Tony unaonyesha kama mutu anaweza kufanya mabadiliko mu maisha?

TONY alikomaa bila kuwa na baba. Alikuwa mwanafunzi ku masomo ya segondere, lakini hakukuwa anafurahia kabisa masomo. Kwa kweli, alikuwa anafikiria kuacha masomo bila kupata diplome. Ku mwisho wa juma, Tony alikuwa anaenda kuangalia filme ao kupitisha wakati pamoja na marafiki wake. Hakukuwa mwenye jeuri na hakukuwa anatumia dawa za kulewesha, lakini hakukuwa na kusudi mu maisha. Hakukuwa hata hakika kama Mungu iko. Siku moja, alikutana na Mashahidi wawili wa Yehova na aliwaambia mashaka yenye alikuwa nayo juu ya Mungu. Walimupatia broshua mbili za kusoma: broshua Uhai​Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai.

2 Wakati walimutembelea Tony, mawazo yake ilikuwa imebadilika. Alikuwa amesoma sana broshua hizo mupaka zikakunjama-kunjama. Tony aliambia Mashahidi hao hivi: “Kunapaswa kuwa Mungu.” Alianza kujifunza Biblia, na pole kwa pole mawazo yake juu ya maisha ilibadilika. Mbele aanze kujifunza Biblia, hakukuwa mwanafunzi muzuri, lakini akakuwa kati ya wanafunzi wazuri kwenye masomo yao! Hata musimamizi wa masomo alishangaa. Alimuambia hivi: “Umefanya maendeleo makubwa katika tabia yako na unaanza kupata alama mingi. Je, umefanya ile maendeleo kwa sababu uko unazungumuza na Mashahidi wa Yehova?” Tony alikubali na akazungumuza na musimamizi wa masomo juu ya mambo yenye alikuwa anajifunza. Alimaliza masomo ya segondere na leo iko painia wa kawaida na mutumishi wa huduma. Tony ni mwenye furaha sana kwa sababu leo iko na Baba mwenye upendo, ni kusema, Yehova!​—Zb. 68:5.

UMUTII YEHOVA, NA UTAPATA MATOKEO YA MUZURI

3. Yehova anapatia vijana shauri gani?

3 Mufano wa Tony unatukumbusha kama Yehova anahangaikia kabisa vijana. Anapenda ukuwe na maisha ya muzuri kabisa na yenye furaha, kwa hiyo, anakushauria ukumbuke “Muumbaji wako Mukubwa katika siku za ujana wako.” (Muh. 12:1) Sikuzote, haiko mwepesi kufanya vile, lakini inawezekana. Kwa musaada wa Mungu, unaweza kuwa na maisha yenye furaha wakati ungali kijana na wakati utakuwa mutu muzima. Ili kutusaidia tuelewe muzuri ile jambo, tutazungumuzia ni nini ilisaidia Waisraeli wakamate Inchi ya Ahadi na ni nini ilimupatia Daudi uwezo wa kushinda Goliati, mutu munene na murefu sana.

4, 5. Namna Waisraeli walishinda Wakanaani na namna Daudi alimushinda Goliati, inaweza kutufundisha nini? (Ona picha ku mwanzo wa habari hii.)

4 Wakati Waisraeli walikuwa karibu kuingia mu Inchi ya Ahadi, Yehova aliwapatia maagizo gani? Aliwaambia wakuwe maaskari wazuri ao wajizoeze kwa ajili ya vita? Hapana! (Kum. 28:1, 2) Aliwaambia wamutii na wamutumainie. (Yos. 1:7-9) Pengine wanadamu waliona kuwa ile shauri haikukuwa na maana, lakini ilikuwa shauri ya muzuri sana kwa ajili ya Waisraeli. Tena na tena, Yehova alisaidia watu wake washinde Wakanaani. (Yos. 24:11-13) Inaomba kuwa na imani ili kumutii Mungu, lakini sikuzote imani hiyo inaleta matokeo ya muzuri. Ilikuwa vile wakati wa zamani, na ni vile pia leo.

