Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu za KUTOKATA Tamaa Maishani

Sababu za KUTOKATA Tamaa Maishani

Faizal alihitaji kufanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo mwaka mmoja hivi baada ya mke wake kufa. Anasema: “Ninaposoma kitabu cha Ayubu, ninaona kwamba Mungu alikiweka kwenye Biblia akiwa na kusudi. Tunaposoma simulizi la Biblia la mtu aliyetaabika moyoni kama tunavyotaabika, tunafarijika sana.” Anasema hivi pia: “Bado kuna sababu za kutokata tamaa.”

Tarsha alikuwa na umri mdogo mama yake alipokufa. Anasema hivi: “Licha ya mambo yote tunayokabili, maisha yana kusudi, tumaini, na shangwe kwa sababu ya kumjua Muumba wetu. Yehova ana uwezo mkubwa sana wa kututegemeza na kutusaidia kukabiliana na hali za kila siku.”

MAKALA zilizotangulia zimeonyesha jinsi matukio yenye kutaabisha yanavyoweza kufanya tuhisi tumelemewa na maisha. Unapokuwa umelemewa na hali yako, huenda ukahisi hamna sababu ya kuendelea kuishi au ukafikiri hakuna yeyote anayekujali. Uwe na uhakika kwamba Mungu anaelewa mahangaiko yako na anakujali. Wewe una thamani kwake.

Mwandishi wa Zaburi ya 86 alionyesha kwamba anamwamini Mungu aliposema: “Ninakuitia wewe katika siku ninayotaabika, kwa maana utanijibu.” (Zaburi 86:7) Lakini huenda ukajiuliza, ‘Mungu atatumia njia gani kunijibu “katika siku ninayotaabika”?’

Ingawa huenda Mungu hataondoa matatizo yako yote papo hapo, Neno lake, Biblia, linatuhakikishia kwamba atakupa amani ya moyoni ambayo itakusaidia kuvumilia: “Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na mawazo yenu.” (Wafilipi 4:6, 7, maelezo ya chini) Maandiko yafuatayo yanatuhakikishia kwamba kweli Mungu anatujali.

Mungu Anakujali

“Mungu hampuuzi [shore] hata mmoja. . . . [Wewe ni mwenye] thamani kuliko shore wengi.”Luka 12:6, 7, maelezo ya chini.

FIKIRIA JAMBO HILI: Ingawa huenda ndege wakaonekana kuwa duni machoni petu, sivyo ilivyo na Mungu. Mungu anawakazia uangalifu hata shore wadogo; kila mmoja wao ni kiumbe mwenye thamani kwake. Hata hivyo, Mungu anawathamini zaidi wanadamu kuliko shore. Wanadamu ndio viumbe wa pekee kati ya uumbaji wote wa Mungu duniani. Wameumbwa kwa “mfano” wake na wana uwezo wa kusitawisha na kuonyesha sifa zake zisizo na kifani.—Mwanzo 1:26, 27.

“Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua. . . . Unatambua mawazo yangu . . . Nipime, uyajue mawazo . . . yanayonihangaisha.”Zaburi 139:1, 2, 23.

FIKIRIA JAMBO HILI: Mungu anakujua vizuri sana. Anajua hisia zako za ndani na mambo yanayokuhangaisha. Ingawa huenda watu wengine wasielewe matatizo yako, Mungu anakujali na anataka kukusaidia. Kujua jambo hilo kunatupatia sababu ya kuendelea kuishi.

Maisha Yako Yana Maana

“Ee Yehova, sikia sala yangu; kilio changu cha kuomba msaada na kikufikie. . . . Nitegee sikio lako; nijibu haraka ninapokuita. . . . Ataisikiliza sala ya maskini.”Zaburi 102:1, 2, 17.

FIKIRIA JAMBO HILI: Tangu wanadamu walipoanza kuteseka, Yehova amekuwa akiona kila chozi linalodondoka. (Zaburi 56:8) Anaona machozi yako pia. Mungu anatambua matatizo na machozi yako yote kwa sababu una thamani kwake.

“Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia . . . Mimi, Yehova Mungu wako . . . [ninakwambia], ‘Usiogope. Nitakusaidia.’”Isaya 41:10, 13.

FIKIRIA JAMBO HILI: Mungu yuko tayari kukusaidia. Ukianguka, atakuinua.

Wakati Ujao Hali Itakuwa Nzuri

“Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”Yohana 3:16.

FIKIRIA JAMBO HILI: Mungu anakupenda sana hivi kwamba alimtoa kwa hiari Mwana wake, Yesu, kuwa dhabihu kwa ajili yako. Kwa msingi wa dhabihu hiyo, una tumaini la kuishi maisha ya furaha yaliyo na kusudi milele. *

Ingawa huenda una matatizo mengi na labda unahisi umelemewa, chunguza Neno la Mungu kwa makini ili ujenge imani yako katika ahadi za Mungu za wakati ujao. Utapata shangwe na ujasiri wa kuendelea kuishi.

^ Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu jinsi dhabihu ya Yesu inavyoweza kukunufaisha, tazama video Kumbuka Kifo cha Yesu kwenye tovuti ya www.pr418.com/sw. Tazama kwenye KUTUHUSU > UKUMBUSHO.