Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 2

Msifu Yehova Katika Kutaniko

Msifu Yehova Katika Kutaniko

“Katikati ya kutaniko nitakusifu.”​—ZAB. 22:22.

WIMBO 59 Msifuni Yah Pamoja Nami

MUHTASARI *

1. Daudi alihisije kumhusu Yehova, na jambo hilo lilimchochea kufanya nini?

MFALME DAUDI aliandika hivi: “Yehova ni mkuu na anastahili kabisa kusifiwa.” (Zab. 145:3) Daudi alimpenda Yehova na upendo huo ulimchochea kumsifu Mungu “katikati ya kutaniko.” (Zab. 22:22; 40:5) Hapana shaka kwamba unampenda Yehova na unakubaliana na maneno haya ya Daudi: “Na usifiwe, Ee Yehova Mungu wa Israeli baba yetu, kwa umilele wote.”​—1 Nya. 29:10-13.

2. (a) Tunaweza kumsifu Yehova jinsi gani? (b) Baadhi ya ndugu na dada hukabili changamoto gani, na tutazungumzia nini?

2 Njia moja tunayomsifu Yehova leo ni kwa kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, ni changamoto kubwa kwa baadhi ya ndugu na dada zetu kufanya hivyo. Wanatamani kutoa maelezo mikutanoni, lakini wanaogopa. Wanaweza kushindaje woga huo? Na sisi sote tunaweza kutumia mapendekezo gani yatakayotusaidia kutoa maelezo yenye kujenga? Kabla ya kujibu maswali hayo, acheni kwanza tuzungumzie sababu nne muhimu ambazo hutuchochea kutoa maelezo mikutanoni.

KWA NINI SISI HUTOA MAELEZO MIKUTANONI?

3-5. (a) Kama andiko la Waebrania 13:15 linavyoonyesha, kwa nini sisi hutoa maelezo mikutanoni? (b) Je, ni lazima sisi sote tutoe maelezo yanayofanana? Eleza.

3 Yehova ametupatia sisi sote pendeleo la kumsifu. (Zab. 119:108) Maelezo tunayotoa mikutanoni ni sehemu ya “dhabihu ya sifa,” na hakuna anayeweza kutoa dhabihu kwa niaba yetu. (Soma Waebrania 13:15.) Je, Yehova anamtarajia kila mmoja wetu atoe dhabihu au maelezo yanayofanana na ya mwenzake? Sivyo, hata kidogo!

4 Yehova anajua kwamba uwezo na hali zetu hutofautiana, naye huthamini sana dhabihu tunazotoa kulingana na uwezo wetu. Fikiria kuhusu dhabihu ambazo alikubali Waisraeli wamtolee. Waisraeli fulani walikuwa na uwezo wa kumtolea mwanakondoo au mbuzi. Lakini Mwisraeli maskini angemtolea “njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga.” Na ikiwa Mwisraeli hakuwa na uwezo wa kupata ndege wawili, Yehova alikubali “sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja ya unga laini.” (Law. 5:7, 11) Unga haukuwa ghali, hata hivyo Yehova alikubali dhabihu hiyo maadamu ilikuwa ya “unga laini.”

5 Mungu wetu mwenye fadhili anahisi vivyo hivyo leo. Tunapotoa maelezo, hatarajii sisi sote tutoe maelezo kwa ufasaha kama Apolo au kwa usadikisho kama Paulo. (Mdo. 18:24; 26:28) Kile ambacho Yehova anatarajia kutoka kwetu ni kwamba tutoe maelezo bora kadiri tuwezavyo—kulingana na uwezo wetu. Mkumbuke yule mjane aliyetoa sarafu mbili ndogo. Yehova alimwona kuwa mwenye thamani kwa sababu alitoa kilicho bora kabisa kulingana na uwezo wake.—Luka 21:1-4.

Kutoa maelezo mikutanoni hutunufaisha sisi na wale wanaotusikiliza(Tazama fungu la 6 na 7) *

6. (a) Kulingana na andiko la Waebrania 10:24, 25, maelezo ya ndugu na dada zetu hufanya tuhisije? (b) Unaweza kuonyeshaje kwamba unathamini maelezo yenye kutia moyo yanayotolewa na wengine?