5 Goliati alikuwa mupiganaji mwenye nguvu. Alikuwa na urefu wa metre karibu tatu, na alikuwa anabeba silaha za hatari sana. (1 Sa. 17:4-7) Lakini Daudi alikuwa tu na kombeo na imani katika Yehova. Mutu mwenye hana imani angewaza kama Daudi alikosa akili kwa sababu alijaribu kupigana na Goliati! Lakini kwa kweli, Goliati njo alikosa akili.​—1 Sa. 17:48-51.

6. Tutazungumuzia nini mu habari hii?

6 Mu habari yenye ilitangulia, tulizungumuzia vitu ine vyenye vinaweza kutufanya tukuwe wenye furaha zaidi na tukuwe na maisha ya muzuri zaidi. Tulijifunza kama tunapaswa kutimiza uhitaji wetu wa kiroho, kutafuta marafiki wazuri wenye kumupenda Mungu, kujiwekea miradi ya muzuri, na kupendezwa na uhuru wenye Mungu anatupatia. Mu habari hii, tutazungumuzia ni katika njia zingine gani tunaweza kupata faida wakati tunafanya ile mambo ya muzuri. Ili kufanya vile, tuzungumuzie basi kanuni fulani zenye tunapata mu Zaburi ya 16.

UTIMIZE UHITAJI WAKO WA KIROHO

7. (a) Kuwa mutu wa kiroho maana yake nini? Fasiria. (b) “Fungu” la Daudi lilikuwa nini, na hilo lilimufanya ajisikie namna gani?

7 Mutu wa kiroho iko na imani katika Mungu na anajikaza kuona mambo namna Mungu anaiona. Anamuacha Yehova aongoze maisha yake na anaazimia kumutii. (1 Ko. 2:12, 13) Daudi ni mufano muzuri wa mutu wa kiroho. Aliimba hivi: “Yehova ni fungu langu.” (Zb. 16:5) Daudi alikuwa mwenye shukrani kwa ajili ya “fungu” lake, ni kusema, urafiki wake wa sana pamoja na Mungu, na alimufanya kuwa kimbilio yake. (Zb. 16:1) Kwa hiyo, angeweza kusema hivi: “Nafsi yangu yote iko na shangwe.” Hakuna jambo ingine yenye ilimuletea Daudi furaha kupita urafiki wake wa sana pamoja na Yehova!​—Soma Zaburi 16:9, 11.

8. Ni mambo gani fulani yenye inaweza kufanya maisha yako ikuwe yenye furaha kabisa?

8 Watu wenye kukaza akili yao juu ya feza ao raha hawawezi kuwa hata kidogo na shangwe ao furaha kama ile yenye Daudi alikuwa nayo. (1 Ti. 6:9, 10) Ndugu mumoja mu inchi ya Kanada alisema hivi: “Haiko mambo yenye tunapata mu maisha njo inatuletea furaha ya kweli, lakini ni mambo yenye tunamupatia Yehova Mungu, mwenye kutoa kila zawadi ya muzuri.” (Yak. 1:17) Kama unakomalisha imani katika Yehova na kumutumikia, utakuwa na maisha yenye kusudi na yenye furaha kabisa. Kwa hiyo, unaweza kufanya nini ili kutia nguvu imani yako? Unapaswa kupitisha wakati pamoja na Yehova kwa kusoma Neno lake, kuangalia vitu vya muzuri vyenye aliumba, na kufikiri juu ya sifa zake, kutia ndani upendo wenye anakuonyesha.​—Ro. 1:20; 5:8.

9. Unaweza kufanya nini ili kuacha Neno la Mungu likufinyange?

9 Wakati fulani, Mungu anatuonyesha upendo wake kwa kuturekebisha wakati tuko na lazima ya kurekebishwa, kama vile tu baba mwenye upendo anafanyaka. Daudi aliona ile marekebisho kuwa ya maana na alisema hivi: “Nitamusifu Yehova, mwenye amenipa shauri. Hata wakati wa usiku, mawazo yangu ya ndani kabisa yananirekebisha.” (Zb. 16:7) Daudi alifikiri sana juu ya mawazo ya Mungu na akakuwa na mawazo kama ya Mungu. Aliruhusu mawazo ya Mungu imufinyange, ni kusema, aliacha imubadilishe ili akuwe mutu muzuri zaidi. Kama na wewe unafanya vile, upendo wako kwa Mungu na tamaa yako ya kumupendeza vitakomaa, na utakuwa Mukristo mwenye kukomaa kiroho. Dada mwenye kuitwa Christin anasema kama wakati anatafuta habari na anafikiri sana juu ya mambo yenye anasoma, anajisikia kuwa Yehova aliandikisha ile mambo kwa ajili yake kabisa!

