Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Atafanya Mambo Gani?

Mungu Atafanya Mambo Gani?

Ikiwa ungekuwa katika hali fulani ngumu, bila shaka ungetazamia rafiki yako wa karibu akusaidie. Kwa msingi huo, baadhi ya watu hawamwoni Mungu kama rafiki yao kwa sababu wanahisi hafanyi chochote ili kuwasaidia. Lakini ukweli ni kwamba, tayari Mungu amefanya mambo mengi yanayotunufaisha na hata atatatua matatizo yote tunayokabili leo. Atafanya hivyo jinsi gani?

ATAKOMESHA UOVU WOTE

Mungu atakomesha uovu wote kwa kuondoa chanzo cha uovu. Biblia inataja chanzo cha uovu inaposema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) “Mwovu” huyo ni Shetani Ibilisi, ambaye Yesu alimwita “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31) Shetani anauongoza ulimwengu, na ndiyo sababu wanadamu wanakabili hali ngumu. Mungu atafanya nini?

Hivi karibuni, Yehova Mungu atamtumia Mwana wake, Yesu Kristo, “[kumwangamiza] yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi.” (Waebrania 2:14; 1 Yohana 3:8) Isitoshe, Biblia inasema hata Shetani mwenyewe anajua kwamba “ana kipindi kifupi cha wakati,” na hivi karibuni ataangamizwa. (Ufunuo 12:12) Pia, Mungu atawaharibu wale wote wanaosababisha uovu.—Zaburi 37:9; Methali 2:22.

ATAIGEUZA DUNIA KUWA PARADISO

Baada ya kukomesha uovu wote, Muumba wetu atachukua hatua ili wanadamu wakamilifu waishi milele katika dunia paradiso, na hivyo kutimiza kusudi lake. Tunaweza kutazamia nini?

Amani ya kudumu na usalama. “Wapole wataimiliki dunia, nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

Chakula kingi chenye lishe. “Kutakuwa na nafaka nyingi duniani; itafurika juu ya milima.”—Zaburi 72:16.

Nyumba nzuri na kazi zenye kuridhisha. “Watajenga nyumba na kuishi ndani yake, nao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. . . . Watu wangu niliowachagua watafurahia kikamili kazi ya mikono yao.”—Isaya 65:21, 22.

Je, unatazamia kwa hamu kuona ahadi hizo zikitimia? Hivyo ndivyo hali zitakavyokuwa hivi karibuni.

ATAKOMESHA MAGONJWA NA KIFO

Leo, kila mmoja wetu anaweza kuwa mgonjwa na kufa, lakini matatizo hayo yanakaribia kukomeshwa. Mungu atatumia dhabihu ya fidia ya Yesu kuhakikisha kwamba, ‘kila mtu anayemwamini haangamizwi bali anapata uzima wa milele.’ (Yohana 3:16) Matokeo yatakuwaje?

Magonjwa yatakomeshwa. “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’ Watu wanaokaa katika nchi watasamehewa dhambi yao.”—Isaya 33:24.

Kifo hakitawahangaisha wanadamu tena. “Atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atafuta kabisa machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.

Watu wataishi milele. “Zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 6:23.

Watu waliokufa watafufuliwa. “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Kwa msingi wa zawadi ya fidia ambayo Mungu alitoa, watu waliokufa watarudishiwa tena uhai.

Mungu atatimiza ahadi zote hizo jinsi gani?

ATASIMAMISHA SERIKALI ISIYO NA KASORO

Mungu atatimiza kusudi lake kwa wanadamu na dunia kupitia serikali ya mbinguni, na amemteua Yesu Kristo kuwa Mtawala. (Zaburi 110:1, 2) Hiyo ndiyo serikali, au ufalme, ambao Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kuuhusu, aliposema hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, . . . Ufalme wako na uje.”—Mathayo 6:9, 10.

Ufalme wa Mungu utaitawala dunia na kukomesha maumivu na mateso yote yaliyopo sasa. Ufalme huo ndio serikali bora kuliko serikali zote zilizowahi kutawala! Ndiyo maana Yesu, alipokuwa duniani, alitangaza kwa bidii sana “habari njema ya Ufalme” na akawafundisha wanafunzi wake wafanye hivyo pia.—Mathayo 4:23; 24:14.

Yehova Mungu ameahidi kufanya mambo hayo yote mazuri kwa sababu anawapenda sana wanadamu. Kujua jambo hilo kunakuchochea utamani kumfahamu vizuri zaidi na kuwa na uhusiano wa karibu na yeye, sivyo? Utanufaikaje ukiamua kusitawisha uhusiano wa karibu na Mungu? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

MUNGU ATAFANYA MAMBO GANI? Mungu atakomesha magonjwa na kifo, atawaunganisha wanadamu kupitia Ufalme wake, na ataigeuza dunia kuwa paradiso