6 Tunatiana moyo kupitia maelezo yetu. (Soma Waebrania 10:24, 25.) Kila mmoja wetu hufurahia kusikia maelezo mbalimbali yanayotolewa kwenye mikutano yetu. Tunafurahia maelezo mafupi na ya unyoofu yanayotolewa na watoto wadogo. Tunaguswa moyo sana tunapomsikia ndugu au dada akitoa maelezo kuhusu kweli fulani aliyojifunza hivi karibuni. Na tunafurahishwa na wale ‘wanaojipa ujasiri’ ili watoe maelezo, hata ingawa wao ni wenye haya au ndiyo wameanza kujifunza lugha yetu. (1 The. 2:2) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini jitihada zao? Baada ya mikutano, tunaweza kuwashukuru kwa maelezo yao yenye kutia moyo. Pia, tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini maelezo yao tunaposhiriki kutoa maelezo mikutanoni. Kwa njia hiyo, tutatiwa moyo katika mikutano yetu na wakati uleule tutawatia moyo wengine.​—Rom. 1:11, 12.

7. Tunanufaikaje tunapotoa maelezo?

7 Tunajinufaisha wenyewe tunapotoa maelezo. (Isa. 48:17) Jinsi gani? Kwanza, ikiwa tunakusudia kutoa maelezo mikutanoni, tutachochewa kujitayarisha vizuri kwa ajili ya mkutano huo. Tunapojitayarisha vizuri, tunalielewa Neno la Mungu kwa kina zaidi. Na kadiri tunavyolielewa vizuri zaidi, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kutumia mambo tunayojifunza. Pili, tutafurahia zaidi mkutano kwa sababu tunashiriki kutoa maelezo. Tatu, kwa sababu jitihada zinahusika ili kutoa maelezo, mara nyingi tutakumbuka kwa muda mrefu mambo tuliyosema.

8-9. (a) Kama andiko la Malaki 3:16 linavyoonyesha, unafikiri Yehova anahisije kuhusu maelezo tunayotoa mikutanoni? (b) Ni changamoto gani ambayo huenda baadhi ya ndugu na dada zetu wanakabili?

8 Tunamfurahisha Yehova tunapozungumza kuhusu imani yetu. Uwe na hakika kwamba Yehova hutusikiliza na anathamini sana jitihada tunazofanya ili kutoa maelezo mikutanoni. (Soma Malaki 3:16.) Yehova anaonyesha kwamba anathamini jitihada zetu kwa kutubariki tunapojitahidi sana kumfurahisha.​—Mal. 3:10.

9 Kwa kweli, tuna sababu nzuri za kutoa maelezo mikutanoni. Ingawa hivyo, baadhi ya ndugu na dada huogopa kuinua mkono. Ikiwa unahisi hivyo, usivunjike moyo. Acheni tuchunguze baadhi ya kanuni za Biblia, mifano michache, na mapendekezo fulani yanayoweza kutusaidia sisi sote kutoa maelezo mara nyingi zaidi mikutanoni.

JINSI YA KUSHINDA WOGA

10. (a) Wengi wetu huogopa kufanya nini? (b) Kwa nini huenda ikawa ishara nzuri mtu anapokuwa na woga wa kutoa maelezo?

10 Je, wewe huhisi ni kana kwamba tumbo linasokota kwa sababu ya wasiwasi kila mara unapofikiria kuinua mkono wako ili kutoa maelezo? Ikiwa ndivyo, si wewe tu ambaye huhisi hivyo. Ukweli ni kwamba wengi wetu hushikwa na kiasi fulani cha woga tunapotoa maelezo. Kabla ya kujua jinsi ya kushinda hisia hizo za woga, unahitaji kutambua chanzo ya woga huo. Je, wewe huogopa kwamba utasahau mambo unayotaka kusema au utatoa maelezo yasiyo sahihi? Je, wewe huwa na wasiwasi kwamba maelezo yako hayatakuwa mazuri kama ya wengine? Kihalisi, kuwa na wasiwasi kuhusu mambo hayo ni ishara nzuri. Wasiwasi huo unaonyesha kwamba wewe ni mnyenyekevu na unawaona wengine kuwa bora kuliko wewe. Yehova anapenda sifa ya unyenyekevu. (Zab. 138:6; Flp. 2:3) Lakini pia Yehova anataka umsifu na uwatie moyo ndugu na dada zako mikutanoni. (1 The. 5:11) Anakupenda na atakupatia ujasiri unaohitaji.