10. Kulingana na Isaya 26:3, kuwa mutu wa kiroho kutakusaidia namna gani?

10 Kama uko mutu wa kiroho, utaona ulimwengu na wakati wake wenye kuja kama vile Yehova. Yehova anakupatia ujuzi na ufahamu huo wa pekee. Juu ya nini? Anapenda ujue mambo yenye kuwa ya maana mu maisha, ukamate maamuzi ya muzuri, na ungojee wakati wenye kuja bila kuogopa! (Soma Isaya 26:3.) Ndugu mwenye kuitwa Joshua, mwenye kuishi mu inchi ya Amerika, anasema kama ikiwa unabakia karibu na Yehova, utaona waziwazi mambo yenye kuwa ya maana na mambo yenye haiko ya maana sana.

UTAFUTE MARAFIKI WAZURI

11. Daudi alichagua marafiki wa namna gani?

11 Soma Zaburi 16:3. Daudi alijua namna ya kupata marafiki wazuri. Alichagua marafiki wenye walimupenda Yehova, na kufanya vile ‘kulimupendeza sana.’ Alisema kama marafiki wake walikuwa “watakatifu,” kwa sababu walijikaza kufuata kanuni za Yehova za mwenendo safi. Muandikaji mwingine wa zaburi alikuwa na mawazo ileile juu ya kuchagua marafiki wazuri na aliandika hivi: “Niko rafiki ya wote wenye kukuogopa na ya wale wenye kushika maagizo yako.” (Zb. 119:63) Kama vile tuliona mu habari yenye ilitangulia, wewe pia unaweza kupata marafiki wazuri kati ya watu wenye kumupenda Yehova na kumutii. Na kwa kweli, haiko lazima marafiki wako wakuwe tu wa miaka yako.

12. Juu ya nini Daudi na Yonatani walikuwa marafiki wazuri?

12 Daudi hakuchagua tu watu wa miaka yake ili wakuwe marafiki wake. Unaweza kutaja jina ya mutu mumoja kati ya marafiki wa sana wa Daudi? Pengine unafikiria Yonatani. Urafiki kati ya Daudi na Yonatani ni kati ya urafiki wa muzuri zaidi wenye kuzungumuziwa mu Biblia. Lakini, ulijua kama Yonatani alimupita Daudi miaka 30? Kwa hiyo, juu ya nini walikuwa marafiki wazuri? Urafiki wao ulitegemea imani yao katika Mungu. Pia, walikuwa wanaheshimiana na walipendezwa na sifa za muzuri zenye kila mumoja wao alikuwa nazo, kama vile ujasiri wenye kila mumoja alionyesha wakati alipigana na maadui wa Mungu.​—1 Sa. 13:3; 14:13; 17:48-50; 18:1.

13. Unaweza kufanya nini ili kuwa na marafiki wengi zaidi? Leta mufano.

13 Kama Daudi na Yonatani, tunaweza kupata furaha kubwa wakati tuko na marafiki wenye kumupenda Yehova na wenye kuwa na imani katika yeye. Kiera, mwenye amemutumikia Mungu kwa miaka mingi anasema hivi: “Nimekuwa na marafiki mu dunia yote, watu wa mahali mbalimbali na desturi mbalimbali.” Na wewe ukifanya vile, utajionea namna Biblia na roho takatifu vinatufanya tukuwe familia moja ya waabudu wa Yehova mu dunia yote.

UJIWEKEE MIRADI YA MUZURI

14. (a) Ni nini inaweza kukusaidia ujiwekee miradi ya muzuri mu maisha? (b) Vijana fulani wanasema nini juu ya miradi yao?

14 Soma Zaburi 16:8. Daudi aliona kuwa jambo la maana zaidi ni kumutumikia Yehova. Kama unamuiga Daudi wakati unajiwekea miradi na kufikiria sikuzote mambo yenye Yehova anapenda ufanye, maisha yako itakuwa yenye furaha. Ndugu mwenye kuitwa Steven, anasema hivi: “Kujikaza ili kufikia muradi fulani, kutimiza muradi huo, na kufikiria maendeleo yenye nimefanya, kunaniletea furaha.” Ndugu mumoja kijana wa inchi ya Ujerumani, mwenye anatumikia sasa mu inchi ingine, anasema hivi: “Wakati nitazeeka, sipendi nifikirie namna nilitumia maisha yangu na kuona kama kila kitu chenye nilifanya kilikuwa kwa ajili ya faida yangu mwenyewe.” Na wewe unajisikia vile? Kama jibu yako ni ndiyo, utumie uwezo wako mbalimbali ili kumuletea Yehova utukufu na kusaidia watu wengine. (Gal. 6:10) Ujiwekee miradi katika utumishi wa Yehova, na umuombe Yehova akusaidie kufikia miradi hiyo. Unaweza kuwa hakika kama atajibu sala yako!​—1 Yo. 3:22; 5:14, 15.

15. Unaweza kujiwekea miradi gani fulani? (Ona kisanduku “ Miradi Fulani ya Kufikiria.”)

15 Ni miradi gani fulani yenye unaweza kujiwekea? Unaweza kujiwekea miradi kama vile kutoa maelezo ku mikutano ya kutaniko mu maneno yako mwenyewe, kuwa painia, ao kutumikia ku Beteli. Unaweza pia kujifunza luga ingine yenye unaweza kutumia ili kutangazia watu wengi zaidi habari njema. Barak, ndugu kijana mwenye kuwa katika utumishi wa wakati wote, anasema hivi: “Wakati ninaamuka kila siku na kujua kama ninaendelea kupatia Yehova nguvu zangu zote, hilo linanifanya nijisikie muzuri, hakuna kazi ingine yenye inaweza kunifanya nijisikie vile.”

UPENDEZWE NA UHURU WENYE MUNGU ANAKUPATIA

16. Daudi alijisikia namna gani juu ya sheria na kanuni za Yehova, na juu ya nini alijisikia vile?

16 Soma Zaburi 16:2, 4. Kama vile tuliona mu habari yenye ilitangulia, wakati tunaishi kulingana na sheria na kanuni za Mungu, tunakuwa huru kabisa. Tunajifunza kupenda mambo ya muzuri na kuchukia mambo ya mubaya. (Amo. 5:15) Daudi alisema kama Yehova alikuwa ‘Chanzo chake cha wema.’ Neno la zamani lenye lilitafsiriwa “wema” linatia pia ndani wazo ya tabia ya muzuri. Yehova ni mwema katika mambo yote, na kila kitu chema ao cha muzuri chenye tuko nacho kinatoka kwake. Daudi alijikaza sana ili kumuiga Yehova na kupenda mambo yenye anapenda. Lakini Daudi alijifunza pia kuchukia mambo yenye Mungu anasema kuwa ni ya mubaya. Jambo moja kati ya ile mambo ni kuabudu sanamu, ni kusema, kuabudu mutu ao kitu fulani kuliko kumuabudu Yehova. Kuabudu sanamu kunashushia watu heshima na kunapatia mutu ao kitu fulani utukufu wenye Yehova anapaswa kupewa.​—Isa. 2:8, 9; Ufu. 4:11.

17, 18. (a) Daudi alisema nini juu ya matokeo ya mubaya ya ibada ya uongo? (b) Leo, ni nini inafanya watu ‘waongeze huzuni zao’?