11. Ni vikumbusho gani kutoka katika Maandiko vinavyoweza kutusaidia?

11 Fikiria kuhusu vikumbusho fulani kutoka katika Maandiko. Biblia husema kwamba sisi sote hukosea kupitia maneno tunayosema na jinsi tunavyoyasema. (Yak. 3:2) Yehova wala ndugu na dada zetu hawatarajii ukamilifu kutoka kwetu. (Zab. 103:12-14) Wao ni sehemu ya familia yetu ya kiroho, na wanatupenda. (Marko 10:29, 30; Yoh. 13:35) Wanaelewa kwamba huenda nyakati nyingine tukashindwa kutoa maelezo kwa njia tuliyokusudia.

12-13. Mfano wa Nehemia na Yona unatufundisha nini?

12 Fikiria kuhusu mifano fulani ya Biblia inayoweza kukusaidia ushinde hisia za woga. Mkumbuke Nehemia. Alitumikia katika makao ya mfalme mwenye mamlaka kubwa. Nehemia alikuwa na huzuni kwa sababu alikuwa amesikia kwamba kuta na malango ya jiji la Yerusalemu yalikuwa yamebomolewa na kuteketezwa. (Neh. 1:1-4) Wazia jinsi alivyokuwa na hofu na wasiwasi mwingi mfalme alipomwomba aeleze sababu iliyomfanya aonekane akiwa mwenye huzuni! Nehemia alisali papo hapo na kisha akamweleza sababu hiyo. Matokeo yake ni kwamba, mfalme aliwasaidia sana watu wa Mungu. (Neh. 2:1-8) Fikiria pia kumhusu Yona. Yehova alipomwagiza aende Ninawi akazungumze na wakaaji wa jiji hilo, Yona aliogopa sana hivi kwamba akakimbilia eneo lingine. (Yona 1:1-3) Lakini kwa msaada wa Yehova, Yona alitimiza mgawo wake. Na maneno aliyosema yaliwasaidia watu wa Ninawi kubadili njia zao. (Yona 3:5-10) Mfano wa Nehemia unatufundisha kuhusu umuhimu wa kusali kabla ya kutoa maelezo. Na mfano wa Yona unatufundisha kwamba Yehova anaweza kutusaidia tumtumikie hata iwe tuna woga mwingi kadiri gani. Kihalisi, je, kuna kutaniko lolote lililo na ndugu na dada wenye kutisha kama Waninawi walivyokuwa?

13 Ni mapendekezo gani yanayoweza kukusaidia kutoa maelezo yenye kutia moyo mikutanoni? Acheni tuchunguze mapendekezo machache.

14. Kwa nini tunapaswa kujitayarisha vizuri kwa ajili ya mikutano, na tunaweza kufanya hivyo wakati gani?

14 Jitayarishe kwa ajili ya kila mkutano. Ikiwa umepanga mapema kutoa maelezo na umejitayarisha vizuri, utahisi ukiwa na uhakika zaidi wa kutoa maelezo. (Met. 21:5) Bila shaka, ratiba zetu za kuandaa mikutano hazifanani. Eloise, dada mjane aliye na umri wa miaka 80 hivi, huanza kutayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi mapema juma linapoanza. Anasema hivi: “Mimi hufurahia mikutano zaidi ikiwa nimejitayarisha mapema.” Joy, dada anayefanya kazi ya kimwili ya wakati wote, hutenga wakati siku ya Jumamosi ili atayarishe Funzo la Mnara wa Mlinzi. Anasema hivi: “Mimi hufanya hivyo ili niweze kukumbuka vizuri zaidi habari hiyo.” Ike, mzee wa kutaniko mwenye shughuli nyingi ambaye pia ni painia anasema hivi: “Badala ya kujifunza kwa muda mrefu kwa wakati mmoja, mimi hupenda kutumia vipindi vifupi-vifupi katika juma ili kujifunza.”

15. Unaweza kufanya nini ili ujitayarishe vizuri kwa ajili ya mikutano?

15 Kujitayarisha vizuri kwa ajili ya mikutano kunahusisha nini? Anza kila kipindi cha kujifunza kwa kumwomba Yehova akupe roho yake takatifu. (Luka 11:13; 1 Yoh. 5:14) Kisha tumia dakika chache kupitia kwa ufupi habari unayotaka kujifunza. Changanua kichwa kikuu, vichwa vidogo, picha, na masanduku ya kufundishia. Sasa unapojifunza kila fungu, jitahidi kadiri uwezavyo kusoma maandiko mengi ambayo hayajanukuliwa. Tafakari kuhusu habari hiyo, na uyape uangalifu wa pekee mambo ambayo ungependa kutaja katika maelezo yako. Ukijitayarisha vizuri, utanufaika zaidi na itakuwa rahisi zaidi kwako kutoa maelezo mikutanoni.​—2 Kor. 9:6.

16. Ni programu gani za kielektroni zinazopatikana katika lugha yako, nawe unazitumiaje?

16 Ikiwezekana, tumia programu za kielektroni zinazopatikana katika lugha yako. Kupitia tengenezo lake, Yehova ametuandalia programu za kielektroni zinazotusaidia kujitayarisha kwa ajili ya mikutano. Programu ya JW Library® hutuwezesha kupakua machapisho ya kujifunza kwenye vifaa vyetu vya mkononi. Kisha tunaweza kujifunza—au hata kusoma na kusikiliza rekodi za sauti za habari hiyo—wakati wowote na mahali popote. Baadhi ya ndugu na dada hutumia programu hiyo kujifunza wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana wakiwa kazini au shuleni au wanaposafiri. Programu ya Watchtower Library na Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO hufanya iwe rahisi kwetu kufanya utafiti kuhusu mambo ambayo tungependa kujifunza kwa undani zaidi.

Wewe hujitayarisha lini kwa ajili ya mikutano? (Tazama fungu la 14-16) *

17. (a) Kwa nini ni vizuri kutayarisha maelezo kadhaa utakayotoa mikutanoni? (b) Video ya Uwe Rafiki ya Yehova—Jitayarishe Kutoa Maelezo ilikufundisha nini?

17 Ikiwezekana, jitayarishe kutoa maelezo kadhaa kwa ajili ya kila sehemu ya mkutano. Kwa nini? Kwa sababu huenda usichaguliwe kutoa maelezo kila mara unapoinua mkono. Huenda wengine pia wakainua mikono yao wakati uleule, na ndugu anayeongoza mkutano huo anaweza kumchagua mmoja wao. Ili kuhakikisha kwamba mkutano unamalizika kwa wakati, huenda ndugu anayeongoza mkutano akawachagua watu wachache tu watoe maelezo kuhusu habari inayozungumziwa. Hivyo, usihisi vibaya au kuvunjika moyo ikiwa hatakuchagua utoe maelezo mwanzoni-mwanzoni mwa funzo. Ikiwa utatayarisha maelezo kadhaa, utakuwa na fursa nyingi zaidi za kushiriki kwenye mikutano. Kusoma andiko ni mojawapo ya maelezo unayoweza kujitayarisha kutoa. Ikiwezekana, unaweza pia kujitayarisha kutoa maelezo kwa kutumia maneno yako mwenyewe. *