17 Wakati wa zamani, mara nyingi uasherati ulikuwa sehemu ya ibada ya uongo. (Ho. 4:13, 14) Watu wengi walifurahia ibada ya uongo kwa sababu walifurahia uasherati. Lakini ibada hiyo ilifanya wakuwe wenye furaha? Hapana hata kidogo! Daudi alisema kama wale wenye kuabudu miungu ya uongo “wanaongeza huzuni zao.” Watu hao walitoa hata watoto wao ili wakuwe zabihu kwa miungu ya uongo! (Isa. 57:5) Yehova alichukia matendo yao ya kukosa huruma. (Yer. 7:31) Kama uliishi katika siku hizo, kwa kweli ungekuwa mwenye shukrani sana ikiwa wazazi wako walikuwa wanamuabudu Yehova.

18 Leo, dini mingi za uongo zinakubali uasherati, kutia ndani hata tendo ya mwanaume kulala na mwanaume na mwanamuke kulala na mwanamuke. Kuishi maisha ya mwenendo muchafu kunaweza kufanya watu wajisikie kuwa huru, lakini kwa kweli “wanaongeza huzuni zao.” (1 Ko. 6:18, 19) Umetambua ile jambo? Kwa hiyo, vijana, mumusikilize Baba yenu wa mbinguni. Ujihakikishie kuwa kumutii Mungu ni jambo ya muzuri kwako. Ufikirie kwa uangalifu matokeo ya mubaya ya uasherati. Utaona kama mwenendo mubaya unaleta raha ya muda, lakini matokeo ya mubaya njo ya mingi sana. (Gal. 6:8) Joshua, mwenye tumekwisha kutaja, anasema hivi: “Tunaweza kutumia uhuru wetu namna tunapenda, lakini kuutumia mubaya hakulete furaha.”

19, 20. Vijana wenye kuwa na imani katika Yehova na wenye kumutii watapata baraka gani?

19 Yesu alisema hivi: “Kama munakaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, na mutajua kweli, na kweli itawaweka ninyi huru.” (Yoh. 8:31, 32) Yehova ametufanya tukuwe huru kutokana na dini ya uongo, kukosa kujua, na mambo ya uchawi. Wakati wenye kuja, tunangojea kupata “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Ro. 8:21) Unaweza kufurahia uhuru huo kwa kadiri fulani hata leo wakati unafuata mafundisho ya Kristo. Mu njia hiyo, utafikia ‘kujua kweli,’ haiko tu kwa kujifunza kweli hiyo lakini pia kwa kuishi kulingana nayo!

20 Vijana, mupendezwe na uhuru wenye Mungu anawapatia. Mutumie uhuru huo kwa hekima. Utawasaidia kukamata maamuzi leo yenye inaweza kuwasaidia mukuwe na wakati muzuri sana wenye kuja. Ndugu mumoja kijana anasema hivi: “Kutumia uhuru kwa hekima wakati uko kijana kunakusaidia kabisa wakati utakamata maamuzi mazito wakati wenye kuja, kama vile kutafuta kazi yenye kufaa ao kuamua kama utaoa ao kuolewa ao utabakia bila kuoa ao kuolewa kwa wakati fulani.”

21. Unaweza kufanya nini ili upate “uzima wa kwelikweli”?

21 Katika ulimwengu huu, hata maisha yenye watu wanaona kuwa maisha ya muzuri ni ya mufupi. Hakuna mutu mwenye anajua mambo itakuwa namna gani kesho. (Yak. 4:13, 14) Kwa hiyo, jambo ya muzuri zaidi yenye unaweza kufanya ni kukamata maamuzi yenye itakusaidia kupata “uzima wa kwelikweli,” ni kusema, uzima wa milele mu ulimwengu mupya wa muzuri sana wa Mungu. (1 Ti. 6:19) Yehova halazimishe mutu yeyote amutumikie. Kila mutu anapaswa kuamua mambo yenye atafanya. Kwa hiyo, umufanye Yehova kuwa “fungu” lako kwa kujikaza kila siku ili kumukaribia zaidi, na kupendezwa na “vitu [vyote] vya muzuri” vyenye anakupatia. (Zb. 103:5) Ukuwe hakika kama Yehova anaweza kukupatia shangwe na furaha kubwa milele!​—Zb. 16:11.