18. Kwa nini tunatiwa moyo kutoa maelezo mafupi?

18 Toa maelezo mafupi. Kwa kawaida, maelezo yenye kutia moyo zaidi ni maelezo mafupi na yaliyo wazi. Hivyo, jiwekee lengo la kutoa maelezo mafupi. Jitahidi kutoa maelezo yasiyozidi sekunde 30. (Met. 10:19; 15:23) Ikiwa umekuwa ukitoa maelezo mikutanoni kwa miaka mingi, una jukumu muhimu la kuwawekea wengine mfano mzuri kwa kutoa maelezo mafupi. Ukitoa maelezo marefu na yenye habari nyingi, huenda wengine wakaogopa kutoa maelezo wakifikiri kwamba hawawezi kujieleza kama wewe. Pia, maelezo mafupi huwapa watu wengi zaidi fursa ya kushiriki katika mikutano. Ikiwa wewe ndiye wa kwanza kuchaguliwa kujibu swali fulani, toa maelezo mafupi yanayojibu moja kwa moja swali lililoulizwa. Usitoe maelezo kuhusu kila jambo lililotajwa kwenye fungu. Baada ya habari ya msingi katika fungu kuzungumziwa, sasa unaweza kutoa maelezo kuhusu habari nyingine za ziada katika fungu hilo.​—Tazama sanduku lenye kichwa “ Ninaweza Kutoa Maelezo Kuhusu Nini?

19. Ndugu anayeongoza mkutano anaweza kukusaidiaje, lakini unahitaji kufanya nini?

19 Ikiwa ungependa kutoa maelezo katika fungu fulani hususa, mjulishe ndugu anayeongoza sehemu hiyo. Ukiamua kufanya hivyo, mweleze ndugu anayeongoza sehemu hiyo mapema kabla ya mkutano kuanza. Wakati wa kutoa maelezo kuhusu fungu hilo unapofika, bila kukawia inua mkono wako juu kabisa ili ndugu anayeongoza aweze kuuona.

20. Ni katika njia gani mikutano ni kama chakula unachoshiriki pamoja na marafiki?

20 Ione mikutano kama chakula unachokula pamoja na marafiki wapendwa. Wazia kwamba marafiki fulani kutanikoni wamepanga kuwa na tafrija, na wamekuomba utayarishe chakula fulani kidogo. Wewe ungefanya nini? Huenda ukawa na wasiwasi kidogo, lakini inaelekea utajitahidi kadiri uwezavyo kuleta chakula ambacho kila mmoja atafurahia. Yehova Ndiye aliyetukaribisha mikutanoni na ameandaa meza yenye vitu vingi vyema kwa ajili yetu. (Zab. 23:5; Mt. 24:45) Naye anafurahi sana tunapoleta zawadi fulani ndogo, lakini nzuri kabisa. Hivyo, jitayarishe vizuri na ushiriki kutoa maelezo mara nyingi kadiri uwezavyo. Ukifanya hivyo, utashiriki zawadi yako pamoja na kutaniko na wakati uleule utafurahia mlo katika meza ya Yehova.

WIMBO 2 Jina Lako Ni Yehova

^ fu. 5 Kama mtunga zaburi Daudi, sisi sote tunampenda Yehova na tunafurahia kumsifu. Tuna fursa ya pekee ya kuonyesha kwamba tunampenda Mungu tunapokutanika pamoja kutanikoni kwa ajili ya ibada. Hata hivyo, baadhi yetu huona kutoa maelezo mikutanoni kuwa jambo gumu. Ikiwa unakabili changamoto hiyo, makala hii itakusaidia kujua kwa nini huenda ukawa na woga wa kutoa maelezo na jinsi ya kushinda woga huo.

^ fu. 17 Tazama video Uwe Rafiki ya Yehova—Jitayarishe Kutoa Maelezo. Kwenye Tovuti ya jw.org/sw. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > WATOTO.

^ fu. 63 MAELEZO YA PICHA: Ndugu na dada kutanikoni wakishiriki kwa shangwe kutoa maelezo kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 65 MAELEZO YA PICHA: Baadhi ya ndugu na dada walioonyeshwa awali walipokuwa wakishiriki katika Funzo la Mnara wa Mlinzi. Ingawa hali za kila mmoja wao zinatofautiana, wote hutenga wakati wa kujitayarisha kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi.